Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Ni Mfano Bora Sana wa Wema

Yehova Ni Mfano Bora Sana wa Wema

Yehova Ni Mfano Bora Sana wa Wema

“Mshukuruni BWANA wa majeshi, maana BWANA ni mwema.”—YEREMIA 33:11.

1. Kwa nini tunachochewa kumsifu Mungu kwa wema wake?

YEHOVA MUNGU ni mwema kabisa. “Wema wake, jinsi ulivyo mwingi!” akasema nabii Zekaria. (Zekaria 9:17) Naam, sifa ya wema huonekana katika yote ambayo Mungu alifanya kuitayarisha dunia ili tufurahie kuishi humo. (Mwanzo 1:31) Hatuwezi kamwe kuelewa sheria tata ambazo Mungu alitumia alipoumba ulimwengu. (Mhubiri 3:11; 8:17) Lakini mambo machache tunayojua kuhusu ulimwengu hutuchochea tumsifu Mungu kwa wema wake.

2. Wema ni nini?

2 Wema ni nini? Ni ubora wa kiadili. Hata hivyo, wema unamaanisha mengi zaidi ya kutokuwa na uovu wowote. Wema, ambao ni tunda la roho, ni sifa inayoonyeshwa kwa matendo. (Wagalatia 5:22, 23) Tunaonyesha sifa ya wema tunapowatendea wengine mambo mazuri yenye kuwanufaisha. Katika mfumo huu wa mambo, huenda mambo ambayo watu fulani huyaona kuwa mema yakaonwa kuwa mabaya na wengine. Hata hivyo, ili tupate amani na furaha, ni lazima kuwe na kiwango kimoja cha wema. Ni nani anayestahili kuweka kiwango hicho?

3. Andiko la Mwanzo 2:16, 17 linaonyesha nini kuhusu kiwango cha wema?

3 Mungu ndiye huweka kiwango cha wema. Mwanzoni mwa historia ya binadamu, Yehova ndiye aliyemwagiza yule mwanadamu wa kwanza hivi: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Naam, wanadamu wanahitaji kumtegemea Muumba wao ili wapate kujua yaliyo mema na yaliyo mabaya.

Wonyesho Usiostahiliwa wa Wema

4. Mungu amewafanyia wanadamu nini tangu Adamu alipofanya dhambi?

4 Matazamio ya mwanadamu ya kupata furaha ya milele akiwa mkamilifu yalihatarishwa Adamu alipofanya dhambi na kukataa haki ya Mungu ya kuweka viwango vya wema. (Mwanzo 3:1-6) Hata hivyo, kabla ya watoto wa Adamu kuzaliwa wakiwa warithi wa dhambi na kifo, Mungu alitabiri kuhusu kuja kwa Mbegu ambaye angekuwa mkamilifu. Akizungumza hasa na “nyoka wa awali,” Shetani Ibilisi, Yehova alisema: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.” (Ufunuo 12:9; Mwanzo 3:15) Yehova alikusudia kuwakomboa wanadamu wenye dhambi. Kwa kweli, Yehova ameonyesha wema usiostahiliwa kwa kufanya mpango huo ili kuwaokoa wale wanaoonyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Mwanawe mpendwa.—Mathayo 20:28; Waroma 5:8, 12.

5. Ingawa tumerithi moyo wenye mwelekeo mbaya, kwa nini tunaweza kuonyesha kiasi fulani cha wema?

5 Hapana shaka kwamba kwa sababu ya dhambi ya Adamu, tulirithi moyo wenye mwelekeo mbaya. (Mwanzo 8:21) Ingawa hivyo, tunafurahi kwamba Yehova hutusaidia kuonyesha kiasi fulani cha wema. Kwa kufuata mambo tuliyojifunza katika maandiko yake matakatifu na yenye thamani, ‘tunakuwa wenye hekima kwa ajili ya wokovu’ na pia tunaweza kufanya lililo jema machoni pa Mungu. (2 Timotheo 3:14-17) Ingawa hivyo, ili kunufaika na mafundisho ya Biblia na kuonyesha sifa ya wema, ni lazima tuwe na mtazamo kama wa mtunga-zaburi aliyeimba: “Wewe [Yehova] U mwema na mtenda mema, unifundishe amri zako.”—Zaburi 119:68.

Wema wa Yehova Watukuzwa

6. Baada ya Mfalme Daudi kuagiza sanduku la agano liletwe Yerusalemu, Walawi waliimba wimbo wenye maneno gani?

6 Mfalme Daudi wa Israeli la kale alitambua wema wa Mungu na kutafuta mwongozo Wake. Daudi alisema: “BWANA yu mwema, mwenye adili, kwa hiyo atawafundisha wenye dhambi njia.” (Zaburi 25:8) Mafundisho ambayo Waisraeli walipokea kutoka kwa Mungu yalitia ndani sheria kumi muhimu, yaani, zile Amri Kumi zilizoandikwa kwenye mabamba mawili ya mawe. Sheria hizo ziliwekwa katika sanduku takatifu lililoitwa sanduku la agano. Baada ya Daudi kuagiza Sanduku hilo liletwe Yerusalemu, jiji kuu la Israeli, Walawi waliimba wimbo wenye maneno haya: “Mshukuruni BWANA kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zake ni za milele.” (1 Mambo ya Nyakati 16:34, 37-41) Ilipendeza kama nini kusikia maneno hayo yakiimbwa na Walawi!

7. Ni nini kilichotokea Sanduku lilipoletwa Mahali Patakatifu Zaidi na baada ya sala ya Solomoni ya kuwekwa wakfu kwa hekalu?

7 Maneno hayo ya sifa yalikaziwa pia wakati wa kuwekwa wakfu kwa hekalu la Yehova lililojengwa na Solomoni mwana wa Daudi. Baada ya sanduku la agano kuwekwa Mahali Patakatifu Zaidi pa hekalu hilo lililokuwa limetoka tu kujengwa, Walawi walianza kumsifu Yehova, ‘kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili-upendo zake ni za milele.’ Wakati huo hekalu lilijawa na wingu kimuujiza, ambalo lilifananisha utukufu wa kuwapo kwa Yehova. (2 Mambo ya Nyakati 5:13, 14) Baada ya Solomoni kutoa sala ya kuwekwa wakfu kwa hekalu, ‘moto ulishuka kutoka mbinguni, ukateketeza sadaka ya kuteketezwa na dhabihu.’ Walipoona hayo, ‘wana wa Israeli wote walisujudu kifulifuli, hata nchi sakafuni, wakaabudu, wakamshukuru BWANA, wakisema, Kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili-upendo zake ni za milele.’ (2 Mambo ya Nyakati 7:1-3) Baada ya msherehekeo wa siku 14, Waisraeli walirudi makwao “wakishangilia na kufurahi moyoni kwa sababu ya wema ambao Mwenyezi-Mungu aliowajalia Daudi, Solomoni na watu wake Israeli.”—2 Mambo ya Nyakati 7:10, Biblia Habari Njema.

8, 9. (a) Ingawa Waisraeli walimsifu Yehova kwa wema wake, walitendaje hatimaye? (b) Yeremia alitabiri nini kuhusu Yerusalemu, nao utabiri huo ulitimizwaje?

8 Yasikitisha kwamba Waisraeli hawakuendelea kuishi kupatana na nyimbo zao za kumsifu Mungu. Baada ya muda, watu wa Yuda ‘walimheshimu Yehova kwa vinywa vyao tu.’ (Isaya 29:13) Badala ya kuishi kupatana na viwango vya Mungu vya wema, walianza kutenda mabaya. Walitenda mabaya gani? Waliabudu sanamu, wakafanya ngono haramu, wakawakandamiza maskini, na kufanya dhambi nyingine nzito! Kwa sababu hiyo, Yerusalemu liliharibiwa na wakazi wa Yuda wakatekwa na kupelekwa Babiloni mwaka wa 607 K.W.K.

9 Hivyo, Mungu akawatia nidhamu watu wake. Lakini kupitia nabii Yeremia, Mungu alitabiri kwamba katika jiji la Yerusalemu kungesikika sauti ya watu wasemao hivi: “Mshukuruni BWANA wa majeshi, maana BWANA ni mwema, rehema [“fadhili-upendo,” NW] zake ni za milele.” (Yeremia 33:10, 11) Utabiri huo ulitimia. Baada ya nchi hiyo kuwa ukiwa kwa miaka 70, mabaki ya Wayahudi walirudi Yerusalemu mwaka wa 537 K.W.K. (Yeremia 25:11; Danieli 9:1, 2) Walijenga tena madhabahu mahali hekalu lilipokuwa kwenye Mlima Moria na wakaanza kutoa dhabihu huko. Msingi wa hekalu uliwekwa mwaka wa pili baada ya wao kurudi. Ulikuwa wakati wa furaha iliyoje! Ezra alisema: “Hata wajenzi walipouweka msingi wa hekalu la BWANA, wakawaweka makuhani, wamevaa mavazi yao, wenye baragumu, na Walawi, wana wa Asafu, wenye matoazi, ili wamhimidi BWANA, kama alivyoagiza Daudi, mfalme wa Israeli. Wakaimbiana, wakimhimidi BWANA, na kumshukuru, wakasema, Kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zake kwa Israeli ni za milele.”—Ezra 3:1-11.

10. Zaburi ya 118 inaanza na kumalizika kwa maneno gani muhimu?

10 Maneno mengine ya kusifu wema wa Yehova yanapatikana katika zaburi kadhaa. Mojawapo ya zaburi hizo ni Zaburi ya 118 iliyoimbwa na familia za Waisraeli walipokuwa wakimalizia maadhimisho ya Pasaka. Zaburi hiyo inaanza na kumalizika kwa maneno haya: “Mshukuruni BWANA kwa kuwa ni mwema, kwa maana fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zake ni za milele.” (Zaburi 118:1, 29) Huenda hayo ndiyo maneno ya mwisho ya sifa ambayo Yesu Kristo na mitume wake waaminifu waliimba usiku uliotangulia kifo chake mwaka wa 33 W.K.—Mathayo 26:30.

“Nakusihi Unionyeshe Utukufu Wako”

11, 12. Baada ya kuona kidogo tu utukufu wa Mungu, Musa alisikia tangazo gani?

11 Uhusiano kati ya wema wa Yehova na fadhili-upendo zake ulioonyeshwa mara ya kwanza karne nyingi kabla ya wakati wa Ezra. Punde tu baada ya Waisraeli kuabudu ndama ya dhahabu nyikani, na wale waliofanya kosa hilo kuuawa, Musa alimwomba Yehova hivi: “Nakusihi unionyeshe utukufu wako.” Kwa kuwa Yehova alijua kwamba Musa hangeweza kuona uso Wake na kuishi, alisema: “Nitapitisha wema wangu wote mbele yako.”—Kutoka 33:13-20.

12 Siku iliyofuata wema wa Yehova ulipita mbele ya uso wa Musa kwenye Mlima Sinai. Wakati huo Musa aliona kidogo tu utukufu wa Mungu na kusikia tangazo hili: “BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa huruma [“rehema,” NW], mwenye fadhili, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema [“fadhili-upendo,” NW] na kweli; mwenye kuwaonea huruma [“ fadhili-upendo,” NW] watu elfu elfu, mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi; wala si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe; mwenye kuwapatiliza watoto uovu wa baba zao, na wana wa wana wao pia, hata kizazi cha tatu na cha nne.” (Kutoka 34:6, 7) Maneno hayo yanaonyesha kwamba wema wa Yehova unahusiana na fadhili-upendo zake na sifa nyingine za utu wake. Kuchunguza maneno hayo kutatusaidia kuonyesha sifa ya wema. Na tuchunguze kwanza sifa inayotajwa mara mbili katika tangazo hili zuri kuhusu wema wa Mungu.

‘Mungu Mwingi wa Fadhili-Upendo’

13. Katika tangazo kuhusu wema wa Mungu, ni sifa gani ambayo imetajwa mara mbili, na kwa nini jambo hilo linafaa?

13 ‘BWANA ni Mungu mwingi wa fadhili-upendo; mwenye kuwaonyesha fadhili-upendo watu elfu elfu.’ Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fadhili-upendo” linamaanisha pia “upendo mwaminifu-mshikamanifu.” Hiyo ndiyo sifa pekee ambayo imetajwa mara mbili katika tangazo la Mungu kwa Musa. Jambo hilo linafaa kama nini kwa kuwa upendo ndiyo sifa kuu ya Yehova! (1 Yohana 4:8) Maneno yanayojulikana sana ya kumsifu Yehova “kwa kuwa ni mwema; kwa maana fadhili [“fadhili-upendo,” NW] zake ni za milele,” hukazia sifa hiyo.

14. Ni nani hasa ambao hufurahia wema na fadhili-upendo za Mungu?

14 Njia moja ambayo Yehova huonyesha wema wake ni kwa kuwa ‘mwingi wa fadhili-upendo.’ Sifa hiyo inaonekana hasa kupitia jinsi anavyowatunza kwa wororo watumishi wake waaminifu wa kibinadamu, ambao wamejiweka wakfu. (1 Petro 5:6, 7) Mashahidi wa Yehova wanaweza kushuhudia kwamba yeye ‘huwaonea fadhili-upendo’ wale wanaompenda na kumtumikia. (Kutoka 20:6) Yehova aliacha kuwaonyesha Waisraeli fadhili-upendo, au upendo mwaminifu-mshikamanifu, kwa sababu walimkataa Mwanawe. Lakini wema wa Mungu na upendo wake mwaminifu-mshikamanifu kwa Wakristo waaminifu wa mataifa yote utadumu milele.—Yohana 3:36.

Yehova Ni Mwenye Rehema na Fadhili

15. (a) Tangazo ambalo Musa alisikia kwenye Mlima Sinai lilianza kwa maneno gani? (b) Rehema inahusisha nini?

15 Tangazo ambalo Musa alisikia kwenye Mlima Sinai lilianza kwa maneno haya: ‘BWANA, BWANA, Mungu mwingi wa rehema, mwenye fadhili.’ Neno la Kiebrania linalotafsiriwa “rehema” laweza kurejezea “matumbo” na linahusiana sana na neno linalotafsiriwa “tumbo la uzazi.” Kwa hiyo, rehema inahusisha hisia za huruma nyororo za ndani kabisa. Lakini rehema inahusisha mengi zaidi ya huruma ya kweli. Rehema yapaswa kutuchochea kuchukua hatua fulani kuwaondolea wengine mateso. Kwa mfano, wazee Wakristo wenye upendo huona uhitaji wa kuwa wenye rehema kwa waamini wenzao, ‘wakionyesha rehema kwa uchangamfu’ inapofaa.—Waroma 12:8; Yakobo 2:13; Yuda 22, 23.

16. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Yehova ni mwenye fadhili?

16 Wema wa Mungu huonyeshwa pia kupitia fadhili yake. Mtu mwenye fadhili “hufikiria sana hisia za wengine” naye huonyesha ‘fadhili zinazomfanya avutie kwa watu wa hali ya chini.’ Yehova huweka mfano bora zaidi wa fadhili anaposhughulika na watumishi wake waaminifu. Kwa mfano, kwa fadhili Mungu alitumia malaika kumtia nguvu nabii Danieli aliyekuwa mzee, na kumjulisha Maria kuhusu pendeleo la kumzaa Yesu. (Danieli 10:19; Luka 1:26-38) Tukiwa watu wa Yehova, kwa kweli tunashukuru kwa jinsi ambavyo yeye hutuvuta kwake kwa fadhili kupitia Biblia. Sisi humsifu kwa jinsi aonyeshavyo sifa hiyo ya wema nasi hujitahidi kuwa wenye fadhili tunaposhughulika na wengine. Wale wenye sifa za kiroho wanapomrekebisha mwamini mwenzao “katika roho ya upole,” wanajitahidi kuwa wanana na wenye fadhili.—Wagalatia 6:1.

Mungu Asiye Mwepesi wa Hasira

17. Kwa nini tunashukuru kwamba Yehova “si mwepesi wa hasira”?

17 ‘Mungu asiye mwepesi wa hasira.’ Maneno hayo yanakazia njia nyingine ambayo Yehova huonyesha wema wake. Kwa subira Yehova huvumilia kasoro zetu na hutupatia wakati wa kushinda udhaifu mbaya na kufanya maendeleo ya kiroho. (Waebrania 5:12–6:3; Yakobo 5:14, 15) Subira ya Mungu pia huwanufaisha wale ambao bado hawajawa waabudu wake. Bado wana wakati wa kusikiliza ujumbe wa Ufalme na kutubu. (Waroma 2:4) Hata hivyo, ingawa Yehova ni mwenye subira, wakati mwingine wema wake humsukuma kuonyesha hasira yake, kama alivyofanya wakati Waisraeli walipoabudu ndama ya dhahabu kwenye Mlima Sinai. Karibuni, hasira ya Mungu itaonyeshwa kwa kiwango kikubwa hata zaidi atakapokomesha mfumo huu mwovu wa Shetani.—Ezekieli 38:19, 21-23.

18. Kuhusiana na kweli, kuna tofauti gani kati ya Yehova na viongozi wa kibinadamu?

18 ‘BWANA ni mwingi wa kweli.’ Yehova ni tofauti kama nini na viongozi wa kibinadamu, ambao hutoa ahadi nyingi, kisha wanakosa kuzitimiza! Tofauti nao, waabudu wa Yehova wanaweza kutumaini mambo yote yaliyosemwa katika Neno lake lililopuliziwa. Kwa kuwa Mungu ni mwingi wa kweli, tunaweza kutumaini ahadi zake sikuzote. Kwa sababu ya wema wake, Baba yetu wa mbinguni hujibu sala zetu za kupata kweli ya kiroho kwa kutoa kweli hiyo kwa wingi.—Zaburi 43:3; 65:2.

19. Ni wonyesho gani wa pekee wa wema ambao Yehova ameonyesha watenda-dhambi wenye kutubu?

19 ‘BWANA mwenye kusamehe uovu na makosa na dhambi.’ Kwa sababu ya wema wake, Yehova yu tayari kuwasamehe watenda-dhambi wanaotubu. Bila shaka, tunashukuru sana kwamba Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo amefanya iwezekane tusamehewe dhambi kupitia dhabihu ya Yesu. (1 Yohana 2:1, 2) Tu wenye furaha kwelikweli kwamba wote walio na imani katika fidia hiyo wanaweza kufurahia uhusiano wa pekee pamoja na Yehova, wakiwa na tumaini la kuishi milele katika ulimwengu mpya alioahidi. Hizi kwa kweli ni sababu za pekee za kumsifu Yehova kwa kuwaonyesha wanadamu wema wake!—2 Petro 3:13.

20. Tuna uthibitisho gani kwamba Mungu havumilii ubaya?

20 “Si mwenye kumhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe.” Hii kwa kweli ni sababu nyingine ya kumsifu Yehova kwa wema wake. Kwa nini? Kwa sababu jambo moja muhimu kuhusu sifa ya wema ni kwamba hauvumilii ubaya kamwe. Isitoshe, “kwenye ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu,” kisasi kitalipizwa juu ya “wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema.” Hao “watapatwa na adhabu ya kihukumu ya uharibifu udumuo milele.” (2 Wathesalonike 1:6-9) Kisha waabudu wa Yehova watakaookoka wataweza kufurahia maisha kikamili bila kusumbuliwa na watu wasiomwogopa Mungu, “wasio na upendo wa mema.”—2 Timotheo 3:1-3.

Iga Wema wa Yehova

21. Kwa nini tuonyeshe sifa ya wema?

21 Bila shaka tuna sababu nyingi za kumsifu na kumshukuru Yehova kwa wema wake. Je, hatutafanya yote tuwezayo kuonyesha sifa hiyo tukiwa watumishi wake? Ndiyo, kwa kuwa mtume Paulo aliwasihi hivi Wakristo wenzake: “Iweni waigaji wa Mungu, mkiwa watoto wapendwa.” (Waefeso 5:1) Baba yetu wa mbinguni huonyesha sifa ya wema daima, nasi twapaswa kufanya hivyo.

22. Tutachunguza nini katika makala ifuatayo?

22 Ikiwa tumejitoa kwa Yehova kwa moyo wote, bila shaka tunataka sana kuiga wema wake. Kwa kuwa sisi ni wazao wa Adamu mwenye dhambi, si rahisi kwetu kufanya lililo jema. Hata hivyo, katika makala ifuatayo tutaona ni kwa nini inawezekana kwetu kuonyesha sifa ya wema. Pia tutachunguza njia mbalimbali ambazo tunaweza na twapaswa kumwiga Yehova ambaye ni mfano bora sana wa wema.

Ungejibuje?

• Wema ni nini?

• Ni maneno gani ya Biblia yanayokazia wema wa Mungu?

• Wema wa Mungu huonekana katika njia zipi?

• Kwa nini twapaswa kuiga mfano wa Yehova wa wema?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 12]

Yehova aliwatia nidhamu watu wake wa kale kwa sababu hawakuishi kupatana na maneno yao ya sifa

[Picha katika ukurasa wa 12]

Mabaki waaminifu walirudi Yerusalemu

[Picha katika ukurasa wa 13]

Musa alisikia tangazo zuri kuhusu wema wa Mungu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Wema wa Yehova unaonekana kwa jinsi anavyotuvuta kwake kupitia Biblia