Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Siridhiki?

Kwa Nini Siridhiki?

SURA YA 27

Kwa Nini Siridhiki?

Wewe hukasirika usipopita mtihani kwa alama za juu zaidi?

□ Ndiyo

□ Hapana

Wewe hujiona kuwa bure kabisa ukikosolewa hata kidogo tu?

□ Ndiyo

□ Hapana

Wewe huona ni vigumu kupata au kudumisha marafiki kwa sababu hakuna anayefikia kiwango chako?

□ Ndiyo

□ Hapana

IKIWA umejibu ndiyo katika swali moja au zaidi, huenda una tatizo la kutoridhika. ‘Kwani kuna ubaya gani kujaribu kufanya mambo yote kikamilifu?’ huenda ukauliza. Bila shaka, hakuna ubaya! Biblia humsifu mtu ambaye ni “stadi katika kazi yake.” (Methali 22:29) Hata hivyo, mtu asiyeridhika, hufanya mambo kupita kiasi.

Kwa mfano, Jason, mwenye umri wa miaka 19 anakiri hivi: “Mwaka wa mwisho nilipokuwa shuleni, nilihisi kana kwamba, ikiwa singeweza kupita mtihani kwa alama za juu zaidi, basi nilikuwa mwanafunzi mjinga. Pia, mimi hupiga piano, nami nilikuwa nikihisi kwamba lazima nipige piano kwa ustadi kama ule wa wapiga-piano katika maonyesho ya muziki.”

Kutoridhika kwaweza hata kuathiri ibada ya mtu. Fikiria kinachoweza kumpata kijana ambaye sikuzote huonwa kuwa mfano mzuri kwa wengine. Kwa kuwa sikuzote anasifiwa, huenda akaanza kuhisi ni kana kwamba anatembea juu ya kamba, kila mtu akichunguza kila kitu anachofanya. Bila shaka, Wakristo, vijana kwa wazee, hufaidika kutokana na mifano mizuri kutanikoni. Hata hivyo, kujaribu kuishi maisha yasiyo na dosari kwaweza kumfanya kijana asiwe na shangwe katika utumishi wa Mungu. Inapofikia hatua hiyo, kijana huyo anahitaji msaada. Lakini huenda asiombe msaada, akihofia kwamba atawavunja moyo wale wanaomwona kuwa ‘mkamilifu.’ Huenda hata akakata tamaa, akifikiri, ‘Ikiwa siwezi kudumisha kiwango changu kikamilifu, kuna haja gani kujisumbua?’

Kupambana na Kutoridhika

Watu wasioridhika huamini kwamba mtu hapaswi kukosea hata kidogo. Lakini, kwa kweli, maoni hayo yana kasoro. Biblia inasema hivi waziwazi: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” (Waroma 3:23) Kwa hiyo, hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kutenda mambo kikamilifu kabisa. Kuamini kwamba unaweza kutenda mambo kikamilifu ni sawa na kuamini kwamba unaweza kuruka kama ndege. Hata uamini hivyo kadiri gani, ni jambo lisilowezekana!

Unaweza kufanya nini ili kuepuka kuwa mtu asiyeridhika na chochote? Jaribu mambo yafuatayo:

Badili maoni yako kuhusu “mafanikio.” Je, unajichosha kwa kujaribu kuwa bora kuliko wengine wote? Biblia inaonyesha kwamba kufanya hivyo kwaweza kuwa kama “kuwinda upepo.” (Mhubiri 4:4, Verbum Bible) Ukweli ni kwamba, ni watu wachache sana wanaofikia kiwango cha kuwa “bora kuliko wote.” Na hata mtu anapofikia kiwango hicho, kwa kawaida muda si muda mwingine hutokea na kuvunja rekodi yake. Mafanikio ni kufanya yote uwezayo—wala si kumshinda mtu mwingine.—Wagalatia 6:4.

Ona mambo kihalisi. Unapaswa kuwa na matazamio yanayolingana na uwezo na mipaka yako. Kujiwekea mradi ulio juu sana ni kukosa kiasi, au hata ni kiburi. Mtume Paulo anatoa shauri zuri: “Namwambia kila mtu hapo kati yenu asijifikirie mwenyewe zaidi kuliko ilivyo lazima kufikiri.” (Waroma 12:3) Kwa hiyo, ona mambo kihalisi. Changanua matarajio yako. Jitahidi kufanya yote uwezayo bali si kuwa mkamilifu.

Legeza kamba! Jaribu kufanya mambo ambayo hujui kufanya, kama vile kupiga chombo fulani cha muziki. Ni kweli kwamba utakosea mara nyingi. Hata hivyo, wakati huu, jitahidi kuyaona makosa yako kwa njia tofauti. Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kucheka.” (Mhubiri 3:4) Kwa hiyo, kwa nini usijifunze kutochukua mambo kwa uzito sana? Kufanya hivyo kutakusaidia kuona kwamba kupotea njia ndiyo kujua njia. Ni kweli kwamba haitakuwa rahisi kwako kuridhika na kazi isiyofikia kiwango unachotaka. Lakini jitahidi kuondoa akilini mwako mawazo yasiyofaa, ya kuchambua-chambua.

Sikuzote kumbuka kwamba Yehova hadai ukamilifu; anataka tu tumtumikie kwa uaminifu. (1 Wakorintho 4:2) Ikiwa unajitahidi kuwa mwaminifu, unaweza kuwa na furaha ya kweli—hata ikiwa hufanyi mambo kikamilifu.

KATIKA SURA INAYOFUATA

Watu wengi leo wanaona ngono kati ya watu wa jinsia moja kuwa jambo linalokubalika. Unaweza kuepuka zoea hilo namna gani? Utafanya nini ukivutiwa na mtu wa jinsia yako?

MAANDIKO MUHIMU

Hakuna mwanadamu aliye mwadilifu duniani ambaye huendelea kufanya mema na asifanye dhambi.Mhubiri 7:20.

PENDEKEZO

Fikiria jambo fulani ambalo umekuwa ukiahirisha-ahirisha kulifanya, kwa sababu tu hutaki kukosea. Kisha weka tarehe ya kumaliza kulifanya.

JE, WAJUA . . .?

Yehova ni mkamilifu, lakini anaposhughulika na wanadamu ambao si wakamilifu, hatazamii ukamilifu kutoka kwao. Anajua na kuzingatia uwezo na mipaka yetu.

HATUA ZA KUCHUKUA!

Nikianza kujiona kwamba sifai, nita ․․․․․

Nikianza kuwa mwenye kudai mengi mno kutoka kwa wengine nita ․․․․․

Mambo ambayo ningependa kuuliza mzazi (wazazi) wangu kuhusu habari hii ni ․․․․․

UNA MAONI GANI?

● Ni katika mambo gani maishani wewe hujiwekea miradi isiyoweza kufikika?

● Ni maandiko gani yanayokusaidia kuona waziwazi kwamba Yehova hatazamii watumishi wake wafanye mambo yanayopita uwezo wao?

● Kwa nini huenda wengine wakajitenga nawe ikiwa unadai mengi mno kutoka kwao?

● Wakati ujao utafanya nini ukikosea?

[Blabu katika ukurasa wa 226]

‘‘Kufanya yote uwezayo na kufanya mambo kikamilifu ni mambo mawili tofauti; la kwanza linaonyesha usawaziko na la pili ukosefu wa usawaziko.’’—Megan

[Sanduku katika ukurasa wa 228]

Kutazamia mengi mno kunaweza kuharibu urafiki

Je, umewahi kuwaepuka watu kwa sababu hawafai machoni pako? Au, je, watu wazuri wamewahi kukuepuka kwa sababu viwango vyako vya urafiki ni vya juu mno visiweze kufikiwa? Biblia inashauri hivi: “Usiwe mwadilifu kupita kiasi, wala kujionyesha kuwa na hekima kupita kiasi. Kwa nini ujiletee ukiwa?” (Mhubiri 7:16) Njia moja ambayo mtu hujiletea ukiwa ni kwa kutoa visingizio mbalimbali ili kuwaepuka watu ambao wangependa kuwa rafiki zake. “Hakuna mtu anayependa kuwa rafiki ya watu wanaomfanya aone hafai,” anasema msichana mmoja anayeitwa Amber, “nami nimeona watu ambao hudai mengi kutoka kwa rafiki zao wakipoteza marafiki wazuri kwa sababu ya mambo madogo sana.”

[Picha katika ukurasa wa 229]

Kujaribu kuwa mkamilifu ni kazi bure kama vile kujaribu kuruka kama ndege