Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nitayatumiaje Maisha Yangu?

Nitayatumiaje Maisha Yangu?

SURA YA 38

Nitayatumiaje Maisha Yangu?

“Mwanzoni sikujali kuhusu wakati ujao. Lakini nilipokaribia kumaliza shule, nilitambua kwamba ninaingia katika ulimwengu wenyewe, ulimwengu wa watu wazima.”—Alex.

WAZIA kwamba unapanga kufunga safari ya kwenda mbali kutoka nyumbani. Labda utatazama ramani kwanza na kuona njia bora itakayokufikisha huko. Ndivyo pia na kupanga maisha yako ya usoni. “Kuna mengi unayoweza kufanya,” asema Michael, kijana ambaye sasa anatumikia katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova. Utaamua namna gani jambo la kufanya? “Kwa kujiwekea miradi,” asema Michael.

Uone mradi kama mahali unapokwenda. Hailekei utafika huko kwa kutangatanga bila kusudi. Ingekuwa afadhali kama ungechukua ramani na kupanga safari yako ya mfano. Ukifanya hivyo, utakuwa ukifuata shauri lililo katika Methali 4:26: “Lainisha mapito ya mguu wako.” Tafsiri ya Biblia Habari Njema inatafsiri hivi mstari huo: “Fikiria njia utakayochukua.”

Miaka ijayo, utafanya maamuzi mengi mazito kuhusu ibada, kazi, ndoa, familia, na mambo mengine muhimu. Itakuwa rahisi zaidi kufanya maamuzi kwa hekima ikiwa unajua unakokwenda. Na unapopanga safari ya maisha yako, kuna jambo moja ambalo kwa kweli hupaswi kupuuza.

“Mkumbuke Muumba Wako”

Ili uwe na furaha ya kweli, lazima uzingatie maneno haya ya Mfalme Sulemani mwenye hekima: “Mkumbuke, sasa, Muumba wako Mkuu katika siku za ujana wako.” (Mhubiri 12:1) Yaani, maamuzi unayofanya maishani yanapaswa kuongozwa na tamaa ya kumpendeza Mungu.

Kwa nini ni muhimu kuzingatia hilo? Biblia inasema hivi katika Ufunuo 4:11: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” Viumbe vyote, mbinguni na duniani, vina deni la kumrudishia shukrani Muumba. Je, unamshukuru kwa kukupa “uhai na pumzi na vitu vyote”? (Matendo 17:25) Je, huchochewi kumfanyia jambo fulani Yehova Mungu ili kumwonyesha shukrani zako kwa yote ambayo amekufanyia?

Wakimkumbuka Muumba wao, vijana wengi ambao ni Mashahidi wa Yehova wameamua kumtumikia wakati wote. Fikiria utumishi mbalimbali wenye kusisimua unaoweza kufanya.

Upainia. Mapainia wa kawaida hutumia muda mwingi katika huduma. Kupitia mazoezi na uzoefu, wameboresha stadi zao wakiwa walimu wa Biblia.

Kutumikia mahali penye uhitaji mkubwa zaidi. Wengine wamehamia sehemu ambazo zina watangazaji wachache wa Ufalme. Wengine hujifunza lugha mpya na kutumikia katika kutaniko la lugha ya kigeni au hata kuhamia nchi ya kigeni. *

Utumishi wa umishonari. Mapainia wanaostahili wenye afya nzuri na nguvu huzoezwa ili wakatumikie katika nchi za kigeni. Wamishonari huishi maisha yenye kusisimua na yenye kusudi.

Utumishi wa Betheli. Washiriki wa familia ya Betheli hutumikia katika ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova. Katika nchi fulani kazi hiyo hutia ndani kuchapisha na kusafirisha vitabu na magazeti ya Biblia.

Utumishi wa kimataifa. Watumishi wa kimataifa husafiri kwenda nchi nyingine ili kusaidia katika ujenzi wa Majumba ya Ufalme, Majumba ya Kusanyiko, na majengo ya ofisi za tawi.

Shule ya Mazoezi ya Kihuduma. Wazee na watumishi wa huduma waseja wanaostahili huzoezwa kushughulikia mambo ya tengenezo na kutoa hotuba. Ndugu fulani waliozoezwa hupata mgawo wa kwenda nchi nyingine.

Kupanga Safari Yako

Utumishi wa wakati wote ni mradi mzuri, nao huleta baraka nyingi. Hata hivyo, utahitaji kufikiria na kupanga mapema. Kwa mfano, jiulize, ‘Nina uwezo na stadi gani zitakazoniwezesha kujitegemeza mwenyewe?’

Kelly alitaka sana kuwa painia, kwa hiyo alipanga kazi atakayofanya. “Nilihitaji kuchagua kazi ambayo ingeniruhusu kujitegemeza mwenyewe huku nikiendelea na huduma yangu,” anasema.

Kelly alipata mafunzo kupitia programu ya mafunzo ya kazi hususa alipokuwa katika shule ya sekondari. Hilo lilimwezesha kufikia mradi wake. “Nilitaka kufanya utumishi wa wakati wote,” asema Kelly. “Mambo mengine yote yalikuwa sehemu ya pili.” Kelly anafurahia uamuzi huo. “Naona kwamba nilifanya uamuzi bora zaidi,” anasema.

Omba Maelekezo

Ikiwa unatembea katika eneo geni, haikosi wakati fulani utahitaji kuomba maelekezo. Unaweza kufanya vivyo hivyo unapopanga maisha yako ya wakati ujao. Omba ushauri kutoka kwa wengine. Andiko la Methali 20:18 linasema: “Kwa shauri mipango yenyewe hufanywa imara.”

Wazazi wako wanaweza kukusaidia sana. Unaweza pia kuomba ushauri kutoka kwa Wakristo wakomavu ambao maisha yao yanaonyesha kwamba wamepata hekima inayotoka kwa Mungu. “Tafuta watu wazima walio mifano mizuri katika kutaniko lenu au makutaniko yaliyo karibu,” anapendekeza Roberto, Mwanabetheli aliye na umri wa miaka 20 na kitu.

Zaidi ya wote, Yehova Mungu anataka kukusaidia ufanye maamuzi maishani yatakayokuletea furaha nyingi. Kwa hiyo, mwombe akusaidie ‘uendelee kufahamu yale yaliyo mapenzi yake’ kuhusu wakati wako ujao. (Waefeso 5:17) Katika kila sehemu ya maisha yako, fuata himizo la Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.”

Unaweza kupata habari zaidi kwa kutazama DVD yenye kichwa: “Young People Ask—What Will I Do With My Life?” Inapatikana katika lugha zaidi ya 30

[Maelezo ya Chini]

MAANDIKO MUHIMU

‘Mnijaribu . . . ,’ Yehova wa majeshi amesema, ‘kama sitawafungulia ninyi malango ya mbinguni na kuwamwagia baraka hata kusiwe na uhitaji tena.’Malaki 3:10.

PENDEKEZO

Zungumza na wale ambao wamekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa muda mrefu. Waulize ni kwa nini walichagua kufanya hivyo na wamepata baraka gani.

JE, WAJUA . . .?

Umeme unaweza kuendesha chombo. Vivyo hivyo, roho takatifu ya Mungu inaweza kukuchochea kutimiza mengi katika utumishi wake.—Matendo 1:8.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Ili niwe na shangwe zaidi katika huduma, nitazungumza na ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Una vipawa na ujuzi gani?

● Unaweza kutumia vipawa vyako jinsi gani ili kumsifu Yehova?

● Ni utumishi gani wa wakati wote uliotajwa katika makala hii unaokuvutia zaidi?

[Blabu katika ukurasa wa 313]

‘‘Nawaheshimu sana wazazi wangu. Bidii yao katika huduma, jinsi ambavyo wamekabiliana na hali ngumu ya kiuchumi, na jinsi walivyonitia moyo nishiriki katika huduma ya wakati wote, yote hayo yalinichochea sana.’’—Jarrod

[Sanduku katika ukurasa wa 314]

Ukurasa wa Mazoezi

Miradi Yangu

Tia alama miradi ambayo ungependa kujiwekea. Tumia nafasi zilizoandaliwa kuongeza miradi mingine ambayo ungependa kuifikia.

Miradi ya Huduma

□ Kuongeza wakati ninaotumia katika huduma kufikia saa ․․․․․ kila mwezi

□ Kuwaachia watu vitabu, magazeti, na vijitabu ․․․․․ kila mwezi

□ Kutumia Biblia ninapozungumzia imani yangu

□ Kufanya ziara za kurudia ․․․․․ kila mwezi

□ Kuanzisha funzo la Biblia

Miradi mingine: ․․․․․

Miradi ya Kujifunza

□ Kusoma kurasa ․․․․․ za Biblia kila siku

□ Kutayarisha mikutano ya kila juma

□ Kufanya utafiti kuhusu habari zifuatazo za Biblia: ․․․․․

Miradi ya Kutimiza Kutanikoni

□ Kutoa angalau maelezo mara moja katika kila mkutano

□ Kuanzisha mazungumzo pamoja na mtu mwenye umri mkubwa ambaye ningependa kumfahamu vizuri

□ Kumtembelea mshiriki wa kutaniko aliye mzee kwa umri au dhaifu kimwili

Miradi mingine: ․․․․․

Tarehe ya Leo ․․․․․

Baada ya miezi sita, chunguza uone umepiga hatua kiasi gani katika kutimiza miradi yako. Fanya mabadiliko au uongeze miradi mingine kulingana na uhitaji.

[Picha katika ukurasa wa 312]

Kuwa na miradi kutakuzuia usipoteze nguvu zako bure na hivyo kutofika popote