Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia Neno la Mungu—Liko Hai!

Tumia Neno la Mungu—Liko Hai!

“Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.”—EBR. 4:12.

1, 2. Yehova alimpa Musa mgawo gani, na alimhakikishia nini?

UNGEHISIJE ikiwa ungesimama mbele ya mtawala mwenye nguvu zaidi duniani na kuwatetea watu wa Yehova? Inaelekea kwamba ungekuwa na wasiwasi, ungejiona hustahili, na kuogopa. Ungejitayarishaje? Ungefanya nini ili uzungumze kwa mamlaka zaidi ukiwa mwakilishi wa Mungu mweza yote?

2 Musa alikabili hali kama hiyo. Yehova alimwambia ‘mtu huyo aliyekuwa mpole zaidi kuliko watu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi’ kwamba anamtuma kwa Farao ili awakomboe watu wa Mungu kutokana na uonevu na utumwa nchini Misri. (Hes. 12:3) Farao alikuwa mtu mwenye dharau na kiburi. (Kut. 5:1, 2) Hata hivyo, Yehova alitaka Musa amwamuru Farao aruhusu mamilioni ya watumwa wake waondoke katika nchi hiyo! Ndiyo sababu Musa alimuuliza Yehova hivi: “Mimi ni nani hata niende kwa Farao, nikawatoe wana wa Israeli kutoka Misri?” Ni wazi kwamba Musa alihisi hastahili na hana uwezo wa kufanya hivyo. Lakini Mungu alimhakikishia kwamba hangekuwa peke yake. Yehova alimwambia hivi: “Nitakuwa pamoja nawe.”—Kut. 3:9-12.

3, 4. (a) Kwa nini Musa aliogopa? (b) Unakabili hali gani ngumu kama ya Musa?

3 Kwa nini Musa aliogopa? Inaonekana Musa aliogopa kwamba Farao hangemkaribisha au kumsikiliza mwakilishi  wa Yehova Mungu. Musa aliogopa pia kwamba watu wake mwenyewe hawangeamini kuwa Yehova alimchagua ili awaongoze kutoka Misri. Hivyo, Musa alimwambia hivi Yehova: “Tuseme hawaniamini wala hawaisikilizi sauti yangu, kwa sababu watasema, ‘Yehova hakukutokea.’”—Kut. 3:15-18; 4:1.

4 Jambo ambalo Yehova alimwambia Musa na matukio yaliyofuata yanaweza kutufundisha somo muhimu. Ni kweli kwamba huenda usisimame kamwe mbele ya ofisa mkuu wa serikali. Lakini je, ni vigumu kwako kuongea na watu wa kawaida tu kumhusu Mungu na Ufalme wake? Ikiwa ndivyo ilivyo, fikiria unayoweza kujifunza kutokana na Musa.

“NI NINI HICHO KILICHO MKONONI MWAKO?”

5. Mungu alitumia nini kilichokuwa mkononi mwa Musa, na hilo lilimpaje Musa uhakika? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 11.)

5 Musa aliposema kwamba huenda wasimwamini, Mungu alimtayarisha kukabiliana na hali hiyo. Kitabu cha Kutoka kinasema hivi: “Yehova akamwambia [Musa]: ‘Ni nini hicho kilicho mkononi mwako?’ naye akajibu: ‘Fimbo.’ Kisha akasema: ‘Itupe chini.’ Basi akaitupa chini, nayo ikawa nyoka; na Musa akaanza kumkimbia. Sasa Yehova akamwambia Musa: ‘Nyoosha mkono wako umkamate kwenye mkia.’ Basi akaunyoosha mkono wake, akamkamata, naye akawa fimbo mkononi mwake. ‘Ili kwamba,’ kama alivyosema, ‘wapate kuamini ya kwamba Yehova . . . amekutokea.’” (Kut. 4:2-5) Naam, Mungu alitumia kitu kilichokuwa mkononi mwa Musa kuthibitisha kwamba ujumbe wake ulitoka kwa Yehova. Huenda watu wangepuuza fimbo hiyo, lakini kwa nguvu za Mungu iligeuka na kuwa nyoka aliye hai! Muujiza huo ungethibitisha wazi kabisa kwamba Yehova alimtuma Musa na alikuwa akimtegemeza. Hivyo, Yehova alimwambia hivi: “Fimbo hii utaichukua mkononi mwako ili uitumie kufanya zile ishara.” (Kut. 4:17) Akiwa na uthibitisho mkononi mwake kwamba amepewa mamlaka na Mungu, Musa alimwakilisha Mungu wa kweli kwa uhakika mbele ya Waisraeli wenzake na mbele ya Farao.—Kut. 4:29-31; 7:8-13.

6. (a) Tunapaswa kuwa na nini mkononi tunapohubiri, na kwa nini? (b) Eleza jinsi ‘neno la Mungu lilivyo hai’ na ‘lilivyo na nguvu.’

6 Huenda swali hili likatuhusu pia tunapoenda kuhubiri ujumbe wa Biblia: “Ni nini hicho kilicho mkononi mwako?” Mara nyingi sisi huwa na Biblia mkononi, na tuko tayari kuitumia. Ingawa huenda wengine wakaiona Biblia kuwa kitabu cha kawaida tu, Yehova huongea nasi kupitia Neno lake lililoandikwa kwa mwongozo wa roho. (2 Pet. 1:21) Lina ahadi za Mungu zitakazotimia wakati wa utawala wa Ufalme wake. Ndiyo sababu mtume Paulo aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu.” (Soma Waebrania 4:12.) Yehova anaendelea kufanya kazi ili kuhakikisha kwamba ahadi zake zote zinatimia hatua kwa hatua. (Isa. 46:10; 55:11) Mtu anapotambua jambo hilo kuhusu Neno la Yehova, mambo anayosoma katika Biblia yanaweza kuwa na nguvu nyingi katika maisha yake.

7. Tunawezaje ‘kulitumia sawasawa neno la kweli’?

7 Naam, Yehova ameweka mkononi mwetu Neno lake lililo hai tunaloweza kutumia kuthibitisha kwamba ujumbe wetu ni wa kweli na unatoka kwake. Haishangazi kwamba baada ya kuwaandikia Waebrania, Paulo alimhimiza hivi Timotheo aliyekuwa akimzoeza: ‘Fanya kabisa yote unayoweza ili ulitumie sawasawa neno la kweli.’ (2 Tim. 2:15) Tunawezaje kutumia shauri la Paulo? Kwa kuchagua vizuri na kusoma kwa sauti maandiko yanayoweza kugusa mioyo ya wale watakaotusikiliza. Trakti zilizotolewa katika mwaka wa  2013 zilikusudiwa kutusaidia kutimiza jambo hilo.

SOMA ANDIKO LILILOCHAGULIWA VIZURI!

8. Mwangalizi mmoja wa utumishi alisema nini kuhusu trakti mpya?

8 Trakti zote mpya zina mpangilio uleule. Hivyo, tukijifunza kutumia mojawapo ya trakti hizo, tutajua kutumia trakti hizo zote. Je, ni vigumu kuzitumia? Mwangalizi mmoja wa utumishi huko Hawaii, Marekani, aliandika hivi: “Hatukujua kwamba trakti hizo mpya zingekuwa na matokeo mazuri sana katika huduma ya nyumba kwa nyumba na hadharani.” Amegundua kwamba trakti hizo zimeandikwa kwa njia inayowachochea watu kuwa tayari kutoa maoni yao, na mara nyingi hilo huongoza kwenye mazungumzo mazuri. Anahisi kwamba watu huchochewa na swali na majibu yaliyo kwenye ukurasa wa kwanza wa trakti hizo. Mwenye nyumba hahitaji kuogopa kwamba atatoa jibu lisilo sahihi.

9, 10. (a) Trakti zetu hutuchocheaje kutumia Biblia? (b) Umetumia trakti gani kwa mafanikio zaidi, na kwa nini?

9 Kila trakti hutuchochea kusoma andiko lililochaguliwa vizuri. Kwa mfano, tazama trakti yenye kichwa Je, Kuteseka Kutaisha? Iwe mwenye nyumba atachagua jibu la “ndio,” “la,” au “labda,” fungua ukurasa wa pili, kisha useme hivi: “Biblia inasema hivi.” Halafu usome andiko la Ufunuo 21:3 na 4.

10 Vivyo hivyo, unapotumia trakti yenye kichwa Una Maoni Gani Kuhusu Biblia? haidhuru mwenye nyumba atachagua jibu gani kati ya majibu matatu yaliyo kwenye ukurasa wa kwanza wa trakti hiyo, fungua ukurasa wa pili na useme hivi: “Biblia inasema kwamba ‘Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu.’” Unaweza kuongezea hivi: “Kwa kweli, mstari huo unataja mambo mengine.” Kisha fungua Biblia yako na usome andiko lote la 2 Timotheo 3:16 na 17.

11, 12. (a) Ni shangwe gani unayopata katika huduma? (b) Trakti zinaweza kukusaidiaje unapojitayarisha kufanya ziara za kurudia?

11 Itikio la mwenye nyumba litakusaidia kuamua kiasi cha habari mtakazosoma na kuzungumzia katika trakti. Vyovyote vile, mbali na kuwapa watu trakti hizo, utapata shangwe inayotokana na kuwasomea watu Neno la Mungu, hata kama ni mstari mmoja au miwili tu. Baadaye, unaweza kuendeleza mazungumzo.

 12 Upande wa nyuma wa kila trakti una swali chini ya kichwa “Jambo la Kufikiria” pamoja na maandiko yanayoweza kuzungumziwa katika ziara ya kurudia. Unapotumia trakti yenye kichwa Una Maoni Gani Kuhusu Wakati Ujao? unaweza kuweka msingi wa ziara ya kurudia kwa kuuliza hivi: “Mungu ataubadilishaje ulimwengu wetu uwe mzuri zaidi?” Andiko la Mathayo 6:9 na 10 na Danieli 2:44 yametajwa. Trakti yenye kichwa Je, Kweli Wafu Wataishi Tena? ina swali hili: “Kwa nini tunazeeka na kufa?” Andiko la Mwanzo 3:17-19 na Waroma 5:12 yametajwa.

13. Eleza jinsi unavyoweza kutumia trakti kuanzisha mafunzo ya Biblia.

13 Tumia trakti hizo kama msingi wa kuanzisha mafunzo ya Biblia. Mtu anapotumia alama ya QR iliyo nyuma ya trakti, ataelekezwa kwenye Tovuti yetu na kuchochewa kujifunza Biblia. Trakti hizo pia zinakazia habari zilizo katika broshua Habari Njema Kutoka kwa Mungu! na kuelekeza kwenye somo hususa katika broshua hiyo. Kwa mfano, trakti yenye kichwa Ni Nani Hasa Anayeuongoza Ulimwengu? inaelekeza kwenye somo la 5 la broshua hiyo. Trakti yenye kichwa Ni Nini Siri ya Kuwa na Familia Yenye Furaha? inaelekeza kwenye somo la 9. Ukitumia trakti hizo ifaavyo, utakuwa na mazoea mazuri ya kutumia Biblia unapohubiri na kufanya ziara za kurudia. Hilo linaweza kukusaidia kuanzisha mafunzo zaidi ya Biblia. Ni nini kingine unachoweza kufanya ili utumie Neno la Mungu kwa ustadi katika huduma yako?

ZUNGUMZIA HABARI ZINAZOWAHANGAISHA WATU

14, 15. Unawezaje kuiga mtazamo wa Paulo katika huduma?

14 Paulo alitamani sana kuelewa hali za “watu walio wengi zaidi” katika huduma yake. (Soma 1 Wakorintho 9:19-23.) Ona kwamba Paulo alitumaini ‘kuwapata Wayahudi, watu walio chini ya sheria, wasio na sheria, na walio dhaifu.’ Naam, alitaka kuwafikia ‘watu wa namna zote, ili kwa vyovyote awaokoe wengine.’ (Mdo. 20:21) Tunawezaje kuiga mtazamo wa Paulo tunapojitayarisha kuwahubiria kweli “watu wa namna zote” katika eneo letu?—1 Tim. 2:3, 4.

15 Kila mwezi, Huduma Yetu ya Ufalme hutoa mapendekezo ya kutumia katika utumishi. Jitahidi kuyatumia. Lakini ikiwa kuna mambo mengine yanayowahangaisha watu katika eneo lenu, tayarisha utangulizi unaofaa mahitaji yao. Fikiria watu, mazingira yao, na mambo yanayowahangaisha sana. Kisha, fikiria andiko linalohusu mahitaji yao. Mwangalizi mmoja wa mzunguko anaeleza jinsi yeye na mke wake wanavyotumia sana Biblia wanapohubiri. Anasema: “Wenye nyumba wengi hukubali tuwasomee mstari mmoja ikiwa tutazungumzia kwa ufupi jambo kuu. Baada ya kuwajulia hali Biblia zetu zikiwa wazi, sisi husoma andiko.” Fikiria mifano michache ya maswali, vichwa, na maandiko yenye matokeo unayoweza kutumia katika eneo lenu.

Je, unatumia Biblia na trakti kwa ustadi katika huduma yako? (Tazama fungu la 8-13)

16. Eleza jinsi tunavyoweza kutumia andiko la Isaya 14:7 katika huduma.

16 Ikiwa unaishi katika eneo lisilo na amani, unaweza kumuuliza mwenye nyumba swali hili: “Je, unafikiri kwamba siku moja vyombo vya habari vitatangaza hivi: ‘Sasa dunia nzima imepumzika, imekuwa huru kutokana na usumbufu. Watu wamechangamka kwa vigelegele vya shangwe’? Hivyo ndivyo Biblia inavyosema katika Isaya 14:7. Kwa kweli, Biblia ina ahadi nyingi za Mungu kuhusu amani tele itakayokuja hivi karibuni.” Kisha soma mojawapo ya ahadi hizo katika Biblia.

17. Unaweza kutumia utangulizi gani kabla ya kusoma Mathayo 5:3 katika mazungumzo?

 17 Je, ni vigumu kwa wanaume wengi katika eneo lenu kupata riziki? Ikiwa ndivyo, unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kuuliza hivi: “Mtu anahitaji kuwa na kiasi gani cha pesa ili familia yake iwe na furaha?” Baada ya mwenye nyumba kujibu, unaweza kuongezea hivi: “Wanaume wengi hupata pesa nyingi kuliko hizo, lakini bado familia zao haziridhiki. Kwa hiyo ni nini hasa kinachohitajiwa?” Kisha soma Mathayo 5:3 na umwonyeshe jinsi unavyoweza kujifunza naye Biblia.

18. Unawezaje kutumia andiko la Yeremia 29:11 kuwafariji wengine?

18 Je, watu katika eneo lenu wanateseka kwa sababu ya msiba uliowakumba hivi karibuni? Unaweza kusema hivi: “Nimekutembelea ili nikufariji. (Soma Yeremia 29:11.) Je, umeona mambo matatu ambayo Mungu anataka tuwe nayo? ‘Amani,’ ‘wakati ujao,’ na ‘tumaini.’ Je, haitii moyo kujua kwamba anataka tuwe na maisha mazuri? Lakini inawezekanaje?” Kisha mwonyeshe somo linalofaa katika broshua Habari Njema.

19. Eleza jinsi tunavyoweza kutumia andiko la Ufunuo 14:6 na 7 tunapowahubiria watu wanaopenda dini.

19 Je, unaishi katika eneo ambalo watu wanapendezwa na dini? Ikiwa ndivyo ilivyo, unaweza kuanzisha mazungumzo kwa kuuliza hivi: “Ikiwa malaika angezungumza nawe, je, ungemsikiliza? (Soma Ufunuo 14:6, 7.) Kwa kuwa malaika huyo anasema ‘mwogopeni Mungu,’ je, si muhimu kujua ni Mungu gani anayemzungumzia? Malaika huyo anadokeza jambo fulani anaposema kwamba ni ‘Yeye aliyezifanya mbingu na dunia.’ Ni nani huyo?” Kisha soma Zaburi 124:8, inayosema hivi: “Msaada wetu uko katika jina la Yehova, Mtengenezaji wa mbingu na dunia.” Kisha mwambie kwamba ungependa kumweleza mengi zaidi kumhusu Yehova Mungu.

20. (a) Andiko la Methali 30:4 linaweza kutumiwaje kumfundisha mtu jina la Mungu? (b) Je, kuna andiko fulani unalotumia kwa matokeo mazuri?

20 Unaweza kuzungumza na kijana kwa kusema hivi: “Ningependa kukusomea andiko linalouliza swali muhimu sana. (Soma Methali 30:4.) Hakuna mwanadamu anayeweza kufanya mambo hayo, kwa hiyo maneno hayo yanamhusu Muumba wetu. * Tunawezaje kujua jina lake? Ningependa kukuonyesha jina hilo katika Biblia.”

TUMIA NGUVU ZA NENO LA MUNGU KATIKA HUDUMA YAKO

21, 22. (a) Andiko lililochaguliwa vizuri linawezaje kubadili maisha ya mtu? (b)Umeazimia kufanya nini unapohubiri?

21 Huwezi kujua jinsi watu watakavyoguswa na andiko lililochaguliwa vizuri. Kwa mfano, Mashahidi wawili nchini Australia walibisha mlango wa mwanamke mmoja kijana. Mmoja wao akamuuliza hivi: “Unajua jina la Mungu?” kisha akasoma andiko la Zaburi 83:18. Mwanamke huyo anasema hivi: “Nilishangaa sana! Walipoondoka, niliendesha gari umbali wa kilomita 56 hadi kwenye duka la vitabu ili nichunguze andiko hilo katika tafsiri nyingine za Biblia na nilitafuta pia jina hilo katika kamusi. Baada ya kujithibitishia kuwa jina la Mungu ni Yehova, nilijiuliza ni mambo gani mengine ambayo sikuyajua.” Muda mfupi baadaye, mwanamke huyo na mchumba wake walianza kujifunza Biblia, na baadaye wakabatizwa.

22 Neno la Mungu hubadili maisha ya wale wanaolisoma na kusitawisha imani katika ahadi za Yehova zilizo hai. (Soma 1 Wathesalonike 2:13.) Ujumbe wa Biblia una nguvu za kugusa moyo wa mtu kuliko jambo lolote tunaloweza kusema. Hivyo, tunapaswa kutumia Neno la Mungu katika kila fursa tunayopata. Liko hai!

^ fu. 20 Tazama “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika Mnara wa Mlinzi, Julai 15, 1987, ukurasa wa 31.