Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, inafaa mhudumu Mkristo atoe hotuba ya mazishi ya mtu aliyejiua?

Kila mhudumu Mkristo anapaswa kujiamulia mwenyewe iwapo kwa dhamiri safi anaweza kutoa hotuba ya mazishi ya mtu ambaye yaelekea alijiua. Anapoamua kufanya hivyo anapaswa kufikiria mambo yafuatayo: Yehova huonaje kujiua? Je, kwa kweli mtu huyo alijiua kimakusudi? Je, mtu huyo alijiua kwa sababu ya ugonjwa wa kiakili au wa kihisia-moyo? Watu wa eneo hilo wanaonaje tendo la kujiua?

Tukiwa Wakristo, tunapendezwa kujua maoni ya Yehova kuhusu kujiua. Yehova huona uhai wa binadamu kuwa wenye thamani na mtakatifu. (Mwanzo 9:5; Zaburi 36:9) Kujiua kimakusudi hakumpendezi Mungu. (Kutoka 20:13; 1 Yohana 3:15) Je, jambo hilo lingezuia kutolewa kwa hotuba ya mazishi ya mtu aliyejiua?

Wazia Mfalme Sauli wa Israeli. Alipotambua kwamba hangeokoka vita yake ya mwisho dhidi ya Wafilisti, badala ya kuacha maadui wake wamtende kikatili, ‘Sauli alitwaa upanga wake akauangukia.’ Wafilisti walipopata mwili wake, waliubandika kwenye ukuta wa jiji la Beth-shani. Wakazi wa Yabesh-gileadi walipogundua jambo ambalo Wafilisti walikuwa wamefanya, waliuondoa mwili huo na kuuchoma. Kisha wakachukua mifupa yake na kuizika na hata wakafunga kwa muda wa siku saba, kama ilivyokuwa desturi ya Waisraeli. (1 Samweli 31:4, 8-13; Mwanzo 50:10) Daudi, mtiwa-mafuta wa Yehova, alipoambiwa jambo ambalo wakazi wa Yabesh-gileadi walikuwa wamefanya, alisema hivi: “Na mbarikiwe ninyi na BWANA, kwa kuwa mmemtendea bwana wenu fadhili hii, yaani, Sauli, mkamzika. BWANA naye sasa awatendee ninyi fadhili na kweli.” (2 Samweli 2:5, 6) Biblia haionyeshi kwamba wakazi wa Yabesh-gileadi walishutumiwa kwa kumzika Mfalme Sauli. Linganisha jambo hilo na wale ambao hawakuzikwa kwa sababu ya makosa yao. (Yeremia 25:32, 33) Huenda mhudumu Mkristo akafikiria simulizi hilo la Sauli anapoamua iwapo atatoa hotuba ya mazishi ya mtu aliyejiua.

Huenda pia mhudumu huyo akafikiria kusudi la hotuba ya mazishi. Tofauti na watu wanaoamini kwamba nafsi haifi, Mashahidi wa Yehova hawafanyi mazishi wakiwa na wazo lisilo la kweli kwamba wanamuaga mtu aliyekufa wakisema ameenda katika ulimwengu mwingine. Kusudi kuu la hotuba ya mazishi si kumfaidi aliyekufa bali ni kuwafariji waliofiwa na kutoa ushahidi kuhusu hali ya wafu kwa watu waliohudhuria. (Mhubiri 9:5, 10; 2 Wakorintho 1:3-5) Sababu nyingine muhimu ya kuwa na hotuba ya mazishi ni kuwasaidia wote waliohudhuria watafakari kuhusu ufupi wa maisha. (Mhubiri 7:2) Je, makusudi hayo yatatimizwa kwa kutoa hotuba kwenye mazishi ya mtu aliyejiua?

Ni kweli kwamba, huenda wengine wakahisi kuwa mtu huyo alijiua kimakusudi, huku akijua kabisa kwamba anatenda dhambi dhidi ya Yehova. Lakini je, inawezekana sikuzote kuthibitisha maoni hayo? Je, alijiua kwa ghafula? Watu fulani ambao hujaribu kujiua hubadili nia yao na hivyo huacha kujiua. Mtu akisha kufa hawezi kutubu kwa yale aliyofanya.

Jambo jingine muhimu kufikiriwa ni magonjwa ya kiakili au ya kihisia-moyo ambayo huwafanya watu wengi wajiue. Kulingana na uchunguzi fulani, asilimia 90 ya watu wanaojiua huwa na tatizo fulani la kiakili, kihisia-moyo, au walikuwa na zoea la kutumia dawa za kulevya. Je, Yehova atasamehe watu wanaojiua kwa sababu ya ugonjwa wa akili? Hatuwezi kuamua iwapo mtu aliyekufa alitenda dhambi isiyoweza kusamehewa machoni pa Yehova. Mhudumu Mkristo anaweza kufikiria hali na afya ya kimwili na ya kiakili ya mtu aliyejiua anapoamua iwapo atatoa hotuba kwenye mazishi yake.

Kuna jambo jingine la kufikiriwa: Watu katika eneo hilo wanaonaje tendo la kujiua na kifo cha mtu huyo? Wazee hasa wanapaswa kuhangaikia jambo hilo kwa sababu wangependa kutaniko la Mashahidi wa Yehova la mahali hapo liwe na sifa nzuri. Ikitegemea mtazamo wa ujumla wa watu wa eneo hilo, na hasa kuhusiana na kisa kinachohusika, huenda wazee wasikubali kusimamia mazishi hayo hadharani au kukubali hotuba itolewe kwenye Jumba la Ufalme.

Hata hivyo, mhudumu Mkristo akiombwa asimamie mazishi, huenda akahisi kwamba huo ni uamuzi wa kibinafsi kwa kuwa hawakilishi kutaniko. Akiamua kufanya hivyo, anapaswa kuwa na busara na kutosema mambo kwa uhakika kuhusu kama mtu huyo atafufuliwa au la. Tumaini la mfu huyo liko mikononi mwa Yehova na hakuna mtu awezaye kusema iwapo mtu huyo atafufuliwa au la. Mhudumu huyo anaweza kukazia kweli za Biblia kuhusu kifo na kuwafariji waliofiwa.