Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SOMO LA 10

Mikutano ya Mashahidi wa Yehova Inaweza Kukunufaishaje?

Mikutano ya Mashahidi wa Yehova Inaweza Kukunufaishaje?

Je, umewahi kualikwa uhudhurie mkutano wa Mashahidi wa Yehova? Ikiwa hujawahi kuhudhuria, huenda ukawa na wasiwasi unapoalikwa uhudhurie kwa mara ya kwanza. Huenda ukajiuliza: ‘Ni nini hufanyika katika mikutano hiyo? Kwa nini mikutano hiyo ni muhimu? Kwa nini ninapaswa kuhudhuria?’ Katika somo hili utajifunza jinsi mikutano hiyo inavyoweza kukunufaisha na kukusaidia uwe na uhusiano wa karibu zaidi na Mungu.

1. Kwa nini ni muhimu sana kukutana pamoja?

Mwandikaji fulani wa Biblia alitaja sababu muhimu zaidi ya kukutana pamoja, alisema: “Katika kutaniko kubwa, nitamsifu Yehova.” (Zaburi 26:12) Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova hufurahia sana kukutana pamoja. Ulimwenguni pote, wao hukutana kila juma ili kumsifu Mungu, kuimba, na kusali. Kila mwaka, wao pia hukutana mara chache katika vikundi vikubwa zaidi ili kumwabudu Mungu.

2. Utajifunza nini katika mikutano yetu?

Katika mikutano, sisi hujifunza Neno la Mungu, “[tunalifafanua] waziwazi na kueleza maana yake.” (Soma Nehemia 8:8.) Ukihudhuria mikutano, utajifunza kumhusu Yehova na sifa zake zenye kupendeza. Unapojifunza mengi kuhusu jinsi anavyokupenda, ndivyo utakavyozidi kuwa na uhusiano wa karibu naye. Vilevile utajifunza jinsi anavyoweza kukusaidia uwe na maisha yenye kuridhisha.​—Isaya 48:17, 18.

3. Utanufaikaje kwa kushirikiana na wengine katika mikutano?

Yehova anatuagiza “tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri, bila kuacha kukutana pamoja.” (Waebrania 10:24, 25) Katika mikutano yetu, utakutana na watu wanaopendana sana na ambao, kama wewe, wanataka kujifunza mengi kumhusu Mungu. Utawasikia wakizungumza kuhusu mambo yenye kutia moyo kutoka kwenye Biblia. (Soma Waroma 1:11, 12.) Vilevile utawafahamu wengine ambao wamefaulu kukabiliana na matatizo yanayowapata watu waliofunga ndoa au ambao hawajafunga ndoa. Hizo ni baadhi ya sababu chache zinazofanya tutii agizo la Yehova la kukutana pamoja kwa ukawaida!

CHIMBA ZAIDI

Jifunze mambo yanayotendeka katika mikutano ya Mashahidi wa Yehova na kwa nini ni muhimu tujitahidi kuhudhuria mikutano hiyo.

4. Mikutano ya Mashahidi wa Yehova

Katika karne ya kwanza, Wakristo walikutana kwa ukawaida ili kumwabudu Yehova. (Waroma 16:3-5) Soma Wakolosai 3:16, kisha mzungumzie swali hili:

  • Wakristo wa karne ya kwanza walimwabudu Yehova jinsi gani?

Leo, Mashahidi wa Yehova hukutana kwa ukawaida katika maeneo yao ya ibada. Ili kuona mambo yanayotendeka katika mikutano, onyesha VIDEO. Kisha, mtazame picha ya mikutano ya kutaniko iliyo kwenye ukurasa huu na mzungumzie maswali haya:

  • Uliona mambo gani katika Jumba la Ufalme ambayo yametajwa kwenye Wakolosai 3:16?

  • Ni jambo gani lingine lililokupendeza kwenye video au picha kuhusu mikutano?

Soma 2 Wakorintho 9:7, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini hakuna malipo ya kiingilio kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova?

Chunguza pamoja na mwalimu wako mambo ambayo yatazungumziwa kwenye mkutano juma hili.

  • Unafikiri utafurahia au kunufaika zaidi na sehemu gani ya mkutano?

Je, wajua?

Kwenye jw.org, unaweza kupata mahali na wakati ambao mikutano hufanywa ulimwenguni pote.

  1. Mikutano yetu inatia ndani hotuba, maigizo, na video. Mikutano huanza na kumalizika kwa wimbo na sala

  2. Katika baadhi ya sehemu za mkutano wasikilizaji hukaribishwa kutoa maelezo

  3. Watu wote wanakaribishwa​—watu wenye familia, waseja, waliozeeka, na watoto

  4. Hakuna malipo ya kiingilio wala sadaka zinazokusanywa kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova

5. Jitihada inahitajika ili kuhudhuria mikutano

Fikiria hali ilivyokuwa katika familia ya Yesu. Kila mwaka, walitembea kwa siku kadhaa umbali wa kilomita 100 hivi kwenye eneo lenye milima kutoka Nazareti hadi Yerusalemu ili kwenda hekaluni. Soma Luka 2:39-42, kisha mzungumzie maswali haya:

  • Je, unafikiri safari hiyo ya kwenda Yerusalemu ilihitaji jitihada zozote?

  • Kwa nini huenda ukahitaji kujitahidi ili uhudhurie mikutano?

  • Je, unafikiri jitihada hizo ni muhimu? Kwa nini?

Biblia inasema kwamba ni muhimu sana kukutana pamoja ili kuabudu. Soma Waebrania 10:24, 25, kisha mzungumzie swali hili:

  • Kwa nini tunapaswa kuhudhuria mikutano kwa ukawaida?

WATU FULANI HUSEMA: “Si lazima ukusanyike pamoja na watu wengine. Inatosha kusoma Biblia ukiwa nyumbani.”

  • Ni andiko au mfano gani ulio katika Biblia unaoonyesha jambo ambalo Yehova anataka tufanye?

MUHTASARI

Kuhudhuria mikutano kutakusaidia ujifunze mengi kumhusu Yehova, uimarishe urafiki wako pamoja naye, na umwabudu ukiwa pamoja na watu wengine.

Ungejibuje?

  • Kwa nini Yehova anatutia moyo tukutane pamoja?

  • Utajifunza mambo gani kwenye mikutano ya Mashahidi wa Yehova?

  • Unafikiri utanufaika kwa njia gani nyingine ukihudhuria mikutano?

Lengo

CHUNGUZA ZAIDI

Vipi ikiwa una wasiwasi kuhusu kuhudhuria mkutano? Ona jambo lililomsaidia mwanamume aliyehisi hivyo apende mikutano.

Hatutasahau Tulivyokaribishwa (4:17)

Ona jinsi kijana fulani alivyofurahia mikutano na jambo alilofanya ili kuendelea kuhudhuria.

Nilifurahia Sana Mikutano! (4:33)

Jifunze jinsi wengine wanavyohisi kuhusu kuhudhuria mikutano.

“Kwa Nini Uhudhurie Mikutano Kwenye Jumba la Ufalme?” (Makala iliyo kwenye mtandao)

Ona jinsi maisha ya mwanamume aliyeshirikiana na wahalifu yalivyobadilika alipohudhuria mkutano wa Mashahidi wa Yehova.

“Nilitembea na Bunduki Kila Wakati” (Mnara wa Mlinzi, Julai 1, 2014)