Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mkaribie Mungu

Yehova Anachukia Ukosefu wa Haki

Yehova Anachukia Ukosefu wa Haki

“MWANADAMU amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Maneno hayo yaliyoandikwa miaka 3,000 hivi iliyopita, yanaonyesha kwa usahihi hali katika ulimwengu tunaoishi. Wanadamu wana mwelekeo wa kutumia mamlaka vibaya bila kujali wao ni nani au wanaishi wapi. Mara nyingi wanawatendea isivyo haki watu wasio na uwezo na wanyonge. Yehova anahisije anapoona ukosefu huo wa haki? Tunapata jibu katika andiko la Ezekieli 22:6, 7, 31.​—Soma.

Katika Sheria aliyowapa Waisraeli, Yehova alitaja waziwazi kwamba watu wenye mamlaka hawakupaswa kutumia mamlaka yao vibaya. Angelibariki taifa hilo ikiwa tu viongozi wao wangewajali na kuwatendea watu wa hali ya chini kwa fadhili. (Kumbukumbu la Torati 27:19; 28:15, 45) Hata hivyo, katika siku za Ezekieli, wakuu huko Yerusalemu na Yuda walitumia vibaya mamlaka yao kwa njia za uovu. Walikuwa wakifanya nini?

Wakuu hao walitumia ‘mkono wao kumwaga damu.’ (Mstari wa 6) Neno “mkono” linawakilisha nguvu au mamlaka. Hivyo, tafsiri nyingine inasema: “Wakuu wa Israeli . . . wametumia nguvu zao kumwaga damu.” Kunawezaje kuwa na haki ikiwa viongozi ambao wanapaswa kudumisha na kuendeleza ufuataji wa sheria wanatumia vibaya nguvu na kuwaua watu wasio na hatia?

Baada ya kusema hayo, Ezekieli anawashtaki viongozi na pia wale waliowaunga mkono kutotii Sheria za Yehova. Ezekieli anasema hivi: “Wamemtendea dharau baba na mama.” (Mstari wa 7) Kwa kudharau jukumu la wazazi, watu hao walivunja msingi wa taifa lao, yaani, familia.​—Kutoka 20:12.

Watu hao wafisadi waliwadhulumu watu wanyonge waliokuwa miongoni mwao. Kila tendo la ukosefu wa sheria lilionyesha kwamba walidharau Sheria za Mungu kwa Waisraeli ambazo zilichochewa na upendo. Kwa mfano, Sheria ya Mungu iliwaagiza Waisraeli wawajali watu walioishi miongoni mwao ambao hawakuwa Waisraeli. (Kutoka 22:21; 23:9; Mambo ya Walawi 19:33, 34) Lakini watu hao walimtendea “kwa upunjaji” mkaaji mgeni.​—Mstari wa 7.

Pia, watu hao waliwatendea vibaya watu ambao hawakuwa na mtu wa kuwalinda, yaani, “mvulana asiye na baba na mjane.” (Mstari wa 7) Yehova huwajali sana wale wanaofiwa na mzazi au mwenzi wa ndoa. Mungu aliahidi kwamba angewaadhibu watu ambao wangewatesa watoto au wajane wasio na mtu wa kuwalinda.​—Kutoka 22:22-24.

Kwa matendo hayo na mengine, Waisraeli katika siku za Ezekieli walivunja Sheria za Mungu na hivyo kutoheshimu sheria hizo zilizoongozwa na upendo. Yehova angefanya nini? Aliahidi hivi: “Nitamwaga shutuma zangu juu yao.” (Mstari wa 31) Alitenda kulingana na maneno yake kwa kuruhusu Wababiloni waharibu Yerusalemu na kupeleka wakaaji wake utekwani mwaka wa 607 K.W.K.

Maneno ya Ezekieli yanatufundisha mambo mawili kumhusu Yehova na jinsi anavyoona ukosefu wa haki: Kwanza, anachukia ukosefu wa haki; pili, anawahurumia wale wanaotendewa isivyo haki. Mungu hajabadilika. (Malaki 3:6) Anaahidi kwamba hivi karibuni ataondoa ukosefu wa haki na watu wanaousababisha. (Methali 2:21, 22) Tunakutia moyo ujifunze mengi kumhusu Mungu huyo ambaye ni “mpenda-haki” na jinsi unavyoweza kumkaribia zaidi.​—Zaburi 37:28.

Usomaji wa Biblia Unaopendekezwa kwa Mwezi wa Agosti:

Ezekieli 21-38

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Yehova alitaja waziwazi kwamba watu wenye mamlaka hawakupaswa kutumia mamlaka yao vibaya