Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushangilia Katika Tumaini Letu

Kushangilia Katika Tumaini Letu

Kushangilia Katika Tumaini Letu

“[Kuna] tumaini la uzima wa milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi nyakati za zamani za kale.”—TITO 1:2.

KWA NJIA YA PITIO

Tunajuaje kwamba kunakuwa na shangwe mbinguni wakati mmoja wa watiwa-mafuta anaposhika utimilifu hadi mwisho?

Kutimizwa kwa tumaini la kondoo wengine kunahusianaje na tumaini la watiwa-mafuta?

Ili tuone tumaini letu likitimizwa, ni lazima tuonyeshe ‘matendo gani matakatifu ya mwenendo’ na ‘vitendo gani vya ujitoaji-kimungu’?

1. Tumaini ambalo Yehova ametupatia linaweza kutusaidia jinsi gani kuvumilia?

YEHOVA ni “Mungu anayetoa tumaini.” Hivyo ndivyo mtume Paulo alivyosema, na kuongeza kwamba Yehova anaweza ‘kutujaza sisi shangwe yote na amani kwa kuamini kwetu, ili tuzidi katika tumaini kwa nguvu za roho takatifu.’ (Rom. 15:13) Ikiwa tumaini hilo liko wazi kabisa katika akili zetu, tutaweza kukabiliana na hali yoyote ambayo inaweza kutokea, mioyo yetu itajaa shangwe na amani. Tumaini hilo litathibitika kuwa “nanga ya nafsi, likiwa hakika na imara” kwa Wakristo wengine, kama ilivyo kwa Wakristo watiwa-mafuta. (Ebr. 6:18, 19) Tunaweza kushikilia kwa uimara tumaini letu tunapokabili misukosuko ya maisha na linaweza kutusaidia tusipeperushwe na kuwa na shaka au kukosa imani.—Soma Waebrania 2:1; 6:11.

2. Wakristo leo wana matumaini gani mawili, na kwa nini “kondoo wengine” wanapendezwa na tumaini ambalo watiwa-mafuta wanalo?

2 Wakristo wanaoishi wakati huu wa mwisho wanakazia uangalifu moja kati ya matumaini mawili. Washiriki wanaobaki wa “kundi dogo” la Wakristo watiwa-mafuta wana tumaini la kupata uhai usioweza kufa huko mbinguni wakiwa wafalme na makuhani pamoja na Kristo katika Ufalme wake. (Luka 12:32; Ufu. 5:9, 10) “Umati mkubwa” wa “kondoo wengine” ambao ndio wengi zaidi, wana tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani wakiwa raia wa Ufalme wa Kimasihi. (Ufu. 7:9, 10; Yoh. 10:16) Kondoo wengine hawapaswi kamwe kusahau kwamba ili waokolewe, ni lazima wawaunge mkono kwa bidii “ndugu” watiwa-mafuta wa Kristo ambao wangali duniani. (Mt. 25:34-40) Watiwa-mafuta watapokea zawadi yao na bila shaka kondoo wengine watapokea pia zawadi yao. (Soma Waebrania 11:39, 40.) Kwanza, acheni tuchunguze tumaini ambalo watiwa-mafuta wamepewa.

“TUMAINI LILILO HAI” LA WAKRISTO WATIWA-MAFUTA

3, 4. Wakristo watiwa-mafuta ‘wanazaliwa upya kwenye tumaini lililo hai’ jinsi gani, na ni tumaini gani hilo?

3 Mtume Petro aliwaandikia barua mbili Wakristo watiwa-mafuta, ambao aliwaita “wale waliochaguliwa.” (1 Pet. 1:1) Petro aliandika habari zenye kina kuhusu tumaini zuri ajabu ambalo kundi dogo wamepewa. Katika barua yake ya kwanza, Petro aliandika hivi: “Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo, kwa maana kulingana na rehema yake kubwa alituzaa sisi upya kwenye tumaini lililo hai kupitia ufufuo wa Yesu Kristo kutoka kwa wafu, kwenye urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia. Huo umewekwa akiba mbinguni kwa ajili yenu, mnaolindwa kwa nguvu za Mungu kupitia imani kwa ajili ya wokovu ulio tayari kufunuliwa katika kipindi cha mwisho cha wakati. Nanyi mnashangilia sana katika jambo hilo.”—1 Pet. 1:3-6.

4 Wakristo wachache wanaochaguliwa na Yehova ili washirikiane na Kristo katika serikali ya mbinguni ya Ufalme ‘wanazaliwa upya’ wakiwa wana wa Mungu waliozaliwa kwa roho. Wanatiwa mafuta kwa roho takatifu ili wawe wafalme na makuhani pamoja na Kristo. (Ufu. 20:6) Petro anasema kwamba ‘kuzaliwa upya’ huko kunawafungulia “tumaini lililo hai,” ambalo analiita “urithi usioharibika na usiotiwa unajisi na usiofifia” uliowekwa akiba “mbinguni” kwa ajili yao. Haishangazi kwamba watiwa-mafuta ‘wanashangilia sana’ katika tumaini lao lililo hai! Hata hivyo, tumaini hilo linaweza kutimia ikiwa tu wataendelea kuwa waaminifu.

5, 6. Kwa nini ni lazima Wakristo watiwa-mafuta wafanye yote wawezayo ili kufanya mwito wao wa mbinguni uwe hakika?

5 Katika barua yake ya pili, Petro aliwahimiza Wakristo watiwa-mafuta ‘wafanye yote wawezayo ili kufanya mwito na kuchaguliwa kwao kuwe hakika.’ (2 Pet. 1:10) Ni lazima wajitahidi sana kukuza sifa za Kikristo kama vile imani, ujitoaji-kimungu, shauku ya kindugu, na upendo. Petro alisema hivi: “Mambo hayo yakikaa ndani yenu na kufurika, yatawazuia kuwa ama wasiotenda au wasiozaa matunda.”—Soma 2 Petro 1:5-8.

6 Kristo aliyefufuliwa alisema hivi katika ujumbe wake kwa wazee waliozaliwa kwa roho katika kutaniko la karne ya kwanza la Filadelfia, huko Asia Ndogo: “Kwa sababu ulilishika neno juu ya uvumilivu wangu, mimi pia nitakulinda kutokana na ile saa ya jaribu itakayokuja juu ya dunia nzima inayokaliwa, ili kuwatia katika jaribu wale wanaokaa duniani. Mimi ninakuja upesi. Endelea kushika sana kile ulicho nacho, ili yeyote asilichukue taji lako.” (Ufu. 3:10, 11) Ikiwa Mkristo mtiwa-mafuta atakosa kuwa mwaminifu, hatapokea “taji la utukufu lisiloweza kufifia” waliloahidiwa wachaguliwa ambao wanabaki waaminifu hadi kifo.—1 Pet. 5:4; Ufu. 2:10.

KUINGIA KATIKA UFALME

7. Ni tumaini gani zuri ajabu ambalo Yuda analitaja katika barua yake?

7 Karibu mwaka wa 65 W.K., Yuda, ndugu wa kambo wa Yesu aliwaandikia barua Wakristo wenzake watiwa-mafuta, ambao aliwataja kuwa “walioitwa.” (Yuda 1; linganisha na Waebrania 3:1.) Alikuwa amekusudia kuwaandikia barua kuhusu tumaini tukufu la wokovu ambalo Wakristo walioitwa katika Ufalme wa mbinguni wa Mungu ‘wanalo kwa pamoja.’ (Yuda 3) Ingawa alikuwa na mambo mengine muhimu ya kuwaeleza, kwenye umalizio wa barua yake fupi, alirejelea tumaini zuri ajabu ambalo Wakristo watiwa-mafuta wanashiriki, aliandika hivi: “Sasa kwake yeye ambaye anaweza kuwalinda ninyi ili msijikwae na kuwaweka muwe bila dosari mbele ya utukufu wake kwa shangwe kuu, kwake Mungu pekee aliye Mwokozi wetu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu, na kuwe utukufu, ukuu, nguvu na mamlaka kwa umilele wote uliopita na sasa na mpaka umilele wote.”—Yuda 24, 25.

8. Kulingana na andiko la Yuda 24, ni nini kinachoonyesha kwamba kuna shangwe mbinguni mmoja wa watiwa-mafuta anapodumisha utimilifu wake hadi mwisho?

8 Bila shaka, kila Mkristo mtiwa-mafuta mwaminifu anataka alindwe ili asijikwae na hivyo kuangamia. Tumaini lao linalotegemea Biblia ni kwamba Yesu Kristo atawafufua kutoka katika wafu, na kuwawezesha waonekane mbele za uso wa Mungu wakiwa viumbe wa roho wakamilifu na wenye shangwe nyingi. Mtiwa-mafuta anapokufa akiwa mwaminifu anakuwa na tumaini hakika la kwamba ‘atafufuliwa akiwa na mwili wa roho,’ atafufuliwa “katika kutoweza kuharibika . . . , katika utukufu.” (1 Kor. 15:42-44) Ikiwa kuna “shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja anayetubu,” hebu wazia shangwe inayokuwa mbinguni wakati mmoja wa ndugu aliyezaliwa kwa roho wa Kristo anapomaliza mwendo wake akiwa mtimilifu. (Luka 15:7) Yehova na viumbe waaminifu wa roho watashangilia pamoja na mtiwa-mafuta ambaye atapokea thawabu yake “kwa shangwe kuu.”—Soma 1 Yohana 3:2.

9. Ni kwa njia gani watiwa-mafuta waaminifu ‘wanawezeshwa kwa wingi’ kuingia katika Ufalme, na tumaini hilo linawachochea jinsi gani watiwa-mafuta ambao wangali duniani?

9 Vivyo hivyo, Petro aliwaandikia Wakristo watiwa-mafuta kwamba ikiwa watafanya mwito na kuchaguliwa kwao kuwe hakika kupitia uaminifu wao, ‘watawezeshwa kwa wingi kuingia katika ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wao Yesu Kristo.’ (2 Pet. 1:10, 11) Watiwa-mafuta ‘watawezeshwa kwa wingi’ kuingia katika thawabu yao mbinguni kwa kudhihirisha kwa uangavu sifa za Kikristo. Maneno ‘kuwezeshwa kwa wingi’ yanaweza pia kumaanisha baraka nyingi ajabu ambazo wale ambao wamejitahidi kabisa katika shindano la mbio ya uzima watafurahia. Watakuwa na shangwe na uthamini mkubwa watakapofikiria maisha yao ya uaminifu. Bila shaka, tumaini hilo linawaimarisha Wakristo watiwa-mafuta ambao wangali duniani ili ‘wakaze akili zao kwa ajili ya utendaji’ unaoendelea.—1 Pet. 1:13.

“MSINGI WA TUMAINI” KWA AJILI YA KONDOO WENGINE

10, 11. (a) Kondoo wengine wana tumaini gani? (b) Kutimizwa kwa tumaini linalohusiana na dunia kunahusiana jinsi gani na Kristo na “kufunuliwa kwa wana wa Mungu”?

10 Mtume Paulo aliandika kuhusu tumaini tukufu la “wana wa Mungu” waliozaliwa kwa roho wakiwa “warithi pamoja” na Kristo. Kisha alitaja tumaini zuri ajabu ambalo Yehova anauahidi umati usio na hesabu wa kondoo wengine: “Uumbaji [wanadamu] unangojea na kutazamia kwa hamu kufunuliwa kwa wana wa Mungu [watiwa-mafuta]. Kwa maana uumbaji ulitiishwa chini ya ubatili, si kwa mapenzi yake wenyewe bali kupitia yeye aliyeutiisha hivyo, juu ya msingi wa tumaini kwamba uumbaji wenyewe pia utawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.”—Rom. 8:14-21.

11 “Msingi wa tumaini” kwa wanadamu uliwekwa na Yehova alipoahidi kuwakomboa kutoka kwa “yule nyoka wa zamani,” Shetani Ibilisi, kupitia “uzao” ulioahidiwa. (Ufu. 12:9; Mwa. 3:15) Yesu Kristo ndiye sehemu ya msingi ya “uzao” huo. (Gal. 3:16) Kupitia kifo na ufufuo wake, Yesu aliandaa msingi thabiti wa tumaini la wanadamu kuwekwa huru kutoka katika utumwa wa dhambi na kifo. Kutimizwa kwa tumaini hilo kunahusiana na “kufunuliwa kwa wana wa Mungu.” Watiwa-mafuta waliotukuzwa ndio sehemu ya pili ya ule “uzao.” ‘Watafunuliwa’ wakati watakaposhiriki pamoja na Kristo kuuharibu mfumo mwovu wa mambo wa Shetani. (Ufu. 2:26, 27) Hilo litawaletea ukombozi kondoo wengine wanaotoka katika dhiki kuu.—Ufu. 7:9, 10, 14.

12. Kufunuliwa kwa watiwa-mafuta kutawaletea wanadamu manufaa gani mazuri?

12 “Uumbaji” wa kibinadamu utapata kitulizo kikubwa kama nini wakati wa Utawala wa ile Miaka Elfu Moja wa Kristo! Wakati huo, “wana wa Mungu” waliotukuzwa ‘watafunuliwa’ hata zaidi watakapotenda wakiwa makuhani pamoja na Kristo, wakitumia faida za dhabihu ya fidia ya Yesu kwa ajili ya wanadamu. Wakiwa raia wa Ufalme wa mbinguni, “uumbaji” wa kibinadamu utaanza kushuhudia ukombozi kutokana na matokeo ya dhambi na kifo. Hatua kwa hatua wanadamu watiifu ‘watawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu.’ Ikiwa wataendelea kuwa waaminifu kwa Yehova wakati wa ile miaka Elfu Moja na wakati wa jaribu litakalokuja mwishoni mwa miaka hiyo, majina yao yataandikwa kwa njia ya kudumu katika “kitabu cha uzima.” Wataingia katika “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Ufu. 20:7, 8, 11, 12) Kwa kweli, hilo ni tumaini zuri ajabu!

KUDUMISHA TUMAINI LETU LIKIWA HAI

13. Tumaini letu linategemea nini, na Kristo atafunuliwa lini?

13 Barua mbili za Petro zilizoongozwa kwa roho zina habari nyingi zinazoweza kuwasaidia watiwa-mafuta na kondoo wengine kuendelea kudumisha tumaini lao likiwa hai. Petro alionyesha wazi kwamba tumaini lao halitegemei kazi zao, bali linategemea fadhili zisizostahiliwa za Yehova. Petro aliandika hivi: “Kazeni tumaini lenu juu ya fadhili zisizostahiliwa zitakazoletwa kwenu wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.” (1 Pet. 1:13) Kristo atafunuliwa atakapokuja kuwathawabisha wafuasi wake waaminifu na kutekeleza hukumu za Yehova dhidi ya watu wasiomwogopa Mungu.—Soma 2 Wathesalonike 1:6-10.

14, 15. (a) Ili kudumisha tumaini letu likiwa hai, ni lazima tukazie fikira nini? (b) Petro alitoa shauri gani?

14 Ili kudumisha tumaini letu likiwa hai, ni lazima tutumie maisha yetu na kukaza akili zetu juu ya “siku ya Yehova” inayokuja. Katika siku hiyo, “mbingu” za sasa, yaani, utawala wa wanadamu, na “dunia,” yaani, jamii ya wanadamu waovu na “vitu vyake vya msingi” vitaharibiwa. Petro aliandika hivi: “Mnapaswa kuwa watu wa namna gani . . . , mkingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova, ambayo kupitia hiyo mbingu zikiwa zimewaka moto zitayeyushwa na vitu vya msingi vikiwa moto sana vitayeyuka!”—2 Pet. 3:10-12.

15 “Mbingu” na “dunia” za sasa zitaondolewa na mahali pake patachukuliwa na “mbingu mpya [serikali ya Ufalme wa Kristo] na dunia mpya [jamii mpya ya wanadamu duniani].” (2 Pet. 3:13) Kisha Petro akatoa shauri la moja kwa moja kwa msingi wa kwamba “tunangojea,” au tunadumisha tumaini letu likiwa hai kuelekea dunia hiyo mpya iliyoahidiwa: “Kwa hiyo, wapendwa, kwa kuwa mnangojea mambo hayo, fanyeni yote mnayoweza ili mwishowe yeye awapate ninyi mkiwa bila doa na bila dosari na mkiwa katika amani.”—2 Pet. 3:14.

KUISHI KULINGANA NA TUMAINI LETU

16, 17. (a) Ni ‘matendo gani matakatifu ya mwenendo’ na ‘vitendo gani vya ujitoaji-kimungu’ tunavyopaswa kuonyesha? (b) Tumaini letu litatimizwaje?

16 Haitoshi tu kudumisha tumaini letu likiwa hai ni lazima pia tuishi kulingana na tumaini letu. Tunapaswa kufikiria kwa makini hali yetu ya kiroho. “Matendo matakatifu ya mwenendo” yanatia ndani ‘kudumisha mwenendo wetu ukiwa mzuri katikati ya mataifa,’ kwa kufanya yale ambayo Mungu anasema kuwa ni sawa. (2 Pet. 3:11; 1 Pet. 2:12) Ni lazima tuwe na ‘upendo kati yetu wenyewe.’ Hilo linatia ndani kufanya yote tuwezayo ili kudumisha umoja wa undugu wetu wa ulimwenguni pote hata katika makutaniko yetu. (Yoh. 13:35) “Vitendo vya ujitoaji-kimungu” ni vitendo tunavyofanya ambavyo vinaonyesha uhusiano wetu wa karibu pamoja na Yehova. Vitendo hivyo vinatia ndani kuboresha sala zetu, kusoma Biblia kila siku, funzo la kibinafsi lenye kina, ibada ya familia, na kushiriki kwa bidii katika kazi ya kuhubiri “habari njema ya ufalme.”—Mt. 24:14.

17 Kila mmoja wetu anataka kuwa aina ya mtu ambaye Yehova anamkubali na atamwokoa wakati mfumo mwovu wa sasa ‘utakapoyeyushwa.’ Hivyo tutaona tumaini letu likitimizwa, “tumaini la uzima wa milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi nyakati za zamani za kale.”—Tito 1:2.

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 22]

Wakristo watiwa-mafuta ‘wanazaliwa upya kwenye tumaini lililo hai’

[Picha katika ukurasa wa 24]

Dumisha tumaini likiwa hai katika familia yako