Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Sehemu ya 13

Wafalme Wazuri na Wafalme Wabaya

Wafalme Wazuri na Wafalme Wabaya

Taifa la Israeli limegawanyika. Wafalme wengi watawala taifa hilo, na wengi wao si waaminifu. Yerusalemu laharibiwa na Wababiloni

KAMA Yehova alivyotabiri, kwa sababu Sulemani aliiacha ibada safi, taifa la Israeli liligawanyika. Mwana wake aliyetawala baada yake, Rehoboamu, alikuwa mkali. Kwa hiyo, makabila kumi ya Israeli yakaasi na kufanyiza ufalme wa kaskazini wa Israeli. Makabila mawili yakaendelea kuwa chini ya mtawala aliyeketi katika kiti cha ufalme cha Daudi jijini Yerusalemu, yakifanyiza ufalme wa kusini wa Yuda.

Falme zote mbili zilikuwa na misukosuko, hasa kwa sababu ya wafalme wake ambao hawakuwa watiifu. Hali ya Israeli ilikuwa mbaya kuliko ya Yuda, kwa kuwa wafalme wake waliunga mkono ibada ya uwongo tangu mwanzo. Licha ya kazi zenye nguvu za manabii kama vile Eliya na Elisha—ambao hata waliwafufua wafu—taifa la Israeli lilirudia njia mbaya tena na tena. Mwishowe, Mungu akawaruhusu Waashuru wauharibu ufalme wa kaskazini.

Ufalme wa Yuda ulidumu miaka mia moja hivi baada ya ufalme wa Israeli kuangamizwa, lakini huo pia ulihukumiwa na Mungu. Ni wafalme wachache wa Yuda waliotii maonyo ya manabii wa Mungu na kujaribu kuliongoza taifa limrudie Yehova. Kwa mfano, Mfalme Yosia alianza kusafisha Yuda, akiondolea mbali ibada ya uwongo na kurekebisha hekalu la Yehova. Nakala ya awali ya Sheria ya Mungu iliyotolewa kupitia Musa ilipopatikana, Yosia alichochewa sana naye akazidisha kampeni yake ya kufanya mabadiliko.

Hata hivyo, inasikitisha kwamba wafalme waliotawala baada ya Yosia hawakufuata mfano wake mzuri. Kwa hiyo, Yehova akaruhusu taifa la Babiloni lishinde Yuda, na kuharibu Yerusalemu pamoja na hekalu lake. Waliookoka walipelekwa uhamishoni Babiloni. Mungu alitabiri kwamba wangekaa uhamishoni kwa miaka 70. Wakati wote huo Yuda palikuwa magofu—hadi, kama ilivyotabiriwa, taifa hilo liliporuhusiwa kurudi katika nchi yao.

Hata hivyo, hakuna wafalme wowote wa ukoo wa Daudi wangetawala hadi utawala wa yule Mkombozi aliyeahidiwa, Masihi aliyetabiriwa. Utawala wa wengi kati ya wafalme walioketi katika kiti cha ufalme cha Daudi jijini Yerusalemu ulionyesha wazi kwamba wanadamu wasio wakamilifu hawastahili kutawala. Masihi tu ndiye angestahili kikweli. Hivyo, Yehova akamwambia mfalme wa mwisho katika ukoo huo wa Daudi: ‘Livue taji. Hakika hili halitakuwa la mtu yeyote mpaka atakapokuja yule aliye na haki ya kisheria, nami nitampa yeye.’—Ezekieli 21:26, 27.

—Inatoka kwenye 1 Wafalme; 2 Wafalme; 2 Nyakati, sura ya 10 hadi 36; Yeremia 25:8-11.