Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kusoma Biblia?

Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kusoma Biblia?

Vijana Huuliza

Ninaweza Kufanya Nini ili Nifurahie Kusoma Biblia?

Wewe husoma Biblia mara nyingi kadiri gani? (Tia alama sanduku moja)

□ Kila siku

□ Kila juma

□ Wakati mwingine ․․․․․

Kamilisha sentensi inayofuata.

Wakati mimi sifurahii kusoma Biblia, kwa kawaida ni kwa sababu . . . (Tia alama kila sanduku linalokuhusu)

□ Nimechoshwa

□ Nimechanganyikiwa

□ Nimekengeushwa

□ Sababu nyingine ․․․․․

JE, WEWE huchoshwa kusoma Biblia? Ikiwa ndivyo, basi huenda ukakubaliana na Will mwenye umri wa miaka 18 aliyesema hivi, “Biblia inaweza kuchosha.” Hata hivyo, aliongeza hivi, “Inakuwa hivyo ikiwa tu hujui jinsi ya kuisoma.”

Kwa nini ujifunze jinsi ya kusoma Biblia? Je, ungependa kujua jinsi ya

kufanya maamuzi mazuri?

kuwa na marafiki wa kweli?

kukabiliana na mfadhaiko?

Biblia ina hazina za hekima kuhusu habari hizo na nyingine nyingi. Kwa kweli, jitihada zinahitajika ili kupata hazina hizo. Ni kama tu jitihada zinazohitajika kupata hazina halisi: Kadiri unavyojitahidi zaidi ndivyo unavyofurahia zaidi matokeo unayopata.—Methali 2:1-6.

Unaweza kupata jinsi gani hazina zilizo katika Biblia? Sanduku linaloweza kukatwa lililo upande wa kulia lina madokezo ya jinsi ya kusoma Biblia na kwenye upande wa nyuma kuna utaratibu unaoweza kufuata unapoisoma. Pia, jaribu kufuata mapendekezo yaliyo kwenye kurasa zinazofuata yanayokupendeza.

Ikiwa unaweza kutumia Intaneti, unaweza kusoma Biblia kwenye Tovuti ya www.watchtower.org

MAMBO YA KUFIKIRIA

Imesemwa kwamba matokeo unayopata kwa kufanya jambo fulani yanategemea jitihada unazotumia.

▪ Hilo linahusiana jinsi gani na kusoma Biblia?

▪ Unaweza kusoma Biblia wakati gani?

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 23]

JINSI YA KUSOMA BIBLIA

Kabla ya kusoma . . .

▪ Hakikisha kwamba umeketi mahali patulivu ili uweze kukaza fikira.

▪ Sali ili uelewe.

Unaposoma . . .

▪ Tumia ramani na picha za masimulizi ya Biblia ili uweze kupiga picha akilini matukio unayosoma.

▪ Chunguza muktadha na uchanganue mambo.

▪ Chunguza maelezo ya chini na marejeo ya pambizoni.

▪ Jiulize maswali kama haya:

MAMBO HAKIKA: Jambo hilo lilitukia wakati gani? Ni nani aliyesema maneno hayo? Maneno hayo yalielekezwa kwa nani?

MAANA: Ninaweza kumweleza mtu mwingine habari hii jinsi gani?

SOMO: Kwa nini Yehova Mungu alitia simulizi hili katika Neno lake? Linafunua nini kuhusu utu wa Mungu au njia yake ya kutenda? Ni masomo gani ninayoweza kutumia maishani?

Baada ya kusoma . . .

▪ Fanya utafiti zaidi. Tumia vichapo vya Mashahidi wa Yehova, kama vile Insight on the Scriptures na “Kila Andiko Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa.”

▪ Sali tena. Mweleze Yehova yale ambayo umejifunza na jinsi unavyopanga kuyatumia. Mshukuru kwa Neno lake, Biblia.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 24]

UTAFUATA UTARATIBU GANI UNAPOSOMA BIBLIA?

 Unaweza . . .

□ Kusoma vitabu vya Biblia kulingana na jinsi vinavyofuatana katika Biblia.

□ Kusoma vitabu kulingana na wakati vilipoandikwa au kulingana na wakati ambapo matukio yalitokea.

□ Kusoma sehemu tofauti ya Maandiko kila siku.

Jumatatu (Siku ya 1): Historia yenye kusisimua (Mwanzo hadi Esta)

Jumanne (Siku ya 2): Maisha na mafundisho ya Yesu (Mathayo hadi Yohana)

Jumatano (Siku ya 3): Kutaniko la Kikristo la kwanza (Matendo)

Alhamisi (Siku ya 4): Unabii na mwongozo kuhusu maadili (Isaya hadi Malaki, Ufunuo)

Ijumaa (Siku ya 5): Mashairi na nyimbo zenye kusisimua (Ayubu, Zaburi, Wimbo wa Sulemani)

Jumamosi (Siku ya Posho): Mashauri yenye hekima kuhusu maisha (Methali, Mhubiri)

Jumapili (Siku ya Yenga): Barua kwa makutaniko (Waroma hadi Yuda)

Hata iwe utachagua utaratibu gani wa kusoma, hakikisha unajua mahali ambapo umefika! Weka alama hii kando ya kila sura baada ya kumaliza kuisoma, au uwe na njia fulani ya kuandika sura ambazo umesoma.

Kata kisanduku hiki na ukiweke katika Biblia yako!

[Sanduku/Mchoro katika ukurasa wa 24]

FANYA USOMAJI UWE HALISI!

Tafuta njia ya kufanya yale unayosoma yapendeze. Kwa mfano:

□ Tumia orodha ya majina ili kufanyiza chati ya majina ya ukoo.

□ Chora mistari inayounganisha mawazo. Kwa mfano, unaposoma kuhusu mtu mwaminifu, chora mstari unaounganisha sifa na matendo ya mtu huyo na baraka alizopokea.—Methali 28:20.

[Mchoro]

Rafiki ya Mungu

Utii

Uaminifu

↑ ↑

Abrahamu

□ Chora picha ili kueleza simulizi.

□ Chora picha kadhaa, kueleza mfuatano wa matukio. Eleza ni nini kinachotendeka katika kila picha.

□ Jenga muundo mdogo wa kitu fulani kama vile, safina ya Noa.—Kwa mfano, ona gazeti Amkeni! la Januari 2007, ukurasa wa 22.

Soma kwa sauti ukiwa pamoja na marafiki au watu wa familia. Pendekezo: Mtu mmoja anaweza kusoma simulizi na wengine wanaweza kugawiwa kusoma sehemu za watu mbalimbali katika simulizi hilo.

□ Chagua simulizi na uliripoti kama mtangazaji wa habari. Tangaza tukio hilo kwa njia mbalimbali kutia ndani “kuwahoji” wahusika wakuu na mashahidi walioshuhudia tukio hilo.

□ Chagua tukio ambalo mhusika alifanya uamuzi mbaya na uwazie matokeo yangekuwa nini ikiwa angefanya uamuzi mzuri! Kwa mfano, fikiria jinsi Petro alivyomkana Yesu. (Marko 14:66-72) Petro angeweza kutenda kwa njia tofauti jinsi gani katika hali hiyo ngumu?

□ Tazama au sikiliza drama za Biblia zilizorekodiwa.

Andika drama yako mwenyewe. Tia ndani mambo unayojifunza kutokana na simulizi hilo.—Waroma 15:4.

WAZO: Igizeni drama hiyo pamoja na kikundi kidogo cha marafiki.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

ILI UCHOCHEWE

▪ Jiwekee mradi! Andika hapa chini tarehe ambayo ungependa kuanza programu yako ya kusoma Biblia.

․․․․․

▪ Chagua sehemu ya Biblia ambayo inakupendeza. (Ona sanduku  “Utafuata Utaratibu Gani Unaposoma Biblia?”) Kisha uandike hapa chini sehemu ya Biblia ambayo utasoma kwanza.

․․․․․

▪ Anza kwa kusoma kwa kipindi kifupi cha wakati. Hata dakika 15 za usomaji wa Biblia ni bora kuliko kukosa kusoma kabisa. Andika hapa chini umetenga kutumia kiasi gani cha wakati kwa utendaji huo.

․․․․․

Dokezo: Uwe na Biblia unayotumia tu kwa ajili ya funzo lako la kibinafsi. Andika mambo makuu ndani yake. Tia alama mistari iliyokugusa moyo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 25]

VIJANA WENZAKO WANASEMA NINI?

“Mimi hujaribu kusoma sehemu fulani ndogo ya Biblia kila usiku kabla ya kulala. Hilo hunipa jambo zuri la kufikiria ninapoenda kulala.”—Megan.

“Mimi hukazia fikira zangu kwenye mstari mmoja kwa dakika 15. Ninasoma maelezo yote ya chini, ninachunguza marejeo ya pambizoni, na kufanya utafiti zaidi. Nyakati nyingine simalizi kufanya utafiti wa mstari mmoja, lakini mimi hufaidika sana kwa kusoma kwa njia hiyo!”—Corey.

“Wakati mmoja nilisoma Biblia yote kwa miezi 10. Kwa kufanya hivyo niliona jinsi sehemu mbalimbali za Biblia zinavyopatana kwa njia ambayo sikuwa nimewahi kutambua hapo awali.”—John.

[Sanduku katika ukurasa wa 25]

CHAGUA!

Chagua tukio. Biblia ina masimulizi mengi ya kweli yenye kusisimua. Chagua simulizi linalokupendeza na ulisome kuanzia mwanzo hadi mwisho.

Dokezo: Kwa madokezo ya jinsi ambavyo unaweza kujifunza mambo mengi kutokana na simulizi, ona ukurasa wa 292 wa kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Chagua kitabu cha Injili. Soma Mathayo (Injili ya kwanza kuandikwa), Marko (Injili ambayo inasimulia matukio mengi sana yenye kusisimua), Luka (inakazia hasa sala na wanawake), au Yohana (inataja mambo machache sana ambayo yametajwa katika Injili zile nyingine).

Dokezo: Kabla hujaanza kusoma, chunguza kwa ufupi habari kuhusu kitabu hicho cha Biblia na mwandikaji wake ili uelewe ni kwa nini Injili hiyo ni tofauti na zile nyingine.

Chagua zaburi fulani. Kwa mfano:

Ikiwa unajihisi mpweke na huna marafiki, soma Zaburi ya 142.

Ikiwa unajihisi umevunjika moyo kwa sababu ya udhaifu wako, soma Zaburi ya 51.

Ikiwa unatilia shaka umuhimu wa viwango vya Mungu, soma Zaburi ya 73.

Dokezo: Ingefaa uweke orodha ya zaburi ulizosoma ambazo zilikutia moyo.

[Sanduku katika ukurasa wa 26]

CHIMBA ZAIDI

Fikiria muktadha. Chunguza wakati, mahali, na hali zilizokuwapo simulizi unalosoma lilipoandikwa.

Mfano: Soma Ezekieli 14:14. Danieli alikuwa na miaka mingapi hivi Yehova alipomtaja kuwa mfano mzuri pamoja na Noa na Ayubu?

Dokezo: Ezekieli sura ya 14 liliandikwa miaka mitano tu baada ya Danieli kupelekwa utumwani Babiloni na huenda alikuwa kijana.

Hazina iliyofichwa: Je, Danieli alikuwa mchanga sana hivi kwamba Yehova hangeona uaminifu wake? Alifanya maamuzi gani mazuri yaliyomletea baraka? (Danieli 1:8-17) Mfano wa Danieli unaweza kukusaidia jinsi gani kufanya maamuzi mazuri?

Changanua mambo. Nyakati nyingine neno moja au mawili ni muhimu.

Mfano: Linganisha Mathayo 28:7 na Marko 16:7. Kwa nini Marko alitia ndani habari kwamba Yesu angewatokea wanafunzi wake “na Petro”?

Dokezo: Marko hakujionea matukio hayo; yaelekea alipata habari hiyo kutoka kwa Petro.

Hazina iliyofichwa: Kwa nini Petro alitiwa moyo kusikia kwamba Yesu alitaka kumwona tena? (Marko 14:66-72) Yesu alionyesha kwa njia gani kwamba yeye alikuwa rafiki wa kweli wa Petro? Unaweza kumwiga Yesu jinsi gani na hivyo uwe rafiki wa kweli?

Fanya utafiti zaidi. Chunguza vichapo vya Biblia ili upate maelezo zaidi.

Mfano: Soma Mathayo 2:7-15. Wanajimu walimtembelea Yesu lini?

Dokezo: Ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 2008, ukurasa wa 31, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Hazina iliyofichwa: Yaelekea Yehova aliandalia familia ya Yosefu, baba mlezi wa Yesu, kwa njia gani walipokuwa Misri? Kumtegemea Mungu kunaweza kukusaidia jinsi gani kukabiliana na hali zenye kufadhaisha?—Mathayo 6:33, 34.