Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kujipenda Mwenyewe?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kujipenda Mwenyewe?

Jibu la Biblia

 Biblia inaonyesha kwamba ni sawa, na huenda hata ni lazima, kujipenda mwenyewe kwa kadiri inayofaa. Kujipenda kwa njia hiyo kunahusisha kujitunza, kujiheshimu, na kujiona kuwa una thamani. (Mathayo 10:31) Badala ya kutukuza ubinafsi, Biblia inatoa maoni yenye usawaziko kuhusu kujipenda.

Tunapaswa kumpenda nani kwanza?

  1.   Tunapaswa kumpenda Mungu kwanza kutoka moyoni. Biblia inafundisha kwamba amri iliyo kuu na ya kwanza kabisa ni: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote.”​—Marko 12:28-30; Kumbukumbu la Torati 6:5.

  2.   Amri iliyo kuu ya pili ndiyo hii: “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.”​—Marko 12:31; Mambo ya Walawi 19:18.

  3.   Ingawa Biblia haina amri hususa inayosema ujipende mwenyewe, amri inayosema “umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe” inaonyesha kwamba kujipenda mwenyewe na kujiheshimu kwa kadiri inayofaa ni jambo la kawaida na linafaa.

Yesu alimpenda nani kwanza?

 Yesu alionyesha jinsi ya kusawazisha upendo kwa Mungu, upendo kwa jirani, na kujipenda mwenyewe, naye aliwafundisha wanafunzi wake jinsi ya kufuata mfano wake.​—Yohana 13:34, 35.

  1.   Alimpenda Yehova Mungu kwanza na akajitoa kutimiza kazi Yake. Alisema hivi: “Ili ulimwengu ujue kwamba ninampenda Baba, ninafanya kama vile Baba alivyoniamuru.”​—Yohana 14:31.

  2.   Yesu alimpenda jirani yake. Alionyesha jambo hilo kwa kushughulikia mahitaji ya wengine kufikia hata kutoa uhai wake.​—Mathayo 20:28.

  3.   Alionyesha kwamba anajipenda kwa kadiri inayofaa kwa kutenga wakati wa kupumzika, kula, na kufurahia ushirika pamoja na wafuasi wake na watu ambao alitarajia wangekuwa wanafunzi wake.​—Marko 6:​31, 32; Luka 5:​29; Yohana 2:​1, 2; 12:2.

Ukitanguliza kuwapenda wengine mbele ya kujipenda mwenyewe je, utapunguza furaha yako na kujiheshimu?

 Hapana, kwa sababu tuliumbwa kwa mfano wa Mungu, ambaye sifa yake kuu ni upendo usio na ubinafsi. (Mwanzo 1:​27; 1 Yohana 4:8) Hilo linamaanisha kwamba tumeumbwa ili tuwaonyeshe wengine upendo. Ingawa inafaa kujipenda mwenyewe kwa kadiri fulani, tunapata furaha zaidi kwa kumpenda Mungu kuliko kitu kingine na kukazia fikira kuwatendea wengine mema. Biblia inasema kwamba “kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.”​—Matendo 20:35.

 Leo baadhi ya watu wanadai kwamba mtu hupata furaha anapojitanguliza. Badala ya ‘kumpenda jirani,’ wao ‘wanajipenda wenyewe.’ Hata hivyo, mambo yaliyoonwa hivi karibuni yanathibitisha kwamba afya na furaha hupatikana mtu anapofuata ushauri huu wa Biblia wenye hekima: “Kila mmoja na aendelee kutafuta, si faida yake mwenyewe, bali faida ya yule mtu mwingine.”​—1 Wakorintho 10:24.