Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nguvu ya Sala

Nguvu ya Sala

Nguvu ya Sala

Jua linatua jijini Nahori huko Mashariki ya Kati. Msiria mmoja aitwaye Eliezeri afika na msafara wa ngamia kumi kwenye kisima fulani nje ya jiji hilo. Japo yaelekea ni mchovu na ana kiu, Eliezeri anahangaikia zaidi mahitaji ya wengine. Ametoka nchi ya kigeni kumtafutia mwana wa bwana-mkubwa wake mke. Isitoshe, ni lazima amtafute mke huyu kutoka kwa watu wa ukoo wa huyo bwana-mkubwa wake. Atatimizaje kazi hii ngumu?

ELIEZERI anaamini kwamba sala ni yenye nguvu. Kwa imani yenye kutokeza, iliyo kama ya mtoto, yeye aomba hivi kwa unyenyekevu: “Ee BWANA, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu, nakuomba mambo yangu uyajalie yawe heri leo, ukamfadhili bwana wangu Ibrahimu. Tazama! nimesimama karibu na kisima cha maji, na binti za watu wa mjini wanatoka kuteka maji, basi na iwe hivi; yule msichana nitakayemwambia, Tua mtungi wako, nakuomba, ninywe; naye akasema, Unywe, nami natawanywesha na ngamia zako pia; basi huyu na awe ndiye uliyemchagulia mtumishi wako Isaka; na kwa hayo nitajua ya kuwa umemfadhili bwana wangu.”—Mwanzo 24:12-14.

Uhakika wa Eliezeri katika nguvu ya sala si wa bure. Kwani, kumbe mwanamke wa kwanza kabisa anayekuja kisimani ni mjukuu wa ndugu yake Abrahamu! Anaitwa Rebeka, naye ni mseja, safi kiadili, na mrembo. Jambo la kutokeza ni kwamba yeye anampa Eliezeri maji ya kunywa na pia anajitolea kwa fadhili kuwanywesha ngamia zake wote. Baadaye, baada ya mashauriano ya kifamilia, Rebeka anakubali kwa utayari kwenda na Eliezeri katika nchi ya mbali akawe mke wa Isaka, mwana wa Abrahamu. Sala ya Eliezeri inajibiwa kwa njia yenye kutokeza na dhahiri kama nini wakati huo ambapo Mungu aliingilia matukio kimwujiza mara moja moja!

Tunaweza kujifunza mengi kutokana na sala ya Eliezeri. Sala hiyo ilionyesha imani yake yenye kutokeza, unyenyekevu, na kuhangaikia mahitaji ya wengine bila ubinafsi. Sala ya Eliezeri pia ilionyesha ujitiisho wake kwa njia ambayo Yehova hushughulika na wanadamu. Yaelekea alijua uhusiano wa pekee uliokuwapo kati ya Abrahamu na Mungu na vilevile ahadi Yake kwamba wanadamu wote wangebarikiwa wakati ujao kupitia Abrahamu. (Mwanzo 12:3) Hivyo, Eliezeri alianza sala yake kwa maneno haya: “Ee BWANA, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu.”

Yesu Kristo alikuwa mzao wa Abrahamu ambaye kupitia kwake wanadamu wote watiifu wangebarikiwa. (Mwanzo 22:18) Tukitaka sala zetu zijibiwe leo, tunahitaji kutambua kwa unyenyekevu njia ya Mungu ya kushughulika na wanadamu kupitia Mwana wake. Yesu Kristo alisema: “Ikiwa nyinyi mwakaa katika muungano nami na semi zangu zakaa katika nyinyi, ombeni lolote lile mtakalo nalo litatukia kwenu.”—Yohana 15:7.

Mfuasi wa Kristo aliyeona ukweli wa maneno hayo ya Yesu ni mtume Paulo. Hapana shaka kwamba imani yake katika sala haikuwa ya bure. Aliwatia moyo Wakristo wenzake wamtwike Mungu mahangaiko yao yote kupitia sala na kushuhudia hivi: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye anipaye nguvu.” (Wafilipi 4:6, 7, 13) Je, hilo lamaanisha kwamba Paulo alipata majibu kwa maombi yake yote ya bidii? Ebu tuone.

Si Sala Zote Zinazojibiwa

Katika huduma yake isiyo na ubinafsi, Paulo aliugua kile alichokiita “mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7) Huenda mwiba huo ulikuwa msononeko wa kiakili na wa kihisia-moyo uliosababishwa na wapinzani na “ndugu wasio wa kweli.” (2 Wakorintho 11:26; Wagalatia 2:4) Au huenda ulikuwa hali yenye kusumbua iliyosababishwa na ugonjwa wa macho wa kudumu. (Wagalatia 4:15) Hata iweje, “mwiba [huo] katika mwili” ulimdhoofisha Paulo. “Mara tatu nilimsihi sana Bwana kwamba upate kuniondoka,” yeye akaandika. Lakini ombi la Paulo halikujibiwa. Paulo alielezwa kwamba manufaa za kiroho ambazo alikuwa amekwisha pata kutoka kwa Mungu, kama vile nguvu za kuvumilia majaribu, zilitosha. Isitoshe, Mungu alisema: “Nguvu yangu inafanywa kamilifu katika udhaifu.”—2 Wakorintho 12:8, 9

Tunajifunza nini kutokana na mifano ya Eliezeri na Paulo? Yehova Mungu kwa kweli husikiliza sala za wale wanaojitahidi kwa unyenyekevu kumtumikia. Lakini hilo halimaanishi kwamba yeye hujibu sala zao sikuzote kwa sababu Mungu hujua mambo yatakayotukia muda mrefu baadaye. Yeye anajua kutushinda yale yanayotufaa zaidi. La maana zaidi ni kwamba sikuzote yeye hutenda kulingana na makusudi yake kama yalivyoandikwa katika Biblia.

Wakati wa Uponyaji wa Kiroho

Mungu anaahidi kuponya wanadamu magonjwa yote ya kimwili, ya kiakili, na ya kihisia-moyo wakati wa Utawala wa Miaka Elfu wa Mwana wake juu ya dunia. (Ufunuo 20:1-3; 21:3-5) Wakristo wa kweli wanangoja kwa hamu wakati huo ujao ulioahidiwa wakiwa na imani kamili kwamba Mungu ana uwezo wa kuuleta. Ingawa hawatarajii kuponywa kimuujiza leo, wao husali kwa Mungu wapate faraja na nguvu zake ili kuvumilia majaribu. (Zaburi 55:22) Wanapokuwa wagonjwa wanaweza pia kusali kupata mwongozo wa Mungu ili wapate matibabu yafaayo zaidi kulingana na uwezo wao wa kifedha.

Dini kadhaa huwatia wagonjwa moyo wasali ili waponywe sasa, wakitaja maponyo ya kimuujiza ambayo Yesu na mitume wake walifanya. Lakini miujiza hiyo ilifanywa kwa kusudi la pekee. Ilifanywa kuthibitisha kwamba Yesu Kristo alikuwa Mesiya wa kweli na kudhihirisha kwamba Mungu alipendelea kutaniko changa la Kikristo bali si taifa la Kiyahudi. Wakati huo, zawadi za kimuujiza zilihitajika ili kuimarisha imani ya kutaniko la Kikristo lililokuwa limefanyizwa karibuni. Zawadi hizo za kimuujiza ‘ziliondolewa mbali’ wakati kutaniko hilo changa lilipoimarika na kukomaa.—1 Wakorintho 13:8, 11.

Katika wakati huu muhimu, Yehova Mungu anawaelekeza waabudu wake katika kazi yenye maana zaidi ya uponyaji wa kiroho. Maadamu wangali na wakati, watu wanahitaji kuitikia haraka ombi hili: “Mtafuteni BWANA, maadamu anapatikana, mwiteni, maadamu yu karibu; mtu mbaya na aache njia yake, na mtu asiye haki aache mawazo yake; na amrudie BWANA, naye atamrehemu; na arejee kwa Mungu wetu, naye atamsamehe kabisa.”—Isaya 55:6, 7.

Uponyaji huo wa kiroho wa watenda-dhambi wenye kutubu unatimizwa kupitia kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mathayo 24:14) Kwa kuwatia nguvu watumishi wake watekeleze kazi hii ya kuokoa uhai, Yehova Mungu anasaidia mamilioni ya watu wa mataifa yote watubu dhambi zao na kuwa na uhusiano wenye upendeleo pamoja naye kabla ya mwisho wa mfumo huu mwovu. Sala za wote wanaosali kwa unyofu ili wapate ponyo hilo la kiroho na za wote wanaosali kupata msaada wa kufanya kazi hii ya kuponya zinajibiwa kwelikweli.

[Picha katika ukurasa wa 3 zimeandiliwa na]

Eliezer and Rebekah/The Doré Bible Illustrations/Dover Publications