Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Mawe ya thamani kwenye kifuko cha kifuani cha kuhani mkuu wa Israeli yalitoka wapi?

Baada ya Waisraeli kuondoka Misri na kuingia nyikani, Mungu aliwapa maagizo ya kutengeneza kifuko cha kifuani. (Kutoka 28:15-21) Kifuko hicho kilikuwa na mawe ya thamani kama vile, zibarijadi, topazi, zumaridi, feruzi, yakuti, yaspi, leshemi, akiki, amethisti, krisolito, shohamu, na yashefi. * Je, kweli Waisraeli wangepata mawe hayo mbalimbali yenye thamani?

Katika nyakati za Biblia watu walithamini sana mawe yenye thamani na hata waliyatumia katika biashara. Kwa mfano, Wamisri wa kale walipata mawe yenye thamani kutoka maeneo ya mbali, kama vile nchi ambazo sasa ni Iran, Afghanistan, na huenda hata India. Migodi iliyokuwa Misri ilikuwa na aina mbalimbali za mawe yenye thamani. Wafalme wa Misri walimiliki uchimbaji wa madini katika maeneo waliyoyadhibiti. Mzee wa ukoo Ayubu alifafanua jinsi rafiki zake walivyotumia vifaa vya kuchimba ili kutafuta hazina. Kati ya mawe yenye thamani yaliyochimbwa ardhini, Ayubu anataja kihususa yakuti na topazi.​—Ayubu 28:1-11, 19.

Simulizi kwenye kitabu cha Kutoka linasema kwamba Waisraeli walipoondoka ‘waliwaacha Wamisri bila chochote.’ (Kutoka 12:35, 36) Kwa hiyo, inawezekana kwamba Waisraeli walitoa Misri mawe yenye thamani waliyoweka kwenye kifuko cha kifuani cha kuhani mkuu.

Kwa nini, divai ilitumiwa kama dawa nyakati za Biblia?

Katika mojawapo ya mifano yake Yesu alitaja kuhusu mwanamume aliyekuwa amepigwa na wanyang’anyi. Yesu alisema kwamba mwanamume huyo alisaidiwa na Msamaria ambaye alifunga majeraha yake na kumwaga “mafuta na divai juu yake.” (Luka 10:30-34) Alipomwandikia rafiki yake Timotheo, mtume Paulo alimshauri hivi: “Usiendelee kunywa maji, bali utumie divai kidogo kwa ajili ya tumbo lako na ugonjwa wako wa mara kwa mara.” (1 Timotheo 5:23) Je, jambo ambalo Yesu alizungumzia na pia ushauri ambao Paulo alitoa ulikuwa sahihi kitiba?

Kitabu kiitwacho Ancient Wine kinaelezea divai kuwa “dawa yenye uwezo wa kupunguza maumivu na pia kuua viini.” Katika nyakati za kale divai ilikuwa muhimu sana katika matibabu huko Misri, Mesopotamia, na Siria. Kitabu The Oxford Companion to Wine kinafafanua divai kuwa “dawa ya zamani zaidi kuwahi kutumiwa na mwanadamu.” Kuhusu ushauri wa mtume Paulo kwa Timotheo, kitabu kinachoitwa The Origins and Ancient History of Wine kinasema hivi: “Imethibitishwa kisayansi kwamba vijidudu vya homa ya matumbo pamoja na vijidudu vingine hatari hufa mara moja vinapochanganywa na divai.” Utafiti wa kisasa umeonyesha kwamba visehemu zaidi ya 500 vinavyopatikana katika divai vina faida hizo na nyingine nyingi za kitiba.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Leo inaweza kuwa vigumu kutambua majina ya kisasa ya mawe hayo.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Wakulima wakikanyaga zabibu, kwenye kaburi la Nakht, Thebes, huko Misri

[Hisani]

Gianni Dagli Orti/​The Art Archive at Art Resource, NY