Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Kuna Sheria Nyingi Sana?

Kwa Nini Kuna Sheria Nyingi Sana?

SURA YA 22

Kwa Nini Kuna Sheria Nyingi Sana?

Andika baadhi ya sheria za familia yenu. ․․․․․

Unakubaliana na sheria zote za familia yenu?

□ Ndiyo □ Hapana

Ni sheria gani unayoiona kuwa ngumu zaidi kutii? ․․․․․

KATIKA kila familia kuna sheria kuhusu mambo kama vile kazi za shule, kazi za nyumbani, wakati maalumu wa kutoka au kurudi nyumbani, na pia kuhusu matumizi ya simu, televisheni, na kompyuta. Huenda pia ukawekewa sheria kuhusu shule na marafiki.

Je, unajiona kama mfungwa kwa sababu ya sheria zote hizo? Huenda unahisi kama vijana wafuatao:

“Sheria niliyowekewa ya kurudi nyumbani kabla ya saa fulani ilinikera kwelikweli! Nilichukizwa sana kwa sababu vijana wengine waliruhusiwa kuchelewa kurudi nyumbani.”—Allen.

“Inaudhi sana simu yako ya mkononi inapokaguliwa-kaguliwa. Naona kwamba ninatendewa kama mtoto!”—Elizabeth.

“Nilihisi wazazi wangu wanataka kuniharibia maisha yangu, ni kana kwamba hawakutaka niwe na rafiki yeyote!”—Nicole.

Ijapokuwa vijana wengi hawapendi sheria zinazowekwa na wazazi wao, wengi wao wanakubali kwamba hali ingekuwa mbaya zaidi ikiwa hakungekuwa na sheria. Hivyo basi, ikiwa sheria zina faida, kwa nini nyingine zinaudhi sana?

“Mimi si Mtoto!”

Labda sheria zinakuudhi kwa sababu unaona kwamba unatendewa kama mtoto. Ukiwa umekasirika, unatamani kuwaambia, “Mimi si mtoto!” Bila shaka, huenda wazazi wako wanaona sheria hizo zinahitajiwa, ili kukulinda na kukutayarisha kwa ajili ya maisha ya baadaye.

Hata hivyo, huenda sheria unazowekewa haziendi sambamba na umri wako. Huenda unaweza kujihisi kwamba umezuiwa kama alivyohisi msichana mmoja aitwaye Brielle, ambaye alisema hivi kuhusu wazazi wake: “Hawajui hata kidogo maisha ya mtu wa umri wangu. Hawataki niseme chochote, nifanye lolote au niwe mtu mzima.” Kijana aitwaye Allison anahisi hivyo pia. Anasema “Wazazi wangu hawaelewi kwamba nina umri wa miaka 18, bali si miaka 10. Wanahitaji kunipa uhuru zaidi!”

Sheria zinaweza kuchukiza zaidi hasa ikiwa ndugu na dada zako wanaendekezwa. Kwa mfano, akikumbuka mambo yalivyokuwa alipokuwa tineja, kijana anayeitwa Matthew anasema hivi kuhusu dada yake mdogo na binamu zake, “Hata kama ‘wangeua mtu,’ hawangefanywa chochote!”

Maisha Yangekuwa Mazuri Bila Sheria?

Huenda ukatamani kutokuwa chini ya sheria za wazazi wako. Lakini je, kweli maisha yangekuwa mazuri bila mwongozo wao? Huenda unawajua vijana fulani wa rika lako ambao wanaweza kuamua kurudi nyumbani wakati wowote wapendao, wanaweza kuvaa chochote wakipendacho, na kwenda na rafiki zao kokote na wakati wowote wapendao. Huenda wazazi wao wana shughuli nyingi sana hivi kwamba hawajui kile ambacho watoto wao wanafanya. Hata sababu ziwe nini, Biblia inaonyesha kwamba wazazi hawawezi kufanikiwa wakimlea mtoto kwa njia hiyo. (Methali 29:15) Kuenea kwa ukosefu wa upendo kunakoonekana leo duniani, kunasababishwa hasa na watu wenye ubinafsi ambao wengi wao walilelewa katika familia ambazo hazikuwa na sheria.—2 Timotheo 3:1-5.

Badala ya kuwaonea wivu rafiki zako ambao wameruhusiwa kufanya chochote wapendacho, zione sheria ambazo wazazi wako wamekuwekea kuwa uthibitisho wa kwamba wanakupenda na wanakujali. Kwa kukuwekea sheria fulani, wanamwiga Yehova Mungu, aliyewaambia watu wake hivi: “Nitakufanya uwe na ufahamu na kukufundisha katika njia unayopaswa kuiendea. Nitakupa shauri jicho langu likiwa linakutazama.”—Zaburi 32:8.

Hata hivyo, huenda nyakati nyingine ukahisi umelemewa na sheria za wazazi wako. Unaweza kufanya nini?

Wasiliana kwa Njia Inayofaa

Iwe unataka uhuru zaidi au kupunguza tu mkazo unaotokana na sheria ambazo wazazi wako wamekuwekea, siri ya kupata mafanikio ni kuwasiliana nao kwa njia inayofaa. Huenda wengine wakasema: ‘Nimejaribu kuzungumza na wazazi wangu, lakini ni kazi bure!’ Ikiwa ndivyo unavyohisi, jiulize: ‘Je, ninaweza kubadili jinsi ninavyowasiliana nao?’ Mawasiliano ni kifaa muhimu kinachoweza (1) kuwasaidia wengine wakuelewe au (2) kukusaidia kuelewa ni kwa nini mambo unayotaka yamekataliwa. Ikiwa unataka utendewe kama mtu mzima, basi lazima ujifunze kuwasiliana nao kama mtu mzima. Unaweza kufanya hivyo jinsi gani?

Jifunze kuzuia hisia zako. Ili kuwasiliana vizuri, lazima uwe na sifa ya kujizuia. Biblia inasema hivi: “Mtu mjinga huiachilia roho yake yote, lakini mwenye hekima huituliza mpaka mwisho.” (Methali 29:11) Hivyo, epuka kunung’unika-nung’unika, kununa-nuna, na kutaka ubembelezwe kama mtoto. Ni kweli kwamba huenda ukataka kubamiza mlango au kupiga-piga miguu chini kwa hasira unapohisi kwamba wazazi wako wanakunyima uhuru. Lakini, kufanya hivyo kutawafanya wakuwekee sheria nyingi hata zaidi.

Jaribu kuwaelewa wazazi wako. Tracy, msichana Mkristo aliyelelewa na mzazi mmoja, anasema, “Mimi hujiuliza, ‘Mama anataka kunifundisha nini?’” Tracy alikata kauli gani? “Anajaribu kunisaidia niwe na sifa nzuri.” (Methali 3:1, 2) Kuelewa hisia za wazazi wako kwa njia hiyo kunaweza kukusaidia kuwasiliana nao vizuri.

Kwa mfano, tuseme wazazi wako wanasita kukupa ruhusa ya kwenda kujumuika na vijana wengine. Badala ya kubishana nao, unaweza kuwauliza, “Namna gani ikiwa kutakuwa na mtu mkomavu anayetegemeka?” Huenda bado wazazi wako wakakataa. Hata hivyo, ukielewa hangaiko lao, huenda ukapendekeza jambo ambalo labda litakubalika machoni pao.

Jiendeshe kwa njia itakayofanya wazazi wako wawe na imani nawe. Wazia mtu amechukua mkopo katika benki. Akiwa na mazoea ya kulipa kwa wakati, benki itamwamini na inaweza kumpa mkopo mkubwa zaidi siku za usoni. Ndivyo ilivyo na nyumbani. Unapaswa kuwatii wazazi wako. Ukifanya hivyo hata katika mambo madogo, wazazi wako watakuamini hata zaidi wakati ujao. Lakini, ukiwatamausha wazazi wako mara kwa mara, usishangae wakikaza kamba au hata kukuzuilia kabisa.

Unapovunja Sheria

Haikosi kuna wakati ambapo utavunja sheria fulani. Huenda ukakosa kufanya kazi ulizopewa, ukatumia simu kwa muda mrefu sana, au ukachelewa kurudi nyumbani. (Zaburi 130:3) Katika hali hiyo, utalazimika kuwaeleza ni kwa nini. Unaweza kuzuiaje hali isiwe mbaya zaidi?

Sema kweli. Usiwape hadithi ndefu. Kufanya hivyo kwaweza kuwafanya wazazi wako wapoteze imani waliyokuwa nayo kukuelekea. Hivyo sema kweli na kutaja mambo waziwazi. (Methali 28:13) Epuka kujitetea au kupunguza uzito wa kosa. Na sikuzote ukumbuke kwamba “jibu, linapokuwa la upole, hugeuza ghadhabu.”—Methali 15:1.

Omba msamaha. Kuwaeleza kwamba unasikitika kwa kuwahangaisha, kuwavunja moyo, au kuwaongezea kazi, ni vizuri na kunaweza kukupunguzia adhabu. Hata hivyo, unapaswa kufanya hivyo kutoka moyoni.

Kubali matokeo. (Wagalatia 6:7) Huenda mwanzoni ukapinga adhabu hiyo, hasa unapoona kwamba unaonewa. Hata hivyo, kukubali makosa na nidhamu huonyesha kwamba wewe ni mkomavu. Jambo la maana ni kujitahidi kuwafanya wazazi wakuamini tena.

Andika unachohitaji kufanyia kazi kati ya hoja tatu ambazo zimezungumziwa. ․․․․․

Kumbuka kwamba wazazi wako wana jukumu la kukuongoza. Ndio maana Biblia inataja “amri ya baba yako” na “sheria ya mama yako.” (Methali 6:20) Hata hivyo, hupaswi kuwa na maoni ya kwamba sheria unazowekewa na wazazi wako zinakunyima uhuru. Badala yake, ukitii mamlaka ya wazazi wako, Yehova anaahidi kwamba mwishowe ‘mambo yatakuendea vema’!—Waefeso 6:1-3.

PATA HABARI ZAIDI KATIKA BUKU LA 1, SURA YA 3

KATIKA SURA INAYOFUATA

Je, mzazi hutumia dawa za kulevya au kunywa pombe kupita kiasi? Sura inayofuata itakusaidia kuona jinsi unavyoweza kukabiliana na hali hiyo.

MAANDIKO MUHIMU

Mheshimu baba yako na mama yako . . . ili mambo yakuendee vema.Waefeso 6:2, 3.

PENDEKEZO

Ikiwa unataka wazazi wako wakupe uhuru zaidi, kwanza, uwe mtiifu. Wanapoona kwamba wewe ni mtiifu sikuzote, bila shaka wanaweza kukupa uhuru zaidi.

JE, WAJUA . . .?

Utafiti unaonyesha kwamba vijana ambao wazazi wao wanawatia nidhamu kwa upendo, hufanya vizuri shuleni, huwa na uhusiano mzuri na wengine, na huwa na furaha.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nikivunja sheria ya familia yetu, nitasema ․․․․․

Ninaweza kuwafanya wazazi wangu waniamini kwa ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

Kwa nini huenda nyakati nyingine ikaonekana kana kwamba wazazi wako wanakuwekea sheria nyingi mno?

Kwa nini nyakati nyingine unachukizwa na sheria unazowekewa?

Unaweza kuboresha jinsi gani mawasiliano kati yako na wazazi wako?

[Blabu katika ukurasa wa 183]

“Wakati ungali mdogo, ni rahisi kufikiri kwamba unajua kila kitu. Hivyo, wazazi wako wanapokuwekea sheria, huenda ukakasirika. Hata hivyo, sheria zao zina faida.’’—Megan

[Sanduku katika ukurasa wa 186]

Ni Upendeleo Kweli?

Umewahi kujiuliza, ‘Kwa nini wazazi hawawatendei watoto wote kwa usawa?’ Ikiwa umewahi kujiuliza hivyo, kumbuka kwamba kuna tofauti kati ya kutendewa kwa usawa na kutendewa kwa haki. Huenda nyakati nyingine isifae kwa wazazi kuwatendea watoto wao wote kwa usawa. Jambo kuu ni, Je, mahitaji yako yanapuuzwa? Kwa mfano, unapohitaji ushauri, msaada, au utegemezo wa wazazi wako, je, wanakusaidia? Ikiwa wanafanya hivyo, je, kweli unaweza kusema kwamba unapuuzwa? Kwa kuwa wewe na ndugu na dada zako ni watu tofauti wenye mahitaji tofauti, haiwezekani sikuzote wazazi wenu wawatendee ninyi nyote kwa usawa. Beth alipata kujua hilo. Sasa, akiwa na umri wa miaka 18, anasema: “Mimi na ndugu yangu ni watu wawili tofauti nasi tuna mahitaji tofauti. Ninapokumbuka yaliyopita, siamini kwamba nilipokuwa mdogo sikuona mambo kwa njia hiyo.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 189]

Ukurasa wa Mazoezi

Zungumza na Wazazi Wako!

Sura mbili zilizotangulia zimezungumzia jinsi unavyoweza kufanya unapolaumiwa na wazazi au unapowekewa sheria. Hata hivyo, utafanya nini ukihisi kwamba wazazi wako wamepita kiasi katika mambo hayo? Unaweza kuanzisha mazungumzo nao jinsi gani?

Chagua wakati ambapo utakuwa umetulia na wazazi wako hawana shughuli nyingi.

Zungumza nao kutoka moyoni, lakini usiropoke tu kwa sababu ya hisia. Wape wazazi wako heshima wanayostahili.

Ikiwa unahisi kwamba wazazi wako wanakulaumu kupita kiasi, unaweza kuwaambia: “Ninajitahidi kufanya yaliyo sawa, lakini si rahisi ikiwa kila wakati ninalaumiwa. Ningependa tuongee kuhusu jambo hilo.”

Andika hapa chini jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu jambo hilo.

․․․․․

PENDEKEZO: Tumia Sura ya  21 ili kuanzisha mazungumzo. Huenda wazazi wako watapenda kuzungumza nawe mambo yaliyo katika sura hiyo.

Ikiwa unahisi kwamba wazazi wako hawakupi uhuru wa kutosha, unaweza kuwaambia: “Ni jambo gani ninalopaswa kufanyia kazi ili wakati ujao niwe mwenye kutegemeka zaidi na kustahili kupata uhuru zaidi?”

Andika hapa chini jinsi unavyoweza kuanzisha mazungumzo na wazazi wako kuhusu jambo hilo.

․․․․․

PENDEKEZO: Chunguza Sura ya 3 katika Buku la  1 yenye kichwa “Niwafanyeje Wazazi Wangu Wanipe Uhuru Zaidi?” Kisha andika maswali yoyote ambayo huenda ukawa nayo baada ya kusoma sura hiyo.

[Picha katika ukurasa wa 184, 185]

Kutii sheria za wazazi wako ni kama kulipa mkopo wa benki, kadiri unavyolipa kwa wakati ndivyo unavyoaminika zaidi