Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Tunapaswa Kukumbuka Kifo cha Yesu Jinsi Gani?

Tunapaswa Kukumbuka Kifo cha Yesu Jinsi Gani?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Kifo cha Yesu kinapaswa kukumbukwa jinsi gani?

Yesu aliwaambia wafuasi wake wakumbuke kifo chake kwa kula mlo wa mfano, wakitumia mkate na divai. Mkate unawakilisha mwili wa Yesu nayo divai inawakilisha damu yake.—Soma Luka 22:19, 20.

Mkate ambao Yesu alitumia haukuwa na chachu. Katika Biblia, mara nyingi chachu hutumiwa kufananisha dhambi. Kwa hiyo, mkate ulikuwa mfano unaofaa wa mwili mkamilifu wa Yesu. Alitoa mwili wake uwe dhabihu, ambayo iliondolea mbali dhabihu za wanyama zilizotolewa kulingana na Sheria ya Musa. (Waebrania 10:5, 9, 10) Divai ilikuwa mfano wa damu ya Yesu yenye thamani iliyomwagwa ili kuwa dhabihu kwa ajili ya dhambi zetu.—Soma 1 Petro 1:19; 2:24; 3:18.

2. Tunapaswa kukumbuka kifo cha Yesu wakati gani?

Yesu alikufa siku ya Pasaka, Nisani 14. Siku ya Kiyahudi huanza baada ya jua kutua. Jioni iliyotangulia kifo chake, Yesu alikula mlo wa Pasaka pamoja na mitume wake na kisha, akaanzisha mlo mpya ili uwe kikumbusho cha kifo chake.—Soma Luka 22:14, 15.

Leo, watu wa Mungu hukumbuka yale ambayo Mungu aliandaa kupitia Yesu ili kuukomboa ulimwengu mzima kutoka katika dhambi na kifo. (Kutoka 12:5-7, 13, 17) Kama vile Pasaka ilivyoadhimishwa mara moja kwa mwaka, Ukumbusho wa kifo cha Yesu hufanywa mara moja kwa mwaka baada ya jua kutua siku ya 14 ya mwezi wa Nisani, kulingana na kalenda ya Biblia.—Soma Yohana 1:29.

3. Ni nani wanaopaswa kula mkate na kunywa divai?

Yesu alipowapa wafuasi wake divai alisema: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya.” (1 Wakorintho 11:25) Agano jipya lilichukua mahali pa agano la Sheria ya Musa. Katika agano hilo Mungu alikuwa amewaahidi Waisraeli kwamba ikiwa wangemtii kabisa, wangekuwa watu wake. (Kutoka 19:5, 6) Hata hivyo, Waisraeli hawakutii sauti ya Mungu. Kwa hiyo, Yehova akaandaa agano jipya.—Soma Yeremia 31:31.

Kupitia agano hilo jipya, Yehova anafanya baraka zipatikane kwa watu wengi kupitia wachache. Watu walio katika agano hilo si wengi. Idadi yao ni 144,000 tu. Kupitia watu hao, mamilioni ya watu kutoka mataifa yote watabarikiwa kwa kupata uzima wa milele katika dunia paradiso. Baadhi ya wale walio katika agano jipya wanamtumikia Yehova duniani leo. Wao pekee ndio wanaopaswa kula mkate na kunywa divai kwa sababu kikombe “kinamaanisha agano jipya.”—Soma Luka 12:32; Ufunuo 14:1, 3.

4. Kukumbuka kifo cha Yesu kunatufaidi jinsi gani?

Kukumbuka kifo cha Yesu kila mwaka huimarisha uthamini wetu kwa upendo wa Yehova usio na kifani. Alimtuma Mwana wake ili afe kwa ajili ya dhambi zetu. Kwa hiyo, tunapohudhuria Ukumbusho, tunapaswa kutafakari kifo cha Yesu kinamaanisha nini kwetu. Tunapaswa kufikiria jinsi tunavyoweza kuonyesha uthamini kwa yale ambayo Yehova na Yesu wametufanyia.—Soma Yohana 3:16; 2 Wakorintho 5:14, 15.

Kwa habari zaidi, ona ukurasa wa 206-208 wa kitabu hiki, Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.