Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

KWA nini mwanamume fulani aliyelelewa katika familia iliyoshikilia sana dini ya Katoliki na ambaye alikuwa amefanikiwa katika mambo ya kisheria alikubali kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova? Ni nini kilichomchochea gaidi fulani aache jeuri na kuwa mhudumu wa kidini? Soma mambo ambayo watu hao wanasema.

“Nilipata ujuzi mwingi zaidi kuhusu mema na mabaya.”​—SEBASTIÃO ALVES JUNQUEIRA

MWAKA WA KUZALIWA: 1946

NCHI: BRAZILI

HISTORIA: HAKIMU

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Familia yetu iliishi mashambani, karibu kilomita sita kutoka mji wa Piquete. Wazazi wangu walikuwa na shamba dogo, na shamba hilo lilitusaidia kupata mahitaji ya lazima. Nilisomea Piquete, hivyo nikanunua baiskeli nzee, ambayo ilifanya iwe rahisi kusafiri hadi mjini. Watu walioishi katika eneo letu walikuwa maskini, lakini mji huo ulikuwa safi na haukuwa na visa vingi vya uhalifu. Wanaume wengi katika mji huo walifanya kazi katika kiwanda cha kutengeneza silaha za kijeshi.

Nilipenda masomo na mwishowe nikafaulu kujiunga na Shule ya Kijeshi iliyofunza mambo ya angani na ufundi wa ndege katika jiji lililokuwa karibu ambako, katika mwaka wa 1966, nilihitimu na kuwa sajenti. Kisha nikajiunga na shule ya mambo ya kisheria na nikapata shahada yangu ya sheria. Baadaye nilituma maombi ya kupata cheo cha mkuu wa polisi. Mwaka wa 1976, nilipita mtihani wa serikali na nikapata kazi hiyo. Nyakati nyingine, kazi yangu ilihusisha kuwa msimamizi katika gereza. Pindi hizo, Mashahidi wa Yehova wangekuja mara kwa mara kuomba ruhusa ili wawahubirie wafungwa. Sikuzote walinihubiria pia ujumbe wa Biblia. Nilimheshimu sana Mungu. Nilifurahi kujifunza kwamba jina la Mungu ni Yehova, na kwamba tunaweza kusitawisha urafiki pamoja naye.

Pole kwa pole, nilipandishwa cheo katika kazi yangu ya mambo ya kisheria. Mwaka wa 1981, nilipita mtihani mwingine wa serikali na nikateuliwa kuwa hakimu wa jimbo. Kisha, mwaka wa 2005, nikateuliwa kuwa hakimu wa mahakama ya rufani katika mahakama ya São Paulo.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Mara tu nilipohitimu kutoka kwenye shule ya mambo ya kisheria, nilianza kusoma Biblia, jambo ambalo lilibadili sana maoni yangu. Nilishikilia kabisa dini ya Katoliki. Katika familia yetu kulikuwa na makasisi na askofu, na nilimsaidia kasisi wakati wa Misa. Kabla hajatoa mahubiri, nilisoma sehemu nilizogawiwa katika kitabu cha sala. Halikuwa jambo la kawaida kusoma Biblia katika familia ya Kikatoliki. Mama yangu alikasirika sana alipotambua kwamba nilikuwa nikisoma Biblia. Alijaribu kunivunja moyo kwa kuniambia kwamba ningerukwa na akili. Hata hivyo, niliendelea kuisoma na sikuona hatari yoyote.

Nafikiri tamaa yangu ya kujua mengi ilinichochea niendelee kusoma Biblia. Nilitaka kujua mengi kuhusu makasisi na daraka lao katika kanisa. Nilianza pia kusoma kuhusu kikundi cha kuchochea kanisa lishiriki katika kutetea mnyanyaso wa kijamii, kisiasa, na kiuchumi lakini njia ambayo wafuasi wake walieleza mawazo yao ilikuwa na makosa sana hivi kwamba sikuielewa.

Wakati huohuo, daktari wangu wa meno, ambaye alikuwa Mbudha, alinipa kitabu alichokuwa amepewa. Kitabu hicho kilikuwa na kichwa Did Man Get Here by Evolution or by Creation? * Nilikikubali, nikifikiri kwamba ningefurahia kukisoma pamoja na kitabu The Origin of Species, cha Charles Darwin. Njia ambayo kitabu Did Man Get Here by Evolution or by Creation? kilieleza mambo ilikuwa yenye nguvu, inayopatana na akili, na yenye kusadikisha. Sasa nikaamini kwamba nadharia ya mageuzi haikuwa na msingi wowote.

Kusoma kitabu hicho cha uumbaji kulichochea zaidi tamaa yangu ya kujua mengi. Nilitaka kupata vitabu vingi zaidi vilivyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Niliambiwa kwamba fundi fulani katika shule ya ndege alikuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Nilizungumza naye, na akanipa vitabu fulani ili nivisome. Wakati huo, nilikataa kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Nilifikiri ningejifunza Biblia mwenyewe.

Nilipoanza kusoma Biblia, niliamua kwamba kwa vile nilikuwa nimefunga ndoa, lingekuwa jambo la hekima kuisoma pamoja na familia yangu. Tulijifunza tukiwa familia kila juma na kusoma Biblia pamoja. Kwa sababu tulikuwa Wakatoliki, familia yetu ilishirikiana sana na makasisi na maaskofu. Hivyo, jambo nililosoma kwenye Yohana 14:6 lilinivutia sana: “Yesu akamwambia [mwanafunzi Tomasi]: ‘Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.’” Baada ya kuchunguza jambo hilo kwa undani, nilisadikishwa kwamba wokovu wetu unatoka kwa Yehova kupitia Yesu. Mwanzoni tulikuwa tumefundishwa na kuamini kwamba wokovu wetu ulitoka kwa makasisi.

Kuna maandiko mengine mawili yaliyobadili mtazamo wangu kuelekea Kanisa Katoliki na mafundisho yake. Andiko moja ni Methali 1:7, linalosema: “Kumwogopa Yehova ndio mwanzo wa ujuzi. Wapumbavu wamedharau hekima na nidhamu.” Na lingine ni Yakobo 1:5, linalosema: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu; naye atapewa hiyo.” Nilikuwa na tamaa kubwa ya kupata ujuzi na hekima, tamaa ambayo haikutoshelezwa kwa kwenda kanisani. Hivyo, nikaacha kuhudhuria.

Mwaka wa 1980, mke wangu alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Nilipokuwa nyumbani, ningeshiriki katika funzo hilo. Baada ya muda, nilikubali funzo la Biblia. Hata hivyo, muda mrefu ulipita kabla hatujakubali kubatizwa na kuwa Mashahidi wa Yehova. Mke wangu alibatizwa mwaka wa 1994, na mimi 1998.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Watoto wangu wanne wamefaidika kwa kuzoezwa kuishi kulingana na viwango vya Yehova. (Waefeso 6:4) Nina wana wawili, wote wanajitahidi kushughulikia mahitaji ya kiroho ya Mashahidi wengine katika makutaniko wanayoshirikiana nayo. Binti zangu wawili wana bidii sana katika kazi ya kuwahubiria wengine. Mke wangu anatumia saa nyingi kila mwezi kuwasaidia watu wajifunze kuhusu Biblia, nami ninafurahia kutumika kama mzee katika kutaniko letu.

Nilipobatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, nilipata ujuzi mwingi zaidi kuhusu mema na mabaya. Nikiwa hakimu, mimi hujaribu kutumia njia ambayo Yehova hushughulikia mambo mbalimbali ninapokuwa mahakamani, huku nikichunguza mambo yote yaliyohusika, kuwa na usawaziko, na kuonyesha huruma ikiwa kuna sababu za kupunguza adhabu dhidi ya wakosaji.

Nimeshughulikia visa vingi vya jeuri, vya uhalifu, na vya kuwatendea watoto vibaya, vilevile visa vingine vya makosa mazito. Hata hivyo, visa hivyo havijaathiri hisia zangu. Ninapotazama habari kwenye televisheni, ninachukizwa na kuenea kwa upotovu wa maadili na uovu duniani. Ninamshukuru Yehova kwa kuwa nimeelewa chanzo cha ongezeko la uhalifu, vilevile tumaini letu la wakati ujao mzuri.

“Gereza Halikurekebisha Tabia Yangu.”​—KEITH WOODS

MWAKA WA KUZALIWA: 1961

NCHI: IRELAND KASKAZINI

HISTORIA: GAIDI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa mwaka wa 1961 huko Portadown, mji wenye shughuli nyingi ulio Ireland Kaskazini. Nililelewa katika familia ya Kiprotestanti, na tuliishi katika eneo lililokuwa na majirani Wakatoliki na Waprotestanti. Familia nyingi zilikuwa maskini. Ingawa hakukuwa na pesa nyingi, sote tulikuwa na uhusiano wa karibu.

Niliishi maisha ambayo sipendi kuyakumbuka. Mwaka wa 1974, nilijihusisha na “Mapigano” yaliyokuwa huko Ireland Kaskazini. Wakati huo, mambo yaliharibika zaidi katika ujirani wetu. Kwa mfano, usiku mmoja, baba yangu ambaye alikuwa msimamizi katika kampuni ya kutengeneza mazulia ya Ulster, alikuwa kazini akiwazoeza vijana wawili Wakatoliki ambao walikuwa jirani zetu. Wakati huohuo, mtu fulani alitupa bomu kupitia dirisha la sebule ya nyumba ambayo wavulana hao Wakatoliki waliishi na kumuua baba, mama, na ndugu yao.

Matatizo yaliongezeka na vita vikatokea. Nyumba za Waprotestanti zilichomwa katika maeneo ya Wakatoliki, nao Wakatoliki wakanyanyaswa katika maeneo ya Waprotestanti. Kisha, eneo tuliloishi likamilikiwa na Waprotestanti. Muda mrefu haukupita kabla sijakamatwa na kufungwa gerezani kwa miaka mitatu kwa sababu ya kujihusisha na ulipuaji wa mabomu.

Nilipokuwa gerezani, nilifanya urafiki na mfungwa fulani aliyejulikana sana wa kikundi cha kisiasa kilichopigania kuunganishwa kwa Ireland Kaskazini na Uingereza. Tulikuwa kama ndugu, na baadaye nikasimamia harusi yake. Gereza halikurekebisha tabia yangu wala yake. Tulipoachiliwa, tulirudi moja kwa moja kwenye shughuli zetu za kisiasa, lakini sasa kwa njia kubwa hata zaidi. Matokeo ni kwamba rafiki yangu alifungwa tena gerezani. Akiwa huko, akauawa.

Mimi pia nilianza kutafutwa, na pindi moja gari langu likalipuliwa. Lakini matukio hayo yaliimarisha zaidi azimio langu la kujishughulisha na kampeni zilizojulikana kama “Mungu na Ulster.”

Wakati huo, nilishiriki katika kutayarisha kipindi kilichohusu “Mapigano,” ambacho kilionyeshwa kwenye televisheni ya Uingereza. Kipindi hicho kilinisababishia matatizo zaidi. Kwa mfano, usiku mmoja nilirudi nyumbani na kutambua kwamba mke wangu alikuwa ameniacha. Muda mfupi baadaye, kwa sababu ya kile kipindi cha televisheni, mwanangu alichukuliwa. Ninakumbuka nikitazama kioo na kujiambia, “Ikiwa kweli Mungu upo, naomba unisaidie.”

Jumamosi iliyofuata nilikutana na Paul, mwanamume niliyemfahamu ambaye alikuwa amebatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Alianza kunieleza kuhusu Biblia. Siku mbili baadaye, Paul alinitumia nakala ya Mnara wa Mlinzi. Makala fulani katika gazeti hilo ilinukuu maneno ya Yesu yaliyoandikwa kwenye Yohana 18:36. Alisema hivi: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungekuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangepigana ili nisitiwe mikononi mwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu hautoki katika chanzo hiki.” Maneno hayo yalinigusa moyo sana. Hiyo ndiyo siku ambayo maisha yangu yalianza kubadilika.

JINSI AMBAVYO BIBLIA ILIBADILI MAISHA YANGU: Paul alianza kujifunza Biblia pamoja nami. Baadaye, Shahidi mwingine anayeitwa Bill aliendelea kujifunza nami. Ninajua kwamba nilikuwa mwanafunzi msumbufu; nilikuwa na maswali mengi sana! Pia, nilileta wahubiri wengi wa kidini nyumbani kwangu ili wamthibitishie Bill kwamba hakujua ukweli. Lakini niliona ukweli wa Neno la Mungu.

Ninakumbuka siku moja nikimwambia Bill asije nyumbani kwangu kwa ajili ya funzo kwa sababu kulikuwa na vizuizi barabarani katika eneo letu na angepokonywa gari lake kisha liteketezwe. Hata hivyo, Bill alikuja kwenye funzo kama kawaida. Aliacha gari lake nyumbani na akatumia baiskeli. Hakuna mtu ambaye angempokonya baiskeli. Pindi nyingine, mimi na Bill tulikuwa tumeketi katika nyumba yangu tukijifunza Biblia polisi na askari-jeshi walipokuja kunikamata. Walipokuwa wakinivuta na kwenda nami, Bill aliniambia kwa sauti nimtegemee Yehova. Pindi hizo zilinigusa moyo sana.

Mara ya kwanza nilipohudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova katika Jumba la Ufalme, bila shaka wengine wao walishtuka. Nilikuwa na nywele ndefu na kipuli, na nilivalia koti la ngozi lililonitambulisha kuwa mshiriki wa kikundi cha kisiasa. Hata hivyo, nilishangazwa sana na jinsi Mashahidi walivyonitendea vizuri. Nilivutiwa sana na fadhili walizonionyesha.

Hata ingawa nilikuwa nikijifunza Biblia, bado nilishirikiana na marafiki wangu wa zamani. Hata hivyo, mwishowe kweli nilizojifunza katika Biblia zilianza kupenya moyoni mwangu. Nilitambua kwamba ikiwa nilitaka kumtumikia Yehova, nilipaswa kubadili maoni yangu ya kisiasa na watu nilioshirikiana nao. Hilo halikuwa jambo rahisi. Lakini nilipozidi kujifunza mengi kuhusu Biblia na kupata nguvu kutoka kwa Yehova, nilifaulu kufanya mabadiliko. Nilinyoa nywele zangu, nikavua kipuli changu, na nikanunua suti. Pia, mambo niliyokuwa nikijifunza yakaanza kubadili mtazamo wangu kuelekea wengine.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Nilikuwa mhalifu na gaidi. Nilijulikana sana na vikundi vya kulinda usalama katika eneo letu. Sasa mambo yamebadilika. Kwa mfano, nilipohudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova kwa mara ya kwanza, ambalo lilifanywa katika mji wa Navan, walinda-usalama walinisindikiza niliposafiri kupitia Ireland na kuingia Ireland Kaskazini. Hata hivyo, sasa ninasafiri kwenda kwenye makusanyiko bila kusindikizwa. Pia, ninashirikiana kwa uhuru pamoja na Mashahidi wenzangu, Paul na Bill na washiriki wengine wa kutaniko katika kazi ya kuhubiri.

Maisha yangu yalipobadilika na kuwa bora, nikawa mshiriki wa kutaniko. Kutanikoni nilikutana na Shahidi anayeitwa Louise, na tukafunga ndoa. Zaidi ya hayo, nilianza tena kuishi na mwanangu.

Ninapokumbuka maisha yangu ya zamani, ninasikitika kwa sababu ya kuwaumiza wengine na kuwasababishia uchungu. Lakini ninaweza kuthibitisha kwamba kwa kweli Biblia inaweza kuwasaidia watu kama mimi wabadilike na kuacha maisha mapotovu na kuishi wakiwa na kusudi na tumaini.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova lakini sasa hakichapishwi tena.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Mama yangu alikasirika sana alipotambua kwamba nilikuwa nikisoma Biblia