Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 IGENI IMANI YAO | NOA

Alilindwa Akiwa “Salama Pamoja na Wengine Saba”

Alilindwa Akiwa “Salama Pamoja na Wengine Saba”

NOA na familia yake walijikusanya pamoja mvua ilipoanza kunyesha kwa nguvu. Hebu wazia nyuso zao zikimulikwa na mwangaza wa taa ya mafuta, wakiwa wamekodoa macho huku wakisikia sauti ya mvua ikipiga paa na kuta za safina. Bila shaka, kelele za mvua hiyo ziliogopesha.

Noa alipotazama nyuso za watu wa familia yake—mkewe mwaminifu na wanawe watatu pamoja na wake zao—bila shaka moyo wake ulijaa shukrani. Katika kipindi hicho kigumu alifarijika kuwa pamoja na watu aliowapenda zaidi. Walikuwa salama salimini. Bila shaka, alianza kusali kwa sauti ili wote wamsikie akitoa shukrani.

Noa alikuwa na imani thabiti. Yehova Mungu alimlinda yeye na familia yake kwa sababu alikuwa na imani. (Waebrania 11:7) Je, waliacha kuwa na imani mvua ilipoanza kunyesha? Hapana, wangehitaji imani zaidi ili kukabiliana na hali ngumu iliyokuwa mbele yao. Sisi pia tunakabili hali kama hiyo. Acheni tuchunguze yale tunayoweza kujifunza kutokana na imani ya Noa.

“SIKU 40 MCHANA NA USIKU”

Nje ya safina, mvua kubwa iliendelea kunyesha kwa “siku 40 mchana na usiku.” (Mwanzo 7:4, 11, 12) Maji yaliendelea kujaa na kufurika. Wakati huo, Noa aliona kwamba Mungu wake, Yehova, alikuwa akilinda waadilifu na wakati huohuo kuwaadhibu waovu.

Gharika hiyo ilikomesha uovu uliokuwa umetokea miongoni mwa malaika. Wakishawishiwa na Shetani, malaika wengi waliacha “makao yao wenyewe yanayofaa” huko mbinguni, wakaja duniani kufanya ngono na wanawake na kuzaa majitu yaliyoitwa Wanefili. (Yuda 6; Mwanzo 6:4) Bila shaka, Shetani alifurahi sana malaika walipozidi kuasi, kwa sababu waliwapotosha viumbe bora zaidi wa Yehova duniani, yaani, wanadamu.

Hata hivyo, gharika ilipozidi kuongezeka, malaika waasi walilazimika kuvua miili yao ya kibinadamu na kurudi kwenye makao ya kiroho, na hawangeweza tena kuvaa miili ya kibinadamu. Waliacha wake na watoto wao ambao waliangamizwa na gharika, pamoja na wanadamu waovu.

Tangu siku za Enoko, karibu miaka mia saba mapema, Yehova alikuwa amewaonya wanadamu kwamba angeangamiza waovu. (Mwanzo 5:24; Yuda 14, 15) Tangu wakati huo, watu walizidi kuwa wabaya, wakaiharibu dunia na kuijaza jeuri. Sasa Yehova alikuwa akiwaangamiza. Je, Noa na familia yake walifurahi kuona watu wakiangamia?

Hapana! Vilevile Mungu mwenye rehema hakufurahi. (Ezekieli 33:11) Yehova alikuwa amejitahidi kuwaokoa wanadamu wengi iwezekanavyo. Alikuwa amemwagiza Enoko awaonye watu, na baadaye akamwambia Noa ajenge safina. Noa na familia yake waliijenga safina hiyo kubwa kwa miaka mingi, mbele ya macho ya watu hao waovu. Kwa kuongezea, Yehova alimwagiza Noa awe “mhubiri wa uadilifu.” (2 Petro 2:5) Kama Enoko aliyeishi kabla yake, Noa aliwaonya watu kuhusu hukumu iliyokuwa ikija juu ya dunia. Watu hao waliitikiaje? Baadaye, Yesu ambaye alishuhudia  matukio hayo akiwa mbinguni alisema hivi kuhusu watu wa siku za Noa: “Hawakujali mpaka gharika ikaja na kuwafagilia mbali wote.”Mathayo 24:39.

Wazia jinsi Noa na familia yake walivyohisi katika kipindi cha siku 40 baada ya Yehova kufunga mlango wa safina. Mvua kubwa ilipozidi kunyesha siku baada ya siku, watu hao wanane bila shaka waliendelea na shughuli za kila siku na pia kuwatunza wanyama ndani ya safina. Hata hivyo, pindi moja jengo hilo kubwa likatikisika na kuanza kusonga. Sasa safina ilikuwa ikielea! Ikiwa juu ya maji yaliyozidi kuongezeka, safina iliinuliwa juu zaidi na zaidi, hadi “ikawa inaelea juu ya dunia.” (Mwanzo 7:17) Huo ulikuwa uthibitisho mkubwa sana wa nguvu za Mungu Mweza-Yote, Yehova!

Bila shaka, Noa alifurahi—si kwa sababu tu alikuwa salama pamoja na familia yake bali pia kwa sababu Yehova alikuwa amewatumia kuonya watu waovu walioangamizwa na gharika. Kwa miaka mingi kazi yao ya kuhubiri ilionekana kuwa ya bure. Watu hawakusikiliza! Fikiria jambo hili—yaelekea Noa alikuwa na ndugu, dada, na watu wengine wa ukoo kabla ya Gharika; hata hivyo, hakuna yeyote aliyesikiliza isipokuwa familia yake ya karibu. (Mwanzo 5:30) Sasa, watu hao wanane wakiwa salama ndani ya safina, walifarijika walipokumbuka jinsi walivyojitahidi kuwasaidia watu waokolewe.

Tangu siku za Noa, Yehova hajabadilika. (Malaki 3:6) Yesu Kristo alisema kwamba siku zetu zinalingana na “siku za Noa.” (Mathayo 24:37) Tunaishi katika nyakati zenye msukosuko zitakazofikia mwisho ulimwengu huu mwovu utakapoharibiwa. Leo, watu wa Mungu wanahubiri ujumbe wenye kuonya kwa wote ambao wako tayari kusikiliza. Je, utasikiliza ujumbe huo? Ikiwa tayari umesikia ujumbe huo wenye kuokoa uhai, je, utashiriki kuwaambia wengine? Noa na familia yake walituwekea mfano bora.

“WALICHUKULIWA SALAMA KUPITIA MAJI”

Safina ilipoendelea kuelea juu ya maji hayo mengi, bila shaka watu waliokuwa ndani walisikia  milio ya mbao kubwa zilizotumiwa kujenga safina. Je, Noa aliogopeshwa na ukubwa wa mawimbi au kuogopa kwamba safina ingevunjika? La hasha. Leo, huenda watu wasio na imani wakawa na shaka, lakini Noa hakuwa hivyo. Biblia inasema: ‘Kwa imani Noa alijenga safina.’ (Waebrania 11:7) Imani katika nini? Yehova alikuwa amefanya agano, mapatano maalumu, ya kumlinda Noa na familia yake wasiangamizwe na Gharika. (Mwanzo 6:18, 19) Unafikiri Yule aliyeumba ulimwengu mzima, dunia, na viumbe hai angeshindwa kuhakikisha kwamba safina haivunjiki? Hangeshindwa kamwe! Hivyo, Noa alikuwa na uhakika kwamba Yehova angetimiza ahadi Yake. Na ndivyo ilivyotukia, yeye na familia yake “walichukuliwa salama kupitia maji.”1 Petro 3:20.

Baada ya siku 40 mchana na usiku kupita, hatimaye mvua iliacha kunyesha. Kulingana na kalenda ya kisasa, ilikuwa Desemba mwaka wa 2370 K.W.K. Lakini bado familia hiyo ingeendelea kuishi ndani ya safina. Safina iliyokuwa imejaa viumbe iliendelea kuelea juu ya bahari iliyokuwa imefunika dunia nzima kutia ndani milima yote. (Mwanzo 7:19, 20) Fikiria kazi ngumu ambayo Noa na wanawe, Shemu, Hamu na Yafethi walifanya ili kuwalisha na kuwatunza wanyama wote. Bila shaka, Mungu ambaye alifanya wanyama hao wawe watulivu na kuingia ndani ya safina alihakikisha kwamba waliendelea kuwa watulivu kipindi chote cha Gharika. *

Bila shaka, Noa aliandika kwa usahihi rekodi ya matukio. Rekodi hiyo inatuambia wakati ambapo mvua ilianza na kwisha. Pia, inafunua kwamba maji yaliifunika dunia kwa siku 150. Mwishowe maji yakaanza kupungua. Siku moja, safina ilitua kwenye “milima ya Ararati” ambayo kwa sasa iko nchini Uturuki. Huenda hilo lilitukia Aprili mwaka wa 2369 K.W.K. Siku 73 baadaye, katika mwezi wa Juni, vilele vya milima hiyo vilianza kuonekana. Miezi mitatu baadaye, katika Septemba, Noa aliamua kuondoa sehemu fulani ya paa la safina. Kazi hiyo haikuwa ya bure kwa sababu sasa safina ilijaa mwangaza na hewa safi. Kabla ya hapo, Noa alikuwa amejaribu kutambua kama hali ilikuwa salama. Alimtuma kunguru nje ya safina ambaye alienda na kurudi mara kadhaa, labda akitua juu ya safina; kisha Noa akamtuma njiwa, ambaye aliendelea kurudi mpaka alipopata mahali pa kujenga kiota.Mwanzo 7:24–8:13.

Bila shaka, Noa aliiongoza familia yake katika ibada hata chini ya hali ngumu

Bila shaka Noa alikazia fikira zaidi mambo ya kiroho. Tunaweza kuwazia Noa na familia yake wakikusanyika kwa ukawaida ili kuzungumza na kusali kwa Baba yao wa mbinguni. Noa alimtegemea Yehova kabla ya kufanya uamuzi wowote. Hata Noa alipoona maji ‘yamekauka’—baada ya kuishi ndani ya safina kwa mwaka mmoja—hakufungua mlango na kutoka nje ya safina. (Mwanzo 8:14) Alingojea agizo la Yehova!

Vichwa vya familia wanaweza kujifunza mengi kutoka kwa mwanamume huyo mwaminifu. Alikuwa mwenye utaratibu, bidii, subira, na aliilinda familia yake. Zaidi ya yote, alitanguliza makusudi ya Yehova Mungu. Tukiiga imani ya Noa kwa kufanya mambo hayo, tutabarikiwa pamoja na wale tunaowapenda.

“TOKA NJE YA SAFINA”

Hatimaye Yehova akatoa agizo. Akamwambia Noa: “Toka nje ya safina, wewe na mke wako na wana wako na wake za wana wako pamoja nawe.” Kwa utiifu, familia ya Noa ilitoka nje, na wanyama wote pia. Jinsi gani? Je walitoka kwa vurugu? La hasha! Simulizi hilo linasema “kulingana na familia zao walitoka nje ya safina.” (Mwanzo 8:15-19) Wakiwa nje, Noa na familia yake walivuta hewa safi kwenye milima ya Ararati, na wakaona dunia iliyosafishwa. Hakukuwa tena na Wanefili, ujeuri, malaika waasi, na watu wote waovu! * Sasa wanadamu walikuwa na fursa ya kuanza maisha mapya.

 Noa alijua alichopaswa kufanya. Alianza kuabudu. Alijenga madhabahu na kutumia baadhi ya wanyama ambao Mungu aliwaona kuwa safi—wale ambao waliingizwa ndani ya safina wakiwa “saba saba”—na akamtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa. (Mwanzo 7:2; 8:20) Je, ibada hiyo ilimpendeza Yehova?

Biblia inajibu hivi: “Yehova akaanza kunusa harufu ya kutuliza.” Uchungu aliohisi wanadamu walipoijaza dunia jeuri ulibadilika na kuwa hisia nzuri yenye kutuliza alipoona familia ya waabudu wake waaminifu duniani walioazimia kufanya mapenzi yake. Yehova hakutarajia wawe wakamilifu. Mstari huo unaendelea kusema: “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Mwanzo 8:21) Fikiria jinsi Yehova alivyoendelea kuwaonyesha wanadamu subira.

Yehova aliondoa laana iliyokuwa duniani. Tangu Adamu na Hawa walipoasi, Mungu alitangaza laana, kwa kufanya kazi ya ukulima iwe ngumu. Baba ya Noa, Lameki, alikuwa amempa mwanawe jina Noa, ambalo huenda linamaanisha “Pumziko,” au “Faraja,” na akatabiri kwamba mwanawe angewaletea wanadamu kipindi cha pumziko kutoka kwenye laana hiyo. Bila shaka, Noa alifurahi alipotambua kwamba angeona utimizo wa unabii huo na kwamba dunia ingetokeza mazao kwa wingi. Si ajabu kwamba muda si muda Noa alianza kulima!Mwanzo 3:17, 18; 5:28, 29; 9:20.

Noa na familia yake walitoka ndani ya safina na kupata dunia iliyosafishwa

Wakati huo huo, Yehova aliwapa wazao wa Noa sheria zisizo na mambo mengi za kuwaongoza maishani—kutia ndani kukataza kuua na matumizi yasiyofaa ya damu. Pia, Mungu aliweka agano na wanadamu, akiwaahidi kwamba hangeleta tena gharika ili kuangamiza uhai duniani. Alitoa uhakikisho wa ahadi yake kwa kuwapa wanadamu ishara ya pekee—upinde wa mvua. Hadi leo, kila tunapoona upinde wa mvua tunakumbuka ahadi ya Yehova yenye upendo.Mwanzo 9:1-17.

Ikiwa hadithi ya Noa ilikuwa ya uwongo, huenda leo hakungekuwa na upinde wa mvua. Lakini Noa alikuwa mtu halisi, na maisha yake hayakuwa rahisi. Siku hizo, watu waliishi muda mrefu sana, na hivyo Noa alihitaji kuvumilia miaka mingine 350, na miaka hiyo alikabili matatizo mengi. Alifanya kosa kubwa alipolewa pindi moja, na kosa hilo lilifanya mjukuu wake, Kanaani afanye dhambi nzito zaidi—ambayo ilileta matokeo mabaya kwa familia ya Kanaani. Noa aliendelea kuishi mpaka kipindi cha Nimrodi na akaona wazao wake wakifanya dhambi kama vile uzinzi na ujeuri. Kwa upande mwingine, Noa aliona mwanawe Shemu akiwekea familia yake mfano mzuri wa imani.Mwanzo 9:21-28; 10:8-11; 11:1-11.

Kama Noa, tunahitaji kuendelea kuwa waaminifu licha ya matatizo. Wengine wanapompuuza Mungu wa kweli au hata kuacha kumtumikia, tunahitaji kuwa washikamanifu kama Noa. Yehova huthamini sana uvumilivu kama huo. Kama Yesu Kristo alivyosema, “yule ambaye atavumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”Mathayo 24:13.

^ fu. 17 Baadhi ya watu wamedai kwamba Mungu aliwafanya wanyama wasile chakula, hivyo kupunguza uhitaji wao wa chakula. Iwe alifanya hivyo au la, bila shaka alitimiza ahadi yake ya kuwalinda wote waliokuwa ndani ya safina.

^ fu. 22 Pia, eneo lililokuwa na Bustani ya Edeni, lilikuwa limeharibiwa na gharika. Ikiwa ndivyo, makerubi waliokuwa wakilinda mwingilio wa bustani walirudi mbinguni, baada ya mgawo wao wa miaka 1600 kukamilika.Mwanzo 3:22-24.