Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uaminifu Katika Ndoa Unamaanisha Nini Hasa?

Uaminifu Katika Ndoa Unamaanisha Nini Hasa?

Maoni ya Biblia

Uaminifu Katika Ndoa Unamaanisha Nini Hasa?

Watu wengi hutazamia wenzi wao wa ndoa wawe waaminifu kwa kutofanya ngono na mtu mwingine. Maoni hayo kuhusu uaminifu katika ndoa yanapatana na ya Biblia, inayosema hivi: “Ndoa na iheshimiwe kati ya wote, na kitanda cha ndoa kiwe bila unajisi.”—Waebrania 13:4.

JE, UAMINIFU katika ndoa unamaanisha tu kutofanya ngono na mtu mwingine nje ya ndoa? Vipi kuhusu kuwazia kufanya ngono na mtu mwingine isipokuwa mwenzi wako? Je, kuwa na urafiki wa karibu sana na mtu wa jinsia tofauti ni “ukosefu wa uaminifu”?

Je, Kuwazia Kufanya Ngono Kuna Madhara?

Biblia inaonyesha kuwa ngono ni jambo la kiasili na linalofaa katika ndoa, chanzo cha shangwe na uradhi kwa wenzi wote wawili. (Methali 5:18, 19) Lakini wataalamu wengi wa kisasa wanaamini kwamba ni jambo la kawaida, na hata linalofaa, kwa watu waliofunga ndoa kuwazia kufanya ngono na watu wengine. Lakini je, mawazo hayo yana madhara yoyote mtu asipotenda kupatana nayo?

Kwa kawaida mtu anayewazia kuhusu ngono anafikiria jinsi ya kujifurahisha yeye mwenyewe tu. Tabia hiyo ya ubinafsi ni kinyume na shauri la Biblia kwa watu waliofunga ndoa. Neno la Mungu linasema hivi kuhusu mahusiano ya ngono: “Mke hana mamlaka juu ya mwili wake mwenyewe, bali mume wake anayo; vivyo hivyo, pia, mume hana mamlaka juu ya mwili wake mwenyewe, bali mke wake anayo.” (1 Wakorintho 7:4) Kufuata shauri la Biblia kunazuia ngono isiwe njia ya kutosheleza tamaa za kibinafsi ambazo hutokana na kuwazia kuhusu ngono. Kwa sababu hiyo, wenzi wote wawili hupata furaha nyingi zaidi.—Matendo 20:35; Wafilipi 2:4.

Kuwazia kufanya ngono nje ya ndoa ni kama kujitayarisha kufanya jambo ambalo litamuumiza sana kihisia mwenzi yule mwingine. Je, kuwa na mawazo ya ngono kunaweza kuongeza uwezekano wa mtu kufanya uzinzi? Jibu ni ndiyo. Biblia inaonyesha uhusiano uliopo kati ya mawazo na matendo: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.”—Yakobo 1:14, 15.

Yesu alisema: “Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” (Mathayo 5:28) Kwa kukataa kukazia fikira mawazo ya uzinzi, ‘unalinda moyo wako’ na ndoa yako.—Methali 4:23.

Kwa Nini Uwe Mwaminifu Kihisia?

Ili uwe na ndoa yenye mafanikio unahitaji “kujitoa kikamili” kwa mwenzi wako. (Wimbo wa Sulemani 8:6; Methali 5:15-18) Hilo linamaanisha nini? Ingawa ni jambo la kawaida kuwa na marafiki wa kiume na wa kike nje ya ndoa, fikira, hisia, na wakati wako zinapaswa kuelekezwa kwa mwenzi wako kwanza. Uhusiano wowote unaochukua kile ambacho kwa haki ni cha mwenzi wako na kupewa mtu mwingine ni aina fulani ya “ukosefu wa uaminifu,” hata ikiwa tendo la ngono halikufanywa. *

Uhusiano kama huo unaweza kuanza kwa njia gani? Mtu fulani wa jinsia tofauti anaweza kuonekana kuwa mwenye kuvutia zaidi au mwenye huruma zaidi kuliko mwenzi wako. Kutumia wakati na mtu kama huyo kazini au katika vikusanyiko vya kirafiki kunaweza kuwafanya muanze kuzungumzia mambo ya kibinafsi, kutia ndani matatizo au magumu katika ndoa yako. Unaweza kuanza kumtegemea mtu huyo kihisia. Kuwasiliana na mtu huyo moja kwa moja, kupita simu, au kwenye Intaneti kunaweza kufanya ufunue mambo ya siri. Kwa kufaa wenzi wa ndoa hutazamia kwamba kuna mambo ambayo hayapaswi kuzungumziwa na mtu mwingine na kwamba “mazungumzo ya siri” hayatafunuliwa.—Methali 25:9.

Jihadhari usijitetee kwamba huna hisia zozote za kimahaba ingawa kwa kweli huenda ukawa unazo! “Moyo ni wenye hila,” inasema Yeremia 17:9. Ikiwa una uhusiano wa karibu na mtu wa jinsia tofauti, jiulize hivi: ‘Je, mimi hujitetea au kuficha uhusiano huo? Je, ingekuwa sawa ikiwa mwenzi wangu angesikia mazungumzo yetu? Mimi ningehisi jinsi gani ikiwa mwenzi wangu angekuwa na urafiki kama huo?’—Mathayo 7:12.

Kuwa na uhusiano usiofaa kunaweza kuharibu ndoa yako, kwa kuwa mtu anapokuza hisia za karibu kuelekea mtu mwingine hilo linaweza kuongoza kwenye uhusiano wa ngono. Kama Yesu alivyoonya, ‘uzinzi hutoka moyoni.’ (Mathayo 15:19) Hata hivyo, hata ikiwa mtu hatafanya uzinzi, inaweza kuwa vigumu kurekebisha madhara yanayosababishwa na kutoaminiwa na mwenzi wako. Mwanamke mmoja anayeitwa Karen * alisema: “Nilipogundua kwamba Mark alikuwa akizungumza kwa siri kwenye simu mara kadhaa na mwanamke mwingine, niliumia sana moyoni. Ilikuwa vigumu sana kuamini kwamba hawajawahi kufanya ngono na mwanamke huyo. Sidhani nitawahi kumwamini tena.”

Usiwe na urafiki wa karibu kupita kiasi na watu wa jinsia tofauti. Usijitetee au kupuuza hisia zisizofaa. Ukihisi kwamba uhusiano fulani unahatarisha ndoa yako, chukua hatua za kuweka mipaka au kukatiza uhusiano huo. Biblia inasema: “Mtu mwerevu ni yule ambaye ameona msiba na kujificha.”—Methali 22:3.

Linda Ndoa Yako

Muumba wetu alikusudia kwamba ndoa iwe ndio uhusiano wa karibu zaidi kati ya wanadamu wawili. Alisema kwamba mume na mke “watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Kuwa mwili mmoja kunahusisha mengi zaidi ya uhusiano wa kingono. Kunatia ndani kuwa na uhusiano wa karibu kihisia ambao unaimarishwa na kutumainiana, kuheshimiana, na kutokuwa na ubinafsi. (Methali 31:11; Malaki 2:14, 15; Waefeso 5:28, 33) Kufuata kanuni hizo kutasaidia kulinda ndoa yako isipatwe na madhara ya kutokuwa na uaminifu kiakili na kihisia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Hata hivyo, ni jambo muhimu kutambua kwamba msingi pekee wa Kimaandiko wa talaka ni ngono nje ya ndoa.—Mathayo 19:9.

^ fu. 14 Majina yamebadilishwa.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Je, mawazo ya ngono yanaweza kumfanya mtu afanye ngono?—Yakobo 1:14, 15.

▪ Je, kuwa na urafiki wa karibu na mtu wa jinsia tofauti kunaweza kuhatarisha ndoa yako?—Yeremia 17:9; Mathayo 15:19.

▪ Unaweza kuimarisha uhusiano wako wa ndoa jinsi gani?—1 Wakorintho 7:4; 13:8; Waefeso 5:28, 33.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

“Kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.”—Mathayo 5:28