Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Umebadilika Kabisa?

Je, Umebadilika Kabisa?

‘Mugeuzwe kwa kufanya upya akili yenu.’​—ROM. 12:2.

1, 2. Namna tulivyolelewa na mahali tunapoishi vina matokeo gani juu yetu?

 NAMNA sisi wote tulivyolelewa na mahali tunapoishi vinatufanya tufikiri ao tutende kwa njia fulani. Kwa mufano, tunazoea kuvaa kwa njia fulani, tunapenda aina fulani ya chakula; na tunatenda kwa njia fulani. Sababu gani? Kwanza, ni kwa sababu watu wanaotuzunguka wanatuchochea kutenda kwa njia fulani ao tunachochewa na hali mbalimbali tunazojionea katika maisha.

2 Hata hivyo, kuna mambo fulani yaliyo ya maana sana kuliko aina ya chakula na mutindo wa mavazi tunayochagua. Kwa mufano, tulipokuwa watoto tulifundishwa kwamba tunapaswa kuona mambo fulani kuwa mazuri na yenye kufaa na kuepuka mambo mengine yaliyo mabaya na yasiyofaa. Lakini watu wengi wana maoni tofauti kuhusu mambo hayo. Zamiri yetu inaweza hata kutuchochea kuchukua maamuzi mazuri ao mabaya. Biblia inaonyesha kwamba mara nyingi ‘watu wa mataifa wasio na sheria wanafanya kwa asili mambo ya sheria.’ (Rom. 2:14) Lakini, je, hilo linamaanisha kwamba ikiwa hakuna sheria ya Mungu iliyo wazi, tunapaswa kufuata desturi na kanuni tulizofundishwa tulipokuwa watoto na zinazopendwa na watu wengi wa mahali tunapoishi?

3. Kuna sababu gani mbili zinazotufanya sisi Wakristo tuepuke desturi na kanuni zinazokubaliwa na watu wengi?

3 Kuna sababu kubwa mbili hivi zinazotufanya sisi Wakristo tuepuke jambo hilo. Sababu ya kwanza, Biblia inatukumbusha hivi: “Kuna njia ambayo imenyooka mbele ya mwanadamu, lakini njia za kifo ndizo mwisho wake baadaye.” (Met. 16:25) Kwa sababu ya hali yetu ya kutokamilika, sisi wanadamu hatuna uwezo wa kuongoza kabisa hatua zetu vizuri. (Met. 28:26; Yer. 10:23) Sababu ya pili, Biblia inaonyesha kwamba desturi na kanuni za ulimwengu zinaongozwa na Shetani, ambaye ni ‘mungu wa mufumo huu wa mambo.’ (2 Kor. 4:4; 1 Yoh. 5:19) Kwa hiyo, ikiwa tunataka kubarikiwa na kukubaliwa na Yehova, tunahitaji kufuata mashauri yanayopatikana katika andiko la Waroma 12:2.​—Soma.

4. Tutazungumuzia nini katika habari hii?

4 Ni lazima tuchunguze kwa uangalifu mambo ya maana yanayozungumuziwa kwenye Waroma 12:2. (1) Sababu gani tunapaswa ‘kugeuzwa’ ao kubadilika? (2) Ni mambo gani tunayopaswa kubadili? na (3) Ni nini inayoweza kutusaidia tubadilike? Acheni tuzungumuzie maulizo hayo.

SABABU GANI TUNAPASWA KUBADILIKA?

5. Maneno ya Paulo kwenye Waroma 12:2 yalihusu zaidi sana nani?

5 Mutume Paulo alipoandika barua yake kwa Waroma, hakuwa akiwaandikia wapagani ao wakaaji wote wa muji wa Roma, lakini aliandikia Wakristo wenzake waliotiwa mafuta. (Rom. 1:7) Aliwashauri wabadilike na ‘waache kufanyizwa kulingana na mufumo huu wa mambo.’ Kwa Wakristo walioishi Roma wakati huo, katika mwaka wa 56 kisha kuzaliwa kwa Yesu, ‘mufumo wa mambo’ ulitia ndani kanuni, desturi, tabia, na namna ya kuvaa ya Waroma. Paulo alitumia neno ‘kuacha’ kwa sababu Wakristo fulani walikuwa wangali wanatenda na kufikiri kama Waroma. Ni mambo gani yaliyofanya ndugu na dada zetu hao wafikie kutenda na kufikiri kama Waroma?

6, 7. Sababu gani namna ya kuishi na ya kuabudu ya Waroma ilikuwa jaribu kwa Wakristo katika siku za Paulo?

6 Leo, wale wanaotembelea muji wa Roma wanaona kila mara sehemu zilizobaki za mahekalu, makaburi, minara ya ukumbusho, viwanja vya michezo, vyumba vya michezo, na mambo mengine ya zamani. Mengi kati ya majengo hayo yalijengwa wakati wa mitume. Majengo hayo ya zamani yanatusaidia kuelewa namna watu walivyoishi na kuabudu katika Roma ya zamani. Tunaweza pia kusoma katika vitabu vya historia kuhusu michezo ya kupigana, mashindano ya magari ya kukokotwa, na michezo ya kufurahisha na muziki uliozungumuzia mambo mbalimbali, na hata mambo ya haya. Roma ilikuwa pia mahali pazuri pa kufanyia biashara, kwa hiyo watu walikuwa na nafasi nyingi za kupata feza.​—Rom. 6:21; 1 Pet. 4:3, 4.

7 Waroma walikuwa na mahekalu mengi na miungu mingi, lakini hawakuwa na uhusiano wa pekee pamoja na miungu waliyoabudu. Kwa Waroma dini ilihusiana tu na desturi fulani, kama vile sherehe za kuzaliwa, ndoa na maziko, ambazo zilikuwa sehemu za maisha yao ya kila siku. Kwa Wakristo wa Roma, hilo lilikuwa jaribu kabisa. Wengi walikomaa katika mazingira hayo, kwa hiyo ni wazi kwamba walipaswa kufanya mabadiliko ili wawe Wakristo wa kweli, na hata kisha wao kubatizwa, walipaswa kuendelea kufanya mabadiliko.

8. Ni nini inayoonyesha kwamba ulimwengu huu ni mahali penye hatari kwa Wakristo leo?

8 Kama vile Roma, ulimwengu wa leo ni mahali penye hatari kwa watumishi wa Yehova. Sababu gani? Kwa sababu roho ya ulimwengu inapatikana mahali pote. (Soma Waefeso 2:2, 3; 1 Yohana 2:16.) Kila siku ulimwengu unatafuta kutuchochea kupitia tamaa, mawazo, kanuni na mwenendo wake, na kila wakati tuko katika hatari ya kunaswa na ulimwengu. Kwa hiyo, tunapaswa kabisa kutii shauri la ‘kuacha kufanyizwa kulingana na mufumo huu wa mambo’ na ‘kugeuzwa.’ Tunapaswa kufanya hivyo namna gani?

NI MAMBO GANI TUNAYOPASWA KUBADILI?

9. Wengi wamefanya mabadiliko gani ili wastahili kubatizwa?

9 Kadiri mutu anavyojifunza kweli ya Biblia na kuitumia katika maisha yake, anaanza kufanya maendeleo ya kiroho. Kwa hiyo, anafanya mabadiliko katika maisha yake kulingana na yale ambayo amejifunza. Anaachana na desturi za dini ya uongo na mwenendo wake mubaya na kuvaa utu mupya. (Efe. 4:22-24) Kila mwaka, tunafurahi kuona wengi wakifanya mabadiliko hayo na kustahili kubatizwa ili kuonyesha kwamba wamejitoa kwa Yehova Mungu. Bila shaka, hilo linafurahisha moyo wa Yehova. (Met. 27:11) Hata hivyo, tunapaswa kufikiria ulizo hili: Je, mabadiliko hayo yanatosha?

Watu wengi wanahitaji kuachana na tabia za ulimwengu wa Shetani na kubadilika (Ona fungu la 9)

10. Namna gani kubadilika kunatofautiana na kufanya hali yetu iwe nzuri kidogo?

10 Bila shaka, kubadilika kunatia ndani mambo mengi zaidi ya kufanya maendeleo ao kufanya hali yetu iwe nzuri kidogo. Kwa mufano, unaweza kuona kwenye chupa ya mafuta ya kujipakaa kumeandikwa “imeboreshwa,” lakini kwa kweli hayakubadilishwa, ni mafuta yaleyale tu. Labda kuna kitu kimoja tu ambacho kimeongezwa ndani, na pengine chupa imebadilishwa ili ivutie zaidi. Kuhusiana na maneno ‘mugeuzwe’ ambayo mutume Paulo alitumia, maelezo katika kitabu kimoja yanasema hivi: “Andiko la Waroma 12:2 linaonyesha tofauti kubwa iliyo kati ya kufanyizwa kijuu-juu tu kulingana na vitu vya wakati huu [ao ulimwengu huu] na kugeuzwa ao kubadilika kwa undani kwa kufanya upya mawazo yetu kupitia uwezo wa Roho Takatifu.” (Vine’s Expository Dictionary) Kwa hiyo, mabadiliko ambayo Mukristo anapaswa kufanya hayamaanishe tu kuachana na tabia mbaya, maneno machafu, na mwenendo mubaya. Hata watu fulani wasiokuwa na ujuzi wa Biblia wanajikaza kwa kiasi fulani kuepuka mambo hayo katika maisha yao. Kwa hiyo basi, Mukristo anapaswa kubadili mambo gani?

11. Paulo alionyesha kwamba mutu anapaswa kubadili mambo gani?

11 Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Mugeuzwe kwa kufanya upya akili yenu.’ Neno “akili” linamaanisha uwezo wetu wa kufikiri. Lakini linapotumiwa katika Biblia linaweza kumaanisha mambo tunayopenda kufikiria, mutazamo, na nguvu zetu za kufikiri. Mwanzoni mwa barua yake kwa Waroma, Paulo alizungumuzia watu waliokuwa katika “hali ya akili iliyokataliwa.” Watu hao walikuwa wenye ‘ukosefu wote wa uadilifu, uovu, tamaa, ubaya, walikuwa wamejaa wivu, uuaji, mizozo, udanganyifu,’ na mambo mengine mabaya. (Rom. 1:28-31) Hiyo ndiyo sababu Paulo aliwatia moyo wale waliokomalia katika hali hizo na ambao walikuwa wamegeuka kuwa watumishi wa Mungu, ‘wageuzwe’ na ‘kufanya upya akili yao.’

‘Uchungu wote wenye uovu na hasira na gazabu na kupiga kelele na matukano na viondolewe mbali kutoka kwenu.’​—Efe. 4:31

12. Watu wengi wana maoni gani leo, na maoni hayo yanaweza kuwafanya Wakristo watende namna gani?

12 Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, tunazungukwa na watu walio kama wale ambao Paulo alizungumuzia. Watu hao wanafikiri kwamba huu si wakati wa kuwakazia watu wafuate kanuni fulani. Waalimu na wazazi wengi wanawaachia watoto uhuru wa kufanya jambo lolote wanalotaka na kufikiri namna wanavyotaka. Wanawafundisha hata kwamba kila mutu ana haki ya kuamua ikiwa jambo fulani ni baya ao nzuri. Wengi hata wanaodai kufuata dini sana wanafikiri kwamba wana uhuru wa kufanya mambo wanayofikiri kuwa mema, hawaone uhitaji wa kutii amri za Mungu. (Zab. 14:1) Wakristo wa kweli wanaweza kuanza kuwa na maoni hayo. Wale wasiokuwa waangalifu wanaweza kuanza kuwa na maoni hayo kuhusu mipango ya kiteokrasi. Wanaweza kukataa kufuata maagizo ya tengenezo la Yehova ao hata kunungunika kwa sababu mambo fulani hayafanywe namna wanavyopenda. Ao wanaweza kuanza kuwa na mashaka kuhusu mashauri ya Biblia kuhusu mambo ya kujifurahisha, kutumia Internete, na kusoma masomo ya juu.

13. Sababu gani sisi wenyewe tunapaswa kujichunguza kwa uangalifu?

13 Kwa hiyo, ili tusiendelee kufanyizwa, ao kufinyangwa kulingana na ulimwengu huu, tunahitaji kuchunguza kwa uangalifu maoni na hisia zetu za ndani, miradi yetu na kanuni zetu. Wengine hawawezi kuona namna tulivyo kwa ndani. Wanaweza hata kutuambia kwamba hatuna shida yoyote ya kiroho. Hata hivyo, ni sisi pekee ndio tunajua ikiwa tumeruhusu kabisa mambo tunayojifunza katika Biblia yatubadili na yaendelee kutubadili katika mambo hayo ya maana sana.​—Soma Yakobo 1:23-25.

NI NINI INAYOWEZA KUTUSAIDIA TUBADILIKE?

14. Ni nini inayoweza kutusaidia kujua mabadiliko ambayo tunahitaji kufanya?

14 Kubadilika kunamaanisha kubadili namna tulivyo kwa ndani, kwa hiyo tunahitaji jambo fulani ambalo linaweza kuingia ndani kabisa katika moyo wetu. Ni nini inayoweza kutusaidia katika njia hiyo? Tunapojifunza katika Biblia yale ambayo Yehova anataka tufanye, namna tunavyotenda kisha kusoma mambo hayo inaonyesha yale yaliyo katika moyo wetu na mabadiliko tunayohitaji kufanya ili kutenda kulingana na “mapenzi ya Mungu yaliyo makamilifu.”​—Rom. 12:2; Ebr. 4:12.

15. Yehova anapotufinyanga, hilo linaweza kutusaidia namna gani?

15 Soma Isaya 64:8. Mufano ambao nabii Isaya anatumia katika andiko hilo unatufundisha jambo fulani la maana. Namna gani Yehova, Mufinyanzi wetu, anatufinyanga sisi udongo? Bila shaka, Yehova habadili hali yetu ya kimwili, labda ili tuwe na sura yenye kuvutia zaidi. Lakini, anatutolea mazoezi ya kiroho. Ikiwa tunakubali atufinyange, atatusaidia kubadili namna tulivyo kwa ndani ao hali yetu ya kiroho. Yehova atatutolea zaidi sana yale tunayohitaji ili kushinda vishawishi vya ulimwengu. Yehova anatufinyanga namna gani?

16, 17. (a) Mufinyanzi anafanya nini ili kutengeneza chombo kizuri cha udongo? Eleza. (b) Namna gani Neno la Mungu linatusaidia tubadilike na kuwa watu wa maana machoni pa Yehova?

16 Mufinyanzi anahitaji udongo muzuri sana ili afanye chombo kizuri. Hata hivyo, kuna mambo mawili anayopaswa kufanya. Kwanza, anapaswa kuondoa uchafu katika udongo. Kisha, anapaswa kuchanga udongo huo na kiasi kinachofaa cha maji ili uweze kukamata umbo fulani atakapoufinyanga.

17 Mufinyanzi anatumia maji ili kuondoa uchafu katika udongo na kufanya uwe rahisi kufinyangwa. Kisha anaweza kuutumia ili kutengeneza chombo fulani, ao hata chombo kinachoweza kuvunjika haraka. Je, Neno la Mungu linaweza kutumika kama maji? Neno la Mungu linaweza kutusaidia tuachane na mawazo tuliyokuwa nayo mbele ya kumujua Mungu na linaweza kutusaidia tubadilike na kuwa watu wa maana machoni pake. (Efe. 5:26) Tumekumbushwa mara nyingi kwamba tunapaswa kusoma Biblia kila siku na kuhuzuria kwa ukawaida mikutano, ambako Neno la Mungu linazungumuziwa. Sababu gani tumetiwa moyo kufanya hivyo? Kwa sababu kwa kufanya hivyo, tunakubali Yehova atufinyange.​—Zab. 1:2; Mdo. 17:11; Ebr. 10:24, 25.

Ikiwa umebadilika, utatatua matatizo vizuri zaidi kuliko zamani (Ona fungu la 18)

18. (a) Sababu gani kutafakari ni kwa maana sana ikiwa tunataka Neno la Mungu lituchochee na kutusaidia kufanya mabadiliko? (b) Ni maulizo gani yanayoweza kutusaidia?

18 Ili Neno la Mungu litusaidie kubadilika, tunapaswa kufanya mengi zaidi ya kusoma na kujifunza Biblia kwa ukawaida. Watu wengi wanasoma Biblia mara kwa mara na kwa hiyo wamejua mambo mengi ambayo inasema. Pengine umekwisha kukutana na watu kama hao katika mahubiri. Wengine wanaweza hata kurudilia yale ambayo mistari fulani ya Biblia inasema bila hata kuwa na Biblia mukononi. * Hata hivyo, hilo haliwasaidie kabisa kubadili mawazo na namna yao ya kuishi. Sababu gani? Ili Neno la Mungu limuchochee mutu na kumusaidia kubadilika, anapaswa kuliruhusu likaziwe kabisa katika moyo wake. (Gal. 6:6) Kwa hiyo, tunahitaji kutumia wakati ili kufikiri sana kuhusu yale tunayojifunza. Ni jambo la maana tujiulize hivi: ‘Je, niko hakika kama hili si fundisho tu la dini? Je, niko hakika kwamba hii ndiyo kweli? Zaidi ya hayo, kuliko tu kufundisha wengine mambo ninayojifunza, namna gani mimi mwenyewe ninaweza kuyatumia katika maisha yangu? Je, niko hakika kwamba Yehova ndiye anayenifundisha mambo haya?’ Kufikiri na kutafakari juu ya maulizo hayo kunaweza kutusaidia tujisikie kuwa karibu na Yehova. Upendo wetu kwake utaongezeka. Mambo tunayojifunza yanapogusa moyo wetu, hilo litatuchochea kufanya mabadiliko.​—Met. 4:23; Lu. 6:45.

19, 20. Ni mashauri gani ya Biblia yanayoweza kutuletea baraka?

19 Kusoma Neno la Mungu kwa ukawaida na kutafakari juu yake kutatuchochea tuendelee kufanya yale ambayo labda tumekwisha kufanya kwa kiasi fulani, ni kusema, ‘kuvua utu wa zamani pamoja na mazoea yake, na kujivika utu mupya ambao kupitia ujuzi sahihi unafanywa kuwa mupya.’ (Kol. 3:9, 10) Tutaendelea kuvaa utu mupya ikiwa tunaelewa vizuri yale tunayojifunza na namna tunavyoweza kuyatumia katika maisha yetu. Utu huo mupya utatusaidia tuepuke mitego ya Shetani.

20 Mutume Petro anatukumbusha hivi: ‘Kama watoto watiifu, acheni kufanyizwa kulingana na tamaa mulizokuwa nazo hapo zamani, bali, iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote.’ (1 Pet. 1:14, 15) Kama tutakavyoona katika habari inayofuata, ikiwa tunafanya yote tunayoweza ili kuachana na mawazo na tabia za zamani na ikiwa tunabadilika, tutapata baraka nyingi.

^ Ona mufano uliotolewa katika Munara wa Mulinzi wa tarehe 01/02/1994, ukurasa wa 9, fungu la 7.