Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Kulihubiri Neno’ Huleta Burudisho

‘Kulihubiri Neno’ Huleta Burudisho

“Njooni Kwangu, . . . Nami Hakika Nitawaburudisha Ninyi”

‘Kulihubiri Neno’ Huleta Burudisho

ALIKUWA mwanadamu mkamilifu aliyekuwa ametumwa kufanya kazi muhimu. Njia zake za kufundisha zilikuwa na matokeo sana hivi kwamba “umati ulishangaa juu ya njia yake ya kufundisha.” (Mathayo 7:28) Pia alihubiri kwa bidii. Alitumia wakati wake, nguvu zake, na mali zake hasa kuhubiri Ufalme wa Mungu. Kwa kweli, Yesu Kristo alisafiri kotekote nchini kwao akihubiri na kufundisha kwa njia isiyo na kifani.—Mathayo 9:35.

Kazi muhimu ya Yesu ilikuwa kuhubiri “habari njema ya ufalme” kwa watu walioishi wakati wake na kuzoeza wanafunzi wake wafanye kazi hiyo ulimwenguni pote. (Mathayo 4:23; 24:14; 28:19, 20) Je, daraka hilo zito la kuhubiri eneo kubwa kwa hima lingewalemea wafuasi wake wenye udhaifu na wasio wakamilifu?

Sivyo! Baada ya kuwaagiza wanafunzi wake waombe “Bwana-mkubwa wa mavuno,” Yehova Mungu, atume wafanyakazi zaidi, Yesu aliwatuma wakawafundishe watu. (Mathayo 9:38; 10:1) Kisha akawapa uhakikisho wa kwamba daraka la kuwa wafuasi wake—kutia ndani kazi ya kuhubiri—lingeleta kitulizo na faraja ya kweli. Yesu alisema: “Njooni kwangu, . . . nami hakika nitawaburudisha nyinyi.”—Mathayo 11:28.

Chanzo cha Furaha

Mwaliko huo ni wa huruma, upendo, na fadhili kama nini! Unaonyesha jinsi Yesu anavyowajali wafuasi wake. Wanafunzi wake hupata burudisho wanapotimiza daraka lao la kuhubiri “habari njema” za Ufalme wa Mungu. Wanapata uradhi na furaha kwa kufanya hivyo.—Yohana 4:36.

Muda mrefu kabla Yesu hajaja duniani, Maandiko yalikazia kwamba utumishi mtakatifu kwa Mungu wapaswa kutolewa kwa furaha. Jambo hilo lilionyeshwa waziwazi mtunga-zaburi alipoimba: “Mfanyieni BWANA shangwe, dunia yote; mtumikieni BWANA kwa furaha; njooni mbele zake kwa kuimba.” (Zaburi 100:1, 2) Leo, watu wa mataifa yote humtukuza Yehova, na sifa wanazomtolea ni kama kelele za shangwe za jeshi lililopata ushindi. Wale ambao wamejitoa kwa Mungu kikweli huenda mbele yake “kwa kuimba.” Na jambo hilo linafaa kwa kuwa Yehova ni “Mungu mwenye furaha,” anayetaka watumishi wake wafurahi wanapojitahidi kuishi kupatana na wakfu wao kwake.—1 Timotheo 1:11.

Wahudumu Walioburudishwa

Inakuwaje kwamba kazi ngumu ya utumishi wa shambani haitulemei bali inatuburudisha? Yesu aliona kufanya kazi ya Yehova kuwa kama chakula kinachotupa nguvu. Alisema: “Chakula changu ni kwamba mimi nifanye mapenzi yake aliyenituma na kumaliza kazi yake.”—Yohana 4:34.

Vivyohivyo, leo wahubiri Wakristo wenye bidii hupata furaha ‘wanapohubiri neno.’ (2 Timotheo 4:2) Connie, Mwanamke Mkristo wa makamo ambaye hutumia zaidi ya saa 70 kila mwezi akihubiri, asema: “Baada ya kushiriki katika huduma, mimi hupata furaha na uradhi, hata ingawa nitakuwa nimechoka ifikapo jioni.”

Namna gani watu wasipokubali ujumbe wa Ufalme? Connie aendelea kusema: “Hata itikio liweje, sijawahi kujuta kushiriki katika huduma. Mbali na kujua kwamba jambo ninalofanya linampendeza Yehova, ninafurahi kuwaeleza wengine kweli kwa sababu nifanyapo hivyo, ninaimarisha moyoni mwangu tumaini zuri la Biblia.”

Wengine huona kwamba kuwasaidia watu wapate ujuzi sahihi juu ya Mungu hufanya maisha yao yawe na kusudi. Meloney, mwanamke mchanga ambaye hutumia zaidi ya saa 50 kwa ukawaida kila mwezi kuhubiri, asema: “Huduma huburudisha kwa kuwa inafanya maisha yangu yawe na kusudi. Ninaposhiriki katika utumishi, sifikirii sana matatizo yangu ya kibinafsi na mikazo ninayopata kila siku.”

Millicent, mhudumu mwingine wa Mashahidi wa Yehova mwenye bidii, asema: “Kila siku huwa yenye thamani ninapoitumia katika huduma nikizungumza na wengine kuhusu makusudi ya Mungu kwa wanadamu na kuwaeleza jinsi Paradiso itakavyorudishwa duniani. Ninaposhiriki huduma, Yehova huwa halisi kwangu kila siku na ninapata kiasi fulani cha amani na furaha ya moyoni isiyoweza kupatikana kwa njia nyingine yoyote.”

Watu Walioburudishwa

Bila shaka wahubiri wa Ufalme huburudishwa na huduma ya Kikristo, na wale wanaokubali ujumbe unaookoa uhai, hupata faraja. Ingawa mwalimu mmoja nchini Ureno alikuwa amefundishwa na watawa wa kike na makasisi, alihisi kwamba mahitaji yake ya kiroho hayakutoshelezwa na kanisa lake. Maswali yake ya Biblia hayakujibiwa. Alipoanza kujifunza Biblia kwa ukawaida na Mashahidi wa Yehova, alianza kufahamu Maandiko hatua kwa hatua. Mwalimu huyo alisisimuka. “Nilitazamia kwa hamu funzo letu la kila Jumatano, na maswali yangu yalijibiwa kwa usadikisho kutoka kwa Biblia,” akasema. Leo, mwanamke huyo ni mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu, naye pia anawaburudisha wengine kwa kweli ya Biblia.

Kwa hiyo, ni wazi kwamba Mashahidi wa Yehova hawalemewi na daraka lao zito la kuhubiri au na ukubwa wa eneo lao linalohusisha dunia yote. Hawavunjwi moyo na ubaridi au upinzani. Wamejitoa kwa bidii kutimiza kazi yao ya kuhubiri Ufalme. Wanawahubiria watu habari njema popote wanapoweza kupatikana—kwenye kituo cha malori nchini Marekani (1), katika uwanja wa ndege huko Korea (2), katika Milima ya Andes (3), au sokoni huko London (4). Wafuasi wa Yesu wa siku hizi wanaendelea kufanya kazi yao yenye kuridhisha ulimwenguni pote kwa furaha. Na kupatana na ahadi yake, amewaburudisha na amewatumia kuburudisha wengine wengi.—Ufunuo 22:17.