Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matatizo ya Wanadamu Yatakwisha Hivi Karibuni!

Matatizo ya Wanadamu Yatakwisha Hivi Karibuni!

Matatizo ya Wanadamu Yatakwisha Hivi Karibuni!

‘MISAADA ya kibinadamu ina thamani ndogo isipohusisha mpango wa kutatua matatizo ya msingi ya kisiasa. Mambo ambayo yametokea mara kwa mara yameonyesha kwamba jitihada ya wanadamu pekee haiwezi kutatua matatizo ya kisiasa hasa.’—The State of the World’s Refugees 2000.

Licha ya jitihada kubwa ambazo wanadamu wamechukua, matatizo ya wanadamu yanaendelea kuongezeka kwa njia isiyoepukika. Je, kuna uwezekano wa kupata suluhisho la kisiasa la kudumu? Uwezekano huo ni mdogo sana. Lakini tunaweza kutafuta wapi suluhisho? Mtume Paulo anaanza barua yake kwa Wakristo wa Efeso, kwa habari muhimu kuhusu jinsi Mungu atakavyokomesha matatizo yote ya wanadamu. Hata anataja chombo ambacho Mungu atatumia kufanya hivyo—chombo kitakachoshughulikia kiini hasa cha matatizo yote yanayotupata leo. Kwa nini usichunguze maneno ya Paulo? Habari hiyo inapatikana katika andiko la Waefeso 1:3-10.

“Kukusanya Tena Pamoja Vitu Vyote Katika Kristo”

Mtume asema kwamba kusudi la Mungu ni “uhudumiaji [au kusimamia mambo] kwenye kikomo kamili cha nyakati zilizowekwa rasmi.” Hilo linamaanisha nini? Linamaanisha kwamba Mungu ameweka wakati ambapo atachukua hatua na hivyo ‘kukusanya tena pamoja vitu vyote katika Kristo, vitu vilivyomo katika mbingu na vitu vilivyo duniani.’ (Waefeso 1:10) Naam, Mungu ameanzisha mpango wa kupatanisha uumbaji wote mbinguni na duniani chini ya mwelekezo wake. Msomi wa Biblia J. H. Thayer asema kwamba usemi ambao umetafsiriwa ‘kukusanya tena pamoja’ unamaanisha: “Kujikusanyia tena mwenyewe . . . vitu vyote na watu wote (ambao hapo awali walitenganishwa na dhambi) ili kuwaunganisha tena katika ushirika na Kristo.”

Jambo hilo linaonyesha kwamba Mungu anahitaji kukusanya vitu hivyo tena pamoja kwa sababu ya mtengano uliotokea hapo awali. Mapema katika historia ya mwanadamu, wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walijiunga na Shetani Ibilisi kumwasi Mungu. Walitaka uhuru wa kujiamulia mema na mabaya. (Mwanzo 3:1-5) Kupatana na haki ya Mungu, walifukuzwa katika familia ya Mungu na kupoteza uhusiano pamoja naye. Wakasababisha hali ya kutokamilika kwa wanadamu pamoja na mambo mabaya yanayotupata leo.—Waroma 5:12.

Uovu Waruhusiwa Uendelee kwa Muda Mfupi

Huenda watu fulani wakauliza, ‘Kwa nini Mungu aliwaruhusu wafanye hivyo? Kwa nini hakutumia uwezo wake mkubwa na kutimiza mapenzi yake kwa nguvu, na hivyo kuzuia maumivu na mateso tunayopata leo?’ Huenda likawa jambo la kawaida kufikiri kwa njia hiyo. Lakini kutumia nguvu nyingi hivyo kungethibitisha nini? Je, ungemheshimu au ungekubaliana na mtu ambaye anapoona upinzani unaanza kutokea anaukomesha mara moja kwa sababu tu ana nguvu za kufanya hivyo? Bila shaka la.

Kwa kweli waasi hao hawakutilia shaka uwezo wa Mungu mweza yote. Walitilia shaka hasa haki na kufaa kwa utawala wake. Ili kusuluhisha kabisa masuala hayo muhimu yaliyotokezwa, Yehova aliwaruhusu viumbe wake wajitawale kwa muda fulani bila yeye kuingilia kati. (Mhubiri 3:1; Luka 21:24) Muda huo utakapokwisha, ataingilia kati na kuitawala dunia tena. Kufikia wakati huo itakuwa dhahiri kwamba njia yake ya kutawala ndiyo njia pekee inayoweza kuleta amani, furaha, na ufanisi kwa wakazi wa dunia. Kisha waonevu wote ulimwenguni wataondolewa kabisa.—Zaburi 72:12-14; Danieli 2:44.

“Kabla ya Kuwekwa Msingi wa Ulimwengu”

Yehova alikusudia kufanya mambo hayo yote muda mrefu uliopita. Paulo anataja kwamba Mungu alikusudia kufanya hivyo “kabla ya kuwekwa msingi wa ulimwengu.” (Waefeso 1:4) Hiyo haikuwa kabla ya dunia au Adamu na Hawa kuumbwa. Ulimwengu huo ulikuwa ‘mwema sana,” na uasi haukuwa umetokea. (Mwanzo 1:31) Basi, mtume Paulo alimaanisha “ulimwengu” gani? Ni ulimwengu wa watoto wa Adamu na Hawa—ulimwengu wenye dhambi na wa wanadamu wasio wakamilifu walio na tumaini la kukombolewa. Yehova alijua jinsi ambavyo angeshughulikia mambo na kuandaa ukombozi kwa wazao wa Adamu wanaoweza kukombolewa hata kabla mtoto yeyote kuzaliwa.—Waroma 8:20.

Bila shaka, hilo halidokezi kwamba Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu anapaswa kushughulikia mambo kama wanadamu. Wanadamu hupanga mbinu mbalimbali za kukabiliana na hali ya dharura inayoweza kutokea. Mungu mweza yote hutangaza kusudi lake na kulitimiza. Hata hivyo, Paulo aeleza jinsi Yehova alivyoamua kusuluhisha mambo ili kuwakomboa kabisa wanadamu. Alichukua hatua gani?

Ni Nani Atakayeleta Ukombozi?

Paulo aeleza kwamba wafuasi watiwa-mafuta wa Kristo wana daraka la pekee la kuondoa madhara yaliyosababishwa na dhambi ya Adamu. Yehova ‘alituchagua katika muungano na Kristo,’ asema Paulo, ili kutawala pamoja na Yesu katika Ufalme wake wa kimbingu. Akitoa maelezo zaidi, Paulo anasema kwamba Yehova “alituagiza kimbele kwenye tendo la kufanywa kuwa wana wake mwenyewe kupitia Yesu Kristo.” (Waefeso 1:4, 5) Bila shaka, Yehova hakuwachagua, au kuwaagiza kimbele wakiwa mtu mmoja-mmoja. Hata hivyo, aliagiza kimbele jamii ya watu waaminifu waliojitoa kwake ambao wangeshiriki pamoja na Kristo kuondoa madhara ambayo Shetani Ibilisi, pamoja na Adamu na Hawa waliletea familia ya kibinadamu.—Luka 12:32; Waebrania 2:14-18.

Ni jambo la kushangaza kama nini! Alipotilia shaka mara ya kwanza haki ya Mungu ya kutawala, Shetani alidokeza kwamba wanadamu walioumbwa na Mungu walikuwa na kasoro—kwamba wakipatwa na mnyanyaso au kushawishiwa, wote wataasi utawala wa Mungu. (Ayubu 1:7-12; 2:2-5) Ili kudhihirisha kwa njia yenye kutokeza “fadhili yake isiyostahiliwa yenye utukufu,” mwishowe Yehova Mungu alionyesha kwamba ana imani katika wanadamu kwa kuchukua baadhi ya watoto wa familia ya Adamu yenye dhambi na kuwafanya kuwa watoto wake wa kiroho. Washiriki wa kikundi hiki kidogo wataenda kutumikia mbinguni. Kwa kusudi gani?—Waefeso 1:3-6; Yohana 14:2, 3; 1 Wathesalonike 4:15-17; 1 Petro 1:3, 4.

Mtume Paulo asema kwamba wanadamu hao waliofanywa kuwa wana wa Mungu, wanakuwa “warithi-washirika pamoja na Kristo” katika Ufalme wake wa kimbingu. (Waroma 8:14-17) Wakiwa wafalme na makuhani, watashiriki kukomboa familia ya kibinadamu kutokana na maumivu na mateso yanayoipata sasa. (Ufunuo 5:10) Kwa kweli, “viumbe vyote vinafuliza kupiga kite pamoja na kuwa katika maumivu pamoja hadi sasa.” Hata hivyo, hivi karibuni Yesu Kristo ataongoza wana hawa ambao hasa wamechaguliwa na Mungu ili ‘kuwaweka huru wanadamu wote kutoka katika utumwa wa uharibifu na kuwa na uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu’ kwa mara nyingine tena.—Waroma 8:18-22.

“Kuachiliwa kwa Njia ya Fidia”

Mambo hayo yote yatawezekana kwa sababu ya fadhili isiyostahiliwa ya Mungu ambayo amedhihirisha kwa ulimwengu wa wanadamu wanaoweza kukombolewa kwa njia yenye kutokeza sana yaani, dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. Paulo aandika hivi: “Kwa njia yake [Yesu Kristo] tuna kuachiliwa kwa njia ya fidia kupitia damu ya huyo, ndiyo, msamaha wa makosa yetu, kulingana na utajiri wa fadhili yake isiyostahiliwa.”Waefeso 1:7.

Yesu Kristo anatimiza fungu muhimu sana katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu. (Waebrania 2:10) Dhabihu yake ya fidia humwandalia Yehova msingi halali wa kuchukua baadhi ya wazao wa Adamu na kuwafanya wawe washiriki wa familia yake ya kimbingu na hivyo kuwaondolea wanadamu matokeo mabaya ya dhambi ya Adamu, pasipo kulegeza kanuni na sheria Zake. (Mathayo 20:28; 1 Timotheo 2:6) Yehova amefanya mambo kwa njia ambayo inatetea uadilifu wake na kutosheleza haki kamili.—Waroma 3:22-26.

“Siri Takatifu” ya Mungu

Kwa maelfu ya miaka, Mungu hakufunua waziwazi jinsi ambavyo angetimiza kusudi lake kwa dunia. Katika karne ya kwanza W.K., ‘alijulisha [Wakristo] siri takatifu ya mapenzi yake.’ (Waefeso 1:9) Paulo na Wakristo wenzake watiwa-mafuta walielewa waziwazi daraka muhimu alilopewa Yesu Kristo ili kutimiza kusudi la Mungu. Pia walianza kuelewa daraka lao la pekee wakiwa warithi washirika pamoja na Kristo katika Ufalme wake wa kimbingu. (Waefeso 3:5, 6, 8-11) Naam, Mungu atatumia Ufalme ukiwa mikononi mwa Yesu Kristo pamoja na watawala wenzake kuleta amani ya kudumu si mbinguni tu bali duniani pia. (Mathayo 6:9, 10) Kupitia Ufalme huo, Yehova atafanya dunia hii iwe kama alivyokusudia mwanzoni.—Isaya 45:18; 65:21-23; Matendo 3:21.

Wakati ambao ameweka wa kuchukua hatua ya moja kwa moja ili kuondoa uonevu na ukosefu wa haki unakaribia. Lakini Yehova alianza kurudisha hali hizo kwenye Pentekoste 33 W.K. Jinsi gani? Wakati huo alianza kukusanya “vitu vilivyomo katika mbingu,” wale watakaotawala na Kristo mbinguni. Hao walitia ndani Wakristo huko Efeso. (Waefeso 2:4-7) Hivi karibuni zaidi, katika wakati wetu, Yehova amekuwa akikusanya “vitu vilivyo duniani.” (Waefeso 1:10) Kupitia kampeni ya kuhubiri ulimwenguni pote, anajulisha mataifa yote habari njema kuhusu Ufalme wake mikononi mwa Yesu Kristo. Wale wanaokubali wanakusanywa mahali palipo na ulinzi na uponyaji wa kiroho. (Yohana 10:16) Hivi karibuni, wakiwa katika dunia iliyosafishwa kuwa paradiso, watapata uhuru kamili kutokana na ukosefu wa haki na kuteseka.—2 Petro 3:13; Ufunuo 11:18.

Wanadamu wamefanya “maendeleo yenye kutokeza” katika jitihada zao za kusaidia watu walioonewa. (The State of the World’s Children 2000) Hata hivyo, hatua ya kutokeza zaidi itakuwa jinsi Kristo Yesu na watawala wenzake katika Ufalme wa kimbingu watakavyoingilia kati hivi karibuni. Wataondoa kabisa mambo yote yanayosababisha vita na maovu yote yanayotupata. Watakomesha matatizo yote ya wanadamu.—Ufunuo 21:1-4.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Wanadamu hawajasuluhisha matatizo yao kupitia jitihada zao

[Picha katika ukurasa wa 6]

Dhabihu ya fidia ya Kristo ilikomboa wanadamu kutokana na dhambi ya Adamu

[Picha katika ukurasa wa 7]

Tunaweza kupata ulinzi na uponyaji wa kiroho leo

[Picha katika ukurasa wa 7]

Hivi karibuni, kupitia Ufalme wa Kimesiya, wanadamu watakombolewa kutokana na matatizo yote