Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumaini Yehova Mungu Aliye Halisi

Mtumaini Yehova Mungu Aliye Halisi

Mtumaini Yehova Mungu Aliye Halisi

Je, umewahi kutazama anga usiku usiokuwa na mawingu na kuona nyota nyingi sana? Je, unaweza kueleza zilitoka wapi?

USIKU wenye utulivu, nyota zilizungumza kwa njia ya mfano na Mfalme Daudi wa Israeli la kale, na hivyo kumchochea aandike hivi: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.” (Zaburi 19:1) Naam, Muumba wala si uumbaji ndiye anayestahili “kupokea utukufu na heshima na nguvu.”—Ufunuo 4:11; Waroma 1:25.

Biblia husema: “Yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4) Kwa kweli, Mungu wa kweli, ‘aitwaye jina lake Yehova, ndiye aliye juu, juu ya nchi yote.’ (Zaburi 83:18) Naye si Mungu wa kuwaziwa tu. Yesu Kristo alisema hivi kuhusu Baba yake wa kimbingu, Yehova: “Yeye aliyenituma ni halisi.”—Yohana 7:28.

Yehova—Mtimizaji wa Makusudi Yake

Jina la Mungu la kipekee, Yehova, hupatikana karibu mara 7,000 katika Maandiko ya Kiebrania pekee. Jina hilo huonyesha kwamba yeye ni Mungu halisi. Maana halisi ya jina la Mungu ni “Yeye Husababisha Iwe.” Kwa hiyo Yehova Mungu hujitambulisha kuwa Mtimizaji wa makusudi yake. Musa alipomwuliza Mungu jina lake, Yehova alifafanua maana ya jina hilo kwa kusema hivi: “Mimi nitathibitika kuwa kile ambacho nitathibitika kuwa.” (Kutoka 3:14, NW) Tafsiri ya Rotherham yasema hivi waziwazi: “Nitakuwa chochote nitakacho kuwa.” Yehova huthibitika kuwa, au huamua kuwa chochote ili kutimiza makusudi na ahadi zake za uadilifu. Kwa hiyo, ana majina mengi ya cheo, kama vile Muumba, Baba, Bwana Mwenye Enzi Kuu, Mchungaji, Yehova wa majeshi, Msikiaji wa sala, Mwamuzi, Mfunzi Mtukufu, Mkombozi.—Waamuzi 11:27; Zaburi 23:1; 65:2; 73:28; 89:26; Isaya 8:13; 30:20, NW; 40:28; 41:14.

Ni Mungu wa kweli peke yake anayefaa kuitwa Yehova, kwa kuwa wanadamu hawawezi kuwa na hakika kwamba mipango yao itafanikiwa. (Yakobo 4:13, 14) Yehova peke yake ndiye anayeweza kusema: “Kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa mtu apandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma.”—Isaya 55:10, 11.

Yehova hutekeleza makusudi yake kwa uhakika sana hivi kwamba mambo ambayo huenda yakaonekana kuwa hayawezekani kwa wanadamu huwezekana kwake. Muda mrefu baada ya Abrahamu, Isaka, na Yakobo kufa, Yesu aliwataja na kusema: “Yeye [Yehova] ni Mungu, si wa wafu, bali wa walio hai, kwa maana kwake, wao wote wako hai.” (Luka 20:37, 38) Wazee hao watatu wa ukoo waaminifu walikuwa wamekufa, lakini kusudi la Mungu la kuwafufua lilikuwa hakika hivi kwamba machoni pake ni kana kwamba walikuwa hai. Si vigumu kwa Yehova kuwafufua waaminifu wa kale kama vile haikuwa vigumu kwake kuumba mwanadamu wa kwanza kutoka mavumbini.—Mwanzo 2:7.

Mtume Paulo ataja mfano mwingine unaoonyesha kwamba Mungu hutimiza makusudi yake. Katika Maandiko, Abrahamu anaitwa “baba ya mataifa mengi.” (Waroma 4:16, 17) Abramu alipokuwa bila mtoto, Yehova alibadili jina lake kuwa Abrahamu, ambalo linamaanisha “Baba ya Umati (Halaiki).” Yehova alifanya jina hilo kuwa halisi kwa kumrudishia Abrahamu na mke wake Sara waliokuwa wamezeeka, uwezo wa kuzaa.—Waebrania 11:11, 12.

Yesu Kristo aliyekuwa amepewa uwezo na mamlaka kubwa, alizungumza kuhusu hali fulani halisi kwa ufahamu mkubwa kuliko wanadamu. Ijapokuwa rafiki yake mkubwa Lazaro alikuwa amekufa, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Lazaro rafiki yetu ameenda kupumzika, lakini ninafunga safari huko ili kumwamsha kutoka usingizini.” (Yohana 11:11) Kwa nini Yesu alisema kwamba mfu huyo alikuwa amelala tu?

Yesu alipofika huko Bethania, jiji alikozaliwa Lazaro, alienda kwenye kaburi na kuagiza kwamba jiwe lililokuwa kwenye mwingilio liondolewe. Baada ya kusali kwa sauti kubwa, aliamuru: “Lazaro, njoo huku nje!” Huku watazamaji wakitazama lile kaburi, “huyo mtu aliyekuwa amekuwa mfu akatoka miguu na mikono yake ikiwa imefungwa vitambaa, na sura yake ilifungwa-fungwa kwa nguo.” Kisha Yesu akasema: “Mfungueni mmwache aende.” (Yohana 11:43, 44) Yesu alimfufua Lazaro—alirudisha uhai wa mtu aliyekuwa amekufa kwa muda wa siku nne! Kristo alisema kweli aliposema kwamba rafiki yake alikuwa amelala. Machoni pa Yehova na Yesu, Lazaro aliyekufa alikuwa kana kwamba amelala tu. Naam, Yesu na Baba yake wa kimbingu hushughulika na mambo halisi.

Yehova Anaweza Kutimiza Matarajio Yetu

Kuna tofauti kubwa kama nini kati ya sanamu zenye kudanganya na Mungu halisi! Waabudu sanamu husema kimakosa kwamba sanamu hizo zina uwezo unaozidi wa kibinadamu. Lakini, hata sanamu zipewe staha ya kadiri gani, haziwezi kufanya miujiza. Kwa upande mwingine, Yehova Mungu anaweza kusema kwamba watumishi wake waliokufa zamani wanaishi kwa kuwa anaweza kuwarudishia uhai. “BWANA ndiye Mungu wa kweli,” naye hawezi kuwadanganya watu wake kamwe.—Yeremia 10:10.

Inafariji kama nini kujua kwamba wafu walio katika kumbukumbu la Yehova watafufuliwa wakati wake barabara ufikapo! (Matendo 24:15) Naam, ufufuo unamaanisha kumfufua mtu akiwa na utu uleule. Kwa kuwa Muumba ana hekima na nguvu zisizo na mipaka, haitakuwa vigumu kwake kufufua wafu wakiwa na utu uleule. (Ayubu 12:13; Isaya 40:26) Kwa kuwa Yehova ana upendo mwingi, atatumia kumbukumbu lake kamilifu kuwafufua wafu katika dunia paradiso na kuwapa utu waliokuwa nao kabla hawajafa.—1 Yohana 4:8.

Mwisho wa ulimwengu wa Shetani unapokaribia, bila shaka wale wanaomtumaini Mungu wa kweli wanaweza kutazamia wakati ujao mzuri. (Mithali 2:21, 22; Danieli 2:44; 1 Yohana 5:19) Mtunga-zaburi atupatia uhakikisho huu: “Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, . . . bali wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” (Zaburi 37:10, 11) Uhalifu na jeuri vitakoma. Haki itakuwepo, na hali ngumu za kiuchumi hazitakuwepo. (Zaburi 37:6; 72:12, 13; Isaya 65:21-23) Hakutakuwepo ubaguzi wa kijamii, wa rangi, na wa kikabila. (Matendo 10:34, 35) Hakutakuwepo vita wala silaha. (Zaburi 46:9) Wakati huo “hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” (Isaya 33:24) Kila mtu atafurahia afya kamilifu. (Ufunuo 21:3, 4) Hivi karibuni dunia itakuwa paradiso. Yehova amekusudia iwe hivyo!

Naam, matarajio yote yanayotegemea Biblia yatatimizwa hivi karibuni. Kwa nini tukubali kudanganywa na sanamu zinazoabudiwa katika ulimwengu wa sasa hali tunaweza kumtumaini Yehova kabisa? Mapenzi yake ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:3, 4) Badala ya kutumia wakati na mali zetu kwa ajili ya vitu visivyo halisi vya mfumo huu na miungu yake, na tuongeze ujuzi kumhusu Mungu aliye halisi na tumtumaini kwa moyo wote.—Mithali 3:1-6; Yohana 17:3.

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 6]

Machoni pa Yehova na Yesu, Lazaro alikuwa amelala tu

[Maelezo ya Picha katika ukurasa wa 7]

Hivi karibuni dunia itakuwa paradiso