Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kushinda Magumu ya Huduma ya Nyumba kwa Nyumba

Kushinda Magumu ya Huduma ya Nyumba kwa Nyumba

Kushinda Magumu ya Huduma ya Nyumba kwa Nyumba

“Tulijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu ili kuwaambia ninyi habari njema ya Mungu kwa kupambana sana.”—1 THE. 2:2.

1. Yeremia alikabili magumu gani, naye aliyashinda jinsi gani?

YEREMIA alikuwa mtu mwenye hisia kama zetu. Yehova alipompa utume wa kuwa “nabii kwa mataifa,” Yeremia alipaaza sauti na kusema: “Ole wangu, Ee Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova! Tazama, mimi hakika sijui jinsi ya kusema, kwa sababu mimi ni mvulana tu.” Hata hivyo, Yeremia alimtegemea Yehova na kukubali mgawo huo. (Yer. 1:4-10) Kwa miaka zaidi ya 40, Yeremia aliwahubiria watu wasiopendezwa, ambao walimkataa, walimdhihaki, na hata kumtendea kijeuri. (Yer. 20:1, 2) Nyakati nyingine, aliona ni afadhali aache kuhubiri. Lakini, alivumilia na kuendelea kutangaza ujumbe usiopendwa wala kukubaliwa na watu wengi. Kwa nguvu za Mungu, Yeremia alitimiza mambo ambayo hangeweza kuyafanya kwa nguvu zake mwenyewe.—Soma Yeremia 20:7-9.

2, 3. Watumishi wa Mungu leo wanakabili jinsi gani magumu kama yale ambayo Yeremia alikabili?

2 Leo, watumishi wengi wa Mungu wanaelewa jinsi Yeremia alivyohisi. Tulipofikiria kuanza kuhubiri nyumba kwa nyumba, wengine wetu tulisema hivi, ‘Siwezi hata kidogo.’ Hata hivyo, tulipotambua kwamba ni mapenzi ya Yehova tutangaze habari njema, tulishinda wasiwasi wetu na tukaanza kuhubiri kwa bidii. Zaidi ya hayo, wengi wetu tulipatwa na hali fulani maishani zilizofanya iwe vigumu, angalau kwa muda fulani, kuendelea kuhubiri. Ndiyo, si rahisi kuanza kuhubiri nyumba kwa nyumba na kuendelea kuhubiri mpaka mwisho.—Mt. 24:13.

3 Namna gani ikiwa umekuwa ukijifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa muda fulani lakini unasita kuanza kuhubiri nyumba kwa nyumba? Au namna gani ikiwa wewe ni Shahidi aliyebatizwa na unaona ni vigumu kuhubiri nyumba kwa nyumba ingawa una nguvu za kufanya hivyo? Uwe na hakika kwamba watu wa aina zote wanashinda magumu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwa msaada wa Yehova, hata wewe unaweza kuyashinda.

Kujipa Ujasiri

4. Ni nini kilichomwezesha mtume Paulo kutangaza habari njema kwa ujasiri?

4 Bila shaka, unatambua kwamba kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote inatimizwa, si kwa uwezo au hekima ya wanadamu, bali kwa roho ya Mungu. (Zek. 4:6) Ndivyo ilivyo pia kuhusu huduma ya kila Mkristo. (2 Kor. 4:7) Fikiria mtume Paulo. Akikumbuka wakati yeye na mwandamani mwenzake mmishonari walivyotendewa vibaya na wapinzani, aliandika hivi: “Baada ya sisi kuwa tumeteseka kwanza na kutendewa kwa dharau . . . katika Filipi, tulijipa ujasiri kwa njia ya Mungu wetu ili kuwaambia ninyi habari njema ya Mungu kwa kupambana sana.” (1 The. 2:2; Mdo. 16:22-24) Ni vigumu kwetu kuwazia kwamba mhubiri mwenye bidii kama Paulo alihitaji kujikaza nyakati nyingine ili kuhubiri. Hata hivyo, kama sisi sote, Paulo alihitaji kumtegemea Yehova ili atangaze habari njema kwa ujasiri. (Soma Waefeso 6:18-20.) Tunaweza kuiga mfano wa Paulo kwa njia gani?

5. Taja njia moja ya kujipa ujasiri wa kuhubiri.

5 Njia moja ya kujipa ujasiri wa kuhubiri ni kusali. Painia mmoja alisema hivi: “Ninasali ili nizungumze kwa uhakika, ninasali ili niweze kufikia mioyo ya watu, na ninasali ili nipate shangwe katika huduma. Hii ni kazi ya Yehova, si kazi yetu, kwa hiyo hatuwezi kufanya chochote bila msaada wake.” (1 The. 5:17) Sote tunahitaji kuendelea kusali ili tupate roho takatifu ya Mungu ambayo itatusaidia kuhubiri kwa ujasiri.—Luka 11:9-13.

6, 7. (a) Ezekieli alipata maono gani, nayo yalimaanisha nini? (b) Watumishi wa Mungu leo wanajifunza somo gani kutokana na maono ya Ezekieli?

6 Kitabu cha Ezekieli kinafunua jambo lingine linaloweza kutusaidia kusema kwa ujasiri. Katika maono, Yehova alimpa Ezekieli kitabu cha kukunjwa kilichokuwa kimeandikwa pande zote mbili “nyimbo za huzuni na maombolezo na vilio” na Yehova akamwambia ale, huku akisema: “Mwana wa binadamu, unapaswa kulisha tumbo lako, ili ujaze matumbo yako kwa kitabu hiki ninachokupa wewe.” Maono hayo yalimaanisha nini? Ezekieli alipaswa kula kabisa ujumbe ambao angetangaza. Ni kana kwamba ujumbe huo ulipaswa kuwa sehemu yake, yaani, ulipaswa kugusa hisia zake za ndani zaidi. Nabii huyo anaendelea kusema hivi: “Nami nikaanza kukila, nacho kikawa kitamu kama asali kinywani mwangu.” Ezekieli aliona kutangaza ujumbe wa Mungu hadharani kuwa jambo la kufurahisha, kama kuonja asali. Aliona kuwa ana pendeleo la pekee la kumwakilisha Yehova na kutimiza mgawo aliopewa na Mungu, hata ingawa hilo lilihusisha kuwatangazia ujumbe mzito watu wasiopendezwa.—Soma Ezekieli 2:8–3:4, 7-9.

7 Maono hayo yana somo la maana kwa watumishi wa Mungu leo. Sisi pia tuna ujumbe mzito wa kuwatangazia watu ambao nyakati nyingine hawathamini jitihada zetu. Ili tuendelee kuiona huduma ya Kikristo kuwa pendeleo kutoka kwa Mungu, lazima tuendelee kujilisha vizuri kiroho. Hatuwezi kulielewa Neno la Mungu kikamili tukijifunza kijuujuu au mara kwa mara tu. Je, unaweza kufanya maendeleo katika usomaji wako wa Biblia na funzo lako la Biblia na kujifunza kwa ukawaida? Je, unaweza kutafakari mara nyingi zaidi yale unayosoma?—Zab. 1:2, 3.

Kuanzisha Mazungumzo ya Biblia

8. Ni njia gani ambayo imewasaidia wahubiri fulani wa Ufalme kuanzisha mazungumzo ya Biblia katika huduma ya nyumba kwa nyumba?

8 Wahubiri wengi wanaona kuanzisha mazungumzo na mwenye nyumba kuwa sehemu ngumu zaidi ya huduma ya nyumba kwa nyumba. Ni kweli kwamba katika maeneo fulani ni vigumu kuanzisha mazungumzo. Wahubiri fulani wanaona ni rahisi kuzungumza na wenye nyumba kwa kuanza mahubiri yao kwa maneno machache yaliyochaguliwa vizuri kisha kumpa mwenye nyumba trakti, kama inavyoonyeshwa katika sanduku. Kichwa cha trakti au picha iliyo juu inaweza kuvuta fikira za mwenye nyumba na kutupa nafasi ya kumweleza kwa ufupi kusudi la kumtembelea na kutokeza swali. Njia nyingine ni kumwonyesha mwenye nyumba trakti tatu au nne na kumwomba achague ile inayompendeza. Bila shaka, kusudi letu si kugawa trakti tu au kuzitumia katika kila nyumba bali kuanzisha mazungumzo ya Biblia yanayoongoza kwenye mafunzo ya Biblia.

9. Kwa nini ni jambo la maana kujitayarisha vizuri?

9 Hata ukitumia njia gani, kujitayarisha vizuri kutakusaidia kuwa mtulivu na mchangamfu katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Painia mmoja alisema hivi: “Ninakuwa mwenye shangwe zaidi ninapojitayarisha vizuri. Kufanya hivyo kunanipa hamu ya kutaka kusema mambo ambayo nimetayarisha.” Painia mwingine alisema, “Ninapojua mambo yaliyo katika vichapo ambavyo nitagawa shambani, ninavitoa kwa uchangamfu.” Ingawa kuna faida ya kupitia kimyakimya mambo utakayosema, wengi wanaona kwamba kuna faida zaidi kufanya mazoezi kwa sauti. Kufanya hivyo kunawasaidia wampe Yehova kilicho bora kabisa.—Kol. 3:23; 2 Tim. 2:15.

10. Ni mambo gani yanayoweza kufanywa ili mkutano wa utumishi uwe wenye kuelimisha na wenye faida?

10 Mikutano ya utumishi wa shambani yenye kuelimisha inatusaidia kupata shangwe na matokeo mazuri katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Ikiwa andiko la siku linahusiana moja kwa moja na kazi ya kuhubiri, linaweza kusomwa na kuzungumziwa kwa ufupi. Hata hivyo, ndugu anayeongoza mkutano wa utumishi wa shambani anapaswa kutumia wakati wa kutosha kuzungumzia au kutoa onyesho kuhusu njia fupi ya kuhubiri inayofaa eneo au habari nyingine inayofaa ambayo inaweza kutumiwa katika huduma siku hiyo. Hilo litawasaidia wale waliohudhuria kutoa ushahidi kwa njia yenye matokeo. Wazee na wengine wanaoongoza mikutano hiyo wakijitayarisha vizuri mapema, wanaweza kutimiza mambo hayo na kumaliza mkutano huo kwa wakati.—Rom. 12:8.

Faida za Kusikiliza

11, 12. Kusikiliza kwa huruma kunaweza kutusaidia kwa njia gani kuwahubiria watu habari njema? Toa mifano.

11 Zaidi ya kujitayarisha vizuri, kupendezwa sana na watu ndilo jambo ambalo linatusaidia hasa kuanzisha mazungumzo ya Biblia na kufikia mioyo yao katika huduma. Njia moja ya kuonyesha kwamba tunapendezwa na watu ni jinsi tunavyosikiliza. Mwangalizi mmoja anayesafiri alisema hivi: ‘Watu wanavutiwa sana unapokuwa mwenye subira na kuonyesha kwamba uko tayari kuwasikiliza, na hilo linaonyesha waziwazi kwamba unapendezwa nao kibinafsi.’ Kusikiliza kwa huruma kunaweza kuwa njia ya kuufikia moyo wa mwenye nyumba, kama kisa kinachofuata kinavyoonyesha.

12 Katika barua iliyochapishwa katika gazeti moja (Le Progrès) la Saint-Étienne, Ufaransa, mwanamke mmoja alieleza kuhusu watu wawili waliomtembelea muda mfupi baada ya kifo cha binti yake mwenye umri wa miezi mitatu. Aliandika hivi: ‘Nilitambua mara moja kuwa wao ni Mashahidi wa Yehova. Nilikuwa karibu kuwaambia kwa upole waende zao, lakini nikaona broshua waliyokuwa nayo. Ilikuwa ikizungumzia sababu ya Mungu kuruhusu kuteseka. Kwa hiyo, nikaamua kuwakaribisha ndani nikiwa na kusudi la kubomoa hoja zao. Mashahidi hao walikaa kwa muda wa saa moja hivi. Walinisikiliza kwa huruma sana, na walipokuwa wakiondoka, nilihisi nafuu, nikakubali wanitembelee tena.’ (Rom. 12:15) Baada ya muda, mwanamke huyo alikubali kujifunza Biblia. Kisa hicho kinatuonyesha kwamba kile ambacho mwanamke huyo alikumbuka kuhusu ziara hiyo ya kwanza, si mambo ambayo Mashahidi walisema, bali jinsi walivyosikiliza.

13. Tunaweza kubadili jinsi gani njia yetu ya kuhubiri habari njema kulingana na hali za watu tunaokutana nao?

13 Tunaposikiliza kwa huruma, tunawapa watu nafasi ya kutueleza kwa nini wanahitaji Ufalme. Hilo linatuwezesha kuwahubiria habari njema. Inaelekea umetambua kwamba wahubiri wenye matokeo ni wale walio na ustadi wa kusikiliza. (Met. 20:5) Wanapendezwa kikweli na watu katika huduma. Hawaandiki tu majina na anwani zao, bali pia mapendezi na mahitaji yao. Mtu anapotaja jambo fulani linalomhangaisha, wanafanya utafiti na kurudi haraka kumweleza matokeo ya utafiti wao. Kama mtume Paulo, wanabadili njia yao ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme kulingana na hali za watu wanaokutana nao. (Soma 1 Wakorintho 9:19-23.) Upendezi huo wa kweli unawafanya watu wavutiwe na habari njema na unaonyesha vizuri sana “huruma nyororo za Mungu wetu.”—Luka 1:78.

Endelea Kuwa na Mtazamo Unaofaa

14. Tunapotimiza huduma yetu, tunaweza kuonyesha jinsi gani sifa za Yehova?

14 Yehova ameonyesha kwamba anatuheshimu kwa kutupa uhuru wa kuchagua. Ingawa yeye ni Mungu Mweza-Yote, hamlazimishi mtu yeyote amtumikie bali anawavuta watu kwa upendo, naye anawabariki wale wanaokubali na kuthamini maandalizi yake mazuri ajabu. (Rom. 2:4) Tukiwa wahudumu wake, kila mara tunapohubiri habari njema tunapaswa kuwa tayari kuhubiri kwa njia inayoonyesha kwamba tunamwiga Mungu wetu mwenye huruma. (2 Kor. 5:20, 21; 6:3-6) Ili kufanya hivyo, tunahitaji kuendelea kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea watu walio katika eneo letu. Ni nini kitakachotusaidia kufanya hivyo?

15. (a) Yesu aliwaagiza mitume wake wafanye nini watu wanapokataa ujumbe wao? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kukazia fikira kuwatafuta wale wanaostahili?

15 Yesu aliwaagiza wafuasi wake wasihangaike kupita kiasi watu fulani wanapokataa ujumbe wao, badala yake wakazie fikira kuwatafuta wale wanaostahili. (Soma Mathayo 10:11-15.) Kujiwekea miradi midogo ambayo tunaweza kufikia kunaweza kutusaidia kufanya hivyo. Ndugu mmoja anapenda kujilinganisha na mtu anayetafuta dhahabu. Kwa kawaida anasema hivi: “Ninatazamia kupata dhahabu leo.” Ndugu mwingine ana mradi wa “kutafuta mtu mmoja mzuri kila juma na kurudi baada ya siku chache ili kukuza upendezi.” Wahubiri fulani wanajitahidi kusoma andiko moja pamoja na kila mwenye nyumba ikiwezekana. Ungependa kujiwekea mradi gani ambao unaweza kuufikia?

16. Tuna sababu gani za kuendelea kuhubiri?

16 Kupata mafanikio katika huduma ya nyumba kwa nyumba hakutegemei tu jinsi watu katika eneo wanavyoitikia. Ni kweli kwamba kazi ya kuhubiri ni ya maana sana katika kuwaokoa watu wenye mioyo minyoofu, lakini pia inatimiza makusudi mengine ya maana. Huduma ya Kikristo inatupa nafasi ya kuonyesha kwamba tunampenda Yehova. (1 Yoh. 5:3) Inatuwezesha kuepuka hatia ya damu. (Mdo. 20:26, 27) Inawaonya watu wasiomwogopa Mungu kwamba “saa ya hukumu [ya Mungu] imefika.” (Ufu. 14:6, 7) Zaidi ya yote, kupitia kazi ya kuhubiri habari njema, jina la Yehova linasifiwa katika dunia yote. (Zab. 113:3) Hivyo, watu wasikilize au wasisikilize, ni lazima tuendelee kutangaza ujumbe wa Ufalme. Ndiyo, jitihada zetu zote za kutangaza habari njema zinapendeza machoni pa Yehova.—Rom. 10:13-15.

17. Watu watalazimika kutambua nini hivi karibuni?

17 Ingawa watu wengi leo wanapuuza kazi yetu ya kuhubiri, hivi karibuni maoni yao yatabadilika. (Mt. 24:37-39) Yehova alimhakikishia Ezekieli kwamba wakati ambapo hukumu alizotangaza zingetimia, nyumba ya Israeli yenye kuasi ‘ingejua pia kwamba nabii alikuwako katikati yao.’ (Eze. 2:5) Vivyo hivyo, wakati ambapo Mungu atatekeleza hukumu zake juu ya mfumo huu wa mambo, watu watalazimika kutambua kwamba ujumbe ambao Mashahidi wa Yehova walihubiri hadharani na nyumba kwa nyumba ulitoka kwa Yehova, yule Mungu mmoja wa kweli, na kwamba Mashahidi hao walimwakilisha. Tuna pendeleo kubwa kama nini la kuitwa kwa jina lake na kutangaza ujumbe wake katika nyakati hizi za maana sana! Kwa nguvu zake, acheni tuendelee kushinda magumu ya huduma ya nyumba kwa nyumba.

Ungesema Nini?

• Tunaweza kufanya nini ili kujipa ujasiri wa kuhubiri?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia kuanzisha mazungumzo ya Biblia katika huduma ya nyumba kwa nyumba?

• Tunaweza kuonyesha kwa njia gani kwamba tunapendezwa kikweli na wengine?

• Ni nini kinachoweza kutusaidia kuendelea kuwa na mtazamo unaofaa kuelekea watu walio katika eneo letu?

[Maswali ya Funzo]

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

Njia Moja ya Kuanzisha Mazungumzo ya Biblia

Kuanzisha mazungumzo:

▪ Baada ya kumsalimu mwenye nyumba, unaweza kumpa trakti na kusema, “Nimekutembelea leo ili nikueleze jambo lenye kutia moyo kuhusu habari hii ya maana.”

▪ Au unaweza kumwonyesha trakti na kusema, “Leo, nimekutembelea kwa muda mfupi tu kwa sababu ningependa kujua maoni yako kuhusu habari hii.”

Akikubali trakti:

▪ Baada ya kutua kidogo, muulize swali rahisi ili ujue maoni yake kuhusu kichwa cha trakti hiyo.

▪ Sikiliza kwa makini na ujitahidi kuelewa maoni ya mwenye nyumba. Mshukuru kwa maoni yake na uyatilie maanani.

Ili kuendeleza mazungumzo:

▪ Soma na uzungumzie andiko moja au mawili, na ubadili mahubiri yako kulingana na mapendezi na mahitaji yake.

▪ Akipendezwa, mpe kichapo na umwonyeshe jinsi funzo la Biblia linavyofanywa, ikiwezekana. Panga kurudi.