Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tumutukuze Kristo—Mufalme Mwenye Utukufu

Tumutukuze Kristo—Mufalme Mwenye Utukufu

‘Katika fahari yako endelea mupaka ufanikiwe [ushinde].’​—ZAB. 45:4.

1, 2. Sababu gani matukio yanayozungumuziwa katika Zaburi ya 45 yanatuhusu?

 MUFALME mwenye utukufu anasonga mbele ili kutetea kweli na haki na anaenda kushinda maadui wake. Kisha kushinda kabisa maadui wake, anafanya ndoa na bibi​-arusi mwenye sura nzuri. Vizazi vinavyotokea baadaye vinaendelea kukumbuka matendo yake na kumushangilia. Hayo ni kati ya matukio ya maana yanayozungumuziwa katika Zaburi ya 45.

2 Lakini, Zaburi ya 45 haizungumuzie tu matukio hayo yanayomalizika na tukio lenye kufurahisha. Matukio yanayozungumuziwa katika zaburi hiyo yanatuhusu. Yanahusu maisha yetu ya sasa, na ya wakati ujao. Acheni, tuchunguze kwa uangalifu maneno ya zaburi hiyo.

“MOYO WANGU UMESISIMUKA KWA SABABU YA JAMBO JEMA”

3, 4. (a) “Jambo jema” linalotuhusu ni jambo gani, na lina matokeo gani juu ya moyo wetu? (b) Namna gani ‘wimbo wetu unahusu mufalme,’ na ni katika maana gani ulimi wetu unakuwa kama kalamu?

3 Soma Zaburi 45:1. “Jambo jema” linalogusa moyo wa mutunga​-zaburi na kuufanya ‘usisimuke’ linahusiana na mufalme. Maana ya kwanza ya neno la Kiebrania linalotafsiriwa “umesisimuka” ni “kububujika,” ao “kutokota.” Jambo hilo jema liliufanya moyo wa mutunga-zaburi ujae furaha na ulimi wake uwe “kama kalamu ya mwandikaji stadi [ao mwenye ufundi].”

4 Maneno hayo yanatuhusu namna gani? Habari njema ya Ufalme wa Masiya ni jambo jema linalofurahisha moyo wetu. Ujumbe wa Ufalme ulikuwa “jambo jema” zaidi sana katika mwaka wa 1914. Tangu mwaka huo, ujumbe huo hauhusu tena Ufalme ambao utaanza kutawala wakati ujao, lakini unahusu serikali ambayo inatawala sasa mbinguni. Hii ndiyo “habari njema ya Ufalme” ambayo tunahubiri “katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.” (Mt. 24:14) Je, moyo wetu ‘unasisimuka,’ ao kufurahi kwa sababu ya ujumbe wa Ufalme? Je, tunahubiri habari njema ya Ufalme kwa bidii? Kama mutunga-zaburi, ‘wimbo wetu unahusu mufalme,’ ni kusema, Mufalme wetu, Yesu Kristo. Tunatangaza kwamba Yesu Kristo ni Mufalme wa Ufalme wa Masiya. Zaidi ya hilo, tunawaalika wote—​watawala na watu wengine wote—​wajitiishe chini ya ufalme wake. (Zab. 2:1, 2, 4-12) Na ulimi wetu unakuwa kama “kalamu ya mwandishi stadi” katika maana ya kwamba tunatumia sana Neno la Mungu lililoandikwa katika kazi yetu ya kuhubiri.

Tunatangaza kwa furaha habari njema inayohusu Mufalme wetu, Yesu Kristo

‘MANENO YENYE KUPENDEZA YANAMIMINIKA KUTOKA KATIKA KINYWA CHA MUFALME’

5. (a) Ni nini iliyomufanya Yesu awe na “sura nzuri”? (b) Namna gani ‘maneno yenye kupendeza yalimiminika kutoka katika kinywa cha Mufalme,’ na namna gani tunaweza kuiga mufano wake?

5 Soma Zaburi 45:2. Maandiko hayazungumuzie sana sura ya Yesu. Hata hivyo, kwa kuwa alikuwa mwanadamu mukamilifu, bila shaka alikuwa na “sura nzuri.” Lakini, jambo lililomufanya awe na sura nzuri kabisa ni uaminifu wake kwa Yehova na ushikamanifu wake usioyumbayumba. Zaidi ya hilo, Yesu alitumia “maneno yenye kuvutia” alipohubiri ujumbe wa Ufalme. (Lu. 4:22; Yoh. 7:46) Je, tunajikaza kuiga mufano wake tunapohubiri na kujaribu kutumia maneno ambayo yatagusa mioyo ya watu?​—Kol. 4:6.

6. Ni katika maana gani Mungu alimubariki Yesu ‘mupaka wakati usio na kipimo’?

6 Kwa sababu Yesu alijitoa kwa Yehova kwa moyo wake wote, Yehova alibariki kazi yake duniani na alimubariki kisha yeye kutoa uzima wake kuwa zabihu. Mutume Paulo aliandika hivi: ‘[Yesu] alipojikuta [ao alipokuja] katika umbo la mwanadamu, alijinyenyekeza naye akawa mutiifu mupaka kifo, ndiyo, kifo juu ya muti wa mateso. Kwa sababu hii pia Mungu alimupandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumupa kwa fazili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya inchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.’ (Flp. 2:8-11) Yehova alimubariki Yesu ‘mupaka wakati usio na kipimo [ao milele]’ kwa kumufufua na kumupatia uzima usioweza kufa.​—Rom. 6:9.

MUFALME ANAFANYWA KUWA MUKUBWA ZAIDI KULIKO ‘WENZAKE’

7. Ni katika maana gani Mungu alimutia Yesu mafuta ‘zaidi kuliko wenzake’?

7 Soma Zaburi 45:6, 7. Kwa sababu Yesu alipenda sana haki na alichukia kila jambo lolote ambalo lingemuzaraulisha Baba yake, Yehova alimufanya kuwa Mufalme wa Ufalme wa Masiya. Yesu alitiwa mafuta kwa “mafuta ya kushangilia” zaidi kuliko ‘wenzake,’ ni kusema, wafalme wa Yuda wa kizazi cha Daudi. Katika maana gani? Kwanza, Yehova mwenyewe ndiye aliyemutia Yesu mafuta. Pili, Yehova alimutia mafuta ili awe Mufalme na Kuhani Mukubwa. (Zab. 2:2; Ebr. 5:5, 6) Tatu, Yesu alitiwa mafuta kwa roho takatifu, wala si kwa mafuta ya kawaida. Mwishowe, ufalme wake utatawala kutoka mbinguni, wala si kutoka duniani.

8. Sababu gani tunaweza kusema kwamba ‘Mungu ni kiti cha ufalme cha Yesu,’ na sababu gani tuko hakika kwamba haki itakuwa katika ufalme wake?

8 Yehova alimufanya Mwana wake kuwa Mufalme wa Ufalme wa Masiya huko mbinguni katika mwaka wa 1914. ‘Fimbo ya ufalme wake ni fimbo ya haki,’ kwa hiyo, haki itakuwa katika ufalme wake na watu watatendewa bila upendeleo. Ana haki ya kuwa Mufalme kwa sababu ‘Mungu ni kiti chake cha ufalme,’ ni kusema, Yehova ndiye amemuchagua kuwa Mufalme. Zaidi ya hilo, Ufalme wake utatawala ‘mupaka wakati usio na kipimo.’ Unafurahia kumutumikia Yehova chini ya Mufalme huyo mwenye nguvu, aliyechaguliwa na Mungu, sivyo?

MUFALME ‘ANAFUNGA UPANGA WAKE’

9, 10. (a) Ni wakati gani Kristo alifunga upanga wake, na kisha aliutumia namna gani? (b) Namna gani Kristo atatumia upanga wake wakati ujao?

9 Soma Zaburi 45:3. Yehova anamuambia Mufalme wake ‘afunge upanga wake kwenye ubavu wake.’ Kwa kufanya hivyo, anamuruhusu Yesu apigane vita na wale wote wanaopinga mamlaka ya Mungu na kuwaangamiza. (Zab. 110:2) Kristo anaitwa “Mwenye nguvu” kwa sababu yeye ni Mufalme​-Shujaa na asiyeshindwa. Alifunga upanga wake katika mwaka wa 1914 na kushinda Shetani na mashetani wake na kuwafukuza mbinguni na kuwatupa kwenye ujirani wa dunia.​—Ufu. 12:7-9.

10 Tukio hilo lilikuwa tu mwanzo wa mwendo wake wa ushindi. Lakini, Mufalme huyo anapaswa “kukamilisha ushindi wake.” (Ufu. 6:2) Yehova hajaharibu sehemu zote za ulimwengu wa Shetani, na Shetani mwenyewe na mashetani wake wanapaswa kuangamizwa. Kwanza, Babiloni Mukubwa, ni kusema, dini zote za uongo, ataharibiwa. Yehova amepanga kutumia wakubwa wa serikali za wanadamu ili kuharibu “kahaba” huyo muovu. (Ufu. 17:16, 17) Kisha, Mufalme​-Shujaa ataelekeza uangalifu wake kwenye viongozi wa serikali za ulimwengu wa Shetani ili kuwaharibu. Kristo, anayeitwa pia “malaika wa abiso,” atakamilisha ushindi wake kwa kumutupa Shetani na mashetani wake katika abiso. (Ufu. 9:1, 11; 20:1-3) Acheni tuone namna Zaburi ya 45 ilivyozungumuzia matukio hayo ya maana.

MUFALME ANASONGA MBELE “ILI KUTETEA KWELI”

11. Namna gani Kristo anasonga mbele ‘ili kutetea kweli’?

11 Soma Zaburi 45:4. Mufalme​-Shujaa hapigane vita ili kuchukua maeneo na kutiisha mataifa. Lakini, anapigana vita ya haki akiwa na makusudi mazuri. Anasonga mbele ili “kutetea kweli na unyenyekevu na uadilifu [ao haki].” Kweli ya kwanza kabisa ambayo anapaswa kutetea ni hii: Yehova ndiye Mutawala Mukubwa wa Ulimwengu Wote Muzima. Alipomuasi Yehova, Shetani alipinga haki yake ya kutawala. Kuanzia wakati huo na kuendelea, mashetani na wanadamu wamepinga haki ya Yehova ya kutawala. Wakati umefika sasa ili Mufalme aliyetiwa mafuta na Yehova aweze kupigana vita na kuonyesha kwamba Yehova ndiye ana haki ya kutawala ulimwengu wote muzima.

12. Namna gani Mufalme anasonga mbele ili ‘kutetea unyenyekevu’?

12 Mufalme anasonga mbele pia ili ‘kutetea unyenyekevu.’ Akiwa Mwana muzaliwa​-pekee wa Mungu, Yesu ameonyesha mufano muzuri sana wa unyenyekevu na ameonyesha utii mushikamanifu kwa Baba yake. (Isa. 50:4, 5; Yoh. 5:19) Raia wote waaminifu wa Mufalme huyo wanapaswa kufuata mufano wake na kujitiisha kwa unyenyekevu chini ya mamlaka ya Yehova katika mambo yote. Ni wale tu wanaofanya hivyo ndio watastahili kuishi katika ulimwengu mupya ambao Mungu ameahidi.​—Zek. 14:16, 17.

13. Namna gani Kristo anasonga mbele ili ‘kutetea uadilifu’?

13 Kristo anasonga mbele pia ili ‘kutetea uadilifu.’ Uadilifu ambao Mufalme anatetea ni “uadilifu wa Mungu,” ni kusema, kanuni za Yehova za mema na mabaya. (Rom. 3:21; Kum. 32:4) Nabii Isaya alitabiri hivi kuhusu Mufalme Yesu Kristo: ‘Mufalme atatawala kwa ajili ya uadilifu.’ (Isa. 32:1) Utawala wa Yesu utaleta ‘mbingu mupya’ na ‘dunia mupya,’ ambamo “uadilifu utakaa.” (2 Pet. 3:13) Kila mutu atakayeishi katika ulimwengu mupya ataombwa aishi kulingana na kanuni za Yehova.​—Isa. 11:1-5.

MUFALME ANAFANYA “MAMBO YENYE KUOGOPESHA”

14. Namna gani mukono wa kuume wa Kristo utafanya “mambo yenye kuogopesha”? (Ona picha mwanzoni mwa habari hii.)

14 Mufalme anasonga mbele akiwa amefunga upanga kwenye ubavu wake. (Zab. 45:3) Lakini wakati umefika sasa ili Mufalme achukue upanga wake katika mukono wake wa kuume na kuanza kuutumia. Mutunga​-zaburi alitabiri hivi: ‘Mukono wako wa kuume utakufundisha [ao utafanya] mambo yenye kuogopesha.’ (Zab. 45:4) Yesu Kristo atafanya “mambo yenye kuogopesha” atakapoenda kuangamiza maadui wa Yehova kwenye vita ya Har-magedoni. Hatujue Kristo ataharibu ulimwengu wa Shetani namna gani. Lakini tunajua kwamba jambo lolote atakalofanya litawaogopesha wakaaji wa dunia ambao hawakutii onyo la Mungu la kujitiisha chini ya utawala wa Mufalme. (Soma Zaburi 2:11, 12.) Katika unabii wake kuhusu wakati wa mwisho, Yesu alisema kwamba watu ‘watazimia kwa woga na tarajio la mambo yanayokuja juu ya dunia inayokaliwa, kwa maana nguvu za mbingu zitatikiswa.’ Kisha aliongeza hivi: “Na ndipo watakapomwona Mwana wa binadamu akija katika wingu akiwa na nguvu na utukufu mwingi.”​—Lu. 21:26, 27.

15, 16. Ni nani watakaokuwa katika “majeshi” yatakayoenda na Yesu kwenye vita?

15 Kinapozungumuzia namna Mufalme anavyokuja “na nguvu na utukufu mwingi” ili kuharibu maadui wa Yehova, kitabu cha Ufunuo kinasema hivi: ‘Nikaona mbingu imefunguliwa, na, tazama! farasi mweupe. Na yeye aliyeketi juu yake anaitwa Mwaminifu na wa Kweli, naye anahukumu na kufanya vita kwa uadilifu. Pia, majeshi yaliyokuwa mbinguni yalikuwa yakimufuata juu ya farasi weupe, nayo yalikuwa yamevikwa kitani bora cheupe, safi. Na upanga murefu mukali unachomoza kutoka kinywani mwake, ili ayapige mataifa nao, naye atawachunga kwa fimbo ya chuma. Yeye anakanyaga pia shinikizo la divai ya hasira ya gazabu ya Mungu Mweza​-Yote.’​—Ufu. 19:11, 14, 15.

16 Ni nani watakaokuwa katika “majeshi” ya mbinguni yatakayoenda na Yesu kwenye vita? Alipofunga upanga wake kwa mara ya kwanza ili kumufukuza Shetani na mashetani wake huko mbinguni, Yesu alisindikizwa na “malaika zake.” (Ufu. 12:7-9) Kwa hiyo tunaweza kusema kwamba, wakati Kristo atapigana vita ya Har-magedoni, malaika waaminifu watakuwa katika majeshi yake. Je, kuna wengine watakaokuwa katika majeshi hayo? Yesu aliwaahidi ndugu zake watiwa​-mafuta hivi: ‘Yeye atakayeshinda na kushika matendo yangu mupaka mwisho nitamupa mamlaka juu ya mataifa, naye atawachunga watu kwa fimbo ya chuma hivi kwamba watavunjwa vipande​-vipande kama vyombo vya udongo, kama vile nilivyopokea kutoka kwa Baba yangu.’ (Ufu. 2:26, 27) Kwa hiyo, ndugu watiwa-mafuta wa Kristo ambao wakati huo watakuwa wamekwisha kuenda mbinguni watakuwa pia katika majeshi hayo. Watawala wenzake watiwa-mafuta watakuwa pamoja naye atakapofanya “mambo yenye kuogopesha” ili kutawala mataifa kwa fimbo ya chuma, ni kusema, kuyaharibu.

MUFALME ANAKAMILISHA USHINDI WAKE

17. (a) Farasi mweupe ambaye Kristo anapanda juu yake anafananisha nini? (b) Upanga na upinde vinafananisha nini?

17 Soma Zaburi 45:5. Farasi mweupe ambaye Mufalme anapanda juu yake anafananisha vita ya haki na inayokubaliwa na Yehova. (Ufu. 6:2; 19:11) Zaidi ya upanga, Mufalme anabeba pia upinde. Tunasoma hivi kwenye Ufunuo 6:2: “Nami nikaona, na, tazama! farasi mweupe; na yule anayeketi juu yake alikuwa na upinde; naye akapewa taji, naye akaenda akishinda na kukamilisha ushindi wake.” Upanga na upinde vinafananisha njia ambazo Kristo atatumia ili kuharibu maadui wake.

Ndege wataalikwa ili kuisafisha dunia (Ona fungu la 18)

18. Namna gani “mishale” ya Kristo itakuwa “mikali”?

18 Kwa kutumia maneno ya mufano, mutunga-zaburi alitabiri kwamba ‘mishale ya Mufalme ni mikali, inatoboa mioyo ya maadui wake’ na ‘kufanya watu waanguke mbele zake.’ Uharibifu utaenea katika dunia yote. Nabii Yeremia alitabiri hivi: ‘Wale waliouawa na Yehova siku hiyo hakika watakuwa kutoka mwisho mumoja wa dunia mupaka mwisho wa pili wa dunia.’ (Yer. 25:33) Unabii mwingine unaofanana na huo unasema hivi: “Nikaona pia malaika amesimama katika jua, naye akapaaza kilio kwa sauti kubwa na kuwaambia ndege wote wanaoruka katikati ya mbingu: ‘Njooni hapa, mukusanyike pamoja kwenye mulo mukubwa wa jioni wa Mungu, ili mupate kula sehemu zenye nyama za wafalme na sehemu zenye nyama za viongozi wa kijeshi na sehemu zenye nyama za watu wenye nguvu na sehemu zenye nyama za farasi na za wale wanaoketi juu yao, na sehemu zenye nyama za wote, za watu huru na vilevile za watumwa na za wadogo na wakubwa.’”​—Ufu. 19:17, 18.

19. Namna gani Kristo ‘ataendelea mupaka afanikiwe’ na kukamilisha ushindi wake?

19 Kisha kuharibu ulimwengu wa Shetani, Kristo ‘ataendelea katika fahari yake mupaka afanikiwe [ashinde].’ (Zab. 45:4) Atakamilisha ushindi wake kwa kumutupa Shetani na mashetani wake ndani ya abiso katika kipindi chote cha Utawala wa Miaka Elfu. (Ufu. 20:2, 3) Kwa kuwa Ibilisi na malaika zake watakuwa wakati huo katika hali inayofanana na kifo ao ya kutotenda, wakaaji wa dunia hawatadanganywa tena na Shetani na mashetani wake na wataweza kujitiisha kabisa kwa Mufalme wao mushindi na mwenye utukufu. Hata hivyo, mbele wajionee namna dunia yote itakavyogeuzwa pole kwa pole na kuwa paradiso, watakuwa na nafasi nyingine ya kufurahi pamoja na Mufalme wao na wale watakaotawala pamoja naye mbinguni. Tutazungumuzia tukio hilo katika habari inayofuata.