Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Katika sala yake ya kielelezo, je, Yesu alimaanisha kwamba mapenzi ya Mungu yalikuwa yakifanywa mbinguni ijapokuwa malaika waovu hawakuwa wamefukuzwa huko?

Katika Mathayo 6:10 Yesu alisema hivi: “Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” Ombi hilo linaweza kueleweka katika njia mbili. Moja, alikuwa akiomba mapenzi ya Mungu yatendeke duniani kama yalivyokuwa yakitendeka mbinguni. Pili, alikuwa akiomba mapenzi ya Mungu yatendeke kikamili mbinguni na duniani. * Maana ya maneno ya Yesu yanayotangulia hayo, “ufalme wako uje,” yanaonyesha kwamba maana ya pili ndiyo inayopatana zaidi na Maandiko. Nayo yanaonyesha hali ilivyokuwa wakati Yesu alipokuwa duniani na muda mrefu baadaye. Jinsi gani?

Kitabu cha Ufunuo kinataja matokeo mawili tofauti kuhusu kusimamishwa kwa Ufalme wa Mungu mbinguni. Kusimamishwa huko kunaathiri kwanza mbingu, kisha dunia. Andiko la Ufunuo 12:7-9, 12 linasema: “Vita vikatokea ghafula mbinguni: Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka mkubwa, naye joka mkubwa na malaika zake wakapigana lakini hakushinda, wala mahali hapakupatikana mbinguni kwa ajili yao tena. Kwa hiyo yule joka mkubwa akatupwa chini, yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa; akatupwa chini duniani, na malaika zake wakatupwa chini pamoja naye. Kwa sababu hiyo furahini, enyi mbingu nanyi mnaokaa ndani yake! Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”

Viumbe waasi wa roho waliondolewa mbinguni kabisa wakati Shetani na roho wake waovu walipofukuzwa huko baada ya mwaka wa 1914. Jambo hilo liliwafurahisha sana wana wa kimalaika wa Yehova walio washikamanifu, ambao ndio wengi kati ya viumbe wake wa roho. (Ayubu 1:6-12; 2:1-7; Ufunuo 12:10) Hivyo, ombi katika sala ya Yesu ya kielelezo kuhusu kufanywa kwa mapenzi ya Mungu mbinguni lilitimizwa. Wote waliobaki katika makao hayo ya kimbingu walikuwa washikamanifu kwa Yehova nao walijitiisha kikamili kwa enzi yake kuu.

Ni lazima ikaziwe kwamba hata kabla ya kufukuzwa, wakati malaika hao waovu walipokuwa bado wanaweza kuingia mbinguni, hawakuwa sehemu ya familia ya Mungu, bali walikuwa wamewekewa vizuizi hususa. Kwa mfano, andiko la Yuda 6 linafunua kwamba katika karne ya kwanza W.K., malaika hao walikuwa tayari ‘wamewekwa akiba wakiwa na vifungo vya milele chini ya giza zito ya kiroho kwa ajili ya hukumu ya ile siku kuu.’ Vivyo hivyo, andiko la 2 Petro 2:4 linasema: “Mungu hakujizuia kuwaadhibu wale malaika waliofanya dhambi, bali, kwa kuwatupa ndani ya Tartaro, [hali ya kushushwa kabisa] aliwatia ndani ya mashimo yenye giza zito [la kiroho] ili wawekwe akiba kwa ajili ya hukumu.” *

Tofauti na wakati ambapo malaika waovu walikuwa wametengwa kiroho wakiwa bado mbinguni, malaika hao wamekuwa na mamlaka makubwa juu ya dunia. Hata Neno la Mungu humwita Shetani “mtawala wa ulimwengu huu” nalo huita roho waovu “watawala wa ulimwengu wa giza hili.” (Yohana 12:31; Waefeso 6:11, 12; 1 Yohana 5:19) Kwa sababu ya mamlaka aliyo nayo, Ibilisi angeweza kumtolea Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo” ili amfanyie tendo moja la ibada. (Mathayo 4:8, 9) Hivyo basi, wakati Ufalme wa Mungu ‘utakapokuja’ utaleta mabadiliko makubwa sana duniani.

Ufalme wa Mungu ‘utakapokuja’ hapa duniani, utaleta mfumo mpya kabisa wa mambo. Ufalme huo utaharibu tawala zote za kibinadamu nao utakuwa serikali pekee itakayotawala dunia. Wakati huohuo, raia za Ufalme huo wanaomwogopa Mungu watafanyiza “dunia mpya.” (2 Petro 3:13; Danieli 2:44) Ufalme huo pia utawaondolea dhambi wanadamu watiifu na baada ya muda utafanya dunia yote kuwa paradiso na hivyo kuondoa kabisa utawala wa kishetani.—Waroma 8:20, 21; Ufunuo 19:17-21.

Mwishoni mwa Miaka Elfu, wakati ambapo Ufalme wa Kimasihi utakuwa umetimiza mapenzi ya Mungu, ‘Mwana mwenyewe atajitiisha pia kwa Yeye aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.’ (1 Wakorintho 15:28) Kisha kutakuwa na jaribu la mwisho, na baada ya hapo Shetani, roho wake waovu, na wanadamu wowote waasi watakaokuwa wamepotoshwa wataharibiwa kabisa katika “kifo cha pili.” (Ufunuo 20:7-15) Baadaye, viumbe wote wenye akili mbinguni na duniani watajitiisha milele na kwa furaha chini ya utawala wenye upendo wa Yehova. Wakati huo ndipo maneno ya Yesu katika sala ya kielelezo yatakapotimia kikamili.—1 Yohana 4:8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Katika tafsiri ya The Bible—An American Translation, sehemu hii ya sala ya kielelezo ya Yesu imetafsiriwa hivi: “Ufalme wako na uje! Mapenzi yako na yatendeke duniani na vilevile mbinguni.”—Mathayo 6:10.

^ fu. 6 Mtume Petro alilinganisha hali hiyo ya kutengwa kiroho na kufungwa “gerezani.” Hata hivyo, yeye hakumaanisha ile “abiso” ya baadaye ambayo roho waovu watatupwa kwa miaka elfu moja.—1 Petro 3:19, 20; Luka 8:30, 31; Ufunuo 20:1-3.