Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova—Mungu Aliye Hodari kwa Nguvu Zake

Yehova—Mungu Aliye Hodari kwa Nguvu Zake

Yehova—Mungu Aliye Hodari kwa Nguvu Zake

“Kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake.”—ISAYA 40:26.

1, 2. (a) Sisi sote hutegemea chanzo gani cha nguvu? (b) Eleza ni kwa nini Yehova ndiye Chanzo kikuu cha nguvu zote.

WENGI wetu hupuuza nguvu. Kwa mfano, sisi hupuuza nguvu za umeme zinazotupa nuru na joto na pia sisi hupuuza kule kuunganisha tu kwenye umeme chombo chochote cha umeme ambacho huenda tukawa nacho. Umeme ukipotea bila kutarajiwa ndipo sisi hutambua kwamba bila nguvu za umeme majiji ya wanadamu yangekoma. Kwa njia isiyo ya moja kwa moja, umeme mwingi tunaotumia hutoka kwenye chanzo cha nguvu ambacho dunia hukitegemea zaidi—jua. * Kwa kila sekunde jua letu hutumia tani milioni tano za fueli ya nyuklia, likitawanyia dunia nishati yenye kuendeleza uhai.

2 Jua hupata wapi nguvu hizo zote? Ni nani aliyeumba jua? Ni Yehova Mungu. Mtunga-zaburi asema hivi akimrejezea kwenye Zaburi 74:16: “Ndiwe uliyeufanya mwanga na jua.” Ndiyo, Yehova ndiye Chanzo kikuu cha nguvu zote, kama alivyo Chanzo cha uhai wote. (Zaburi 36:9) Haitupasi kamwe kupuuza nguvu zake. Kupitia nabii Isaya, Yehova atukumbusha tutazame vitu vinavyoonekana angani, kama jua na nyota, na kutafakari juu ya jinsi vilivyotokea. “Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina; kwa ukuu wa uweza wake, na kwa kuwa yeye ni hodari kwa nguvu zake; hapana moja isiyokuwapo mahali pake.”—Isaya 40:26; Yeremia 32:17.

3. Tunanufaikaje na maonyesho ya nguvu za Yehova?

3 Kwa kuwa Yehova ni hodari kwa nguvu zake, tuna hakika kwamba jua litaendelea kutoa nuru na joto ambazo uhai wetu wategemea. Hata hivyo, sisi hutegemea nguvu za Mungu kwa mambo mengi zaidi kuliko mahitaji yetu ya kimwili ya msingi. Ukombozi wetu kutokana na dhambi na kifo, tumaini letu la wakati ujao, na itibari yetu kwa Yehova, zote zinahusiana kabisa na jinsi anavyotumia nguvu zake. (Zaburi 28:6-9; Isaya 50:2) Biblia imejaa mifano inayothibitisha kwamba Yehova ana nguvu za kuumba na kukomboa, za kuokoa watu wake na kuwaangamiza adui zake.

Nguvu za Mungu Ni Dhahiri Katika Uumbaji

4. (a) Daudi aliitikiaje alipotazama anga la usiku? (b) Vitu vya angani vinafunua nini kuhusu nguvu za Mungu?

4 Mtume Paulo alieleza kwamba ‘nguvu za milele za Muumba zafahamiwa wazi kwa vitu alivyovifanya.’ (Waroma 1:20) Karne nyingi awali, mtunga-zaburi Daudi, ambaye akiwa mchungaji ni lazima awe alitazama anga la usiku mara nyingi, aliona utukufu wa ulimwengu na uweza wa Mfanyi wake. Aliandika: “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie?” (Zaburi 8:3, 4) Japo hakujua sana juu ya vitu vya angani, Daudi alifahamu kwamba yeye si kitu akilinganishwa na Muumba wa ulimwengu wetu mkubwa. Leo, wataalamu wa anga wanafahamu zaidi ukubwa wa ulimwengu na nguvu inayoudumisha. Kwa mfano, wao hutuambia kwamba kwa kila sekunde moja jua letu hutoa nishati inayotoshana na mlipuko wa tani milioni mara milioni 100,000 za TNT. * Na ni sehemu ndogo sana ya nguvu hizo inayofikia dunia; nayo inatosha kuendeleza uhai wa viumbe vyote duniani. Isitoshe, jua letu si nyota yenye nguvu zaidi katika mbingu. Nguvu ambazo nyota fulani hutoa kwa sekunde moja tu hutoshana na nguvu ambazo jua hutoa kwa siku nzima. Basi, ebu wazia nguvu za Muumba wa nyota hizo! Hakika, maneno haya ya Elihu yalikuwa kweli: “Yeye mwenyezi hamwezi kumwona; yeye ni mkuu mwenye uweza.”—Ayubu 37:23.

5. Tunapata ushuhuda gani wa nguvu za Yehova katika matendo yake?

5 ‘Tukiyafikiria matendo ya Mungu’ kama alivyofanya Daudi, tutaona uthibitisho wa nguvu zake kila mahali—katika pepo na mawimbi, katika ngurumo na radi, katika mito mikubwa na milima yenye fahari. (Zaburi 111:2; Ayubu 26:12-14) Na zaidi, kama Yehova alivyomkumbusha Yobu, wanyama hushuhudia nguvu Zake. Miongoni mwa wanyama hao mna Behemothi, au kiboko. Yehova alimwambia Yobu: “Nguvu zake ni katika viuno vyake . . . Mbavu zake ni kama vipande vya chuma.” (Ayubu 40:15-18) Katika nyakati za Biblia fahali wa mwitu alijulikana sana kuwa mwenye nguvu za kutisha, na Daudi alisali ili aokolewe kutokana na “kinywa cha simba, na pembe za fahali wa mwitu.”—Zaburi 22:21, NW; Ayubu 39:9-11.

6. Fahali hufananisha nini katika Maandiko, na kwa nini? (Ona kielezi-chini.)

6 Kwa sababu ya nguvu zake, fahali hutumiwa katika Biblia kufananisha uwezo wa Yehova. * Ono la mtume Yohana la kiti cha enzi cha Yehova laonyesha viumbe-hai wanne, na mmojawapo ana uso kama fahali. (Ufunuo 4:6, 7) Inaonekana kwamba mojawapo ya sifa kuu nne za Yehova zinazoonyeshwa na makerubi hao ni nguvu. Sifa nyinginezo ni upendo, hekima, na haki. Kwa kuwa nguvu ni sehemu muhimu sana ya utu wa Mungu, kufahamu vizuri nguvu zake na jinsi anavyozitumia kutatuvuta karibu zaidi naye na kutusaidia kuiga mfano wake kwa kutumia vizuri nguvu zetu.—Waefeso 5:1.

“Yehova wa Majeshi, Mwenye Nguvu”

7. Kwa nini tuna hakika kwamba wema utashinda uovu?

7 Katika Maandiko, Yehova anaitwa “Mungu Mweza-Yote,” mtajo unaotukumbusha kwamba hatupaswi kupuuza nguvu zake au kutilia shaka uwezo wake wa kushinda kabisa adui zake. (Mwanzo 17:1; Kutoka 6:3) Huenda mfumo mwovu wa Shetani ukaonekana kama umeimarika sana, lakini machoni pa Yehova “mataifa ni kama tone la maji katika ndoo, huhesabiwa kuwa kama mavumbi membamba katika mizani.” (Isaya 40:15) Kwa sababu Mungu ana nguvu hizo, hakuna shaka kwamba wema utashinda uovu. Wakati huu ambapo uovu umeenea, twaweza kupata faraja tukijua kwamba “Yehova wa majeshi, Mwenye Nguvu wa Israeli” ataondoa uovu milele.—Isaya 1:24, NW; Zaburi 37:9, 10.

8. Ni majeshi gani ya mbinguni yanayomtumikia Yehova, na ni jambo gani linaloonyesha nguvu zao?

8 Usemi “Yehova wa majeshi,” ambao umetajwa mara 285 katika Biblia (NW), unatukumbusha pia juu ya nguvu za Mungu. “Majeshi” yanayotajwa hapa ni viumbe-roho wanaomtumikia Yehova. (Zaburi 103:20, 21; 148:2) Katika usiku mmoja tu, mmoja wa malaika hao aliwaua wanajeshi 185,000 wa Ashuru ambao walikuwa wakitisha Yerusalemu. (2 Wafalme 19:35) Tukitambua nguvu za majeshi ya mbinguni ya Yehova, wapinzani hawatatutisha kwa urahisi. Nabii Elisha hakutishika walipozingirwa na kikosi kizima cha wanajeshi ambao walikuwa wakimtafuta kwa sababu, tofauti na mtumishi wake, yeye angeweza kuona kupitia imani kikosi kikubwa sana cha majeshi ya mbinguni kilichomwunga mkono.—2 Wafalme 6:15-17.

9. Kama Yesu, kwa nini tuwe na hakika katika ulinzi wa Mungu?

9 Vilevile, Yesu alijua kwamba anaungwa mkono na malaika alipokabili umati wa watu waliokuwa na mapanga na marungu katika bustani ya Gethsemane. Baada ya kumwambia Petro arudishe upanga wake mahali pake, Yesu alimwambia kwamba ikiwa lazima, anaweza kumwomba Baba yake “malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika.” (Mathayo 26:47, 52, 53) Sisi pia tukifahamu kwamba Mungu anaweza kutumia majeshi ya mbinguni, tutaitibari kabisa kwamba atatutegemeza. Mtume Paulo aliandika: “Basi, tutasema nini kuhusu mambo haya? Ikiwa Mungu yuko upande wetu, nani atakayekuwa dhidi yetu?”—Waroma 8:31.

10. Yehova hutumia nguvu zake kwa niaba ya akina nani?

10 Basi tuna sababu nyingi za kuitibari ulinzi wa Yehova. Sikuzote yeye hutumia nguvu zake kwa njia yenye kuleta manufaa na kwa kupatana na sifa zake nyinginezo—haki, hekima, na upendo. (Ayubu 37:23; Yeremia 10:12) Ingawa watu wenye uwezo huwakandamiza maskini na wanyenyekevu ili kujinufaisha kibinafsi, Yehova ‘humwinua mnyonge kutoka mavumbini’ na yeye ni “hodari wa kuokoa.” (Zaburi 113:5-7; Isaya 63:1) Kama alivyoelewa Maria, mama ya Yesu aliyekuwa mwenye kiasi na mpole, “Mwenye nguvu” hutumia nguvu zake bila ubinafsi kwa niaba ya wale wanaomhofu, akiwadhalilisha wenye kiburi na kuwainua wenye hali ya chini.—Luka 1:46-53.

Yehova Aonyesha Watumishi Wake Nguvu Zake

11. Waisraeli waliona uthibitisho gani wa nguvu za Mungu mwaka wa 1513 K.W.K.?

11 Yehova aliwaonyesha watumishi wake uweza wake katika pindi kadhaa. Mojawapo ya pindi kama hizo ilikuwa kwenye Mlima Sinai mwaka wa 1513 K.W.K. Katika mwaka huo tayari Waisraeli walikuwa wameona uthibitisho mkubwa sana wa nguvu za Mungu. Mapigo kumi mazito sana yalionyesha jinsi Yehova alivyokuwa na nguvu na jinsi miungu ya Misri ilivyokuwa bure. Punde tu baadaye, kule kuvuka Bahari Nyekundu na kuangamizwa kwa majeshi ya Farao kulithibitisha hata zaidi nguvu za Mungu. Miezi mitatu baadaye, chini ya Mlima Sinai, Yehova aliwaalika Waisraeli wawe ‘tunu kwake kuliko makabila yote ya watu.’ Waisraeli nao wakaahidi: “Hayo yote aliyoyasema BWANA tutayatenda.” (Kutoka 19:5, 8) Kisha, Yehova akadhihirisha wazi nguvu zake. Kulikuwa na ngurumo na radi, na sauti kubwa ya baragumu huku Mlima Sinai ukitoa moshi na kutetemeka. Watu waliokuwa wamesimama mbali kidogo waliogofywa. Lakini Musa akawaambia kwamba mambo hayo waliyoona yapasa kuwafundisha kumhofu Mungu, hofu ambayo ingewasukuma wamtii Mungu wao Yehova, aliye wa pekee na wa kweli na ambaye ni mweza-yote.—Kutoka 19:16-19; 20:18-20.

12, 13. Ni hali zipi zilizomfanya Eliya aache mgawo wake, lakini Yehova alimwimarishaje?

12 Karne kadhaa baadaye, wakati wa Eliya, Mungu alionyesha nguvu zake tena kwenye Mlima Sinai. Tayari nabii huyo alikuwa ameshuhudia nguvu za Mungu. Kwa miaka mitatu na nusu, Mungu ‘alizifunga mbingu zisiwe na mvua’ kwa sababu taifa la Israeli liliasi. (2 Mambo ya Nyakati 7:13) Katika ukame uliofuata, kunguru walimlisha Eliya katika kijito cha Kerithi, na baadaye unga kidogo na mafuta kidogo ya mjane mmoja zikaendelezwa kimuujiza ili kumlisha Eliya. Yehova hata alimpa Eliya nguvu za kumfufua mwana wa mjane huyo. Hatimaye, katika jaribu lenye kutokeza la Uungu kwenye Mlima Karmeli, moto ukatoka mbinguni na kuteketeza dhabihu ya Eliya. (1 Wafalme 17:4-24; 18:36-40) Hata hivyo, punde tu baadaye, Eliya akaogopa na kuvunjika moyo Yezebeli alipotisha kumwua. (1 Wafalme 19:1-4) Alitoroka nchi hiyo, akifikiri kwamba kazi yake ya unabii ilikuwa imekwisha. Ili kumfariji na kumwimarisha, kwa fadhili Yehova mwenyewe alimwonyesha Eliya nguvu zake.

13 Eliya alipokuwa amejificha katika pango, aliona wonyesho wenye kustaajabisha sana wa nguvu tatu ambazo Yehova hudhibiti: upepo mkali, tetemeko la ardhi, na hatimaye moto. Lakini Yehova alipozungumza na Eliya, alisema kwa ‘sauti ndogo ya utulivu.’ Yehova alimpa kazi zaidi ya kufanya akimwambia kwamba katika nchi hiyo kungali kuna waabudu 7,000 wa Yehova walio waaminifu. (1 Wafalme 19:9-18) Kama Eliya, tukivunjika moyo kwa sababu ya kukosa matokeo katika huduma yetu, tunaweza kumwomba Yehova atupe “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida”—nguvu iwezayo kutuimarisha kuendelea kuhubiri habari njema bila kuacha.—2 Wakorintho 4:7.

Nguvu za Yehova Huhakikisha Kwamba Ahadi Zake Zatimizwa

14. Jina la Yehova binafsi lamaanisha nini, na nguvu zake zahusianaje na jina lake?

14 Nguvu za Yehova pia zahusiana sana na jina lake na kutekelezwa kwa mapenzi yake. Jina la kipekee la Yehova, linalomaanisha “Yeye Husababisha Iwe,” laonyesha kwamba yeye hujisababisha kuwa Mtimizaji wa ahadi. Hakuna kitu chochote kile ama mtu yeyote yule awezaye kumzuia Mungu asitimize ahadi zake, hata kama wenye kutilia shaka wanaona kama ahadi hizo haziwezi kutimizwa. Ni kama Yesu alivyowaambia mitume wake pindi moja, “kwa Mungu mambo yote yawezekana.”—Mathayo 19:26.

15. Abrahamu na Sara walikumbushwaje kwamba hakuna neno lililo gumu la kumshinda Yehova?

15 Kwa mfano, pindi moja Yehova alimwahidi Abrahamu na Sara kwamba angefanya wazao wao kuwa taifa kubwa. Hata hivyo walikaa bila kupata mtoto kwa miaka mingi. Wote wawili walikuwa wazee sana Yehova alipowaambia kwamba ahadi ile ilikaribia kutimizwa na Sara akacheka. Malaika akajibu: “Kuna neno gani lililo gumu la kumshinda BWANA?” (Mwanzo 12:1-3; 17:4-8; 18:10-14) Karne nne baadaye, hatimaye Musa alipowakusanya wazao wa Abrahamu—sasa wakiwa taifa kubwa—kwenye Uwanda wa Moabu, aliwakumbusha kwamba Mungu alitimiza ahadi yake. Musa alisema: “Kwa sababu [Yehova] aliwapenda baba zenu, kwa sababu hiyo aliwachagua wazao wao baada yao, akakutoa katika Misri kwa kuwako pamoja nawe, kwa uweza wake mwingi, ili kufukuza mbele yako mataifa, walio wakubwa, wenye nguvu kukupita wewe, ili kukuingiza, na kukupa nchi yao iwe urithi, kama ilivyo leo.”—Kumbukumbu la Torati 4:37, 38.

16. Kwa nini Masadukayo walikosea kwa kukana kuwa hakuna ufufuo wa wafu?

16 Karne kadhaa baadaye, Yesu aliwakemea Masadukayo, ambao hawakuamini ufufuo. Kwa nini walikataa kuamini ahadi ya Mungu ya kwamba angewafufua wafu? Yesu aliwaambia: “Hamjui wala Maandiko wala nguvu ya Mungu.” (Mathayo 22:29) Maandiko hutuhakikishia kwamba ‘wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti ya Mwana wa binadamu na kutoka.’ (Yohana 5:27-29) Tukijua isemavyo Biblia juu ya ufufuo, uhakika wetu katika nguvu za Mungu utatusadikisha kwamba wafu watafufuliwa. Mungu ‘atameza mauti hata milele. BWANA amenena hayo.’—Isaya 25:8.

17. Ni katika siku gani katika wakati ujao ambapo itakuwa muhimu sana kuitibari Yehova kwa njia ya pekee?

17 Karibuni, wakati utafika ambapo kila mmoja wetu atahitaji kuitibari nguvu zenye kuokoa za Mungu katika njia ya pekee. Shetani Ibilisi ataanza kushambulia watu wa Mungu, ambao wataonekana kana kwamba hawana ulinzi. (Ezekieli 38:14-16) Kisha Mungu atadhihirisha nguvu zake nyingi kwa niaba yetu, na kila mtu atalazimika kujua ya kwamba yeye ni Yehova. (Ezekieli 38:21-23) Huu ndio wakati wa kujenga imani na uhakika katika Mungu Mweza-Yote ili tuwe imara katika pindi hiyo muhimu.

18. (a) Tunapata manufaa zipi tunapotafakari juu ya nguvu za Yehova? (b) Ni swali gani litakalozungumziwa katika makala ifuatayo?

18 Bila shaka, kuna sababu nyingi za kutafakari juu ya nguvu za Yehova. Tunapotafakari juu ya matendo yake, twasukumwa kwa unyenyekevu kumsifu Muumba wetu Mtukufu na kushukuru kwamba yeye hutumia nguvu zake katika njia yenye hekima na yenye upendo. Hatuwezi kutishika kamwe tukimtumaini Yehova wa majeshi. Imani yetu katika ahadi zake itakuwa imara. Lakini kumbuka kwamba tumeumbwa kwa mfano wa Mungu. Hivyo, hata sisi tuna nguvu—japo kwa kadiri kidogo. Tunaweza kumwigaje Muumba wetu katika njia ambayo tunatumia nguvu zetu? Jambo hilo litazungumziwa katika makala ifuatayo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Wengi wanaamini kwamba fueli zinazopatikana ardhini kama vile mafuta na makaa-mawe—ambazo ndizo hutegemewa sana na vituo vya umeme—hupata nishati kutoka kwenye jua.

^ fu. 4 Kwa kulinganisha, bomu la nyuklia lenye nguvu zaidi ambalo limewahi kulipuliwa katika majaribio lilikuwa na nguvu zinazotoshana na tani milioni 57 za TNT.

^ fu. 6 Yaelekea kwamba fahali wa mwitu anayetajwa katika Biblia ni auroch (Kilatini urus). Miaka elfu mbili iliyopita, wanyama hawa waliishi Gaul (ambayo sasa ni Ufaransa), na Juliasi Kaisari aliandika hivi juu yao: “Wanyama hao, uri, karibu watoshane na tembo, lakini tabia yao, rangi yao na umbo lao ni kama fahali. Wana nguvu nyingi sana, na wana mbio sana: hawamwachi mtu wala mnyama mara wanapowaona.”

Je, Unaweza Kujibu

• Uumbaji unashuhudiaje nguvu za Yehova?

• Yehova anaweza kutumia majeshi gani kuunga mkono watu wake?

• Ni zipi baadhi ya pindi ambazo Yehova alionyesha nguvu zake?

• Tuna uhakikisho gani kwamba Yehova atatimiza ahadi zake?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 10]

“Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi?”

[Hisani]

Photo by Malin, © IAC/RGO 1991

[Picha katika ukurasa wa 13]

Kutafakari juu ya maonyesho ya nguvu za Yehova hujenga imani katika ahadi zake