Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Faida za Kuwa Mnyoofu

Kuna Faida za Kuwa Mnyoofu

Kuna Faida za Kuwa Mnyoofu

“Mkate unaopatikana kwa udanganyifu humpendeza mtu, lakini baadaye kinywa chake kitajaa changarawe.”​—Methali 20:17.

JE, NI lazima mtu awe mdanganyifu ili biashara yake ifanikiwe? Jibu ni la. Mara nyingi kukosa kuwa mnyoofu huleta hasara. Kwa nini? Kwa sababu unyoofu hufanya mtu aaminiwe, na hilo ni muhimu ili mtu aendelee kufanikiwa.

Faida za Kuaminika

Unyoofu wako huathiri mafanikio yako​—iwe unajua au hujui. Kisa cha Franz, aliyetajwa katika makala iliyotangulia, kinaonyesha jambo hilo. “Nilipoajiriwa,” anasema, “waajiri wangu walijaribu unyoofu na uaminifu wangu mara kadhaa bila mimi kujua. Nilikuja kujua baadaye kwamba nilipita mtihani huo. Kwa sababu hiyo, nimepewa madaraka zaidi na uhuru zaidi na waajiri wangu wamenithawabisha kwa sababu ya kuwa mnyoofu. Ninajua kwamba kuna watu wanaoweza kufanya kazi yangu kwa njia bora zaidi na walio na akili kuliko mimi. Hata hivyo, nadhani sijafutwa kazi kwa muda wote huu kwa sababu waajiri wangu wananiamini.”

Epuka Kujasiria Mambo

David, mfanyabiashara aliyenukuliwa katika makala iliyotangulia anasema hivi: “Ninapowaona watu wakivunja sheria ili wapate faida ya muda mfupi tu, mimi hujiambia, ‘Mtu atavuna anachopanda, hata kama si mara hiyohiyo.’ Yaani hatimaye, kukosa kuwa mnyoofu kutakuletea matatizo kwa njia moja au nyingine. Tulikataa biashara nyingi zenye kutiliwa shaka. Kampuni nyingi ambazo zilijihusisha katika biashara hizo zilitoweka baadaye, na watu fulani wakashtakiwa. Kampuni yetu iliepuka matatizo hayo yote.”

Alipokuwa akianzisha shamba la kufuga ng’ombe huko kusini-mashariki mwa Afrika, Ken angeweza kushawishiwa awape rushwa maofisa fulani ili aweze kuuza haraka bidhaa zake nje ya nchi na wamsaidie kuepuka kulipa ushuru. Anasema hivi: “Wafugaji wengine wengi walijihusisha katika zoea hilo. Kwa kuwa tulifanya mambo kwa unyoofu, ilichukua miaka kumi ili tupate kila kitu tulichohitaji katika shamba letu. Je, tulifaidika kwa kuwa wanyoofu? Ndiyo! Wale waliotoa rushwa walisumbuliwa kila mara na maofisa wafisadi ambao walitaka rushwa zaidi.”

Kukabiliana na Matatizo ya Kiuchumi

Biashara inapokabili hatari ya kuanguka, watu hushinikizwa waache kuwa wanyoofu. Hata hivyo, hali hizo zinaweza kuonyesha faida ya kuwa mnyoofu.

Fikiria mfano wa Bill, ambaye biashara yake ya ujenzi ilianguka wakati biashara ya nyumba nchini Marekani ilikumbwa na matatizo. Anasema hivi: “Wengi wa wateja wetu wakubwa walifilisika na kwenda na deni letu la maelfu ya dola. Nilipoona kwamba hakuna tumaini, nilimfikia mtu aliyekuwa akifanya biashara kama yangu na kumwomba aniajiri pamoja na wafanyakazi wangu. Saa 48 hivi baada ya mkutano huo, waliniajiri mimi pamoja na wengi wa wafanyakazi wangu. Niliambiwa kwamba nilikuwa na sifa ya kutoa huduma nzuri na kuwa mnyoofu.”

Visa vyote vilivyotajwa hapa ni vya watu ambao ni Mashahidi wa Yehova. Viwango wanavyofuata katika biashara, sawa na viwango wanavyofuata maishani vinategemea Biblia. Kama vile makala hii imeonyesha, badala ya unyoofu wao kuwazuia wafanikiwe katika biashara, umewasaidia kupata faida.

Hata hivyo, huenda nyakati nyingine ikaonekana kwamba kuna faida ya kutokuwa mnyoofu chini ya hali fulani. Je, faida za kifedha tu ndizo zinaonyesha kwamba mtu amefanikiwa?

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Unyoofu wako huathiri mafanikio yako​—iwe unajua au hujui

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Niliambiwa kwamba sifa yangu ya kutoa huduma nzuri na unyoofu wangu ulijulikana sana.”​—Bill, Marekani