Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dini Yangu Ni Chaguo Langu au la Wazazi Wangu?

Je, Dini Yangu Ni Chaguo Langu au la Wazazi Wangu?

Je, Dini Yangu Ni Chaguo Langu au la Wazazi Wangu?

NCHINI Poland watu wengi wanawaambia Mashahidi wa Yehova, “Nilizaliwa katika dini yangu na nitakufa katika dini hiyo.” Hilo linaonyesha kwamba, kulingana na maoni yao, dini inapitishwa kutoka kwa kizazi kimoja mpaka kingine. Je, watu katika eneo lenu wana maoni kama hayo kuhusu dini? Mara nyingi mtazamo kama huo una matokeo gani? Watu wenye mtazamo huo wanafuata dini kwa sababu tu ya desturi au kwa sababu ni dini ya familia. Je, inaweza kuwa hivyo kwa Mashahidi wa Yehova ambao wamepokea urithi mzuri ajabu wa kiroho kutoka kwa wazazi wao au kutoka kwa babu na nyanya yao?

Haikuwa hivyo kwa Timotheo ambaye alisaidiwa na mama na nyanya yake waliomwogopa Mungu, ili amwamini na kumpenda Mungu wa kweli. Timotheo alijua maandishi matakatifu “tangu utoto mchanga.” Baada ya muda, Timotheo akiwa pamoja na mama na nyanya yake, walisadiki kwamba Ukristo ulikuwa ndio njia ya kweli. ‘Alishawishiwa kuamini’ mambo aliyosikia kutoka kwa Maandiko kumhusu Yesu Kristo. (2 Tim. 1:5; 3:14, 15) Hivyo basi, ingawa wazazi Wakristo leo wanajitahidi kabisa kuwasaidia watoto wao wawe watumishi wa Yehova, watoto wenyewe wanahitaji kusitawisha tamaa ya kumtumikia Yehova.—Marko 8:34.

Ni lazima kila mtu ashawishiwe kuamini kupitia sababu zenye kusadikisha ili amtumikie Yehova kwa kuchochewa na upendo na adumishe utimilifu chini hali zozote zile. Kisha imani yake itakuwa yenye nguvu na yenye msingi mzuri.—Efe. 3:17; Kol. 2:6, 7.

Daraka la Watoto

Albert, * ambaye alilelewa katika familia ya Mashahidi anaeleza hivi: “Sikuzote nimehisi kwamba Mashahidi wa Yehova wana dini ya kweli, lakini haikuwa rahisi kwangu kuamini mambo waliyokuwa wakisema kuhusu vile ninavyopaswa kuishi.” Ikiwa wewe ni kijana, huenda ukawa na maoni kama ya Albert. Kwa nini usijitahidi kuona mambo yanayohusika katika namna ya maisha ambayo Mungu anataka tuishi kisha upendezwe kufanya mapenzi yake? (Zab. 40:8) Albert anasema: “Nilianza tu kusali. Mwanzoni, ilikuwa vigumu. Lakini nilijilazimisha kusali. Hata hivyo, baada ya muda, nilihisi kwamba ningekuwa mwenye thamani mbele za Mungu ikiwa ningejaribu kufanya yaliyo sawa. Hilo lilinitia nguvu kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa.” Ukisitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova, unaweza kukuza tamaa ya kufanya mambo anayotaka tufanye.—Zab. 25:14; Yak. 4:8.

Hebu fikiria mchezo ambao umewahi kucheza, kama vile mchezo wa kandanda. Ikiwa hujui sheria za mchezo huo, au huwezi kuucheza vizuri, huenda ukakuchosha. Hata hivyo, ikiwa ulijifunza sheria za mchezo huo na kujua kuucheza vizuri, bila shaka utakuwa na hamu ya kuucheza na hata utatafuta nafasi za kucheza. Ndivyo ilivyo na utendaji wa Kikristo. Kwa hiyo, chukua hatua ya kutayarisha mikutano ya Kikristo. Shiriki katika mikutano hiyo. Hata ukiwa na umri gani, unaweza kuwatia wengine moyo kupitia mfano wako!—Ebr. 10:24, 25.

Ndivyo ilivyo pia kuhusu kuwaambia wengine juu ya imani yako. Hilo pia linapaswa kufanywa kwa sababu ya upendo, bali si kwa kulazimishwa. Jiulize hivi: ‘Kwa nini ninataka kuwaambia wengine kumhusu Yehova? Ni sababu gani zinazonifanya nimpende Yehova?’ Unahitaji kumjua Yehova akiwa Baba mwenye upendo. Yehova alisema hivi kupitia Yeremia: “Kwa kweli mtanitafuta na kunipata, kwa maana mtanitafuta kwa moyo wenu wote.” (Yer. 29:13, 14) Huenda ukalazimika kufanya nini? Jakub anasema hivi: “Nililazimika kubadili njia yangu ya kufikiri. Nimekuwa nikihudhuria mikutano na kwenda katika utumishi tangu nilipokuwa mtoto, lakini nilianza kuyaona mambo hayo kuwa ya kawaida. Ni baada tu ya kumjua Yehova vizuri zaidi na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye ndipo nilipoanza kuipenda kweli.”

Ushirika mzuri wenye kujenga unaweza kukusaidia sana kufurahia utumishi wako. Methali iliyoongozwa na roho ya Mungu inasema hivi: “Anayetembea na watu wenye hekima atakuwa na hekima.” (Met. 13:20) Kwa hiyo, tafuta marafiki ambao wanafuatia miradi ya kiroho na ambao wanafurahia kumtumikia Yehova. Jola anasema: “Nilitiwa moyo sana kwa kushirikiana na vijana wengi ambao walikazia fikira utumishi wao kwa Yehova. Nilianza kuhubiri kwa ukawaida nikiwa na shangwe nyingi.”

Daraka la Wazazi

Jola anasema: “Ninawashukuru sana wazazi wangu kwa kunifundisha kumhusu Yehova.” Ndiyo, wazazi wanaweza kuwa na uvutano mkubwa juu ya maamuzi ambayo watoto wao wanafanya. Mtume Paulo aliandika hivi: “Akina baba, . . . endeleeni kuwalea [watoto wenu] katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Shauri hilo lililoongozwa na roho ya Mungu linaonyesha waziwazi kwamba daraka la wazazi ni kuwafundisha watoto wao njia za Yehova, bali si zao wenyewe. Badala ya kukazia katika akili za watoto wako mambo ambayo huenda ulitaka kutimiza, ni jambo bora kama nini ikiwa ungewasaidia kujiwekea mradi wa kuishi kupatana na makusudi ya Yehova!

Unaweza kuyakazia maneno ya Yehova ndani ya watoto wako na “kuyasema unapoketi katika nyumba yako na unapotembea barabarani na unapolala na unapoamka.” (Kum. 6:6, 7) Ewa na Ryszard, wazazi wa wavulana watatu wanakumbuka hivi: “Tulizungumza sana kuhusu aina mbalimbali za utumishi wa wakati wote.” Matokeo yalikuwa nini? “Wavulana wetu walitaka kujiandikisha katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi wakiwa wachanga, wakawa wahubiri, na mwishowe wakaamua wenyewe kubatizwa. Baadaye, walitumika Betheli au wakawa mapainia.”

Mfano mzuri wa wazazi ni wa maana sana. Ryszard anasema, “Tulikuwa tumeazimia kutoishi maisha ya unafiki, yaani, kutenda kwa njia fulani nyumbani na kwa njia tofauti katika kutaniko.” Kwa hiyo, jiulize hivi: ‘Watoto wangu wanaona nini katika maisha yangu? Je, wanaona kwamba ninampenda Yehova kikweli? Je, wanaona upendo huo kupitia sala zangu na zoea langu la kujifunza kibinafsi? Je, wanauona katika mtazamo wangu kuelekea utumishi wa shambani, burudani, na vitu vya kimwili na katika mambo ninayosema kuhusu washiriki wengine wa kutaniko?’ (Luka 6:40) Watoto watachunguza maisha yako ya kila siku na watatambua ikiwa kuna tofauti yoyote kati ya mambo unayosema na yale unayofanya.

Nidhamu ni jambo la maana sana katika kuwalea watoto. Ingawa hivyo, Neno la Mungu lililoongozwa na roho linatuambia ‘tumlee mvulana kulingana na njia inayomfaa.’ (Met. 22:6) Ewa na Ryszard wanasema hivi: “Tulitumia wakati wa kutosha ili kujifunza Biblia na kila mtoto.” Kwa kweli, wazazi ndio watakaoamua ikiwa itafaa kujifunza na kila mtoto. Kwa vyovyote vile, kila mtoto anahitaji kutendewa kama mtu binafsi. Hilo linahitaji kubadili ratiba na kuwa na usawaziko. Kwa mfano, badala ya kuwaambia tu watoto wako kwamba muziki fulani ni mbaya, kwa nini usiwafundishe jinsi wanavyoweza kufanya maamuzi yenye hekima, na jinsi kanuni za Biblia zinavyohusika?

Huenda watoto wako wakajua vizuri jambo unalotaka wafanye na inaweza kuonekana kwamba wanatii maagizo yako. Hata hivyo, unahitaji kufikia mioyo yao. Kumbuka kwamba “shauri moyoni mwa mtu ni kama kilindi cha maji, lakini mtu mwenye utambuzi ataliteka.” (Met. 20:5) Uwe na utambuzi, chunguza dalili za tatizo lolote ambalo huenda limejificha ndani ya mioyo ya watoto wako, na uchukue hatua mara moja. Bila kuwashutumu, onyesha kwamba jambo hilo linakuhangaisha, na uwaulize maswali yanayofaa. Hata hivyo, uwe mwangalifu ili usiulize maswali mengi kupita kiasi. Ukipendezwa nao kikweli, utawafikia moyo na hilo litakuwezesha kuwasaidia.

Daraka la Kutaniko

Ukiwa mmoja wa watumishi wa Mungu, je, unaweza kuwasaidia vijana katika kutaniko wathamini urithi wa kiroho ambao wamepokea? Ingawa ni daraka la wazazi kuwazoeza watoto wao, washiriki wengine wa kutaniko, hasa wazee, wanaweza kuwasaidia. Ni jambo la maana hasa kusaidia familia ambazo zina mzazi mmoja ambaye si Shahidi wa Yehova.

Wazee wanaweza kufanya nini ili kuwasaidia vijana wampende Yehova na wahisi kwamba wanahitajiwa na kuthaminiwa? Mariusz, ambaye anatumikia akiwa mwangalizi katika kutaniko moja huko Poland, anasema hivi: “Wazee wanapaswa kuwasiliana, kuwasiliana, kuwasiliana na vijana. Hawapaswi kuwasiliana tu wakati matatizo yanapotokea, bali pia kwenye pindi nyingine, kama vile katika utumishi wa shambani, baada ya mikutano, na katika vikao vingine visivyo rasmi.” Kwa nini usiwaulize vijana maoni yao kuhusu kutaniko? Mawasiliano kama hayo yaliyo wazi yanawavuta vijana karibu zaidi na kutaniko na yanawafanya wajihisi kwamba wao ni sehemu ya kutaniko.

Ikiwa wewe ni mzee, je, unajitahidi kuwafahamu vijana katika kutaniko lenu? Ingawa sasa anatumikia akiwa mzee, Albert aliyetajwa mwanzoni, alipata majaribu mbalimbali alipokuwa kijana. Anasema hivi: “Nilipokuwa kijana, nilitamani kufanyiwa ziara ya uchungaji.” Wazee wanaweza pia kuonyesha kwamba wanapendezwa kibinafsi na vijana kwa kusali ili vijana wafaulu katika kumtumikia Mungu na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye.—2 Tim. 1:3.

Ni jambo zuri kwa vijana kushiriki katika utendaji wa kutaniko. Ikiwa sivyo, huenda wakakazia fikira kufuatia miradi ya kilimwengu. Ninyi mlio na umri mkubwa, je, mnaweza kuhubiri na kuanzisha urafiki pamoja nao? Tumia wakati wako wa kupumzika pamoja na vijana, ili wakuamini na kuwa marafiki wako. Jola anakumbuka: “Dada mmoja painia alipendezwa na mimi kibinafsi. Yeye ndiye mtu wa kwanza ambaye nilienda naye katika utumishi kwa sababu nilitaka.”

Chaguo Lako la Kibinafsi

Vijana, jiulizeni hivi: ‘Nina miradi gani? Ikiwa bado sijabatizwa, je, nina mradi wa kubatizwa?’ Uamuzi wa kubatizwa unapaswa kuchochewa na kumpenda Yehova kutoka moyoni bali si kwa sababu ya kulazimishwa au kufuata desturi ya familia.

Ndiyo, Yehova na awe Rafiki yako wa kweli, na ukweli uwe hazina yako. Yehova alisema hivi kupitia nabii Isaya: “Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako.” Yehova atakuwa pamoja nawe ikiwa tu utakuwa rafiki yake. Kwa kweli, atakutia nguvu na ‘kukushika kwelikweli kwa mkono wake wa kuume wa uadilifu.’—Isa. 41:10.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 6 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Jaribuni kutambua mambo yaliyo ndani ya moyo wa mtoto wenu

[Picha katika ukurasa wa 6]

Uamuzi wa kubatizwa unachochewa na kumpenda kabisa Yehova kutoka moyoni