Hamia kwenye habari

Bikira Maria​—Biblia Inasema Nini Kumhusu?

Bikira Maria​—Biblia Inasema Nini Kumhusu?

 Jibu la Biblia

 Biblia inasema kwamba Maria, mama ya Yesu, alikuwa na pendeleo la kumzaa Yesu akiwa bikira bado. Biblia ilitabiri muujiza huo katika kitabu cha Isaya na kuripoti utimizo wake katika Injili ya Mathayo na Luka.

 Katika unabii kuhusu kutokea kwa Masihi, Isaya alitabiri hivi: “Tazama! Mwanamke kijana atapata mimba naye atazaa mwana.” (Isaya 7:​14) Akiongozwa na roho ya Mungu, mwandikaji wa Injili ya Mathayo alitumia unabii wa Isaya kuhusu kutungwa kwa mimba ya Yesu. Baada ya kuripoti kwamba Maria alipata mimba kimuujiza, Mathayo alisema hivi pia: “Kwa kweli, yote hayo yalitukia ili kutimiza maneno haya yaliyosemwa na Yehova kupitia nabii wake: ‘Tazama! Bikira a atapata mimba naye atazaa mwana, nao watamwita jina Imanueli,’ ambalo linapotafsiriwa linamaanisha, ‘Mungu Yuko Pamoja Nasi.’”​—Mathayo 1:​22, 23.

 Mwandikaji wa Injili Luka pia aliripoti kuhusu mimba ya kimuujiza ya Maria. Aliandika kwamba Mungu alimtuma malaika Gabrieli “kwa bikira aliyeitwa Maria, mchumba wa mwanamume aliyeitwa Yosefu wa nyumba ya Daudi.” (Luka 1:​26, 27) Maria alithibitisha kwamba alikuwa bikira. Baada ya kusikia kwamba angekuwa mama ya Yesu, ambaye angekuwa Masihi, Maria aliuliza: “Hilo litawezekanaje, kwa kuwa sina uhusiano wa kingono na mwanamume?”​—Luka 1:​34.

 Bikira anawezaje kuzaa?

 Maria alipata mimba kupitia roho takatifu, ambayo ni nguvu za utendaji za Mungu. (Mathayo 1:​18) Maria aliambiwa hivi: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa hiyo yule atakayezaliwa ataitwa mtakatifu, Mwana wa Mungu.” b (Luka 1:​35) Mungu alihamisha uhai wa Mwana wake kimuujiza hadi kwenye tumbo la Maria, na kumfanya apate mtoto.

 Ni nini lililokuwa kusudi la bikira kuzaa?

 Mungu alitumia uzazi wa aina hiyo ili Yesu awe na mwili mkamilifu na hivyo aweze kuwaokoa wanadamu kutokana na dhambi na kifo. (Yohana 3:​16; Waebrania 10:5) Mungu aliuhamisha uhai wa Yesu hadi kwenye tumbo la Maria. Baadaye, roho takatifu ya Mungu ilizuia kiini-tete hicho kisipate hali yoyote ya kutokamilika.​—Luka 1:​35.

 Hivyo, Yesu alizaliwa akiwa mkamilifu, na hivyo alilingana na Adamu kabla ya kufanya dhambi. Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Yeye hakufanya dhambi.” (1 Petro 2:​22) Akiwa mwanadamu mkamilifu, Yesu angeweza kulipa fidia ya kuwakomboa wanadamu kutokana na dhambi na kifo.​—1 Wakorintho 15:21, 22; 1 Timotheo 2:​5, 6.

 Je, Maria aliendelea kuwa bikira?

 Biblia haifundishi kwamba Maria aliendelea kuwa bikira. Badala yake, inaonyesha kwamba Maria alikuwa na watoto wengine.​—Mathayo 12:46; Marko 6:3; Luka 2:7; Yohana 7:5.

Biblia inafundisha kwamba Yesu alikuwa na ndugu na dada kadhaa

 Je, kuzaliwa kwa Yesu na bikira kunamaanisha Maria alichukuliwa mimba bila dhambi ya asili?

 Hapana. Kulingana na kitabu New Catholic Encyclopedia, fundisho la kwamba Maria alichukuliwa mimba bila dhambi “linamaanisha kwamba Bikira Maria hakuwa na DHAMBI YA ASILI tangu mwanzo wa maisha yake, yaani, tangu alipochukuliwa mimba. Wanadamu wengine wanarithi dhambi . . . Lakini Maria, kupitia NEEMA ya pekee, alilindwa asipate dhambi ya asili.” c

 Tofauti na hilo, Biblia haisemi popote kwamba Maria hakuwa na dhambi ya asili. (Zaburi 51:5; Zaburi 5:​12) Kwa kweli, Maria alionyesha kwamba alikuwa na dhambi alipotoa dhabihu ya kufunika dhambi ambayo kulingana na Sheria ya Musa ilipaswa kutolewa na akina mama. (Mambo ya Walawi 12:​2-8; Luka 2:​21-​24) Kitabu New Catholic Encyclopedia kinasema: “Wazo la kwamba Maria alichukuliwa mimba bila dhambi halifundishwi waziwazi katika Maandiko . . . Ni fundisho la Kanisa.”

 Tunapaswa kumwonaje Maria?

 Maria aliweka mfano mzuri wa imani, utii, unyenyekevu, na hali nzuri ya kiroho. Yeye ni mmoja kati ya watu waaminifu tunaopaswa kuwaiga.​—Waebrania 6:​12.

 Hata hivyo, ingawa alikuwa na jukumu la pekee akiwa mama ya Yesu, Biblia haifundishi kwamba tunapaswa kumwabudu Maria au kusali kwake. Yesu hakusema kwamba mama yake anapaswa kupewa heshima ya pekee, wala hakuwaambia wafuasi wake wafanye hivyo. Kwa kweli, mbali na masimulizi ya Injili na kutajwa mara moja katika kitabu cha Matendo, Maria hatajwi katika vitabu 22 vilivyosalia vya Agano Jipya.​—Matendo 1:​14.

 Maandiko hayatoi uthibitisho wowote kwamba Maria alikaziwa uangalifu kwa njia ya pekee​—sembuse kuabudiwa​—na Wakristo wa karne ya kwanza. Badala yake, Biblia inafundisha kwamba Wakristo wanapaswa kumwabudu Mungu peke yake.​—Mathayo 4:​10..

a Neno la Kiebrania ʽal·mahʹ linalotafsiriwa “mwanamke kijana” katika unabii wa Isaya linaweza kumrejelea bikira au mwanamke ambaye si bikira. Hata hivyo, Mathayo akiongozwa na roho ya Mungu alitumia neno hususa zaidi la Kigiriki par·theʹnos, ambalo linamaanisha “bikira.”

b Watu fulani wanapinga matumizi ya neno “Mwana wa Mungu,” wakiamini kwamba inamaanisha Mungu alifanya ngono na mwanamke. Hata hivyo, wazo hilo halifundishwi katika Maandiko. Badala yake, Biblia inamwita Yesu “Mwana wa Mungu” na “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” kwa sababu yeye ndiye aliyeumbwa kwanza na yeye tu ndiye aliyeumbwa moja kwa moja na Mungu. (Wakolosai 1:​13-​15) Biblia pia inamtaja mwanadamu wa kwanza, Adamu, kuwa “mwana wa Mungu.” (Luka 3:38) Anaitwa hivyo kwa sababu Adamu aliumbwa na Mungu.

c Toleo la Pili, Buku la 7, ukurasa wa 331.