Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kataa Kabisa Uwongo wa Shetani

Kataa Kabisa Uwongo wa Shetani

Kataa Kabisa Uwongo wa Shetani

‘MSIDANGANYWE. Mungu wenu hatawasaidia. Salimuni amri au mkione cha mtema kuni!’ Huo ndio ujumbe ambao Rabshake, mjumbe wa Mfalme Senakeribu wa Ashuru aliwapa wakaaji wa Yerusalemu. Majeshi ya mfalme huyo yalikuwa yamevamia nchi ya Yuda. Maneno ya mjumbe huyo yalikusudiwa kuwavunja moyo watu wa Yerusalemu na kuwatisha ili wasalimu amri.—2 Fal. 18:28-35.

Waashuru walijulikana kwa sababu ya unyama na ukatili wao. Waliwaogopesha maadui wao kwa kusimulia mambo ya kikatili sana waliyowatendea mateka wao. Mwanahistoria Philip Taylor, anasema kwamba walitumia “ukatili pamoja na propaganda, zilizokusudiwa kuwaogopesha watu walioshindwa, na waliwatisha maadui kwa kueneza habari za kinyama na zenye kutisha.” Propaganda au habari za uwongo zina matokeo sana. “Zinapotosha akili,” anasema Taylor.

Wakristo wa kweli ‘wanashindana mweleka, si juu ya damu na mwili, bali juu ya majeshi ya roho waovu,’ yaani, juu ya viumbe wa roho waliomwasi Mungu. (Efe. 6:12) Shetani Ibilisi ndiye adui yetu mkubwa zaidi. Yeye pia anatumia vitisho pamoja na propaganda au habari za uwongo.

Shetani anadai kwamba anaweza kuvunja utimilifu wa kila mmoja wetu. Katika siku za mzee wa ukoo, Ayubu, Shetani alimwambia hivi Yehova Mungu: “Kila kitu alicho nacho mtu atakitoa kwa ajili ya nafsi yake.” Yaani, mwanadamu akiteswa vya kutosha, muda si muda, atavunja utimilifu wake kwa Mungu. (Ayu. 2:4) Je, Shetani anasema ukweli? Je, kweli kuna mateso ambayo yanaweza kutufanya tushindwe kudumisha utimilifu wetu na kutufanya tuache msimamo wetu? Shetani angependa tuamini hivyo. Kwa hiyo, anatumia uwongo wenye kudhuru ili kutufanya tuamini hivyo. Acheni tuchunguze njia fulani ambazo anatumia kutupotosha ili tuone jinsi tunavyoweza kumpinga.

“Msingi Wao Umo Mavumbini”

Shetani alimtumia Elifazi, mmoja kati ya marafiki watatu waliomtembelea Ayubu, kudai kwamba wanadamu ni dhaifu sana hivi kwamba hawawezi kuendelea kuwa waaminifu. Elifazi alisema kwamba wanadamu ‘wanakaa katika nyumba za udongo,’ kisha akamwambia Ayubu hivi: “Msingi wao umo mavumbini! Mtu huwaponda upesi kuliko nondo. Kuanzia asubuhi mpaka jioni wao hupondwa vipande-vipande; wao huangamia milele bila yeyote kutia hilo moyoni.”—Ayu. 4:19, 20.

Maandiko mengine yanasema sisi ni kama “vyombo vya udongo,” vyungu vya udongo wa mfinyanzi vinavyovunjika kwa urahisi. (2 Kor. 4:7) Sisi ni dhaifu kwa sababu tumerithi dhambi na hali ya kutokamilika. (Rom. 5:12) Hatuwezi kushinda mashambulizi ya Shetani kwa uwezo wetu wenyewe. Lakini tukiwa Wakristo, Yehova anaweza kutusaidia. Hata ingawa tuna udhaifu mbalimbali, sisi ni wenye thamani machoni pa Mungu. (Isa. 43:4) Kwa kuongezea, Yehova anawapa roho takatifu wale wanaomwomba. (Luka 11:13) Roho yake inaweza kututia “nguvu zinazopita zile za kawaida,” na kutuwezesha kuvumilia hali yoyote ngumu ambayo Shetani anatuletea. (2 Kor. 4:7; Flp. 4:13) Tukimpinga Ibilisi huku ‘tukiwa imara katika imani,’ Mungu atatuimarisha na kutufanya tuwe wenye nguvu. (1 Pet. 5:8-10) Kwa hiyo, hatuna sababu ya kumwogopa Shetani Ibilisi.

Mtu ‘Anakunywa Ukosefu wa Uadilifu’

Elifazi aliuliza hivi: “Mwanadamu anayeweza kufa ni nani ndipo awe safi, au ndipo yeyote aliyezaliwa na mwanamke awe upande wa haki?” Kisha akajibu: “Tazama! [Mungu] hana imani na watakatifu wake, na mbingu zenyewe kwa kweli si safi machoni pake. Sembuse mtu anayechukiza na aliye mpotovu, mtu anayekunywa ukosefu wa uadilifu kama maji!” (Ayu. 15:14-16) Elifazi alikuwa akimwambia Ayubu kwamba Yehova hamwoni mwanadamu yeyote kuwa mwadilifu. Pia, tunapojiona hatufai, Ibilisi anatumia hali hiyo kutudhuru. Anataka tukazie fikira makosa yetu ya zamani, tujilaumu kupita kiasi, na kufikiri kwamba hatuwezi kukombolewa. Anataka pia tufikiri kwamba matakwa ya Yehova ni mazito mno na makosa yetu ni mengi sana hivi kwamba Yehova hawezi kuturehemu, kutusamehe, na kututegemeza.

Bila shaka, sisi sote ‘tumefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.’ Wanadamu wasio wakamilifu hawawezi kutimiza viwango vikamilifu vya Yehova. (Rom. 3:23; 7:21-23) Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba hatuna thamani yoyote machoni pake. Yehova anajua kwamba “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani,” ndiye anayetumia hali yetu ya dhambi kujifaidi. (Ufu. 12:9, 10) Mungu anaelewa hali yetu naye ‘haendelei kutafuta makosa’ yetu wakati wote kwa sababu anakumbuka kwamba “sisi ni mavumbi.”—Zab. 103:8, 9, 14.

Tukiacha mwenendo mwovu na kumfikia Yehova kwa moyo wenye masikitiko na roho ya toba, ‘atatusamehe kwa njia kubwa.’ (Isa. 55:7; Zab. 51:17) Biblia inasema kwamba hata dhambi zetu “zikiwa nyekundu, zitafanywa kuwa nyeupe kama theluji.” (Isa. 1:18) Kwa hiyo, acheni tuazimie kuendelea kufanya mapenzi ya Mungu.

Katika hali yetu ya dhambi, hatuwezi kamwe kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Mungu kwa sababu ya matendo yetu. Adamu na Hawa walipoteza ukamilifu na tumaini lao na letu pia la kupata uzima wa milele. (Rom. 6:23) Hata hivyo, kwa sababu ya upendo wake mkubwa kwa wanadamu, Yehova amefanya mpango wa kutusamehe dhambi zetu tukionyesha imani katika fidia au dhabihu ya ukombozi ya Mwana wake, Yesu Kristo. (Mt. 20:28; Yoh. 3:16) Huo ni wonyesho mzuri kama nini wa “fadhili zisizostahiliwa” za Mungu! (Tito 2:11) Tunaweza kukombolewa kutoka katika dhambi! Basi, tusimruhusu Shetani atufanye tufikiri kwamba hatuwezi kukombolewa.

‘Gusa Kufikia Mfupa Wake na Nyama Yake’

Shetani alidai kwamba Ayubu angeacha kuwa mwaminifu ikiwa angepoteza afya yake nzuri. Ibilisi alimwambia hivi Yehova: ‘Gusa kufikia mfupa wake na nyama yake, uone kama hatakulaani wewe mbele za uso wako.’ (Ayu. 2:5) Bila shaka, Adui huyo wa Mungu atafurahi sana akifaulu kutufanya tuhisi kwamba hatufai kamwe kwa sababu ya udhaifu wetu.

Hata hivyo, Yehova hatuachi kwa sababu hatuwezi tena kufanya mambo yote tuliyokuwa tukifanya zamani katika utumishi wake. Tungefanya nini ikiwa rafiki yetu angeshambuliwa na kuumizwa? Je, upendo wetu kumwelekea ungepungua kwa sababu hawezi tena kufanya mambo aliyokuwa akifanya zamani? Bila shaka, hatuwezi kufanya hivyo! Bado tungeendelea kumpenda na kumtunza, hasa ikiwa aliumizwa akijaribu kutusaidia. Vivyo hivyo, Yehova hawezi kamwe kuwasahau marafiki wake. Biblia inasema: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.”—Ebr. 6:10.

Maandiko yanamtaja “mjane fulani mwenye uhitaji” ambaye huenda alitegemeza ibada ya Mungu kwa miaka mingi. Yesu alipomwona akitumbukiza “sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana” katika sanduku la hazina hekaluni, je, alimdharau na kuona kuwa mchango wake hauna thamani yoyote? Badala ya kufanya hivyo, alimsifu sana mwanamke huyo kwa sababu alifanya yote aliyoweza katika hali zake ili kutegemeza ibada ya kweli.—Luka 21:1-4.

Tukidumisha utimilifu wetu, tunaweza kuwa na hakika kwamba uhusiano wetu pamoja na Yehova utabaki ukiwa imara, hata tukidhoofika sana kimwili kwa sababu ya uzee au ugonjwa. Mungu hatawaacha kamwe watu waaminifu kwa kuwa tu hawawezi kufanya mengi katika utumishi wake kwa sababu ya udhaifu wao wa kimwili.—Zab. 71:9, 17, 18.

Kubali “Kofia ya Chuma ya Wokovu”

Tunaweza kujilinda jinsi gani kutokana na uwongo wa Shetani? Mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kujipatia nguvu katika Bwana na katika uwezo wa nguvu zake. Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara kupinga hila za Ibilisi.” Sehemu moja ya mavazi hayo ya silaha za kiroho ni “kofia ya chuma ya wokovu.” (Efe. 6:10, 11, 17) Ili kujilinda na uwongo wa Shetani, tunapaswa kuhakikisha kwamba tunapokea na kuvaa kofia hiyo ya chuma. Kofia ya chuma inalinda kichwa cha askari-jeshi. ‘Tumaini letu la wokovu’ ni uhakika wa kwamba ahadi ya Mungu ya kuleta ulimwengu mpya mtukufu itatimia. Tumaini hilo litalinda akili zetu kutokana na uwongo wa Shetani. (1 The. 5:8) Tunahitaji kujifunza Maandiko kibinafsi kwa bidii ili tumaini hilo liwe wazi na hakika zaidi.

Ayubu alivumilia mashambulizi makali ya chuki kutoka kwa Shetani. Imani ya Ayubu katika ufufuo ilikuwa na nguvu sana hivi kwamba hakuogopeshwa na tishio la kifo. Badala yake, alimwambia Yehova hivi: “Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.” (Ayu. 14:15) Hata ikiwa Ayubu angekufa kwa sababu ya kudumisha utimilifu wake, alikuwa na hakika kwamba upendo ungemchochea Mungu awaite watumishi Wake waaminifu kutoka kwa wafu.

Na tuwe na uhakika huohuo katika Mungu wa kweli. Yehova anaweza kuondoa madhara yoyote ambayo Shetani na wawakilishi wake wanaweza kutuletea. Pia, kumbuka kwamba Paulo anatuhakikishia hivi: “Mungu ni mwaminifu, naye hatawaacha ninyi mjaribiwe kupita mnavyoweza kuhimili, bali pamoja na hilo jaribu ataifanya pia njia ya kutokea kusudi mweze kulivumilia.”—1 Kor. 10:13.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Yehova anathamini utumishi wako wa uaminifu

[Picha katika ukurasa wa 21]

Pokea na kuvaa kofia ya chuma ya wokovu