Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sikuchelewa Mno Kuwa Rafiki ya Mungu

Sikuchelewa Mno Kuwa Rafiki ya Mungu

Sikuchelewa Mno Kuwa Rafiki ya Mungu

Limesimuliwa na Olavi J. Mattila

“Je, umewahi kujua kwamba unaweza kupata ujuzi sahihi kumhusu Muumba?” Niliulizwa swali hilo na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, na lilinifanya nifikirie sana. Wakati huo nilikuwa na umri wa zaidi ya miaka 80 na nilikuwa nimefahamiana na watu wengi mashuhuri, na viongozi wa kisiasa pia. Hata hivyo, nikiwa na umri huo, je, kweli ningeweza kumjua Mungu na kuwa rafiki yake?

NILIZALIWA mnamo Oktoba 1918 huko Hyvinkää, Finland. Nilipokuwa na umri mdogo, nilisaidia kazi ndogondogo za shambani. Nyumbani, tulifuga ng’ombe, farasi, kuku, na bata bukini. Nilijifunza kufanya kazi kwa bidii na kujivunia kazi yangu.

Kadiri nilivyokua, wazazi wangu walinitia moyo kufuatilia elimu. Kwa hiyo, nilipomaliza shule ya sekondari, niliondoka nyumbani na kwenda chuoni. Nilianza pia kujiingiza katika riadha na nikaja kufahamiana na mwenyekiti wa Shirika la Wanariadha nchini Finland, Urho Kekkonen. Sikujua kwamba Bw. Kekkonen angekuja kuwa waziri mkuu nchini Finland na baadaye kuwa rais wa taifa, wadhifa ambao alishikilia kwa miaka 30 hivi. Isitoshe, sikujua angekuwa na uvutano mkubwa maishani mwangu.

Maisha ya Umashuhuri na Mamlaka

Mwaka wa 1939, uhasama ulizuka kati ya Finland na ule Muungano wa Sovieti. Ilipofika Novemba ya mwaka huo, niliandikishwa jeshini. Mwanzoni nilitumika kama mkufunzi wa kikosi cha jeshi la akiba na baadaye nikawa kamanda wa kikosi cha wanaobeba bunduki mimina-risasi. Karelia, eneo lililoko kwenye mpaka wa Finland na Muungano wa Sovieti ndio uliokuwa uwanja wa mapigano. Katika majira ya kiangazi ya mwaka wa 1941, tulipokuwa tukipigana vita karibu na mji wa Vyborg, nilijeruhiwa vibaya na vipande kadhaa vya vyuma kutoka kwenye kombora na nikapelekwa kwenye hospitali ya jeshi. Majeraha niliyopata yalinizuia kwenda vitani tena.

Mnamo Septemba 1944, niliacha kufanya kazi jeshini na kurudi tena chuoni. Niliendelea na shughuli zangu katika riadha. Nilikuwa bingwa wa taifa mara tatu, mara mbili katika mbio za kupokezana vijiti, na mara moja katika mbio za kuruka viunzi. Pia, nilipata shahada za chuo kikuu katika nyanja ya teknolojia na uchumi.

Kufikia wakati huo, Urho Kekkonen alikuwa mwanasiasa mwenye uvutano mkubwa. Katika mwaka wa 1952, alipokuwa waziri mkuu, aliniambia niwe balozi nchini China. Nilipokuwa huko, nilikutana na maafisa wengi wa serikali, kutia ndani Mao Tse-tung, aliyekuwa kiongozi wa China wakati huo. Hata hivyo, mtu wa maana zaidi niliyekutana naye nchini China alikuwa msichana mrembo aliyeitwa Annikki, aliyekuwa akifanya kazi katika ofisi za Wizara ya Nchi za Kigeni ya Finland. Tulioana mnamo Novemba 1956.

Mwaka uliofuata, nilihamishwa hadi kwenye ofisi za ubalozi nchini Argentina. Tukiwa huko, tulipata watoto wetu wawili wa kwanza, wavulana. Tukarudi Finland mnamo Januari 1960. Baadaye kidogo, tukapata mtoto wetu wa tatu, msichana.

Kwenye Nyadhifa Kuu Kabisa Serikalini

Ingawa sikuwahi kuwa katika chama chochote cha kisiasa, katika Novemba 1963, Rais Kekkonen aliniambia niwe waziri wake wa biashara ya kimataifa. Miaka 12 iliyofuata, nilikuwa waziri katika wizara sita mbalimbali, mara mbili nikiwa waziri wa masuala ya nchi za kigeni. Wakati huo, niliamini kabisa kwamba werevu wa wanadamu unaweza kutatua matatizo katika ulimwengu. Lakini nikatambua haraka kwamba mwanadamu ana tamaa kubwa ya kujipatia mamlaka tu. Nilijionea matokeo mabaya ya watu kutoaminiana na kuoneana wivu.​—Mhubiri 8:9

Hata hivyo, niliona wengine wengi ambao kwa unyoofu, walijaribu kuboresha mambo. Lakini hatimaye, hata viongozi wenye nia nzuri hushindwa kufikia miradi yao.

Katika majira ya kiangazi ya mwaka wa 1975, wakuu wa nchi 35 walikuja Helsinki kuhudhuria Kongamano la Usalama na Ushirikiano Barani Ulaya. Wakati huo, nilikuwa waziri wa masuala ya nchi za kigeni na mshauri wa karibu wa Rais Kekkonen. Nilipewa daraka la kupanga kongamano hilo na nilikutana na wakuu wote wa nchi waliohudhuria.

Katika siku hizo chache, uwezo wangu wa kibalozi ulijaribiwa kabisa. Jambo dogo tu kama kuwaonyesha wanachama mahali pa kuketi lilizua vurugu! Hata hivyo, nilihisi kwamba kongamano hilo, pamoja na mikutano kadhaa iliyopangwa baada ya hapo, ilichangia kwa njia fulani kuboresha haki za kibinadamu na kuboresha uhusiano kati ya serikali kuu ulimwenguni.

Kuutambua Uhitaji Wangu wa Kiroho

Katika mwaka wa 1983, nilistaafu na tukahamia nchini Ufaransa, ambako binti yangu alikuwa anaishi. Kisha msiba ukatokea. Novemba  1994, iligunduliwa kuwa mke wangu Annikki ana kansa ya matiti. Mwaka huohuo, nilijipata mashakani kwa kujiingiza katika biashara, kumbe ilikuwa ya ulaghai. Nilikuwa nimejitahidi sana kudumisha jina zuri maishani mwangu. Lakini uamuzi huo mmoja mbaya ulinipaka matope kabisa.

Nilikuwa nimekutana na Mashahidi wa Yehova mara nyingi. Ingawa nilithamini ziara zao, na nilikubali magazeti yao, nilikuwa na mambo mengi ya kufanya na sikuwa na wakati kwa ajili ya mambo ya kiroho. Hata hivyo, kufikia mwaka wa 2000, nilikuwa nikimtunza Annikki, aliyekuwa bado akiugua kansa. Siku moja katika mwezi wa Septemba 2002, mmoja wa Mashahidi wa Yehova alinitembelea nyumbani. Aliniuliza swali lililotajwa mwanzoni mwa makala hii. Nikaanza kujiuliza: ‘Je, kwa kweli mtu anaweza kujifunza ukweli kumhusu Mungu? Je, kweli inawezekana kuwa rafiki yake?’ Niliitafuta Biblia yangu, ambayo ilikuwa imejaa vumbi kwa sababu sikuwa nimeisoma kwa muda mrefu, na nikaanza kuwa na mazungumzo ya Biblia ya kawaida pamoja na Mashahidi.

Mnamo Juni 2004, mke wangu mpendwa alikufa, na nikabaki peke yangu. Hata hivyo, watoto wangu walinifariji sana. Lakini bado nilijiuliza ni nini hutupata tunapokufa. Niliwauliza makasisi wawili Walutheri swali hilo. Walinijibu hivi, “Eeh! hayo ni maswali magumu.” Sikuridhishwa na majibu yao. Hapo ndipo nilitambua hata zaidi kwamba nina uhitaji wa kiroho.

Kadiri nilivyojifunza Biblia pamoja na Mashahidi, ndivyo nilivyopata ujuzi sahihi niliotamani sana. Kwa mfano, Biblia inaeleza kwamba kifo ni hali ya kutofahamu jambo lolote, kama usingizi, na kwamba wafu wana tumaini la kuishi tena duniani wakiwa wanadamu. (Yohana 11:25) Jambo hilo lilinipa tumaini na kunifariji kwelikweli.

Kwa hiyo, niliisoma Biblia yote mwenyewe. Andiko moja lililonivutia sana ni lile la Mika 6:8, linalosema: “Yehova anataka nini kutoka kwako ila kutenda haki na kupenda fadhili na kuwa na kiasi katika kutembea na Mungu wako?” Hekima ya kweli hiyo inayoelezwa kwa njia rahisi ilinivutia sana. Pia ilinifunulia kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo na mwenye haki sana.

Tumaini la Wakati Ujao

Kadiri nilivyojifunza kweli kumhusu Mungu, imani na uhakika wangu kumwelekea ulizidi kuongezeka. Urafiki wa kweli kati yangu na Muumba wangu ulikuwa ukisitawi! Nilivutiwa na maneno yake yanayopatikana katika kitabu cha Isaya 55:11: “Ndivyo litakavyokuwa neno langu linalotoka katika kinywa changu. Halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.” Ama kweli, Mungu ametimiza ahadi zake kufikia sasa, na ataendelea kufanya hivyo. Atatimiza miradi ambayo serikali nyingi za wanadamu na makongamano mengi ya kisiasa yamejaribu kutimiza bila mafanikio. Kwa mfano, Zaburi 46:9 inasema hivi: “Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.”

Nimepata faida nyingi sana kwa kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova. Nimejionea mwenyewe upendo halisi wa Kikristo ambao ndio kitambulisho cha wafuasi wa kweli wa Yesu. (Yohana 13:35) Upendo huo unashinda mipaka ya kitaifa na haupatikani kabisa katika ulimwengu wa kisiasa na kibiashara.

Pendeleo Kubwa Zaidi

Sasa nina umri wa miaka 90, na ninahisi kwamba sijawahi kupata pendeleo kubwa zaidi kuliko kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Kiu yangu ya mambo ya kiroho imetoshelezwa. Nimepata pendeleo la kujua kusudi la maisha na ukweli kumhusu Mungu.

Ninafurahi kama nini kwamba licha ya umri wangu, ninashiriki kadiri ninavyoweza katika kazi ya kuhubiri na kuhudhuria mikutano. Ingawa nimekutana na watu wengi wenye mamlaka na kubeba madaraka mazito katika maisha yangu, siwezi kulinganisha mambo hayo na pendeleo la kumjua Muumba wangu, Yehova Mungu, na kuwa rafiki yake. Ninamshukuru kama nini, na ninataka kumsifu kwa kunipa fursa ya kuwa mmoja wa “wafanyakazi wenzi” wake. (1 Wakorintho 3:9) Sikuchelewa mno kuwa rafiki ya Muumba, Yehova Mungu!

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na Rais Kekkonen na Rais Ford wa Marekani kwenye kongamano la Helsinki la 1975

[Picha katika ukurasa wa 25]

Nikiwa na Rais Kekkonen na kiongozi wa Sovieti, Brezhnev

[Picha katika ukurasa wa 26]

Ninashiriki katika utendaji wa Kikristo

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 25]

Lower left: Ensio Ilmonen/​Lehtikuva; lower right: Esa Pyysalo/​Lehtikuva