Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAONI YA BIBLIA

Shetani

Shetani

Je, Shetani ni kiumbe halisi?

“Yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.”—Ufunuo 12:9.

WATU HUSEMA NINI?

Watu fulani wanaamini kwamba Shetani Ibilisi si kiumbe halisi, bali ni uovu ulio ndani ya kila mtu.

BIBLIA INASEMA NINI?

Shetani ni kiumbe halisi. Yeye ni malaika mwasi, kiumbe wa roho anayempinga Mungu. Biblia inamwita Shetani “mtawala wa ulimwengu huu.” (Yohana 12:31) Yeye hutumia “ishara za uwongo” na “udanganyifu” kutimiza makusudi yake.—2 Wathesalonike 2:9, 10.

Biblia inataja mazungumzo yaliyotokea mbinguni kati ya Shetani na Mungu. Ikiwa Shetani ni uovu ulio ndani ya kila mtu, inawezekanaje kwamba Mungu, ambaye ni mkamilifu na hana ukosefu wowote wa maadili azungumze na uovu fulani ulio ndani yake mwenyewe? (Kumbukumbu la Torati 32:4; Ayubu 2:1-6) Ni wazi kwamba Shetani ni kiumbe halisi na si uovu ulio ndani ya kila mtu.

KWA NINI SWALI HILO NI MUHIMU?

Shetani anataka uamini kwamba yeye si kiumbe halisi, sawa tu na vile mhalifu huficha utambulisho wake ili aendelee kuvunja sheria bila kugunduliwa. Ili ujilinde dhidi ya Shetani, unahitaji kwanza kukubali kwamba yeye ni kiumbe halisi.

 Shetani anaishi wapi?

“Ole wa dunia . . . kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu.”—Ufunuo 12:12.

WATU HUSEMA NINI?

Wengi wanaamini kwamba Shetani anaishi mahali penye moto wa mateso chini kabisa ya dunia. Wengine wanadhani kwamba yeye huishi ndani ya watu wabaya.

BIBLIA INASEMA NINI?

Shetani ni kiumbe wa roho, kwa hiyo yeye anaishi katika makao yasiyoonekana. Kwa kipindi fulani, Shetani aliruhusiwa atembee huku na huku mbinguni mahali ambapo Mungu na malaika wake waaminifu huishi. (Ayubu 1:6) Hata hivyo, sasa amefukuzwa kutoka mbele za Mungu na, akiwa pamoja na roho wengine waovu, amezuiliwa kwenye ujirani wa dunia.—Ufunuo 12:12.

Je, hilo linamaanisha kwamba Shetani anakaa mahali fulani hususa duniani? Kwa mfano, huenda umesoma kuhusu jiji la kale la Pergamamu ambalo lilisemekana kuwa mahali “anapokaa Shetani.” (Ufunuo 2:13) Kwa kweli, maneno hayo yalimaanisha kwamba ibada ya kishetani ilikuwa imekita mizizi mahali hapo. Shetani haishi mahali fulani hususa duniani. Kinyume cha hilo, Biblia inasema kwamba “falme zote za dunia inayokaliwa” ni mali yake.—Luka 4:5, 6.

Je, Shetani anaweza kuwadhuru au kuwaongoza watu?

“Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.”—1 Yohana 5:19.

BIBLIA INASEMA NINI?

Wanadamu wengi wamejiacha washindwe na uvutano wenye kupotosha wa Shetani na kwa hiyo wako chini ya nguvu zake. (2 Wakorintho 11:14) Jambo hilo linatusaidia kuelewa ni kwa nini wanadamu wameshindwa kuboresha hali ulimwenguni.

Biblia pia inataja visa ambapo Shetani na malaika wengine waasi wamewafanya watu kuwa chini ya uvutano wao na kuwadhuru kimwili.—Mathayo 12:22; 17:15-18; Marko 5:2-5.

UNAWEZA KUFANYA NINI?

Hupaswi kuogopa nguvu za Shetani. Ili uepuke kushindwa na uvutano wake, unahitaji kujua jinsi anavyowadanganya watu, ili ‘usikose kuzijua mbinu zake.’ (2 Wakorintho 2:11) Kwa kusoma Biblia, unaweza kupata ujuzi muhimu kuhusu mbinu za Shetani na hivyo uepuke kunaswa naye.

Tupilia mbali vitu vyovyote vinavyohusiana na utendaji wa roho waovu. (Matendo 19:19) Vitu hivyo vinatia ndani hirizi, vitabu, video, muziki, na programu za kompyuta ambazo zinaendeleza zoea la kuwasiliana na pepo au uaguzi.

“Mpingeni Ibilisi,” Biblia inasema, “naye atawakimbia ninyi.” (Yakobo 4:7) Ukitii shauri lenye hekima la Biblia, unaweza kujilinda dhidi ya hila za Shetani.—Waefeso 6:11-18.