Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 21

Yesu Yuko Hai!

Yesu Yuko Hai!

Yesu awatokea wafuasi wake ili kuwapa maagizo na kuwatia moyo

SIKU ya tatu baada ya kifo cha Yesu, wanawake fulani waliokuwa wanafunzi wake waligundua kwamba jiwe lililokuwa kwenye mwingilio wa kaburi limeondolewa. Isitoshe, kaburi lilikuwa tupu!

Malaika wawili wakatokea. Mmoja wao akasema: “Mnamtafuta Yesu Mnazareti. . . . Alifufuliwa.” (Marko 16:6) Bila kukawia, wanawake hao wakakimbia kwenda kuwaambia mitume. Wakiwa njiani, wakakutana na Yesu. Akawaambia: “Msiogope! Nendeni, mkawajulishe ndugu zangu, ili wapate kwenda zao Galilaya; na huko wataniona.”—Mathayo 28:10.

Baadaye siku hiyo, wanafunzi wawili walikuwa wakitembea kutoka Yerusalemu kuelekea kijiji cha Emau. Mtu wasiyemjua alijiunga nao na kuwauliza wanazungumzia nini. Mtu huyo alikuwa Yesu aliyefufuliwa, aliyewatokea katika umbo ambalo hawakutambua mwanzoni. Wakiwa na nyuso zenye huzuni wakamjibu kwamba wanaongea kuhusu Yesu. Kisha mtu huyo akaanza kuwaeleza mambo kuhusu Masihi katika Maandiko yote. Kwa kweli, Yesu alikuwa ametimiza mambo yote yaliyotabiriwa kuhusu Masihi. * Wanafunzi hao walipotambua kwamba ni Yesu aliyefufuliwa akiwa na mwili wa roho, akatoweka.

Wanafunzi hao wawili wakarudi Yerusalemu mara moja. Wakawakuta mitume wamekusanyika katika chumba kilichokuwa kimefungwa. Walipokuwa wakisimulia mambo waliyokuwa wamejionea, Yesu akatokea. Wafuasi wake walioduwaa hawakuamini macho yao! Yesu akawauliza: “Kwa nini shaka zinatokea mioyoni mwenu?” Kisha akawaambia: “Imeandikwa kwamba Kristo angeteseka na kufufuliwa kutoka kati ya wafu siku ya tatu.”—Luka 24:38, 46.

Kwa siku 40 baada ya kufufuliwa, Yesu aliwatokea wanafunzi wake katika pindi tofauti-tofauti. Katika pindi moja, aliwatokea wanafunzi zaidi ya 500! Pengine katika pindi hiyo ndiyo alipowapa mgawo huu mzito: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 28:19, 20.

Alipokutana kwa mara ya mwisho pamoja na mitume wake 11 waliokuwa waaminifu, Yesu aliwaahidi: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Matendo 1:8) Kisha Yesu akapanda juu na mawingu yakamfunika.

—Inatoka kwenye Mathayo, sura ya 28; Marko, sura ya 16; Luka, sura ya 24; Yohana, sura ya 20 na 21; 1 Wakorintho 15:5, 6.

^ fu. 6 Unabii mbalimbali wa Kimasihi ambao Yesu alitimiza unazungumziwa katika broshua hii Sehemu ya 14, Sehemu ya 15 na Sehemu ya 16 pia nyongeza yenye kichwa “Yesu Kristo—Masihi Aliyeahidiwa” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?