Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU: JE, TUNANUNUA VITU KUPITA KIASI?

Kwa Nini Sisi Hununua Vitu?

Kwa Nini Sisi Hununua Vitu?

Matokeo ya uchunguzi uliofanywa ulimwenguni pote ambayo yalitolewa mwaka wa 2012 yalionyesha kwamba nusu ya waliohojiwa walikiri walinunua vitu ambavyo hawakuvihitaji. Asilimia 66 wana wasiwasi kwamba watu wananunua vitu kupita kiasi. Huenda wana sababu nzuri ya kuwa na wasiwasi. Wanunuzi wengi wameshindwa kulipa madeni yao yanayozidi kuongezeka. Watafiti wanasema kwamba badala ya kutuletea uradhi, kununua vitu kupita kiasi kunaweza kusababisha mikazo mingi na kukosa furaha! Basi, kwa nini tunanunua vitu kupita kiasi?

WANUNUZI hufurikwa na mbinu nyingi za wauzaji bidhaa. Lengo la wauzaji ni nini? Ni kufanya uamini unahitaji vitu ambavyo si vya lazima. Wauzaji wanajua kwamba wanunuzi huchochewa sana na hisia. Kwa hiyo matangazo ya kibiashara na ununuzi wenyewe umekusudiwa uwasisimue wanunue.

Kitabu Why People Buy Things They Don’t Need (Kwa Nini Watu Hununua Vitu Ambavyo Hawahitaji) kinasema hivi: “Wanapopanga kununua bidhaa mpya, mara nyingi wanunuzi huanza kujiwazia wakitafuta bidhaa hiyo, wakiipata, na mwishowe kuinunua.” Wataalamu fulani husema kwamba wanunuzi wanaweza kusisimuka sana wanaponunua vitu, hivi kwamba homoni ya adrenalini inaongezeka mwilini. Jim Pooler, ambaye ni mtaalamu wa uuzaji anaeleza hivi: “Muuzaji anapotambua hisia hizo za mnunuzi, anaweza kutumia msisimuko huo kwa faida yake na hivyo kumfanya mteja ashindwe kujizuia kununua bidhaa fulani.”

Unawezaje kujilinda dhidi ya mbinu za werevu za wauzaji bidhaa? Usiathiriwe na hisia zako, linganisha mambo ambayo wauzaji wanakuahidi na mambo halisi.

 AHADI: “Boresha Maisha Yako”

Ni jambo la kawaida kutaka kuwa na maisha bora. Makampuni ya matangazo ya kibiashara hutoa ujumbe wa kwamba tamaa zetu zote, iwe ni kuwa na afya nzuri, usalama, kutuliza mkazo, na kuboresha mahusiano, zinaweza kutoshelezwa kwa kununua vitu vinavyofaa.

UKWELI WA MAMBO:

Kadiri tunavyozidi kuwa na vitu vingi, ndivyo hali yetu ya maisha inavyozorota. Mtu anahitaji wakati na pesa za ziada ili kutunza vitu vya ziada anavyonunua. Mkazo huongezeka kwa sababu ya madeni, na mtu anakosa wakati wa kuwa pamoja na familia na marafiki.

Kadiri tunavyozidi kuwa na vitu vingi, ndivyo hali yetu ya maisha inavyozorota

Kanuni: “Uhai wa mtu hautegemei wingi wa vitu alivyo navyo.”Luka 12:15, Biblia Habari Njema.

AHADI: “Jipatie Umashuhuri na Heshima”

Si watu wengi watakubali kwamba wao hununua vitu ili wawapendeze wengine. Hata hivyo, Jim Pooler anasema hivi: “Watu wanaponunua vitu, jambo muhimu linalowachochea ni kutaka kushindana na marafiki, majirani, wafanyakazi, na watu wa ukoo.” Kwa sababu hiyo, makampuni yanapotangaza bidhaa fulani mara nyingi yanaonyesha watu waliofanikiwa maishani na matajiri wakitumia bidhaa hizo. Ujumbe ambao matangazo hayo unapitisha kwa wanunuzi ni: “Hata wewe unaweza kufanikiwa na kuwa tajiri.”

UKWELI WA MAMBO:

Kupima thamani yetu kwa kujilinganisha na wengine hutufanya tusiridhike. Mtu akipata kitu alichokuwa akitamani, mara moja anaanza kutamani kitu kingine.

Kanuni: “Anayependa fedha hatatosheka na fedha.”Mhubiri 5:10.

AHADI: “Jionyeshe Wewe Ni Nani”

Kitabu Shiny Objects (Vitu Vinavyong’aa) kinaeleza hivi: “Njia moja ambayo tunawaonyesha wengine sisi ni watu aina gani (au tungependa kuonwa kuwa watu wa aina gani) ni jinsi tunavyotumia au kuonyesha mali zetu.” Wauzaji bidhaa wanatambua jambo hilo na wao huhusianisha bidhaa zenye majina maarufu—hasa bidhaa za bei ghali—na mtindo fulani wa maisha au kiwango cha maisha.

Una maoni gani kujihusu, na ungependa watu wawe na maoni gani kukuhusu? Je, ungependa kuonekana kuwa mtu anayependa mitindo ya kisasa ya kifahari au mwenye umbo lenye kuvutia? Chochote unachotamani, wauzaji bidhaa wanakuahidi kwamba ukinunua bidhaa za kampuni fulani, unaweza kuwa mtu yeyote yule unayetaka.

UKWELI WA MAMBO:

Hakuna bidhaa yoyote unayonunua inayoweza kukubadili au kukupa sifa zenye kupendeza kama vile unyoofu na kushikilia kanuni za maadili.

Kanuni: “Kujipamba kwenu kusiwe . . . kule kujivika mapambo ya dhahabu au kuvaa mavazi ya nje, bali kuwe yule mtu wa siri wa moyoni.”1 Petro 3:3, 4.