Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nimewajulisha Jina Lako”

“Nimewajulisha Jina Lako”

“Nimewajulisha Jina Lako”

“Nimelifunua jina lako kwa watu ulionipa kutoka ulimwenguni. . . . Nimewajulisha jina lako nami nitalijulisha.”—YOHANA 17:6, 26.

Inamaanisha Nini? Yesu aliwajulisha watu jina la Mungu kwa kulitumia katika huduma yake. Yesu alipokuwa akisoma Maandiko, kama alivyofanya mara nyingi, alitamka jina la kibinafsi la Mungu. (Luka 4:16-21) Aliwafundisha wafuasi wake kusali hivi: “Baba, jina lako na litakaswe.”—Luka 11:2.

Wakristo wa Mapema Walifanyaje Hivyo? Mtume Petro aliwaambia wanaume wazee huko Yerusalemu kwamba Mungu alikuwa amechukua kutoka katika mataifa “watu kwa ajili ya jina lake.” (Matendo 15:14) Mtume huyo na wengine walihubiri kwamba “kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.” (Matendo 2:21; Waroma 10:13) Pia, walitumia jina la Mungu katika maandishi yao. Mkusanyo wa sheria za Wayahudi unaoitwa The Tosefta, ambao ulikamilishwa karibu mwaka wa 300 W.K., unasema hivi kuhusu maandishi ya Wakristo yaliyoteketezwa na wapinzani: “Wanaviteketeza vitabu vya Waevanjeli na vitabu vya minim [watu wanaodhaniwa kuwa Wakristo Wayahudi]. Vinaruhusiwa viteketee mahali vinapopatikana, . . . pamoja na marejeo ya Jina la Mungu lililo ndani ya vitabu hivyo.”

Ni Nani Wanaofanya Hivyo Leo? Biblia ya Revised Standard Version, iliyoidhinishwa rasmi na Baraza la Kitaifa la Makanisa ya Kristo nchini Marekani, inasema hivi katika utangulizi: “Mazoea ya kutumia jina la kibinafsi la Mungu wa pekee, kana kwamba kuna miungu mingine anayopaswa kutofautishwa nayo, yaliacha kufuatwa katika dini ya Kiyahudi kabla ya enzi ya Ukristo na hayafai kwa imani ya Kanisa la Kikristo la ulimwenguni pote.” Hivyo, Biblia hiyo inatumia jina la cheo “BWANA” badala ya kutumia jina la Mungu. Hivi karibuni, Vatikani iliwaagiza makasisi wake hivi: “Katika sala na nyimbo, jina la Mungu ambalo linawakilishwa na herufi YHWH * za tetragramatoni halipaswi kutumiwa wala kutamkwa.”

Ni nani ambao leo wanatumia na kuwajulisha watu jina la kibinafsi la Mungu? Sergey alipokuwa tineja huko Kyrgyzstan, aliona video iliyosema kwamba jina la Mungu ni Yehova. Kwa miaka kumi hivi, hakulisikia tena jina hilo. Baadaye, Sergey alipohamia Marekani, Mashahidi wawili wa Yehova walimtembelea nyumbani mwake na kumwonyesha jina la Mungu katika Biblia. Sergey alifurahi sana kupata kikundi kilichotumia jina Yehova. Inapendeza kuona kwamba chini ya jina “Yehova Mungu,” kamusi ya Webster’s Third New International Dictionary inatoa ufafanuzi huu: “Mungu mkuu anayetambuliwa kuwa Mungu wa pekee ambaye anaabudiwa na Mashahidi wa Yehova.”

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Katika Kiswahili, kwa kawaida jina la Mungu linatafsiriwa “Yehova.”