Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huwafunulia Wanyenyekevu Utukufu Wake

Yehova Huwafunulia Wanyenyekevu Utukufu Wake

Yehova Huwafunulia Wanyenyekevu Utukufu Wake

“Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.”—METHALI 22:4.

1, 2. (a) Kitabu cha Matendo kinaonyeshaje kwamba Stefano alikuwa “mwanamume mwenye kujaa imani na roho takatifu”? (b) Kuna uthibitisho gani kwamba Stefano alikuwa mnyenyekevu?

STEFANO alikuwa “mwanamume mwenye kujaa imani na roho takatifu.” Pia alikuwa “amejaa neema na nguvu.” Kwa kuwa alikuwa mmoja wa wanafunzi wa mapema wa Yesu, Stefano alikuwa akifanya ishara kubwa na mambo ya ajabu kati ya watu. Pindi moja, wanaume fulani walijitokeza ili kubishana naye, lakini “bado hawakuweza kufaulu katika pambano juu ya hekima na roho aliyokuwa akisema kwayo.” (Matendo 6:5, 8-10) Ni wazi kwamba Stefano alikuwa mwanafunzi mwenye bidii wa Neno la Mungu, naye alilitetea kwa ustadi mbele ya viongozi wa kidini Wayahudi wa siku zake. Ushuhuda wake unaopatikana katika kitabu cha Matendo sura ya 7, unathibitisha kwamba alipendezwa sana na kufunuliwa kwa kusudi la Mungu hatua kwa hatua.

2 Stefano alikuwa mnyenyekevu tofauti na viongozi hao wa kidini, ambao vyeo na ujuzi wao vilifanya wajione kuwa bora kuliko watu wa kawaida. (Mathayo 23:2-7; Yohana 7:49) Ingawa aliyajua sana Maandiko, aliridhika sana kupewa mgawo wa “kugawa chakula mezani” ili mitume waweze kujitoa “kwa sala na kwa huduma ya neno.” Stefano alikuwa na sifa nzuri miongoni mwa akina ndugu kwa hiyo alichaguliwa kuwa mmoja wa wanaume saba waliothibitishwa ambao wangesimamia kugawanywa huko kwa chakula kila siku. Alikubali mgawo huo kwa unyenyekevu.—Matendo 6:1-6.

3. Stefano alijionea wonyesho gani wenye kutokeza kuhusu fadhili zisizostahiliwa za Mungu?

3 Yehova alitambua mwelekeo wa unyenyekevu wa Stefano, hali yake ya kiroho, na utimilifu wake. Stefano alipokuwa akiwatolea ushahidi viongozi wa Kiyahudi wenye uadui katika Sanhedrini, wapinzani wake ‘waliona kwamba uso wake ulikuwa kama uso wa malaika.’ (Matendo 6:15) Uso wake ulikuwa kama wa mjumbe wa Mungu, wenye amani inayotoka kwa Yehova, Mungu mwenye utukufu. Baada ya kuwatolea ushahidi kwa ujasiri washiriki wa Sanhedrini, Stefano alijionea wonyesho wenye kutokeza wa fadhili zisizostahiliwa za Mungu. “Yeye, akiwa amejaa roho takatifu, akakaza macho mbinguni, akaona utukufu wa Mungu na wa Yesu akiwa amesimama kwenye mkono wa kuume wa Mungu.” (Matendo 7:55) Stefano alipopata maono hayo yenye kutokeza, yalithibitisha tena cheo cha Yesu kuwa Mwana wa Mungu na Masihi. Maono hayo yalimwimarisha Stefano mnyenyekevu na kumsadikishia kwamba alikuwa na kibali cha Yehova.

4. Yehova huwafunulia watu gani utukufu wake?

4 Kama maono aliyopewa Stefano yanavyoonyesha, Yehova hufunua utukufu na kusudi lake kwa watu wanaomwogopa, na ambao huthamini uhusiano wao pamoja naye. Biblia inasema: “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.” (Methali 22:4) Kwa hiyo, ni muhimu tuelewe unyenyekevu wa kweli ni nini, jinsi tunavyoweza kusitawisha sifa hiyo muhimu, na jinsi tunavyonufaika kwa kuionyesha katika sehemu zote za maisha.

Unyenyekevu Ni Sifa ya Kimungu

5, 6. (a) Unyenyekevu ni nini? (b) Yehova ameonyeshaje unyenyekevu? (c) Unyenyekevu wa Yehova unapaswa kuwa na matokeo gani kwetu?

5 Huenda watu fulani wakashangaa kwamba Yehova Mungu, aliye mkuu na mwenye utukufu zaidi katika ulimwengu wote, ndiye kielelezo bora zaidi cha unyenyekevu. Mfalme Daudi alimwambia Yehova hivi: “Utanipa ngao yako ya wokovu, na mkono wako mwenyewe wa kuume utanitegemeza, na unyenyekevu wako mwenyewe utanifanya kuwa mkuu.” (Zaburi 18:35) Akimfafanua Yehova kuwa mnyenyekevu, Daudi alitumia neno la Kiebrania ambalo kihalisi linamaanisha “kuinama.” Mbali na neno “unyenyekevu,” maneno mengine yanayohusiana nalo ni “upole” na “kujishusha.” Kwa hiyo, Yehova alionyesha unyenyekevu alipojishusha ili kushughulika na Daudi, mwanadamu asiye mkamilifu, na kumtumia kuwa mfalme aliyemwakilisha. Kama maandishi ya utangulizi ya Zaburi ya 18 yanavyoonyesha, Yehova alimlinda na kumtegemeza Daudi, akimkomboa “kutoka mkononi mwa adui zake wote na kutoka mkononi mwa Sauli.” Vivyo hivyo, Daudi alijua kwamba, umashuhuri au utukufu wowote ambao angepata akiwa mfalme ungetegemea jinsi ambavyo Yehova angetenda kwa unyenyekevu kwa niaba yake. Utambuzi huo ulimsaidia Daudi adumishe unyenyekevu.

6 Namna gani sisi? Yehova ameamua kutufunza kweli, na huenda ametupa mapendeleo ya pekee ya utumishi kupitia tengenezo lake, au huenda ametutumia kwa njia fulani kufanya mapenzi yake. Tunapaswa kuhisije kuhusu mambo hayo yote? Je, hayapaswi kufanya tuwe wanyenyekevu? Je, hatupaswi kumshukuru Yehova kwa unyenyekevu wake na kuepuka kujitukuza, jambo ambalo bila shaka lingetuletea msiba?—Methali 16:18; 29:23.

7, 8. (a) Yehova alionyeshaje unyenyekevu aliposhughulika na Manase? (b) Yehova na Manase wanatuwekea kielelezo gani cha kufuata katika kuonyesha unyenyekevu?

7 Yehova ameonyesha unyenyekevu mwingi kwa kushughulika na wanadamu wasio wakamilifu na pia amekuwa tayari kuwarehemu wale walio wanyenyekevu wa akili, hata kuwainua, au kuwatukuza wale wanaojinyenyekeza. (Zaburi 113:4-7) Kwa mfano, fikiria kisa cha Mfalme Manase wa Yuda. Alitumia vibaya cheo chake cha heshima akiwa mfalme ili kuendeleza ibada isiyo ya kweli, naye ‘akafanya kwa kiasi kikubwa yale yaliyokuwa mabaya machoni pa Yehova, na kumtia uchungu.’ (2 Mambo ya Nyakati 33:6) Mwishowe, Yehova alimwadhibu Manase kwa kumruhusu mfalme wa Ashuru amwondoe kwenye kiti chake cha ufalme. Akiwa gerezani, Manase ‘aliutuliza uso wa Yehova Mungu wake, akaendelea kujinyenyekeza sana’ hivi kwamba Yehova akamrudisha kwenye kiti cha ufalme huko Yerusalemu, naye Manase “akapata kujua kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli.” (2 Mambo ya Nyakati 33:11-13) Naam, mwishowe, unyenyekevu wa akili wa Manase ulimpendeza Yehova naye akaonyesha unyenyekevu kwa kumsamehe na kumweka kuwa mfalme tena.

8 Nia ya Yehova ya kusamehe na mtazamo wa Manase wa kuonyesha toba hutufunza mambo muhimu kuhusu unyenyekevu. Tunapaswa kukumbuka daima kwamba jinsi tunavyowatendea wale wanaotukosea na mtazamo tunaoonyesha tunapotenda dhambi, unaweza kuathiri jinsi Yehova anavyoshughulika nasi. Ikiwa tuko tayari kusamehe wengine makosa yao na kukubali makosa yetu kwa unyenyekevu, basi huenda Yehova akaturehemu.—Mathayo 5:23, 24; 6:12.

Utukufu wa Kimungu Hufunuliwa kwa Wanyenyekevu

9. Je, unyenyekevu ni ishara ya udhaifu? Eleza.

9 Hata hivyo, unyenyekevu na sifa nyingine zinazohusiana nao, hazipaswi kuonwa kuwa ishara ya udhaifu au mwelekeo wa kupuuza makosa. Kama Maandiko Matakatifu yanavyothibitisha, Yehova ni mnyenyekevu, lakini yeye huonyesha ghadhabu ya uadilifu na nguvu zenye kutisha inapokuwa lazima kufanya hivyo. Kwa sababu ya unyenyekevu wake, Yehova huwapa kibali au huwafikiria kwa njia ya pekee wale ambao ni wanyenyekevu wa akili, huku akijitenga na wenye kiburi. (Zaburi 138:6) Yehova amewaonyeshaje ufikirio wa pekee watumishi wake walio wanyenyekevu?

10. Yehova huwafunulia wanyenyekevu nini kama inavyoonyeshwa katika andiko la 1 Wakorintho 2:6-10?

10 Katika wakati wake unaofaa na kupitia njia yake ya mawasiliano, Yehova amewafunulia wanyenyekevu habari kamili kuhusu jinsi atakavyotimiza kusudi lake. Mambo hayo matukufu hayajafunuliwa kwa wale wenye kiburi, ambao hutegemea ama kufuata kwa ushupavu hekima au kufikiri kwa kibinadamu. (1 Wakorintho 2:6-10) Lakini kwa kuwa wanyenyekevu wamepewa ufahamu sahihi wa kusudi la Yehova, wanachochewa kumtukuza kwa sababu wanathamini hata zaidi utukufu wake wenye kutokeza.

11. Katika karne ya kwanza watu fulani walikosaje kuonyesha unyenyekevu, nao walipatwa na madhara gani?

11 Katika karne ya kwanza, wengi, kutia ndani watu fulani waliodai kuwa Wakristo, hawakuonyesha unyenyekevu nao walikwazwa na mambo ambayo mtume Paulo aliwafunulia kuhusu kusudi la Mungu. Paulo alikuwa “mtume kwa mataifa,” lakini si kwa sababu ya elimu, umri, taifa lake, au matendo mazuri aliyofanya kwa muda mrefu. (Waroma 11:13) Mara nyingi, watu wasio wa kiroho huona mambo hayo kuwa ndiyo ambayo huamua yule anayepaswa kutumiwa na Yehova kama chombo chake. (1 Wakorintho 1:26-29; 3:1; Wakolosai 2:18) Hata hivyo, Yehova alimchagua Paulo kupatana na kusudi lake adilifu na fadhili zake zenye upendo. (1 Wakorintho 15:8-10) Wale ambao Paulo aliwataja kuwa ‘mitume walio bora,’ na vilevile wapinzani wengine, walikataa kumkubali Paulo na hoja alizotoa kutokana na Maandiko. Ukosefu wao wa unyenyekevu uliwazuia wasipate ujuzi na ufahamu kuhusu njia tukufu ambayo Yehova hutimiza kusudi lake. Na tusiwapuuze kamwe au kuwahukumu kimbele wale ambao Yehova anachagua kuwatumia ili kutimiza mapenzi yake.—2 Wakorintho 11:4-6.

12. Kielelezo cha Musa huonyeshaje kwamba Yehova huwapendelea wanyenyekevu?

12 Kwa upande mwingine, kuna vielelezo vingi vinavyotajwa katika Biblia ambavyo vinakazia jinsi watu wanyenyekevu wanavyopendelewa kuona utukufu wa Mungu. Musa, aliyekuwa “mpole zaidi” kuliko watu wote, aliona utukufu wa Mungu naye alikuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. (Hesabu 12:3) Mtu huyo mnyenyekevu, aliyefanya kazi ya hali ya chini ya uchungaji kwa miaka 40— ambayo yaelekea miaka mingi kati ya hiyo alikuwa katika Peninsula ya Arabia—alipendelewa sana na Muumba katika njia nyingi. (Kutoka 6:12, 30) Kwa msaada wa Yehova, Musa alipata kuwa mnenaji na msimamizi mkuu wa taifa la Israeli. Aliwasiliana na Mungu kwa njia ya moja kwa moja. Kupitia maono, aliona “sura ya Yehova.” (Hesabu 12:7, 8; Kutoka 24:10, 11) Wale waliomkubali mtumishi huyo mnyenyekevu aliyekuwa mwakilishi wa Mungu walibarikiwa pia. Vivyo hivyo, tutabarikiwa tukimtambua na kumtii nabii aliye mkubwa zaidi kuliko Musa, yaani, Yesu, na vilevile “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye amewekwa rasmi naye.—Mathayo 24:45, 46; Matendo 3:22.

13. Utukufu wa Yehova ulifunuliwaje kwa wachungaji wa hali ya chini katika karne ya kwanza?

13 ‘Utukufu wa Yehova ulimulikia’ nani malaika walipotangaza habari njema ya kuzaliwa kwa “Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana”? Haukuwamulikia viongozi wa kidini wenye kiburi au watu mashuhuri wenye vyeo, bali uliwamulikia wachungaji wa hali ya chini ‘walioishi nje, wakichunga makundi yao usiku.’ (Luka 2:8-11) Watu hao hawakuheshimiwa sana kwa ustadi na kazi yao. Hata hivyo, Yehova aliwatambua hao na kuamua kuwaeleza kwanza kuhusu kuzaliwa kwa Masihi. Naam, Yehova huwafunulia wanyenyekevu na wale wanaomwogopa utukufu wake.

14. Mungu huwathawabishaje wale ambao ni wanyenyekevu?

14 Vielelezo hivyo vinatufunza nini? Vinatuonyesha kwamba Yehova huwapendelea na kuwafunulia wanyenyekevu ujuzi na ufahamu kuhusu kusudi lake. Yeye huchagua watu ambao huenda hawana sifa ambazo wengine wangetazamia wawe nazo na kuwatumia ili kuwajulisha wengine kusudi lake tukufu. Hilo lapaswa kutuchochea tuendelee kutafuta mwongozo kutoka kwa Yehova, Neno lake la kinabii, na tengenezo lake. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ataendelea kuwajulisha watumishi wake wanyenyekevu kuhusu kufunuliwa kwa kusudi lake tukufu. Nabii Amosi alisema: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hatafanya lolote isipokuwa awe amewafunulia watumishi wake manabii jambo lake la siri.”—Amosi 3:7.

Sitawisha Unyenyekevu na Upate Kibali cha Mungu

15. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kudumisha unyenyekevu, na jambo hilo linakaziwaje na kisa cha Mfalme Sauli wa Israeli?

15 Ili tuendelee kuwa na kibali cha Mungu, ni lazima tudumishe unyenyekevu. Mtu anaweza kuwa mnyenyekevu leo lakini asiendelee kudumisha sifa hiyo. Anaweza kupoteza sifa ya unyenyekevu na kuwa mwenye kiburi na mwenye kujiinua, tabia ambazo hutokeza kimbelembele na msiba. Sauli, mfalme wa kwanza wa Israeli aliyetiwa mafuta alifanya vivyo hivyo. Mwanzoni alipochaguliwa, alihisi ‘kuwa mdogo machoni pake.’ (1 Samweli 15:17) Hata hivyo, baada ya kutawala kwa miaka miwili tu, alitenda kwa kimbelembele. Alipuuza mpango wa Yehova wa kutoa dhabihu kupitia nabii Samweli, naye akatunga sababu za kujitetea ili kutoa dhabihu. (1 Samweli 13:1, 8-14) Huo ulikuwa mwanzo wa mfululizo wa matukio ambayo bila shaka yalionyesha kwamba hakuwa mnyenyekevu. Matokeo ni kwamba alipoteza roho na kibali cha Mungu, na mwishowe akafa kifo cha aibu. (1 Samweli 15:3-19, 26; 28:6; 31:4) Tunajifunza jambo hili ambalo ni wazi: Ni lazima tujitahidi kudumisha unyenyekevu na ujitiisho na kuzuia hisia za kujiona kuwa bora, hivyo kuepuka kutenda kwa kimbelembele kwa njia yoyote na kupoteza kibali cha Yehova.

16. Kutafakari uhusiano wetu pamoja na Yehova na wanadamu wenzetu kunaweza kutusaidiaje kusitawisha unyenyekevu?

16 Tunapaswa kusitawisha sifa ya kimungu ya unyenyekevu ingawa haiko katika orodha ya matunda ya roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22, 23; Wakolosai 3:10, 12) Kwa kuwa sifa hiyo inahusisha hali ya akili, yaani, jinsi tunavyojiona na kuwaona wengine, kusitawisha unyenyekevu hutaka tujitahidi sana. Kufikiria kwa uzito na kutafakari juu ya uhusiano wetu pamoja na Yehova na wanadamu wenzetu kunaweza kutusaidia kudumisha unyenyekevu. Machoni pa Mungu, wanadamu wote wasio wakamilifu ni kama nyasi inayokua kwa muda kisha hunyauka. Wanadamu ni kama panzi tu shambani. (Isaya 40:6, 7, 22) Je, unyasi mmoja unaweza kuwa na sababu ya kujigamba kwa sababu tu ni mrefu kidogo kuliko nyasi nyingine? Je, panzi ana sababu ya kujigamba kuhusu uwezo wake wa kuruka kwa sababu tu anaweza kuruka mbali zaidi kuliko panzi wengine? Lingekuwa jambo la upumbavu kufikiri hivyo. Hivyo, mtume Paulo aliwakumbusha hivi Wakristo wenzake: “Ni nani anayekufanya wewe kuwa tofauti na mwingine? Kwa kweli, una nini ambacho hukupokea? Basi, ikiwa kwa kweli ulikipokea, kwa nini unajisifu kana kwamba hukukipokea?” (1 Wakorintho 4:7) Kutafakari maandiko kama hayo ya Biblia kunaweza kutusaidia kusitawisha na kuonyesha unyenyekevu.

17. Ni nini kilichomsaidia nabii Danieli asitawishe unyenyekevu, na ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya vivyo hivyo?

17 Nabii Mwebrania Danieli, alitajwa kuwa “mtu mwenye kutamanika sana” machoni pa Mungu kwa sababu ya “kujinyenyekeza” mwenyewe, yaani, kwa sababu ya unyenyekevu wake. (Danieli 10:11, 12) Ni nini kilichomsaidia Danieli asitawishe unyenyekevu? Kwanza, alimtegemea Yehova kabisa, akisali kwake kwa ukawaida. (Danieli 6:10, 11) Isitoshe, Danieli alikuwa mwenye nia njema na mwanafunzi mwenye bidii wa Neno la Mungu ambalo lilimsaidia kukazia fikira kusudi tukufu la Mungu. Pia alikuwa tayari kukubali makosa yake, wala si ya watu wake tu. Kwa kweli alipendezwa kutegemeza uadilifu wa Mungu, wala si wake mwenyewe. (Danieli 9:2, 5, 7) Je, tunaweza kujifunza kutokana na kielelezo bora cha Danieli na kujitahidi kusitawisha na kuonyesha unyenyekevu katika sehemu zote za maisha yetu?

18. Wale wanaoonyesha unyenyekevu leo watapata utukufu gani?

18 Methali 22:4 inasema: “Matokeo ya unyenyekevu na kumwogopa Yehova ni utajiri na utukufu na uzima.” Naam, Yehova huwapa kibali wanyenyekevu, na matokeo ni utukufu na uzima. Mtunga-zaburi Asafu alikuwa karibu kuacha utumishi wake kwa Mungu lakini Yehova akarekebisha fikira zake. Baadaye alikiri hivi kwa unyenyekevu: “Utaniongoza kwa shauri lako, na baadaye utanipeleka kwenye utukufu.” (Zaburi 73:24) Namna gani leo? Wale wanaoonyesha unyenyekevu watapata utukufu gani? Zaidi ya kuwa na uhusiano wenye furaha pamoja na Yehova, wanaweza kutazamia kuona utimizo wa maneno haya ya Mfalme Daudi yaliyoongozwa na roho ya Mungu: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” Huo ni wakati ujao ulio mtukufu kwelikweli!—Zaburi 37:11.

Je, Unakumbuka?

• Stefano anaweka kielelezo gani cha mtu mnyenyekevu ambaye Yehova alimfunulia utukufu Wake?

• Yehova Mungu ameonyesha unyenyekevu katika njia zipi?

• Ni vielelezo gani vinavyoonyesha kwamba Yehova huwafunulia wanyenyekevu utukufu wake?

• Kielelezo cha Danieli kinaweza kutusaidiaje tusitawishe unyenyekevu?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku katika ukurasa wa 12]

Mwenye Nguvu Lakini Mnyenyekevu

Mnamo mwaka wa 1919 kwenye kusanyiko la Wanafunzi wa Biblia (ambao leo wanajulikana kuwa Mashahidi wa Yehova), huko Cedar Point, Ohio, Marekani, J. F. Rutherford, mwenye umri wa miaka 50 ambaye alikuwa akisimamia kazi wakati huo, alijitolea kufanya kazi ya mhudumu wa hoteli kwa furaha, huku akibeba mizigo na kuwasindikiza wahudhuriaji kwenye vyumba vyao. Siku ya mwisho ya kusanyiko hilo, alisisimua wahudhuriaji 7,000 kwa maneno haya: “Wewe ni balozi wa Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana, unayewatangazia watu . . . ufalme wenye utukufu wa Bwana wetu.” Ndugu Rutherford alikuwa mtu mwenye masadikisho imara, aliyejulikana kuwa msemaji mwenye nguvu na ambaye alishikilia kwa dhati mambo aliyoamini kuwa ya kweli. Pia alikuwa mnyenyekevu kikweli mbele za Mungu, mara nyingi akionyesha hilo katika sala alizotoa kwenye ibada ya asubuhi huko Betheli.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Stefano, aliyeyajua Maandiko vizuri, aligawa chakula kwa unyenyekevu

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yehova alipendezwa na hali ya akili ya unyenyekevu ya Manase

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ni nini kilichofanya Danieli awe “mtu mwenye kutamanika sana”?