Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 30

Wapendwa Wako Wanaweza Kuwa Hai Tena!

Wapendwa Wako Wanaweza Kuwa Hai Tena!

Kifo husababisha majonzi na huzuni nyingi. Hiyo ndiyo sababu Biblia inasema kifo ni adui. (1 Wakorintho 15:26) Katika Somo la 27, ulijifunza kwamba Yehova atamwangamiza adui huyo. Lakini itakuwaje kwa watu ambao tayari wamekufa? Katika somo hili, utajifunza mengi kuhusu ahadi nyingine ya Yehova yenye kupendeza. Atafufua mabilioni ya watu ili wafurahie kuishi milele. Atafanya wawe hai tena! Je, kweli hilo linawezekana? Je, watafufuliwa ili waishi mbinguni au duniani?

1. Yehova atawafanyia nini wapendwa wetu waliokufa?

Yehova anatamani sana kuwafufua watu waliokufa. Mwanamume mwenye imani Ayubu, alikuwa na uhakika kwamba ikiwa angekufa Mungu hangemsahau. Alimwambia Mungu hivi: “Utaita, nami nitakujibu [kutoka kaburini].”​—Soma Ayubu 14:13-15.

2. Tunajuaje kwamba watu waliokufa wanaweza kufufuliwa?

Yesu alipokuwa duniani, Mungu alimpa nguvu za kuwafufua watu. Yesu alimfufua msichana mwenye umri wa miaka 12 na mwana wa mjane. (Marko 5:41, 42; Luka 7:12-15) Baadaye, Lazaro, rafiki ya Yesu alikufa. Ingawa Lazaro alikuwa amekufa na mwili wake ulikuwa kaburini kwa siku nne, Yesu alimfufua. Baada ya Yesu kusali kwa Mungu, aliita hivi kwa sauti kubwa: “Lazaro, njoo huku nje!” Kisha “mtu huyo aliyekuwa amekufa akatoka” akiwa hai! (Yohana 11:43, 44) Wazia jinsi marafiki na watu wa familia ya Lazaro walivyofurahi!

3. Kuna tumaini gani kwa wapendwa wako waliokufa?

Biblia inaahidi hivi: “Kutakuwa na ufufuo.” (Matendo 24:15) Watu ambao Yesu aliwafufua alipokuwa duniani hawakuwa wameenda mbinguni. (Yohana 3:13) Walifurahia kufufuliwa hapa duniani. Vivyo hivyo, hivi karibuni Yesu atafufua mabilioni ya watu ili wafurahie kuishi milele katika paradiso duniani. Alisema kwamba “wote walio katika makaburi ya ukumbusho” watafufuliwa, kutia ndani wale tunaofikiri wamesahaulika lakini wako katika kumbukumbu ya Mungu.​—Yohana 5:28, 29.

CHIMBA ZAIDI

Chunguza uthibitisho ulio katika Biblia kwamba watu waliokufa wanaweza kufufuliwa na watafufuliwa wakati ujao. Jifunze jinsi ufufuo unavyoweza kukufariji na kukupa tumaini.

4. Yesu alithibitisha kwamba ana uwezo wa kuwafufua waliokufa

Jifunze mengi kuhusu mambo ambayo Yesu alimfanyia Lazaro rafiki yake. Soma Yohana 11:14, 38-44, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Tunajuaje kwamba kwa kweli Lazaro alikuwa amekufa?​—Ona mstari wa 39.

  • Ikiwa Lazaro alikuwa ameenda mbinguni, je, unafikiri Yesu angemrudisha aishi tena duniani?

Onyesha VIDEO.

5. Watu wengi watafufuliwa!

Soma Zaburi 37:29, kisha mzungumzie swali hili:

  • Mabilioni ya watu watakaofufuliwa wataishi wapi?

Yesu atawafufua watu wengi sana, si wale tu waliomwabudu Yehova. Soma Matendo 24:15, kisha mzungumzie swali hili:

  • Ungependa kumwona nani akifufuliwa?

Fikiria jambo hili: Ni rahisi kwa Yesu kumfufua mtu kama vile baba anavyomwamsha mtoto wake ambaye amelala usingizi

6. Ufufuo unaweza kukupatia faraja na tumaini

Simulizi la Biblia kuhusu binti ya Yairo limewafariji na kuwatia moyo watu wengi wanaoomboleza. Soma simulizi hilo la mambo yaliyotokea kihalisi kwenye Luka 8:40-42, 49-56.

Kabla ya kumfufua binti ya Yairo, Yesu alimwambia hivi baba yake: “Usiogope, uwe tu na imani.” (Ona mstari wa 50.) Tumaini la ufufuo linaweza kukusaidiaje . . .

  • mpendwa wako anapokufa?

  • uhai wako unapokuwa hatarini?

Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Tumaini la ufufuo limewafariji na kuwatia moyo jinsi gani wazazi wa Phelicity?

WATU FULANI HUSEMA: “Wazo la kuwafufua watu waliokufa ni ndoto tu.”

  • Wewe una maoni gani?

  • Unaweza kutumia andiko gani ili kuonyesha kwamba kutakuwa na ufufuo?

MUHTASARI

Biblia inaahidi kwamba mabilioni ya watu waliokufa watafufuliwa. Yehova anataka waishi tena na amempa Yesu nguvu za kuwafufua.

Ungejibuje?

  • Yehova na Yesu wanahisije kuhusu kuwafufua watu waliokufa?

  • Mabilioni ya watu watakaofufuliwa wataishi wapi, mbinguni au duniani? Kwa nini unajibu hivyo?

  • Kwa nini una uhakika kwamba wapendwa wako waliokufa wanaweza kuishi tena?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Chunguza mambo unayoweza kufanya ili kukabiliana na huzuni unapofiwa.

“Kukabiliana na Huzuni ya Kufiwa” (Amkeni! Na. 3, 2018)

Je, kweli kanuni za Biblia zinaweza kumsaidia mtu anayeomboleza?

Mpendwa Wako Anapokufa (5:06)

Watoto wanaweza kufanya nini ili kukabiliana na huzuni mtu wanayempenda anapokufa?

Fidia (2:07)

Je, kuna watu watakaofufuliwa ili waishi mbinguni? Ni nani ambao hawatafufuliwa?

“Ufufuo Ni Nini?” (Makala iliyo kwenye mtandao)