Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Maswali Matatu Ambayo Watu Wangependa Kumwuliza Mungu

Maswali Matatu Ambayo Watu Wangependa Kumwuliza Mungu

SUSAN alianza kuuliza maswali kuhusu Mungu alipokuwa na umri wa miaka saba. Wakati huo, rafiki yake anayeitwa Al, aliyekuwa na umri wa miaka tisa alilazwa hospitalini baada ya kuugua polio na kuwekwa kwenye chombo cha kumsaidia kupumua. Aliandika jambo hilo katika gazeti la The New York Times la Januari 6, 2013.

Baada ya kumtembelea Al hospitalini, Susan alimwuliza hivi mama yake: “Mungu anawezaje kumtendea hivi mtoto mdogo kama huyu?”

Mama yake alimjibu hivi: “Kasisi husema Mungu ana sababu za kufanya hivyo, ingawa sizijui.”

Miaka miwili baadaye, katika mwaka wa 1954, Jonas Salk aligundua kinga ya polio, na mama yake Susan alidai kwamba Mungu ndiye aliyemsaidia kugundua.

Susan akasema: “Lakini Mungu angewasaidia madaktari mapema ili Al asiwekwe kwenye chombo cha kumsaidia kupumua.”

Susan alieleza hivi mwishoni mwa simulizi lake: “[Al] alikufa miaka nane baadaye, na kufikia wakati huo niliamini kabisa kwamba hakuna Mungu.”

Kama Susan, watu wengi waliopatwa na matatizo makubwa au kuyashuhudia, wameshindwa kupata majibu yenye kuridhisha ya maswali yao kumhusu Mungu. Baadhi yao hawaamini kuna Mungu. Huenda wengine hawakatai kabisa kwamba Mungu yupo, lakini wana mashaka.

Si kwamba watu wanaoamini hakuna Mungu au walio na mashaka ikiwa yupo hawajui kuhusu dini. Mara nyingi mambo waliyojionea katika dini yamewafanya waache kumwamini Mungu. Huenda wanahisi kuwa dini zimeshindwa kujibu maswali muhimu maishani. Ni maswali gani hayo? Inashangaza kwamba ni maswali yaleyale wanayouliza watu wanaodai wanamwamini Mungu. Fikiria maswali matatu ambayo watu wangependa kumwuliza Mungu, na majibu ambayo Biblia inatoa.

1 “KWA NINI UNARUHUSU WATU WATESEKE?”

Kwa nini watu huuliza swali hilo?

Watu wengi wanasema, ‘Mungu mwenye upendo angezuia majanga yanayotokea maishani.’

JAMBO LA KUFIKIRIA: Huenda tukaona mazoea na desturi za watu kutoka tamaduni nyingine kuwa za ajabu—au hata zenye kuchukiza. Huenda tukaelewa vibaya mambo wanayofanya. Kwa mfano, katika tamaduni fulani watu huona kwamba kutazamana machoni ni ishara ya unyofu; lakini wengine huona hilo kuwa ukosefu wa adabu. Hata hivyo, haimaniishi kwamba wanakosea, badala yake tunahitaji kuwajua vizuri.

Je, hali kama hiyo inaweza kutokea tunapojitahidi kumjua Mungu? Watu wengi wanaamini mateso yanathibitisha kwamba hakuna Mungu. Hata hivyo, wale wanaojua sababu inayomfanya Mungu aruhusu mateso, wana hakika kwamba yuko.

BIBLIA INASEMA NINI? Mawazo na njia za Mungu ni tofauti na zetu. (Isaya 55:8, 9) Kwa sababu hiyo, huenda mwanzoni tukashangazwa na matendo yake na sababu zinazomfanya asichukue hatua haraka.

Hata hivyo, Biblia inapinga maoni ya watu kwamba kazi za Mungu hazieleweki. Badala yake inatutia moyo kujifunza mengi kumhusu Mungu, na inatusaidia kuelewa kwa nini ameacha mambo fulani yatukie. * Tunaweza kumkaribia.—Yakobo 4:8.

2 “KWA NINI KUNA UNAFIKI MWINGI KATIKA DINI?”

Kwa nini watu huuliza swali hilo?

Huenda watu fulani wakadai kwamba, ‘ikiwa Mungu anapenda unyofu, kusingekuwa na unafiki mwingi katika dini.’

JAMBO LA KUFIKIRIA: Wazia mtoto anayekataa malezi mazuri ya baba yake na kuamua kuondoka nyumbani ili akaishi maisha mapotovu. Ingawa baba yake hapendi jambo hilo, anamruhusu mwana wake aondoke. Je, wale watakaokutana na mwana huyo watakuwa sahihi wakisema ana baba asiyefaa, au hata kwamba hana baba? Hapana! Vivyo hivyo, unafiki katika dini unathibitisha kwamba Mungu huruhusu watu wajifanyie maamuzi yao maishani.

BIBLIA INASEMA NINI? Mungu anachukia unafiki ulio katika dini. (Yeremia 7:29-31; 32:35) Wakati huohuo, amewapa watu uhuru wa kuchagua. Wengi wanaodai kumwamini Mungu wanafuata mafundisho ya kidini yaliyoanzishwa na wanadamu na kujiwekea viwango vyao vya maadili.—Mathayo 15:7-9.

Hata hivyo, Mungu anakubali dini isiyo na unafiki. * “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Upendo huo uwe “bila unafiki.” (Waroma 12:9) Dini nyingi zimeshindwa kufanya hivyo. Kwa mfano, mauaji ya kimbari yalipotokea nchini Rwanda mwaka wa 1994, wanadini wengi waliwaua waumini wenzao kwa sababu tu walikuwa watu wa kabila tofauti. Kinyume na hilo, Mashahidi wa Yehova hawakujihusisha katika mauaji hayo, na wengi wao waliwalinda waamini wenzao na watu wengine hata ingawa kufanya hivyo kulihatarisha maisha yao. Jambo hilo linathibitisha kwamba si dini zote zenye unafiki.

3 “NI NINI KUSUDI LA MAISHA?”

Kwa nini watu huuliza swali hilo?

Wengine wanaweza kujiuliza hivi: ‘Kwa nini wanadamu wanaishi kwa miaka 80 au 90 hivi na hatimaye kufa? Ni nini kusudi la maisha hayo?’

JAMBO LA KUFIKIRIA: Watu wengi wasiomwamini Mungu wanatambua kwamba utata na utaratibu ulio katika uumbaji haukujitokeza wenyewe. Wanatambua kwamba mwezi, sayari yetu, na sayari nyingine zimewekwa katika njia inayofaa ili kutegemeza uhai duniani. Wanasema kuwa sheria na utaratibu wa asili unaoongoza ulimwengu uko katika kiwango kinachofaa hivi kwamba badiliko lolote likitokea linaweza kuhatarisha uhai wa viumbe duniani.

BIBLIA INASEMA NINI? Ingawa watu wengi huona kuwa maisha yetu mafupi yanathibitisha hakuna Mungu, uumbaji unatupa sababu ya msingi ya kuamini kuna Muumba. (Waroma 1:20) Aliumba vitu hivi akiwa na kusudi, na sababu ya kuwepo kwetu inategemea kusudi lake. Mungu aliwaumba wanadamu waishi milele duniani, na bado anakusudia hivyo.—Zaburi 37:11, 29; Isaya 55:11.

Kujua kwamba Mungu yupo na baadhi ya sifa zake zinazoonekana kupitia uumbaji, si njia ambayo Mungu alikusudia tutambue kusudi lake. Tunahitaji kuwasiliana na Mungu ili tujue kusudi lake na pia kusudi la maisha. Anatumia Biblia kuwasiliana nasi kwa njia rahisi. * Mashahidi wa Yehova wanakutia moyo uisome ili upate majibu.

^ fu. 17 Ili ujue sababu inayomfanya Mungu aruhusu watu wateseke, soma sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia kinapatikana kwenye www.jw.org/sw.

^ fu. 23 Kwa habari zaidi, soma sura ya 15 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia kinapatikana kwenye www.jw.org/sw.

^ fu. 29 Kwa habari zaidi, soma sura ya 3 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia kinapatikana kwenye www.jw.org/sw.