Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi

Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi

Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi

WEWE ungesema ni nani aliyekuwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi? Je, ni Noa ambaye aliokoka gharika na akawa babu ya kila mtu aliye hai leo? (Mwanzo 7:1, 21, 22; 9:18, 19) Au je, ungesema ni Nebukadneza, mtawala wa kale wa ulimwengu na mjenzi wa jiji lenye fahari aliloita Babiloni Mkubwa? (Danieli 4:28-30) Au ni Aleksanda Mkuu, anayetajwa hata katika unabii wa Biblia kwa sababu ya mambo aliyofanya? (Danieli 8:5-8, 21-22) Au je, ni Kaisari Yulio yule mtawala Mroma maarufu?

Karibu miaka 45 hivi baada ya kifo cha Kaisari huyo, mtoto anayeitwa Yesu alizaliwa huko Bethlehemu. Je, alikuwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi? Miaka 100 hivi iliyopita kitabu The Historians’ History of the World kilisema: “Uvutano wa utendaji [wa Yesu] katika historia ulikuwa wenye nguvu sana kuliko utendaji wa mtu mwingine katika historia, hata kwa maoni yasiyo ya kidini. Ni jambo linalojulikana hata miongoni mwa jamii zilizostaarabika sana ulimwenguni kwamba enzi mpya ilianza Yesu alipozaliwa.”

Hadi leo hii, kuna upendezi mwingi sana kuhusu Yesu Kristo. Miaka michache iliyopita magazeti maarufu ya Marekani Time, Newsweek, na U.S.News and World Report yalikuwa na masimulizi kumhusu yeye wakati uleule, kwenye makala za kwanza. Kwa kweli, inaonekana kwamba upendezi kumhusu Yesu unaongezeka. Gazeti Toronto Star lilisema hivi mnamo 2004: “Uvutano wake unaonekana wazi katika sinema, muziki na hata katika mitindo ya nguo. Amekuwa mmoja kati ya mashujaa wetu mashuhuri zaidi.”

Hata hivyo, inashangaza kwamba hivi majuzi watu fulani walibisha kuwa Yesu hakuwahi kuishi. Bruno Bauer (1809-1882) alikuwa mwalimu maarufu ambaye alidai hivyo. Karl Marx alikuwa mmoja wa wanafunzi wake. Hivi karibuni, Robert E. Van Voorst, aliandika hivi katika kitabu chake Jesus Outside the New Testament: “Katika mafundisho yake, Marx aliingiza maoni yaliyobuniwa ya Bauer kuhusu mwanzo wa Yesu, na vichapo rasmi vya Wasovieti na propaganda nyingine ya Wakomunisti zilieneza madai hayo.”

Hata hivyo, leo ni wachache tu wanaokataa kwamba Yesu aliwahi kuishi. Kwa kweli, watu wengi hukubali kwa utayari kwamba Yesu ni mtu halisi na muhimu sana. Kichwa cha makala moja katika gazeti Wall Street Journal la Desemba 2002 lilisema hivi: “Sayansi Haiwezi Kumpuuza Yesu.” Mwandishi wa makala hiyo alimalizia kwa kusema: “Wasomi wengi, isipokuwa wale ambao nyakati nyingine wanaamini kwamba hakuna Mungu, wamemkubali Yesu wa Nazareti kuwa mtu halisi wa kihistoria.”

Lakini Yesu hakuwa tu mtu wa kihistoria. Gazeti Time liliripoti hivi: “Mtu angehitaji mbinu ya hali ya juu kukanusha kwamba mtu mwenye uvutano mkubwa zaidi, si tu katika miaka 2,000 iliyopita bali katika historia yote ya wanadamu, ni Yesu wa Nazareti.” Liliongezea hivi: “Hakuna mtu anayeweza kutoa hoja yenye nguvu kuthibitisha kwamba maisha ya mtu mwingine yeyote yamekuwa na uvutano wenye kudumu kama ya Yesu.”

Bado kuna maswali yanayosalia: Kwa kweli, yeye alikuwa nani? Alitoka wapi? Kusudi lake duniani lilikuwa nini? Na kwa nini ni muhimu sana tujue kila kitu tunachoweza kumhusu?