Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Mambo Tunayojifunza Kutokana na ‘Picha ya ile Kweli’

Mambo Tunayojifunza Kutokana na ‘Picha ya ile Kweli’

Mambo Tunayojifunza Kutokana na ‘Picha ya ile Kweli’

“[Una] picha ya ujuzi na ya ile kweli katika Sheria.”​—ROM. 2:20.

TAFUTA MAJIBU KWA MAULIZO YAFUATAYO:

Katika Sheria ya Musa, zabihu zilikuwa kivuli cha nini?

Kuna ulinganifu gani kati ya zabihu fulani ambazo Wayahudi walikuwa wakitoa na zile zinazotolewa na Wakristo leo?

Ni nini itakayoamua ikiwa zabihu fulani itakubaliwa na Yehova ao hapana?

1. Kwa nini ni jambo la lazima tuelewe maana ya Sheria ya Musa?

 BILA barua za mutume Paulo, barua alizoandika kwa uongozi wa roho ya Mungu, ingekuwa vigumu kwetu kuelewa mambo mbalimbali ya Sheria ya Musa. Kwa mufano, katika barua yake kwa Waebrania, alieleza vizuri jinsi Yesu, ‘kuhani mukuu na mwaminifu’ alitoa mara moja kwa wakati wote ‘zabihu ya upatanisho’ ili wale walio na imani katika zabihu hiyo wapate “ukombozi wa milele.” (Ebr. 2:17; 9:11, 12) Paulo alieleza kwamba maskani ilikuwa tu “kivuli cha vitu vya mbinguni” na kwamba Yesu alikuwa Mupatanishi wa “agano [lililo] bora” kuliko agano lile ambalo Musa alikuwa mupatanishi. (Ebr. 7:22; 8:1-5) Maelezo hayo yalikuwa ya maana kwa Wakristo wa siku za Paulo, na hata leo. Yanatusaidia pia tuwe wenye shukrani sana kwa mambo yote ambayo Mungu ametufanyia.

2. Wakristo Wayahudi walikuwa na pendeleo gani ambalo Watu Wasio Wayahudi hawakuwa nalo?

2 Paulo alipowaandikia Wakristo wa Roma, alielekeza maelezo yake fulani kwa washiriki wa kutaniko ambao walikuwa Wayahudi wa asili na waliofundishwa Sheria ya Musa. Alitambua wazi kwamba kwa kuwa Wayahudi hao walifahamiana na Sheria ya Mungu, walikuwa na pendeleo la kuwa na “picha ya ujuzi na ya ile kweli” kuhusu Yehova na kanuni zake za uadilifu. Kuelewa vizuri ‘picha ya ile kweli’ na kuiheshimu kwa moyo wote, kuliwasaidia Wakristo Wayahudi, kuongoza, kufundisha, na kufasiria wale ambao hawakujua Sheria ambayo Yehova aliwatolea watu wake; Wayahudi waaminifu walifanya hivyo pia hapo mbele.​—Soma Waroma 2:17-20.

MAMBO YALIYOKUWA KIVULI CHA ZABIHU YA YESU

3. Namna gani tunafaidika kwa kujifunza zabihu ambazo Wayahudi walikuwa wakimutolea Mungu?

3 Picha ya ile kweli ambayo mutume Paulo alizungumuzia ingali bado ya maana kwetu ili tuelewe makusudi ya Yehova. Kanuni zinazopatikana katika Sheria ya Musa bado zingali za maana kwetu. Kwa hiyo, acheni tuzungumuzie tu sehemu moja ya ile Sheria​—yaani jinsi zabihu na matoleo mbalimbali viliwaongoza Wayahudi wanyenyekevu kwa Kristo na kuwasaidia waelewe yale ambayo Mungu alitaka wafanye. Na kwa kuwa kanuni za Yehova kuelekea watumishi wake hazibadilike, tutaona pia kwamba sheria za Mungu kwa Israeli kuhusu zabihu na matoleo, zinaweza kutusaidia tuchunguze jinsi tunavyomutumikia.​—Mal. 3:6.

4, 5. (a) Sheria ya Musa iliwakumbusha Wayahudi nini? (b) Sheria ya Mungu kuhusu zabihu, ilikuwa kivuli cha nini?

4 Mambo mengi yaliyohusiana na Sheria ya Musa yaliwakumbusha Wayahudi kwamba walikuwa wafanya zambi. Kwa mufano, mutu yeyote aliyegusa maiti ya mutu, aliombwa atakaswe. Kwa hiyo, ngombe mwekundu asiye na kilema alichinjwa na kuteketezwa. Majivu yake yaliwekwa ili kuyachanganya na “maji ya kutakasa,” ambayo yalinyunyizwa juu ya mutu aliyepaswa kutakaswa siku ya tatu na siku ya saba kisha kuchafuliwa kwake. (Hes. 19:1-13) Na ili kukumbusha Wayahudi kwamba mutu anapozaliwa anazaliwa na zambi na kutokukamilika, mwanamuke aliyezaa alibaki katika hali ya kutokuwa safi kwa muda wa kipindi fulani, baada ya hapo aliombwa afanye upatanisho kupitia zabihu.​—Law. 12:1-8.

5 Katika mambo mengine ya maisha ya kila siku, Wayahudi waliombwa kutoa zabihu za wanyama ili wasamehewe zambi. Iwe Wayahudi walijua ao hapana, zabihu hizo—na zile zilizotolewa baadaye kwenye hekalu la Yehova​—zilikuwa “kivuli” cha zabihu kamilifu ya Yesu.​—Ebr. 10:1-10.

NINI ILIPASWA KUMUCHOCHEA MUTU KUTOA ZABIHU?

6, 7. (a) Waisraeli walipaswa kufikiria mambo gani walipokuwa wakichagua zabihu ya kumutolea Yehova, na hilo lilikuwa kivuli cha nini? (b) Tunaweza kujiuliza maulizo gani?

6 Kanuni ya musingi kuhusu zabihu ya munyama yeyote ambaye Mwisraeli alipaswa kumutolea Yehova ni kwamba munyama huyo hapaswi kuwa na kilema chochote—yaani asiwe kipofu, asiwe na kidonda, ao asiwe mugonjwa ao mwenye kuharibika. (Law. 22:20-22) Waisraeli walipomutolea Yehova zabihu za matunda ao nafaka, iliomba yawe ‘matunda ya kwanza,’ ‘yaliyo bora zaidi’ ya mavuno yao. (Hes. 18:12, 29) Yehova hakukubali zabihu ambayo haikuwa bora zaidi. Agizo hilo la maana kuhusu zabihu ya wanyama lilionyesha kwamba zabihu ya Yesu haitakuwa na kilema ao kasoro yoyote wala doa, na kwamba Yehova angetoa zabihu iliyo bora zaidi na yenye samani kubwa sana ili kuwakomboa wanadamu.​—1 Pet. 1:18, 19.

7 Ikiwa mutu anayetoa zabihu alikuwa kweli mwenye shukrani kwa Yehova kwa sababu ya mambo yote mema ambayo Amemufanyia, angechagua munyama aliye bora zaidi kati ya wale alio nao ili kumutolea Yehova, sivyo? Kila mutu alikuwa huru kutoa kilicho bora zaidi ao hapana. Lakini alijua kwamba, Yehova hangependezwa na zabihu yenye kilema ao kasoro, kwa kuwa kutoa zabihu kama hiyo kungeonyesha kwamba mutu huyo aliona zabihu kuwa si jambo la lazima ao hata kwamba Yehova alikuwa akimuuzi. (Soma Malaki 1:6-8, 13.) Hilo linapaswa kutufanya tufikiri kwa uzito kuhusu utumishi tunaomutolea Mungu. Tunaweza kujiuliza: ‘Kwa nini ninamutumikia Yehova? Je, ninahitaji kubadili namna ninavyomutumikia? Je, ninamutolea kilicho bora zaidi?’

8, 9. Kwa nini tufikirie kile kilichowachochea Waisraeli watoe zabihu?

8 Ikiwa Mwisraeli alimutolea Yehova zabihu kwa kujipendea ili kuonyesha shukrani, ao ikiwa angetoa zabihu ya kuteketezwa ili kukubaliwa na Mungu, kwa hiyo, hangekuwa na magumu ya kumutolea Yehova munyama aliye bora zaidi. Angekuwa mwenye furaha kwa kumutolea Yehova kilicho bora zaidi. Leo, Wakristo hawaombwi kutoa zabihu kulingana na Sheria ya Musa; lakini wanatoa zabihu mbalimbali katika maana ya kwamba wanatumia wakati, nguvu, na mali yao ili kumutumikia Yehova. Mutume Paulo alisema kwamba ‘tangazo la hazarani’ ambalo Mukristo anafanya kuhusu tumaini lake na “kutenda mema na kushiriki vitu pamoja na wengine” kuwa ni zabihu zinazomupendeza Mungu. (Ebr. 13:15, 16) Maoni yetu na jinsi tunavyoshiriki katika utendaji huo vinaonyesha kwa kadiri gani tunashukuru na kupendezwa na yote ambayo Mungu ametutolea. Kwa hiyo, maoni yetu juu ya kazi ya Mungu na kile kinachotuchochea tushiriki katika kazi hiyo vinalingana na zabihu ambazo Waisraeli walimutolea Mungu kwa kujipendea.

9 Tuseme nini basi kuhusu jambo la kwamba Sheria ya Musa iliomba toleo la zambi ao toleo la hatia litolewe na mutu kwa sababu ya makosa fulani? Hata ikiwa sheria ililazimisha zabihu zitolewe, je, hilo linamaanisha kwamba nia ya kujipendea haikuwa tena lazima? Je, ilifaa zabihu kama hizo, labda mutu azitoe kwa kinyongo? (Law. 4:27, 28) Haingekuwa hivyo ikiwa mutu aliyetoa zabihu alitaka kabisa kuendelea kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Yehova.

10. Wakristo wanaweza kutoa “zabihu” gani ili kutengeneza uhusiano wao na wengine ao na Mungu?

10 Leo pia, tunaweza kuwakwaza ndugu zetu bila kujua ao kwa kutojali wala kwa kutokufikiri mbele ya kusema. Zamiri yako inaweza kukuambia kwamba umekosea katika mwenendo wako. Kila mutu anayechukua uhusiano wake na Yehova kwa uzito atafanya yote awezayo ili kutengeneza hali yake, sivyo? Hilo linaweza kumaanisha kumwomba musamaha yule uliyekosea ao ikiwa ni kosa nzito, kuwaendea wazee wa kutaniko ili kupata musaada wa kiroho. (Mt. 5:23, 24; Yak. 5:14, 15) Kwa hiyo inaomba kufanya jambo fulani ili kurudisha uhusiano wetu na mutu tuliyekosea ao na Mungu. Kufanya hivyo ni kama kutoa zabihu, na tunapotoa “zabihu” kama hizo, tunatengeneza uhusiano wetu pamoja na Mungu na ndugu wetu na tunakuwa na zamiri safi. Hilo linatuhakikishia kwamba njia za Yehova ni nzuri zaidi.

11, 12. (a) Matoleo ya ushirika yalikuwa nini? (b) Katika ibada ya kweli leo, namna gani matoleo ya ushirika yanatolewa?

11 Zabihu zingine katika Sheria ya Musa ziliitwa matoleo ya ushirika. Zilionyesha kwamba mutu ana amani pamoja na Yehova. Mutu aliyetoa toleo kama hilo, yeye na familia yake walikula pamoja nyama ya munyama ambaye walitoa kama zabihu, labda katika chumba kimoja cha kulia katika hekalu. Kuhani aliyeshugulikia zabihu hiyo pamoja na makuhani wengine wanaotumika katika hekalu walipewa pia sehemu. (Law. 3:1; 7:31-33) Mutu alikuwa akitoa zabihu hiyo kwa kuwa alipenda tu awe na uhusiano muzuri pamoja na Mungu. Ilikuwa kama, yeye na familia yake, makuhani, na Yehova walikuwa wakikula chakula pamoja kwa furaha na kwa amani.

12 Je, hauoni kuwa ni pendeleo kubwa kabisa, kwa njia ya mufano, kumwalika Yehova kwenye chakula kama hicho, na yeye anakubali kuja? Kwa kawaida, mwenye kualika angetamani kutoa kilicho bora zaidi kwa ajili ya mugeni huyo mwenye kuheshimika. Mupango kuhusu matoleo ya ushirika, sehemu ya picha ya ile kweli ya Sheria, ulionyesha kwamba kupitia zabihu kuu ya Yesu, wanadamu wote wanaotaka wanaweza kuwa na uhusiano wa karibu na wenye amani pamoja na Muumbaji wao. Leo, tunaweza kuwa na urafiki pamoja na Yehova ikiwa kwa kujipendea tunatoa mali yetu na kutumia nguvu zetu katika kazi yake.

ZABIHU AMBAZO MUNGU HAKUKUBALI

13, 14. Kwa nini Yehova hakukubali zabihu ambayo Mufalme Sauli alitaka kumutolea?

13 Kulingana na Sheria ya Musa, kwa kawaida, Yehova alikubali zabihu ya mutu ikiwa aliitoa akiwa na maoni yanayofaa na pia kwa moyo muzuri. Biblia inazungumuzia watu fulani ambao walitoa zabihu ambazo hazikukubaliwa na Mungu. Kwa nini Mungu hakuzikubali? Acheni tuzungumuzie mifano miwili.

14 Nabii Samweli alimwambia Mufalme Sauli kwamba wakati umefika ili Yehova awahukumu Waamaleki. Kwa hiyo, Sauli alipaswa kuharibu taifa hilo adui pamoja na wanyama wake wa kufuga. Lakini, kisha ushindi, Sauli aliruhusu maaskari wake wasimwuue Agagi, mufalme wa Waamaleki. Pia, hakuwaua wanyama wao wa kufuga wazuri akifikiri kwamba wanyama hao wanaweza kutolewa kwa Yehova kama zabihu. (1 Sam. 15:2, 3, 21) Yehova alifanya nini? Alimukataa Sauli kwa sababu hakutii agizo lake. (Soma 1 Samweli 15:22, 23.) Tunajifunza nini kutokana na hilo? Tunajifunza kwamba ili zabihu yetu ikubaliwe na Mungu, tunapaswa kutii amri zake.

15. Mwenendo mubaya wa Waisraeli fulani wa siku za Isaya waliotoa zabihu kwa Mungu ulionyesha nini?

15 Mufano mwingine unapatikana katika kitabu cha Isaya. Katika siku za Isaya, Waisraeli walimutolea Yehova zabihu kidesturi tu. Tabia yao mbaya ilifanya Yehova asikubali zabihu walizomutolea. Yehova aliwauliza hivi: ‘Zabihu zenu nyingi zina faida gani kwangu? Nimetosheka na matoleo mazima ya kuteketezwa ya kondoo-dume na mafuta ya wanyama waliolishwa vizuri; nami sikupendezwa na damu ya ngombe-dume wachanga na wana-kondoo na mbuzi-dume. Acheni kuleta ndani matoleo zaidi ya nafaka yasiyo na samani. Uvumba—ni chukizo kwangu.’ Kwa nini Mungu alisema hivyo? Mungu aliwaambia hivi: ‘Hata mujapotoa sala nyingi, mimi sisikilizi; mikono yenu imejaa umwagaji wa damu. Jiosheni; jisafisheni; ondoeni ubaya wa matendo yenu mbele za macho yangu; acheni kutenda mabaya.’​—Isa. 1:11-16.

16. Ni nini kinachoamua ikiwa Yehova atakubali zabihu fulani ao hapana?

16 Yehova hakukubali zabihu zilizotolewa na wafanya zambi wasiotubu. Lakini, alikubali sala na zabihu za wale waliojikaza kuishi kulingana na amri zake. Picha ya Sheria iliwafundisha watu hao kwamba walikuwa wafanya zambi na kwamba walihitaji musamaha. (Gal. 3:19) Kujua hilo kungewasaidia watubu. Leo pia, tunapaswa kuelewa kwamba tunahitaji zabihu ya Kristo, ambayo ina uwezo wa kufunika zambi. Ikiwa tunaelewa jambo hilo, basi, Yehova “atapendezwa” na kila jambo tunalomutolea katika utumishi wetu kwake.​—Soma Zaburi 51:17, 19.

UWE NA IMANI KATIKA ZABIHU YA YESU!

17-19. (a) Namna gani tunaweza kumwonyesha Yehova shukrani yetu kwa sababu ya zabihu ya Yesu? (b) Tutajifunza nini katika habari inayofuata?

17 Sisi tuna pendeleo kushinda Waisraeli; wao waliona “kivuli tu” cha makusudi ya Mungu lakini sisi tunaona ukweli wake. (Ebr. 10:1) Sheria zilizohusu zabihu ziliwasaidia Wayahudi wajue mambo ambayo wanapaswa kufanya ili kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu​—kumushukuru kabisa, kumutolea kilicho bora zaidi, na kujua kwamba walihitaji ukombozi. Kupitia Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki tunaweza kuelewa kwamba kupitia zabihu ya ukombozi ya Yesu, Yehova ataondoa kwa milele matokeo yote ya zambi na kwamba hata sasa anatuwezesha kuwa na zamiri iliyo safi mbele yake. Zabihu ya ukombozi ya Yesu ni yenye samani sana kwetu!​—Gal. 3:13; Ebr. 9:9, 14.

18 Kwa kweli, ili kufaidika na zabihu ya ukombozi kuna mambo mengi tunayopaswa kufanya kuliko kujua tu kwamba kuna mupango huo. Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Sheria imekuwa mutunzaji wetu kutuongoza kwa Kristo, ili tutangazwe kuwa waadilifu kutokana na imani.’ (Gal. 3:24) Imani kama hiyo inapaswa kuonyeshwa kwa matendo. (Yak. 2:26) Kwa sababu hiyo Paulo aliwatia moyo Wakristo wa wakati wake waliokuwa na picha ya ujuzi kuhusu Sheria ya Musa ili kutumikisha ujuzi huo. Kwa kufanya hivyo, mwenendo wao ungepatana na kanuni za Mungu ambazo walifundishwa.​—Soma Waroma 2:21-23.

19 Ijapokuwa leo Wakristo hawaombwi kushika Sheria ya Musa, wanapaswa kuendelea kumutolea Yehova zabihu zinazokubalika. Katika habari inayofuata, tutajifunza jinsi tunavyoweza kumutolea Yehova zabihu zinazokubalika.

[Maulizo ya Funzo]

[Wazo la fungu kwenye ukurasa 17]

Kanuni za Yehova kuelekea watumishi wake hazibadilike

[Picha katika ukurasa wa 18]

Wewe ungemutolea Yehova munyama gani?

[Picha katika ukurasa wa 19]

Wale wanaomutolea Yehova zabihu zenye kukubalika wanakubaliwa naye