Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Vibaya Kunywa Kileo?

Je, Ni Vibaya Kunywa Kileo?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Vibaya Kunywa Kileo?

“DIVAI ni mdhihaki, kileo husababisha msukosuko, na kila mtu anayepotezwa nacho hana hekima.” Je, andiko hilo la Biblia linalopatikana katika Methali 20:1, linaonyesha kwamba ni vibaya kunywa kileo? Wengine wanafikiri hivyo. Ili kuthibitisha hilo, wao hutaja masimulizi ya Biblia ambapo watu walifanya mambo mabaya kwa sababu ya matumizi mabaya ya kileo.—Mwanzo 9:20-25.

Kisha kuna matokeo mabaya ya kutumia kileo kupita kiasi, yaani, magonjwa mbalimbali kama vile kunyauka kwa ini, aksidenti mbaya, kufilisika, kutesa familia, na kutokeza madhara kwa kitoto ambacho hakijazaliwa. Huenda kwa sababu ya madhara hayo, “dini nyingi zilifundisha kwamba kunywa kileo kunapingana na kanuni za maadili,” kinasema kitabu The World Book Encyclopedia. Lakini je, kunywa kileo kunapingana na kanuni za maadili? Je, Biblia inakataza kunywa aina yoyote au kiasi chochote cha kileo?

Biblia Inasema Nini?

Biblia inaonya kuhusu matokeo mabaya ya kunywa kileo kupita kiasi. Waefeso 5:18 inasema: “Pia, msiwe mkilewa divai, ambayo ina upotovu ndani yake.” Vilevile, Methali 23:20, 21 inahimiza hivi: “Usiwe kati ya watu wanaokunywa divai mno, kati ya watu wanaokula nyama kwa ulafi. Kwa maana mlevi na mlafi watakuwa maskini.” Na Isaya 5:11 inasema: “Ole wao wanaoamka asubuhi na mapema ili watafute tu kileo, wanaokawia mpaka giza la jioni sana hivi kwamba divai inawawasha!”

Biblia hueleza pia kuhusu furaha na manufaa ya kunywa kwa kiasi. Kwa mfano, Zaburi 104:15 inasema kwamba kati ya zawadi nyingi ambazo Mungu hutoa moja ni “divai ambayo hufanya moyo wa mwanadamu anayeweza kufa ushangilie.” Na Mhubiri 9:7 inasema kwamba thawabu ya kufanya kazi nzuri ni ‘kula chakula chako kwa kushangilia na kunywa divai yako kwa moyo mchangamfu.’ Akijua faida za kitiba za kunywa divai, Paulo alimwambia Timotheo ‘asiendelee kunywa maji, bali atumie divai kidogo kwa ajili ya tumbo lake na ugonjwa wake wa mara kwa mara.’ (1 Timotheo 5:23) Vilevile, Biblia inaonyesha uwezo wa kileo wa kumsaidia mtu kuvumilia matatizo.—Methali 31:6, 7.

Ni wazi kwamba Biblia haikatazi kunywa kileo. Hata hivyo, inashutumu kunywa kileo kupita kiasi na ulevi. Hivyo, Paulo aliwahimiza waangalizi Wakristo, watumishi wa huduma, na wanawake wenye umri mkubwa hawapaswi “kunywa divai nyingi,” na alimwambia Timotheo anywe “divai kidogo.” (1 Timotheo 3:2, 3, 8; Tito 2:2, 3) Wakristo wote wanakumbushwa kwamba “walevi . . . hawataurithi ufalme wa Mungu.”—1 Wakorintho 6:9, 10.

Kumbuka kwamba Biblia inahusianisha ulevi na ulafi, na kuonyesha kwamba mambo yote mawili yanapaswa kuepukwa. (Kumbukumbu la Torati 21:20) Ikiwa mwongozo huo unamaanisha kwamba hatupaswi kunywa kileo kabisa, je, haingemaanisha kwamba kula chakula ni vibaya pia? Badala ya hivyo, kunywa au kula kupita kiasi ndiko kunakokatazwa na Biblia bali si kula au kunywa kwa kiasi.

Yesu Alifanya Nini?

Mtume Petro anasema kwamba Kristo aliacha ‘kielelezo ili tufuate hatua zake kwa ukaribu. Yeye hakufanya dhambi.’ (1 Petro 2:21, 22) Kwa hiyo, Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu kileo? Muujiza wake wa kwanza ulikuwa ule wa kugeuza maji kuwa divai. Yesu aligeuza maji kuwa divai ya aina gani? “Msimamizi wa karamu” alimpongeza bwana-arusi kwa sababu ya divai hiyo iliyotokezwa kimuujiza. Alisema: “Wengine wote hutoa divai nzuri kwanza, na ile hafifu wakati ambapo watu wameingiwa na kileo. Wewe umehifadhi divai nzuri mpaka sasa.”—Yohana 2:9, 10.

Kunywa divai kulikuwa sehemu ya sherehe ya Pasaka, naye Yesu alitumia divai alipoanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana. Akiwapa wanafunzi wake kikombe cha divai, aliwaambia hivi: “Kinyweeni, ninyi nyote.” Akijua kwamba alikuwa karibu kufa, aliongeza hivi: “Tangu sasa sitakunywa kamwe divai yoyote ya mzabibu mpaka siku ile nitakapokunywa ikiwa mpya, pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.” (Mathayo 26:27, 29) Naam, watu walijua kwamba Yesu alikunywa divai.—Luka 7:34.

Tunapaswa Kufanya Nini?

Ingawa Biblia haikatazi kunywa kileo, hilo halimaanishi kwamba ni lazima tufanye hivyo. Kuna sababu nyingi za kuepuka kunywa. Kwa mfano, mtu ambaye zamani alikuwa mlevi anajua hatari ya kunywa pombe hata kidogo tu. Mwanamke mjamzito anaweza kuepuka kunywa kwa sababu ya kuogopa kudhuru kitoto chake. Na kwa sababu dereva anajua kwamba kileo hudhoofisha uwezo wa kuamua na utendaji wa ubongo, ataepuka kufanya jambo lolote ambalo litahatarisha maisha yake au ya wengine.

Mkristo hangependa kumkwaza yeyote ambaye dhamiri yake inashutumu kunywa kileo. (Waroma 14:21) Ataepuka kunywa kileo anaposhiriki katika utumishi wa shambani. Ni jambo linalostahili kufikiriwa kwamba katika Sheria ya Mungu kwa Israeli la kale, makuhani hawakuruhusiwa ‘kunywa divai wala kileo’ walipokuwa wakifanya utumishi rasmi. (Mambo ya Walawi 10:9) Pia, katika nchi ambako hairuhusiwi au kuna masharti ya kunywa kileo, Mkristo anapaswa kutii sheria.—Waroma 13:1.

Ingawa ni uamuzi wa kibinafsi ikiwa mtu atakunywa au hatakunywa, au ni kiasi gani atakunywa, Biblia inapendekeza kufanya hivyo kwa kiasi. Inasema: “Kama mnakula au mnakunywa au mnafanya jambo lingine lolote, fanyeni mambo yote kwa utukufu wa Mungu.”—1 Wakorintho 10:31.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Ni onyo gani linalotajwa katika Maandiko kuhusu kunywa kileo?—1 Wakorintho 6:9, 10.

▪ Je, Yesu Kristo alikunywa kileo?—Luka 7:34.

▪ Ni nini huwaongoza Wakristo wa kweli kuhusu mambo ya kula na kunywa?—1 Wakorintho 10:31.