Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waazteki wa Kisasa Wajifunza na Kuwa Wakristo wa Kweli

Waazteki wa Kisasa Wajifunza na Kuwa Wakristo wa Kweli

Waazteki wa Kisasa Wajifunza na Kuwa Wakristo wa Kweli

“Mahekalu yalianguka, yakawa vumbi na majivu, sanamu ziliharibiwa, navyo vitabu vitakatifu vikateketezwa kwa moto, lakini miungu ya kale bado inakaa katika mioyo ya Wahindi.”—Las antiguas culturas mexicanas (Tamaduni za Kale za Mexico).

MEXICO ndiyo makao ya Waazteki ambao katika karne ya 13 walikuwa kabila dogo tu lililokuwa limehamia nchini humo. Hata hivyo, waliongezeka na kuwa milki yenye nguvu, sawa na milki ya Wainka nchini Peru. Ingawa milki ya Waazteki, au Wanahuatl, ilianguka wakati Hispania ilipoteka jiji la Tenochtitlán mwaka wa 1521, lugha yao ya Kinahuatl bado inazungumzwa. * Lugha hiyo inazungumzwa na wenyeji milioni moja na nusu hivi katika majimbo yapatayo 15 nchini Mexico. Lugha hiyo imesaidia kuhifadhi mambo ambayo Waazteki waliamini zamani, kama vile inavyoonyeshwa na maneno ya mtafiti Walter Krickeberg yaliyonukuliwa hapo juu. Waliamini mambo gani?

Desturi za Ajabu Lakini Zenye Kujulikana

Yaelekea desturi ya Waazteki ya kutoa watu dhabihu ndiyo inayojulikana zaidi. Waliamini kwamba jua lingekufa kama halingelishwa damu na mioyo ya wanadamu. Kasisi Mhispania, Diego Durán anasema kwamba katika mwaka wa 1487, wakati hekalu kubwa jijini Tenochtitlán lilipokuwa likiwekwa wakfu, watu 80,000 walitolewa dhabihu katika muda wa siku nne.

Ingawa Wahispania walichukizwa na zoea hilo, walishangaa kutambua kwamba mambo mengi ambayo Waazteki waliamini yalifanana na mafundisho ya kanisa lao la Katoliki. Kwa mfano, Waazteki walikuwa na zoea la kukutana pamoja na kula sanamu za miungu yao zilizotengenezwa kwa mahindi. Pia, nyakati fulani nyama za watu waliotolewa dhabihu zililiwa. Waazteki walitumia msalaba, wakatubu kwa kuelezea makosa yao, na kubatiza watoto wachanga. Yaelekea ibada ya bikira Tonantzin, “Mama wa Miungu,” ambaye Waazteki walimwita Mama Yetu Mdogo, ndilo jambo linalofanana zaidi kati ya ibada ya Waazteki na ya Wakatoliki.

Inasemekana kwamba kwenye mlima uleule ambapo Waazteki walimwabudu Tonantzin, Bikira wa Guadalupe wa Wakatoliki alimtokea Mwazteki fulani katika mwaka wa 1531. Pia, inasemekana kwamba bikira huyo aliyezungumza Kinahuatl hakuwa na ngozi nyeupe sana. Jambo hilo lilichochea Waazteki wengi wajiunge na Kanisa Katoliki. Bikira huyo alijengewa kanisa kubwa kwenye msingi wa hekalu la Tonantzin. Kila Desemba 12, mamia ya maelfu ya Wamexico hutembelea kanisa hilo, na wengi wao wanazungumza Kinahuatl.

Katika makao yao yaliyo milimani, Wanahuatl hufanya sherehe nyingi za kuwakumbuka watakatifu walezi. Baadhi ya sherehe hizo huendelea kwa siku nyingi au hata kwa majuma kadhaa. Kitabu El universo de los aztecas (Ulimwengu wa Waazteki) kinasema kwamba Wanahuatl “wanahusianisha ibada ya watakatifu wa Kanisa Katoliki na sherehe zilizofanywa kabla ya [uvamizi wa] Cortés.” Pia, wao hujihusisha sana na zoea la kuwasiliana na pepo. Wanapokuwa wagonjwa, wanaenda kwa waponyaji ambao hufanya desturi za kitamaduni za kuwatakasa na pia kutoa dhabihu za wanyama. Zaidi ya hayo, wengi wao hawajui kusoma wala kuandika; hawawezi kusoma Kinahuatl wala Kihispania. Watu hao wametengwa na jamii nyingine kwa kuwa ni maskini kupindukia na wanafuata sana mapokeo na lugha yao.

Ukweli wa Biblia Wawafikia Waazteki wa Kisasa

Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova nchini Mexico wamejitahidi kuwahubiria watu wote “habari njema ya ufalme.” (Mathayo 24:14) Katika mwaka wa 2000, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Mexico ilianzisha mradi wa kuwahubiria watu wote wanaozungumza Kinahuatl na kuanzisha makutaniko ya lugha hiyo kwa ajili ya wale waliokuwa wakihudhuria mikutano ya Kihispania. Kikundi cha watafsiri kilianzishwa ili kutafsiri machapisho yanayotegemea Biblia katika Kinahuatl. Jitihada pia zilifanywa ili kuwafundisha Wanahuatl kusoma na kuandika lugha yao. Kumekuwa na matokeo gani? Fikiria mambo yafuatayo.

Mwanamke fulani mwenyeji aliposikia hotuba ya Biblia katika Kinahuatl kwa mara ya kwanza, alisema: “Tumekuwa tukihudhuria mikutano kwa miaka kumi na kurudi nyumbani tukiumwa na kichwa kwa sababu hatukuelewa Kihispania vizuri. Lakini sasa, ni kana kwamba tumeanza maisha upya!” Juan, mwenye umri wa miaka 60 amekuwa akijifunza Biblia na kuhudhuria mikutano ya Kihispania pamoja na mke wake na watoto wao kwa miaka minane bila kufanya maendeleo yoyote. Kisha, akaanza kujifunza Biblia katika Kinahuatl. Katika muda usiozidi mwaka mmoja, alibatizwa na kuwa Shahidi!

Kama mambo hayo yaliyoonwa yanavyoonyesha, wengi walihubiriwa ujumbe wa Biblia mara ya kwanza katika Kihispania, lakini hawakuuelewa vizuri. Kuhudhuria mikutano, makusanyiko, na kupata machapisho katika lugha yao wenyewe kumewasaidia kujua kweli za Biblia na kuelewa majukumu yao wakiwa Wakristo.

Kushinda Matatizo

Wanahuatl wanakabili matatizo fulani wanapofanya maendeleo ya kiroho. Kwa mfano, kuna shinikizo kubwa la kushiriki katika sherehe za kidini. Katika mji wa San Agustín Oapan, Mashahidi wa Yehova walikatazwa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kulikuwa na wasiwasi kwamba jambo hilo lingewachochea watu waache kutoa pesa za kulipia sherehe hizo. Wakati Florencio na kikundi kidogo cha Mashahidi Wanahuatl walipokuwa wakihubiri, watatu kati yao walikamatwa. Katika muda wa dakika 20, umati ulikusanyika ili kuamua hatua ambayo wangewachukulia.

“Walitaka kutuua papo hapo,” Florencio anasema. “Baadhi yao walisema tufungwe na kutupwa mtoni ili tufe maji! Tulikaa gerezani usiku mmoja. Siku iliyofuata, Shahidi aliyekuwa wakili na Mashahidi wengine wawili walikuja kutusaidia. Wao pia wakatupwa gerezani. Mwishowe, wenye mamlaka walikubali kutuachilia ikiwa tu tungeondoka katika mji huo.” Licha ya hayo, kutaniko lilianzishwa mwaka mmoja baadaye, likiwa na Mashahidi 17 waliobatizwa na watu 50 hivi walihudhuria mikutano.

Alberto, ambaye ni Shahidi wa Yehova, alikaribishwa kwenye sherehe ya jamii ya Wanahuatl wa Coapala. Alikataa na akatupwa gerezani. Watu wa jamii hiyo walifanya mkutano, na baadhi yao wakapendekeza anyongwe ili kuwatisha watu wengine ambao wangetaka kujiunga na dini yake na kuacha desturi zao. Mashahidi wengine walijaribu kumsaidia ili aachiliwe, lakini wao pia wakakamatwa. Wote waliachiliwa baada ya sherehe hiyo ya juma moja. Upinzani ulipoendelea, Mashahidi walilazimika kutafuta msaada kwa wenye mamlaka ya juu, hivyo, agizo likatolewa la kukomesha mateso hayo. Inapendeza kwamba mwanamume aliyekuwa mpinzani mkuu alikubali kweli ya Biblia na muda si muda, akabatizwa. Sasa kuna kutaniko katika mji huo.

Tayari kwa Mavuno

Mashahidi wengi wanajifunza Kinahuatl kwa sababu wameona kuna uwezekano wa kuwa na ongezeko kubwa katika eneo la Wanahuatl. Hata hivyo, jambo hilo si rahisi. Wanahuatl wana haya sana na hawapendi kuzungumza lugha yao kwa sababu ya jinsi ambavyo wamekuwa wakitendewa. Pia, Kinahuatl kina lahaja nyingi.

Sonia, mhudumu wa wakati wote, anaeleza kilichomchochea ajifunze lugha hiyo. “Kuna wahamiaji 6,000 hivi wanaozungumza Kinahuatl ambao wanaishi karibu na nyumbani kwangu. Wanaishi katika vibanda vyenye ua na walinzi. Watu hao wamefedheheshwa na hawana usalama,” asema Sonia. “Hali zao zilinihuzunisha sana kwa sababu pindi moja walijivunia maisha yao, nao ndio chanzo cha utamaduni wetu. Tulikuwa tumewahubiria kwa Kihispania kwa miaka 20, lakini hawakupendezwa sana wala kuuelewa vizuri ujumbe wetu. Hata hivyo, nilipojifunza maneno machache ya lugha yao, hali ilibadilika. Walikuwa wakinizunguka wakitaka kusikiliza. Nilijitolea kumfundisha mwanamke mmoja kusoma na kuandika kama angenifundisha Kinahuatl. Sasa wananijua kwenye vibanda vyote kuwa ‘mwanamke anayezungumza Kinahuatl.’ Ninahisi kama mmishonari katika nchi yangu.” Sasa kuna kutaniko la Kinahuatl katika eneo hilo.

Maricela, mhudumu mwingine wa wakati wote, anajitahidi kujifunza Kinahuatl. Mwanzoni, alijifunza Biblia akitumia Kihispania na mzee wa miaka 70 aitwaye Félix. Maricela aliendelea kujifunza Kinahuatl, kwa hiyo, akaanza kumfundisha Félix katika lugha yake. Matokeo yalikuwa mazuri. Aliguswa moyo sana wakati Félix alipomuuliza: “Je, Yehova husikiliza ninapozungumza naye katika Kinahuatl?” Félix alifurahi kujua kwamba Yehova anaelewa lugha zote. Sasa Félix amebatizwa na anahudhuria mikutano kwa ukawaida hata ingawa analazimika kutembea kwa miguu kwa muda wa saa moja na nusu ili kufika mikutanoni. Maricela anasema, “Ninafurahi sana kushirikiana na malaika ambaye ana habari njema ya kuwatangazia watu wote!”—Ufunuo 14:6, 7.

Kwa kweli shamba la Wanahuatl ni ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa.’ (Yohana 4:35) Tunatumaini kwamba Yehova Mungu ataendelea kuwakaribisha watu wa mataifa yote, kutia ndani Waazteki wa kisasa, waende kwenye mlima wake ili kufundishwa njia zake.—Isaya 2:2, 3.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Kinahuatl ni moja kati ya lugha mbalimbali zinazotumiwa na jamii za wenyeji wa Amerika Kaskazini kama vile Hopi, Shoshone, na Comanche. Kiingereza kimekopa maneno mengi kutoka Kinahuatl, kama vile avocado (parachichi), chocolate (chokoleti), coyote (koyoti), na tomato (nyanya).

[Ramani katika ukurasa wa 13]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

JIJI LA MEXICO

IDADI YA WAAZTEKI KATIKA KILA JIMBO

150,000

CHINI YA 1,000