Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Madhara Yanayosababishwa na Ponografia

Madhara Yanayosababishwa na Ponografia

Madhara Yanayosababishwa na Ponografia

HABARI ya kila aina kuhusu ngono inapatikana kwa urahisi kupitia televisheni, sinema, video za muziki, na Internet. Je, ni kweli kwamba habari hizo chungu nzima za ponografia hazina madhara, kama watu wengi wanavyotaka tuamini? *

Jinsi Ponografia Inavyowaathiri Watu Wazima

Hata watetezi waseme nini, ponografia inaathiri sana maoni ya watu kuhusu ngono na maadili. Watafiti kwenye Hazina ya Taifa ya Utafiti na Uelimishaji wa Jamii walikata kauli kwamba “kutazama ponografia kunaweza kuwafanya watazamaji wafanye ngono potovu.” Ripoti hiyo inasema “imani ya kwamba wanawake husababisha na hufurahia ubakaji, na kwamba wabakaji ni watu wa kawaida imeenea sana miongoni mwa wanaume wenye zoea la kutazama ponografia.”

Watafiti fulani wanasema kwamba kuzoea kutazama ponografia kunaweza kuathiri uwezo wa kufurahia na kufanya ngono katika ndoa. Dakt. Victor Cline, mtaalamu wa kutibu watu wanaotawaliwa na mambo ya ngono, ametambua kwamba watu wanaotazama ponografia huendelea tu bila kuacha. Mtu anayeanza kutazama ponografia kidogo-kidogo, asipoacha mwishowe anaweza kuwa na zoea la kusoma habari na kutazama picha chafu zaidi za ponografia. Cline anadai kwamba zoea hilo linaweza kuongoza kwenye matendo mapotovu ya ngono. Wanasayansi wanaochunguza tabia za wanadamu wanakubaliana na jambo hilo. Dakt. Cline anaripoti kwamba “upotovu wowote wa ngono unaweza kuanza hivyo . . . na kwamba mtu hawezi kuacha hata akisumbuliwa sana na dhamiri.” Hatimaye, huenda mtu anayetazama ponografia akajaribu kufanya mambo yasiyo ya adili aliyoona, na mara nyingi matokeo huwa mabaya.

Tatizo hilo linaweza kuanza hatua kwa hatua bila kutambuliwa, asema Cline. Aongeza: “Huongezeka na kuenea kama kansa. Kwa kawaida zoea hilo halikomi, wala haliwezi kutatuliwa kwa urahisi. Haishangazi kwamba mara nyingi wanaume waliozoea kutazama ponografia hawakubali kwamba wana tatizo, na ni kawaida kwa wenzi wa ndoa kukosana, nyakati nyingine kutalikiana, na hata mahusiano mengine ya karibu huharibika kwa sababu hiyo.”

Jinsi Vijana Wanavyoathiriwa

Takwimu zinaonyesha kwamba watazamaji wengi wa ponografia ni wavulana wenye umri wa kati ya miaka 12 na 17. Kwa kweli, wengi wao hujifunza masuala ya ngono hasa kupitia ponografia. Hilo lina matokeo mabaya sana. Ripoti moja yasema kwamba “ponografia hazionyeshi kamwe mimba za matineja na magonjwa yanayoambukizwa kingono kama UKIMWI, na hilo hutokeza wazo la uwongo la kwamba mambo yanayoonyeshwa katika ponografia hayana madhara.”

Watafiti fulani husema kwamba kutazama ponografia kunaweza pia kuathiri ukuzi wa kawaida wa ubongo wa mtoto. Dakt. Judith Reisman, mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Vyombo vya Habari, akata kauli: “Uchunguzi wa athari za sauti na picha za ponografia katika utendaji wa kawaida wa ubongo unaonyesha kwamba kutazama ponografia huathiri kabisa uwezo wa kawaida wa kufikiri. Pia hudhuru ubongo wa watoto unaoathiriwa kwa urahisi kwa sababu hufanya wasione mambo kihalisi na hudhuru afya yao ya kiakili na ya kimwili, na huwazuia kupata furaha.”

Jinsi Mahusiano Yanavyoathiriwa

Ponografia huathiri mitazamo na tabia. Ujumbe wake unavutia hasa kwa sababu si halisi na hivyo unaifanya ionekane kuwa yenye kusisimua zaidi kuliko mambo halisi. (Ona sanduku “Utakubali Ujumbe Gani?”) “Watu wanaotazama ponografia hutarajia mambo yasiyo halisi ambayo huharibu mahusiano,” yasema ripoti moja.

Ponografia inaweza kuwafanya wenzi wa ndoa wakose kuwa wanyofu na wakose kuaminiana, sifa ambazo ni muhimu katika ndoa. Kwa sababu ponografia hutazamwa hasa faraghani, mara nyingi humfanya mtu atumie hila na uwongo. Wenzi wa ndoa huhisi kwamba wamesalitiwa. Hawaelewi kwa nini mwenzi wao havutiwi nao tena.

Madhara ya Kiroho

Ponografia husababisha madhara mabaya ya kiroho. Inaweza kuwa kizuizi kikubwa kwa mtu anayetaka kuwa na uhusiano na Mungu. * Biblia huhusianisha hamu ya ngono na tamaa na ibada ya sanamu. (Wakolosai 3:5) Mtu anayetamani kitu huwa na hamu kubwa sana ya kukipata hivi kwamba kinakuwa jambo kuu maishani mwake kuliko vitu vingine vyote. Kwa kweli, wale ambao wamezoea ponografia hutanguliza tamaa zao za ngono badala ya Mungu. Kwa hiyo wanazifanya kuwa sanamu yao. Amri ya Yehova Mungu inasema: “Usiwe na miungu mingine ila mimi.”—Kutoka 20:3.

Ponografia huharibu mahusiano yenye upendo. Mtume Petro, ambaye alikuwa amefunga ndoa, aliwahimiza waume Wakristo wawaheshimu wake zao. Mungu hatasikiliza sala za mume anayekosa kufanya hivyo. (1 Petro 3:7) Je, mtu anayetazama picha chafu za wanawake faraghani anamheshimu mke wake? Mke angehisije akigundua? Na Mungu ambaye “ataleta hukumuni kila kazi” na ambaye “huzipima roho” angeonaje? (Mhubiri 12:14; Mithali 16:2) Je, mtu anayetazama ponografia anaweza kumtarajia Mungu asikilize sala zake?

Ponografia hukazia kutosheleza tamaa za mtu binafsi kwa vyovyote vile. Kwa hiyo, kutazama ponografia ni kukosa upendo. Hudhoofisha uwezo wa Mkristo wa kudumu akiwa safi kiadili na kuwa mwadilifu mbele za Mungu. “Haya ndiyo mapenzi ya Mungu,” akaandika mtume Paulo, “kwamba mjiepushe na uasherati; kwamba kila mmoja wenu apaswe kujua jinsi ya kupata umiliki wa chombo chake mwenyewe katika utakaso na heshima, si katika hamu yenye tamaa ya ngono . . . , kwamba yeyote asifikie hatua ya kudhuru na kuziingilia haki za ndugu yake.”—1 Wathesalonike 4:3-7.

Ponografia huwatumia vibaya hasa wanawake na watoto. Huwavunjia heshima na pia huwashushia hadhi na kuwanyima haki zao. Yule anayetazama ponografia hushiriki na kuunga mkono matumizi hayo mabaya ya wanawake na watoto. ‘Hata mtu akijiona kuwa mwema kadiri gani,’ wasema watafiti Steven Hill na Nina Silver, ‘anapotazama au kukubali ponografia, anakuwa asiyejali au hata mwenye chuki kuelekea mtu anayedai eti anamjali.’

Kuacha Zoea la Kutazama Ponografia

Vipi ikiwa unapambana na zoea la kutazama ponografia? Je, kuna lolote unaloweza kufanya ili kuacha zoea hilo? Biblia hutoa tumaini! Kabla ya kumjua Kristo, baadhi ya Wakristo wa awali walikuwa waasherati, wazinzi, na wenye pupa. Hata hivyo, Paulo alisema, “lakini mmeoshwa mkawa safi.” Hilo liliwezekanaje? Paulo ajibu: “Mmetakaswa . . . kwa roho ya Mungu wetu.”—1 Wakorintho 6:9-11.

Usipuuze kamwe nguvu za roho takatifu ya Mungu. “Mungu ni mwaminifu,” yasema Biblia, “naye hatawaacha nyinyi mshawishwe kupita vile mwezavyo kuhimili.” Kwa kweli, ataandaa njia ya kutokea. (1 Wakorintho 10:13) Kusali kwa bidii—kumwambia Mungu shida zako daima—kutakuwa na matokeo mazuri. Neno lake hutia moyo hivi: “Umtwike BWANA mzigo wako naye atakutegemeza.”—Zaburi 55:22.

Bila shaka, lazima utende kupatana na sala zako. Unahitaji kuazimia kutoka moyoni kukataa ponografia. Rafiki unayemtumaini au mshiriki wa familia anaweza kukusaidia sana, akikupa utegemezo na kitia-moyo unachohitaji ili kushikamana na azimio lako. (Ona sanduku “Kupata Msaada.”) Kukumbuka kwamba hatua hiyo itampendeza Mungu kwaweza kukusaidia uendelee kushikamana na azimio lako. (Mithali 27:11) Kwa kuongezea, kujua kwamba kutazama ponografia kunamchukiza Mungu kwaweza pia kukuchochea uache zoea hilo. (Mwanzo 6:5, 6) Haitakuwa rahisi, lakini unaweza kufaulu. Unaweza kuacha zoea la ponografia!

Kwa kweli, ni hatari kutazama ponografia. Inadhuru na kuharibu. Inawapotosha wale wanaoitayarisha na pia wale wanaoitazama. Huwashushia heshima wanaume na wanawake, ni hatari kwa watoto, na ni zoea ambalo linapasa kupingwa.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Ukitaka kupata habari zaidi juu ya hatari za ponografia kwenye Internet, tafadhali soma mfululizo wa makala zenye kichwa “Ponografia Kwenye Internet—Yaweza Kuleta Madhara Gani?” katika Amkeni! la Juni 8, 2000, ukurasa 3-10.

^ fu. 14 Unaweza kupata habari zaidi juu ya maoni ya Biblia kuhusu ponografia katika Amkeni! la Julai 8, 2002, ukurasa wa 19-21.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Kupata Msaada

Pambano la kuacha zoea la kutazama ponografia halipaswi kuchukuliwa kijuujuu tu; linaweza kuwa pambano gumu. Dakt. Victor Cline ambaye ametibu mamia ya watu wenye zoea la kutazama ponografia asema hivi: “Ahadi hazitoshi. Haitoshi kuwa na makusudio mema. [Mtu mwenye zoea la kutazama ponografia] hawezi kufaulu peke yake.” Cline asema kwamba hatua ya kwanza ya tiba ni kumhusisha mwenzi wake ikiwa amefunga ndoa. Anadai kwamba “Tiba hufaulu haraka ikiwa wote wawili wanahusishwa. Wote wawili wameumia. Wote wanahitaji msaada.”

Ikiwa mtu ni mseja, mara nyingi rafiki mwenye kuaminika au mshiriki wa familia anaweza kumwimarisha. Haidhuru ni nani anayehusika katika tiba hiyo, Cline hutoa sheria moja thabiti: Sema waziwazi kuhusu tatizo hilo na unapotumbukia tena katika zoea hilo. “Siri ‘huua’,” yeye asema. “Huleta aibu na dhamiri mbaya.”

[Chati katika ukurasa wa 9]

Utakubali Ujumbe Gani?

Ujumbe wa Ponografia Maoni ya Biblia

▪ Kufanya ngono na mtu ▪ “Acheni ndoa iwe yenye kuheshimika yeyote, wakati wowote, katika miongoni mwa wote, na kitanda

hali zozote, na kwa njia cha ndoa kiwe bila kutiwa

yoyote si kosa wala hakuna unajisi, kwa maana Mungu

madhara. atawahukumu waasherati na

wazinzi.”Waebrania 13:4.

“Yeye azoeaye uasherati anafanya dhambi

dhidi ya mwili wake mwenyewe.”

1 Wakorintho 6:18;

ona pia Waroma 1:26, 27.

▪ Ndoa inawazuia watu ▪ “Umfurahie mke wa ujana wako. . .

kutosheka kingono. Na kwa upendo wake ushangilie

daima.”Mithali 5:18, 19; ona pia

Mwanzo 1:28; 2:24; 1 Wakorintho 7:3.

▪ Wanawake wana kusudi ▪ [Mimi Yehova Mungu] nitamfanyia

moja tu—kutosheleza mahitaji msaidizi wa kufanana naye.”

ya wanaume ya ngono. —Mwanzo 2:18; ona pia Waefeso 5:28.

▪ Wanaume na wanawake ni ▪ “Kwa hiyo, fisheni viungo vya mwili

watumwa wa hamu zao wenu vilivyo juu ya dunia kwa

za ngono. habari ya uasherati, ukosefu wa

usafi, hamu ya ngono, tamaa yenye

kuumiza, na tamaa, ambako ni ibada ya

sanamu.”Wakolosai 3:5.

“Kila mmoja wenu apaswe kujua jinsi ya

kupata umiliki wa chombo chake mwenyewe

katika utakaso na heshima.”

1 Wathesalonike 4:4.

Wasihi sana “wanawake wazee zaidi kama

mama, wanawake vijana zaidi kama dada kwa

usafi wote wa kiadili.”

1 Timotheo 5:1, 2;

ona pia 1 Wakorintho 9:27.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Watafiti fulani husema kwamba kutazama ponografia kunaweza kuathiri ukuzi wa kawaida wa ubongo wa mtoto

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ponografia inaweza kuwafanya wenzi wa ndoa wakose kuwa wanyofu na wakose kuaminiana

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kusali kwa bidii kutakuwa na matokeo mazuri