Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JINSI YA KUFURAHIA KAZI NGUMU

Jinsi ya Kufurahia Kazi Ngumu

Jinsi ya Kufurahia Kazi Ngumu

“Kila mtu ale, naam, anywe na kuona mema kwa ajili ya kazi yake yote iliyo ngumu. Hiyo ndiyo zawadi ya Mungu.” (Mhubiri 3:13) Kwa sababu Mungu anataka tufurahie kazi, anatueleza jinsi ya kufanya hivyo. (Isaya 48:17) Inapendeza kwamba Mungu hutueleza kupitia Neno lake, Biblia. Chunguza kanuni zifuatazo zinazotegemea Biblia ili ufurahie kazi yako.

SITAWISHA MTAZAMO MZURI KUHUSU KAZI

Iwe kazi yako inahitaji utumie akili nyingi, au inahitaji utumie nguvu nyingi, au yote mawili, unapaswa kutambua kwamba “kwa kila kazi ngumu hutokea faida.” (Methali 14:23) Faida gani hiyo? Kwanza, kazi hutusaidia kupata mahitaji yetu ya lazima. Ni kweli kwamba Mungu anaahidi kuwaandalia mahitaji wale wanaomwabudu. (Mathayo 6:31, 32) Hata hivyo, anataka tutimize sehemu yetu kwa kufanya kazi kwa bidii na kupata pato la haki.—2 Wathesalonike 3:10.

Kwa hiyo, tunapaswa kuona kazi kuwa njia ya kutimiza malengo yetu. Kufanya kazi ni njia bora ya kutimiza majukumu yetu. Joshua, mwenye umri wa miaka 25 anasema hivi: “Kujitafutia riziki ni jambo jema. Ikiwa unaweza kujilipia gharama zako, basi kazi yako inatimiza kusudi muhimu.”

Zaidi ya hayo, kazi ngumu inakufanya ujiheshimu. Hata hivyo, hakuna kazi rahisi! Lakini tunapokuwa na nidhamu ya kufanya kazi—hata kama inaonekana yenye kuchosha au ngumu—tunaweza kuridhika kwa kujua kwamba tumefaulu kufanya kazi kwa bidii. Tutakuwa tumeshinda tamaa ya kutaka kufanya kazi rahisi tu. (Methali 26:14) Hivyo, tutaridhika sana! Aaron, aliyetajwa kwenye makala ya kwanza anasema hivi: “Baada ya kufanya kazi ngumu kutwa nzima, mimi huhisi nimeridhika. Hata kama nimechoka, au hata ikiwa kazi yangu haitambuliwi sana na wengine, ninajua kwamba nimetimiza jambo muhimu.”

FANYA KAZI KWA BIDII

Biblia inamsifu mwanamume aliye “stadi katika kazi yake” na mwanamke ambaye “hufanya kazi yoyote inayopendeza mikono yake.” (Methali 22:29; 31:13) Kwa kweli kuwa stadi katika kazi kunahitaji jitihada. Kwa kawaida watu hupenda kufanya kazi wanazozijua vizuri. Huenda wakashindwa kufurahia kazi zao kwa sababu hawajitahidi kuboresha ustadi wao katika kazi.

Kwa kweli, mtu akiwa na mtazamo mzuri kuhusu kazi, na akaazimia kufanya kazi vizuri atafurahia kufanya kazi yoyote ile. William, mwenye umri wa miaka 24 anasema hivi: “Unapotia bidii kazini na kuona matunda ya kazi yako, unaridhika sana. Huwezi kuridhika ikiwa utatumia njia za mkato au kufanya kazi kivivu.”

FIKIRIA JINSI KAZI YAKO INAVYOWANUFAISHA WENGINE

Epuka mtego wa kufikiria tu pesa unazopata kutokana na kazi yako. Badala yake jiulize maswali haya: ‘Kazi yangu ina umuhimu gani? Itakuwaje ikiwa sitafanya kazi au ikiwa sitaifanya vizuri? Kazi yangu inawanufaishaje wengine?’

Swali la mwisho ni muhimu kwa sababu kazi huridhisha zaidi inapowanufaisha wengine. Yesu mwenyewe alisema hivi: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.” (Matendo 20:35) Mbali na wale wanaonufaika moja kwa moja na kazi yetu, kama vile wateja au waajiri, kuna wengine wanaonufaika kutokana na kazi yetu ya jasho. Wanatia ndani watu wa familia yetu na vilevile wenye uhitaji au maskini.

Familia yako. Kichwa cha familia anapofanya kazi kwa bidii ili kuandaa mahitaji, familia yake hufaidika kwa angalau njia mbili. Kwanza, anahakikisha wanapata mahitaji ya lazima, yaani, chakula, mavazi, na malazi. Kwa kufanya hivyo anakuwa ametimiza jukumu alilopewa na Mungu la kuwaandalia “mahitaji wale walio wake mwenyewe.” (1 Timotheo 5:8) Pili, mfano wake wa kufanya kazi kwa bidii unawafundisha umuhimu wa kuwa wachapa-kazi. Shane, aliyetajwa kwenye makala iliyopita anasema hivi kumhusu baba yake: “Baba yangu ni mfano bora wa mtu anayefanya kazi kwa bidii. Yeye ni mnyoofu na amefanya kazi kwa bidii maisha yake yote, muda mrefu akiwa seremala. Nimejifunza kutoka kwake thamani ya kufanya kazi kwa bidii ili kuwanufaisha wengine.”

Wenye uhitaji. Mtume Paulo aliwashauri Wakristo wafanye “kazi ya bidii . . . ili [wawe] na kitu cha kumgawia mtu aliye na uhitaji.” (Waefeso 4:28) Kwa kweli, tunapofanya kazi kwa bidii na kuruzuku familia zetu, tunaweza pia kuwasaidia wale wenye uhitaji. (Methali 3:27) Kwa hiyo, kufanya kazi kwa bidii kunatuwezesha kupata furaha inayotokana na kuwasaidia wengine.

FANYA MENGI ZAIDI

Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema: “Mtu fulani aliye na mamlaka akikulazimisha uingie katika utumishi wa kilometa moja, nenda pamoja naye kilometa mbili.” (Mathayo 5:41) Unawezaje kutumia andiko hilo katika kazi yako? Badala ya kufanya kazi kidogo, jitahidi kufanya zaidi. Jiwekee malengo au miradi unayotaka kutimiza; jitahidi kufanya kazi vizuri na kwa haraka. Furahia yote unayotimiza katika kazi yako.

Unapofanya mengi zaidi, inaelekea utafurahia kazi yako. Kwa nini? Kwa sababu unafanya hivyo kwa hiari. Unafanya kazi zaidi kwa sababu unapenda, na si kwa sababu umelazimishwa. (Filemoni 14) Jambo hilo linatukumbusha kanuni inayopatikana kwenye andiko la Methali 12:24: “Mkono wa wenye bidii ndio utakaotawala, lakini mkono mlegevu utakuja kufanya kazi ya kulazimishwa.” Ni kweli kwamba wengi wetu hatuko chini ya utumwa au hata hatulazimishwi kufanya kazi. Hata hivyo, mtu anayetaka kufanya mambo machache tu huenda akajiona kama mtumwa wengine wanapotaka afanye mengi zaidi. Lakini mtu anayetimiza mengi zaidi kwa sababu amechagua kufanya hivyo, huridhika na maisha yake kwa kuwa anafanya mambo yote kwa hiari.

UWE NA USAWAZIKO KUHUSU KUFANYA KAZI

Ni vizuri kufanya kazi kwa bidii, hata hivyo tunapaswa kukumbuka kwamba kuna mambo mengine muhimu maishani. Biblia inatutia moyo tuwe na bidii. (Methali 13:4) Lakini haituhimizi tufanye kazi kupita kiasi. Andiko la Mhubiri 4:6 linasema hivi: “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.” Andiko hilo linatufundisha nini? Mtu anayefanya kazi kupita kiasi huenda asifurahie matunda ya kazi yake, hasa ikiwa kazi hiyo inachukua nguvu na muda wake wote. Kwa hiyo kazi yake inakosa kusudi kama tu “kufuatilia upepo.”

Biblia inaweza kutusaidia tuwe na maoni yanayofaa kuhusu kazi zetu. Ingawa inasema kwamba tunapaswa kufanya kazi kwa bidii, inatushauri pia ‘tuhakikishe mambo yaliyo ya maana zaidi.’ (Wafilipi 1:10) Ni mambo gani hayo yaliyo ya maana zaidi? Yanatia ndani kutumia wakati pamoja na familia na marafiki. Hata hivyo, mambo ya kiroho kama vile kusoma Biblia na kutafakari, ndiyo mambo muhimu zaidi maishani.

Inaelekea kwamba watu wenye usawaziko katika maisha yao watafurahia kazi zao. William, aliyetajwa mapema anasema hivi: “Mwajiri wangu wa zamani ni miongoni mwa watu wenye maadili mazuri ya kufanya kazi. Anafanya kazi kwa bidii, na ana uhusiano mzuri na wateja wake kwa sababu ya kazi zake nzuri. Muda wa kazi unapoisha, anaacha kazi ili awe pamoja na familia yake na apate muda kwa ajili ya mambo ya kiroho. Na kwa maoni yangu, yeye ni mtu mwenye furaha kwelikweli.”