Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imani Yao Ilithawabishwa

Imani Yao Ilithawabishwa

Wapiga-mbiu wa Ufalme Waripoti

Imani Yao Ilithawabishwa

MTUME Paulo alikuwa na imani yenye kutokeza, naye aliwatia moyo waamini wenzake pia wasitawishe imani. Alisema: “Amkaribiaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Mambo yafuatayo yaliyoonwa kutoka Msumbiji yadhihirisha jinsi ambavyo Yehova huthawabisha imani yenye nguvu na kujibu sala za bidii.

• Dada mmoja mjane katika wilaya ya kaskazini ya Niassa alikuwa na wasiwasi juu ya jinsi ambavyo yeye na watoto wake sita wangehudhuria Mkusanyiko wa Wilaya wa “Njia ya Mungu ya Maisha.” Njia yake pekee ya kupata fedha ilikuwa kuuza bidhaa kwenye soko la kwao, lakini siku ya mkusanyiko ilipokaribia, alikuwa na fedha zilizotosha tu kujilipia yeye na kulipia familia yake nauli ya gari-moshi kwa safari ya kwenda tu. Hata hivyo, aliazimia kutumaini maandalizi ya Yehova na kuendelea kujitayarisha kuhudhuria mkusanyiko huo.

Alipanda gari-moshi pamoja na watoto wake sita. Walipokuwa safarini kondakta akamfikia akitaka alipe nauli. Alipoona beji yake, akataka kujua amevalia kitambulisho cha aina gani. Dada huyo alimwambia kwamba beji hiyo ilikusudiwa kumtambulisha kuwa mjumbe kwenye mkusanyiko wa wilaya wa Mashahidi wa Yehova. “Mkusanyiko huo utafanyiwa wapi?” kondakta huyo akauliza. Alipoelezwa kwamba mkusanyiko huo ulikuwa katika wilaya jirani ya Nampula, umbali wa kilometa 300 hivi, kondakta huyo akamlipisha nusu ya nauli aliyopaswa kulipa bila dada huyo kutarajia! Kisha akampa yeye na familia yake tikiti za kurudi kwa nusu ya fedha za nauli zilizosalia. Alifurahi kama nini kwa kumtumaini Yehova!—Zaburi 121:1, 2.

• Kwa miaka 25 hivi, mwanamke mmoja aliyemcha Mungu sana alisali ili amwonyeshe jinsi ya kumwabudu ifaavyo. Kanisa aliloshirikiana nalo lilichanganya sherehe za kidini na desturi za kimapokeo naye alikuwa na shaka kama aina hiyo ya ibada inampendeza Mungu.

Yeye asimulia: “Nilikumbuka sikuzote maneno ya Yesu yaliyoandikwa kwenye Mathayo 7:7: ‘Fulizeni kuomba, nanyi mtapewa; fulizeni kutafuta sana, nanyi mtapata; fulizeni kubisha hodi, nanyi mtafunguliwa.’ Nikikumbuka andiko hilo nilisali kwa Mungu kwa ukawaida ili aniongoze kupata kweli. Siku moja kasisi wa kanisa letu akawaomba wote waliofanya kazi katika soko la mahali hapo walete kiasi fulani cha fedha pamoja na baadhi ya bidhaa zao ili azibariki. Niliona ombi hilo kuwa kinyume cha Maandiko, hivyo mimi sikuleta chochote. Kasisi huyo alipoona kwamba sikuwa nimeleta ‘sadaka,’ akaanza kunitukana mbele ya waumini wote wa kanisa. Siku hiyo nikang’amua kwamba Mungu hataki aabudiwe kwa njia hiyo, hivyo nikaacha kanisa hilo. Wakati huohuo, nikadumu katika sala ili niipate kweli.

“Hatimaye, nilipiga moyo konde na kuwasiliana na mtu wa ukoo ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Alinipa trakti, na nilipoisoma, nikang’amua mara moja kwamba Mungu alikuwa akijibu sala zangu. Hatimaye, mwenzi wangu pia akaanza kuthamini kweli za Biblia, hivyo tukahalalisha ndoa yetu. Lakini baadaye mume wangu akawa mgonjwa sana. Lakini hadi kifo chake, alinitia moyo nidumu katika njia ya ile kweli ili tuweze kukutana tena katika Paradiso.

“Nitamshukuru Yehova daima kwa kujibu sala zangu na kunionyesha njia ifaayo ya kumwabudu. Sala zangu zimejibiwa pia kwa sababu nimewasaidia watoto wangu wote wanane kuwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu