Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 21

Jinsi Habari Njema Inavyohubiriwa

Jinsi Habari Njema Inavyohubiriwa

Hivi karibuni, Yehova atatumia Ufalme wake kuondoa matatizo yetu yote. Hizo ni habari njema ambazo kila mtu anapaswa kusikia. Yesu aliwaagiza wafuasi wake wawahubirie watu wote ujumbe huo! (Mathayo 28:19, 20) Mashahidi wa Yehova wametii jinsi gani amri hiyo ya Yesu?

1. Andiko la Mathayo 24:14 linatimizwaje leo?

Yesu alitabiri hivi: “Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa.” (Mathayo 24:14) Mashahidi wa Yehova wanafurahia kufanya kazi hiyo muhimu. Tunahubiri habari njema ulimwenguni pote katika lugha zaidi ya elfu moja! Kazi hiyo kubwa inahitaji jitihada nyingi na mipango mizuri. Kazi hiyo haiwezi kufanikiwa bila msaada wa Yehova.

2. Tunafanya jitihada gani ili kuwahubiria watu?

Tunahubiri mahali popote ambapo tunaweza kuwapata watu. Kama Wakristo wa karne ya kwanza, tunahubiri “nyumba kwa nyumba.” (Matendo 5:42) Kupitia njia hiyo, tunahubiri kikamili na kuwafikia mamilioni ya watu kila mwaka. Kwa kuwa wakati mwingine si rahisi kuwapata watu nyumbani, tunahubiri pia katika maeneo mengi ya hadharani. Sikuzote tunatafuta fursa za kuwaambia wengine kumhusu Yehova na makusudi yake.

3. Ni nani walio na jukumu la kuhubiri habari njema?

Wakristo wote wa kweli wanapaswa kuwahubiria wengine habari njema. Tunachukua jukumu hilo kwa uzito. Tunahubiri kwa bidii kwa sababu tunajua kwamba uhai wa watu uko hatarini. (Soma 1 Timotheo 4:16.) Hatulipwi mshahara tunapofanya kazi hii kwa sababu Biblia inasema hivi: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:7, 8) Si kila mtu ambaye atakubali ujumbe wetu. Lakini tunaendelea kuhubiri kwa sababu hiyo ni sehemu ya ibada yetu, na tunamfurahisha Yehova.

CHIMBA ZAIDI

Jifunze kuhusu jitihada za Mashahidi wa Yehova za kuhubiri ulimwenguni pote na uone jinsi Yehova anavyotusaidia.

4. Tunajitahidi sana ili kuwafikia watu wote

Mashahidi wa Yehova hufanya jitihada za pekee ili kuwahubiria watu habari njema kila mahali. Onyesha VIDEO, kisha mzungumzie swali linalofuata.

  • Ni nini kinachokuvutia kuhusu jitihada za Mashahidi wa Yehova za kuhubiri?

Soma Mathayo 22:39 na Waroma 10:13-15, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Kazi yetu ya kuhubiri inaonyeshaje kwamba tunawapenda jirani zetu?

  • Yehova anahisije kuhusu wale wanaohubiri habari njema?​—Ona mstari wa 15.

5. Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu

Mambo mengi yaliyoonwa yanathibitisha kwamba Yehova anaongoza kazi yetu. Kwa mfano, nchini New Zealand, ndugu anayeitwa Paul alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba, alikutana na mwanamke fulani alasiri moja. Siku hiyohiyo asubuhi, mwanamke huyo alikuwa amesali kwa Mungu akitumia jina la Mungu, Yehova, na akamwomba amtume mtu amtembelee. Paul anasema: “Saa tatu baadaye, nilibisha mlango wake.”

Soma 1 Wakorintho 3:9, kisha mzungumzie swali hili:

  • Mambo yaliyoonwa, kama hilo lililotokea huko New Zealand, yanathibitishaje kwamba Yehova anaongoza kazi ya kuhubiri?

Soma Matendo 1:8, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini tunahitaji msaada wa Yehova ili tutimize huduma yetu?

Je, wajua?

Katika kila mkutano wetu wa katikati ya juma, tunapata mazoezi ya jinsi ya kuhubiri. Ikiwa umewahi kuhudhuria mkutano huo, una maoni gani kuhusu mazoezi yanayotolewa?

6. Tunatii amri ya Mungu ya kuhubiri

Katika karne ya kwanza, wapinzani walijaribu kuwazuia wanafunzi wa Yesu ili wasihubiri. Wakristo wa mapema walitetea haki yao ya kuhubiri kwa “kuithibitisha kisheria habari njema.” (Wafilipi 1:7) Mashahidi wa Yehova wanafanya vivyo hivyo leo. a

Soma Matendo 5:27-42, kisha mzungumzie swali hili:

HUENDA MTU AKAULIZA: “Kwa nini Mashahidi wa Yehova wanahubiri nyumba kwa nyumba?”

  • Wewe ungejibuje swali hilo?

MUHTASARI

Yesu aliwaagiza wafuasi wake wahubiri habari njema katika mataifa yote. Yehova anawasaidia watu wake kufanya kazi hiyo.

Ungejibuje?

  • Kazi ya kuhubiri habari njema inafanywaje ulimwenguni pote?

  • Kazi yetu ya kuhubiri inaonyeshaje kwamba tunawapenda jirani zetu?

  • Je, unafikiri kazi ya kuhubiri inaweza kutuletea furaha? Kwa nini?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Ona jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyowahubiria watu katika majiji makubwa.

Mahubiri ya Pekee ya Hadharani Jijini Paris (5:11)

Mashahidi wa Yehova wamewasaidiaje wakimbizi?

Kutosheleza Kiu ya Kiroho Miongoni Mwa Wakimbizi (5:59)

Sikiliza maelezo ya dada fulani aliyefurahia kutumia maisha yake katika utumishi wa wakati wote.

Ninafurahi Kwamba Nilichagua Mradi Huu (6:29)

Jifunze kuhusu ushindi wa kesi mahakamani ambao umesaidia kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema.

“Wahubiri wa Ufalme Wanapeleka Kesi Mahakamani” (Ufalme wa Mungu Unatawala!, sura ya 13)

a Mungu ndiye ametupatia amri ya kuhubiri. Hivyo, Mashahidi wa Yehova hawahitaji kibali cha serikali za wanadamu ili kuhubiri habari njema.