Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Wakati wa Kukaa Kimya”

“Wakati wa Kukaa Kimya”

“Wakati wa Kukaa Kimya”

“KUZUNGUMZA ni fedha, kukaa kimya ni dhahabu.” Hivyo ndivyo inavyosema methali moja ya kale inayosemekana kuwa ya nchi za Mashariki. Kitabu kimoja (Brewer’s Dictionary of Phrase and Fable) kinasema kwamba methali ya Kiebrania inayofanana na hiyo ni: “Ikiwa neno moja lina thamani ya shekeli moja, kukaa kimya kuna thamani ya shekeli mbili.” Naye Sulemani, Mfalme wa Israeli mwenye hekima, aliandika hivi: “Kwa kila kitu kuna majira yake, na wakati kwa kila kusudi chini ya mbingu . . . wakati wa kunyamaza, na wakati wa kusema.”—Mhu. 3:1, 7, Zaire Swahili Bible.

Hata hivyo, ni wakati gani unaofaa wa kukaa kimya badala ya kuzungumza? Maneno “kimya” na “nyamaza” yanaonekana mara nyingi sana katika Biblia. Maandiko ambayo yanatumia maneno hayo yanaonyesha umuhimu wa kukaa kimya angalau katika sehemu tatu za maisha. Acheni tuchunguze kwa makini zaidi hali ya kukaa kimya ikiwa ishara ya heshima, uthibitisho wa busara na utambuzi, na pia njia inayotusaidia kutafakari.

Ishara ya Heshima

Kukaa kimya ni ishara ya heshima. Nabii Habakuki alisema hivi: “Yehova yumo katika hekalu lake takatifu. Kaa kimya mbele zake, dunia yote!” (Hab. 2:20) Waabudu wa kweli ‘wanangojea, ndiyo, kimyakimya, wokovu wa Yehova.’ (Omb. 3:26) Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Kaa kimya mbele za Yehova na kumngojea kwa kutamani. Usijionyeshe umewaka hasira kwa sababu ya mtu yeyote anayeifanikisha njia yake.”—Zab. 37:7.

Je, tunaweza kumsifu Yehova bila kuzungumza? Nyakati nyingine, je, hatupigwi na bumbuazi tunapoona uzuri wa uumbaji? Kufikiria uumbaji huo wenye utukufu ni mojawapo ya njia za kumsifu Muumba katika mioyo yetu. Mtunga-zaburi Daudi alianza moja ya nyimbo zake kwa kusema: “Kwa ajili yako kuna sifa—kimya—, Ee Mungu, katika Sayuni; na kwako wewe nadhiri itatimizwa.”—Zab. 65:1.

Kama vile Yehova anavyostahili kuheshimiwa, ndivyo tunavyopaswa kuheshimu maneno yake. Kwa mfano, Musa, nabii wa Mungu alipotoa hotuba ya kuliaga taifa la Israeli, yeye na makuhani walimhimiza hivi kila mtu aliyekuwapo: “Kaa kimya . . . , nawe uisikilize sauti ya Yehova Mungu wako.” Hata watoto walihitaji pia kusikiliza kwa makini wakati Waisraeli walipokusanyika kusikiliza Sheria ya Mungu ikisomwa. Musa alisema: “Wakutanishe watu, wanaume na wanawake na watoto wadogo . . . ili wajifunze.”—Kum. 27:9, 10; 31:11, 12.

Katika nyakati zetu, ni jambo linalofaa sana kwamba waabudu wa Yehova wasikilize kwa makini maagizo wanayopokea kwenye mikutano ya Kikristo, kutia ndani makusanyiko makubwa. Kweli za maana sana za Biblia zinapofundishwa kutoka jukwaani, tunaonyesha kwamba hatuliheshimu Neno la Mungu na tengenezo lake tunapozungumza-zungumza na wengine bila sababu. Programu inapoendelea, ni wakati wa kukaa kimya na kusikiliza.

Hata tunapozungumza na wengine faraghani, kuwa msikilizaji mzuri ni ishara ya heshima. Kwa mfano, mzee wa ukoo Ayubu aliwaambia hivi washtaki wake: “Mnifundishe, nami, kwa upande wangu, nitanyamaza.” Ayubu alikuwa tayari kusikiliza akiwa kimya walipokuwa wakisema. Na ulipofika wakati wake wa kusema, aliwaambia hivi: “Nyamazeni mbele yangu, ili mimi mwenyewe nipate kusema.”—Ayu. 6:24; 13:13.

Uthibitisho wa Busara na Utambuzi

Biblia inasema: “Anayezuia midomo yake anatenda kwa busara.” “Mtu mwenye utambuzi mwingi hukaa kimya.” (Met. 10:19; 11:12) Ona jinsi Yesu alivyoonyesha busara na utambuzi kwa kukaa kimya. Alipotambua kwamba kuzungumza katikati ya maadui wake hakungesaidia jambo lolote, ‘Yesu aliendelea kukaa kimya.’ (Mt. 26:63) Baadaye, alipokuwa akihukumiwa mbele ya Pilato, Yesu “hakujibu.” Kwa busara, aliamua kuacha mambo aliyofanya yathibitishe ukweli.—Mt. 27:11-14.

Ni jambo la hekima kwetu pia kuzuia midomo yetu, hasa tunapochokozwa. Methali moja inasema: “Yule ambaye si mwepesi wa hasira ana utambuzi mwingi, lakini anayekosa subira anainua upumbavu.” (Met. 14:29) Kujibu haraka katika hali fulani ngumu kunaweza kumfanya mtu aseme bila kufikiri na mwishowe aje kujuta. Chini ya hali kama hizo, huenda maneno yetu yakaonekana kuwa ya upumbavu, na pia huenda tukapoteza amani yetu ya akili.

Ni jambo la busara kuzuia midomo yetu wakati tunapokuwa mbele ya watu waovu. Tunapokabiliana na wadhihaki katika kazi yetu ya kuhubiri, huenda ikawa vizuri kukaa kimya. Zaidi ya hayo, nyakati nyingine, ni jambo la hekima kukaa kimya ili kuonyesha kwamba hatukubaliani na wanafunzi wenzetu au wafanyakazi wenzetu wanapofanya mizaha michafu au kutumia lugha chafu. (Efe. 5:3) Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Nitaweka lijamu kama mlinzi wa kinywa changu mwenyewe, maadamu mtu yeyote mwovu yuko mbele yangu.”—Zab. 39:1.

Mtu mwenye “utambuzi mwingi” hafunui siri. (Met. 11:12) Mkristo wa kweli haropoki-ropoki na hivyo kufunua mambo ya siri. Kuhusu hilo, wazee Wakristo wanapaswa hasa kuwa waangalifu ili wasikose kutumainiwa na washiriki wa kutaniko.

Kukaa kimya kunaweza kuwa na matokeo mazuri. Mwandikaji mmoja Mwingereza wa karne ya 19, Sydney Smith, aliandika hivi kuhusu mtu mmoja aliyeishi wakati wake: “Pindi zake za kukaa kimya, zilifanya mazungumzo yake yawe yenye kupendeza sana.” Kwa kweli, marafiki wawili wanapozungumza kila mmoja wao anapaswa kushiriki katika mazungumzo. Mtu anayejua kuwasiliana vizuri anapaswa pia kuwa msikiaji mzuri.

Sulemani alitoa onyo hili: “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na kosa, lakini anayezuia midomo yake anatenda kwa busara.” (Met. 10:19) Hivyo, kadiri maneno yetu yanavyokuwa machache, ndivyo inavyokuwa vigumu kusema jambo fulani lisilo la busara. Kwa kweli, “hata mtu mpumbavu, anapokaa kimya, ataonwa kuwa mwenye hekima; yeyote anayefunga midomo yake, ataonwa kuwa mwenye uelewaji.” (Met. 17:28) Hivyo basi, na tumwombe Yehova ‘aweke mwangalizi juu ya mlango wa midomo yetu.’—Zab. 141:3.

Kukaa Kimya Kunatusaidia Kutafakari

Kuhusu mtu anayefuata njia ya uadilifu, Maandiko yanatuambia kwamba ‘anaisoma sheria ya Mungu kwa sauti ya chini mchana na usiku.’ (Zab. 1:2) Andiko hilo linasomeka hivi katika Biblia Habari Njema: “Huifurahia sheria ya Mwenyezi-Mungu, na kuitafakari mchana na usiku.” Ni hali gani nzuri inayomsaidia mtu kutafakari kwa njia hiyo?

Isaka, mwana wa mzee wa ukoo Abrahamu, “alikuwa nje akitembea ili atafakari shambani karibu na wakati wa jioni.” (Mwa. 24:63) Alichagua wakati mtulivu na mahali patulivu kwa ajili ya kutafakari. Mfalme Daudi alitafakari wakati wa makesha ya usiku yenye utulivu. (Zab. 63:6) Mwanamume mkamilifu Yesu alijitahidi sana kutosheleza uhitaji wake wa kuwa peke yake na kutafakari, kwa kwenda milimani, jangwani, na mahali pengine pa faragha mbali na kelele za umati.—Mt. 14:23; Luka 4:42; 5:16.

Kukaa kimya kunatusaidia kuwa na afya nzuri. Kunaweza kumsaidia mtu kujichunguza kwa njia inayofaa, na hivyo kujirekebisha. Kukaa kimya kunaweza kutokeza amani ya akili. Kutafakari katika pindi zenye utulivu kunaweza kutusaidia kusitawisha sifa ya kiasi na unyenyekevu na hivyo kuongeza uthamini wetu kwa ajili ya mambo yaliyo ya maana zaidi maishani.

Ni vizuri kukaa kimya, lakini pia kuna “wakati wa kusema.” (Mhu. 3:7) Waabudu wa kweli leo wana kazi nyingi ya kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu “katika dunia yote inayokaliwa.” (Mt. 24:14) Kelele za shangwe zinazotokana na kazi hiyo zinasikika kadiri hesabu ya waabudu inavyoongezeka. (Mika 2:12) Kwa vyovyote vile, acheni tuwe kati ya wale walio na bidii ya kutangaza habari njema ya Ufalme na kusema kuhusu kazi za ajabu za Mungu. Tunaposhiriki katika kazi hii ya maana sana, maisha yetu pia na yaonyeshe tunatambua kwamba kukaa kimya, nyakati nyingine, ni dhahabu.

[Picha katika ukurasa wa 3]

Wakati wa mikutano yetu ya Kikristo, tunapaswa kusikiliza na kujifunza

[Picha katika ukurasa wa 4]

Tunapotukanwa katika huduma yetu, huenda ikawa vizuri kukaa kimya

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kukaa kimya kunasaidia katika kutafakari