Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukweli Kuhusu Dhambi

Ukweli Kuhusu Dhambi

Ukweli Kuhusu Dhambi

JE, MGONJWA anaweza kuthibitisha kwamba yeye si mgonjwa kwa kuvunja kipima-joto? Bila shaka, hapana! Ndivyo ilivyo na dhambi. Ijapokuwa watu wengi wanakataa maoni ya Mungu kuhusu dhambi, haimaanishi kwamba hakuna dhambi. Neno lake, Biblia, lina mengi ya kusema kuhusu habari hiyo. Linasema nini hasa kuhusu dhambi?

Sote Tumepungukiwa

Miaka elfu mbili hivi iliyopita, mtume Paulo alieleza jinsi alivyovunjika moyo kutokana na ukweli wa kwamba ‘lile jema analotaka halifanyi, bali lile baya asilotaka ndilo analozoea kulifanya.’ (Waroma 7:19) Ikiwa sisi ni wanyoofu, tunapaswa kukubali kwamba hali yetu ni sawa na ya Paulo. Huenda tungependa kuishi kulingana na zile Amri Kumi au labda kulingana na viwango vingine vya maadili, hata hivyo, tupende tusipende sote tumepungukiwa. Si kwamba tunapenda kuvunja sheria kimakusudi, ni kwamba tu sisi ni dhaifu. Hilo linamaanisha nini? Paulo anatoa jibu: “Basi, ikiwa lile nisilotaka ndilo ninalofanya, anayelifanya hilo si mimi tena, bali ni ile dhambi inayokaa ndani yangu.”—Waroma 7:20.

Kama Paulo, wanadamu wote wameathiriwa na udhaifu wa kiasili—jambo linalothibitisha kwamba wote wamerithi dhambi na kutokamilika. Mtume Paulo alisema: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” Hali hiyo inasababishwa na nini? Paulo aendelea: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 3:23; 5:12.

Watu wengi hawakubali kwamba dhambi ambayo wazazi wetu wa kwanza walifanya ilitutenganisha na Mungu na kufanya tupoteze ukamilifu. Hata hivyo, hilo ndilo jambo ambalo Biblia inafundisha. Kwa kunukuu sura za kwanza za kitabu cha Mwanzo, Yesu alionyesha kwamba anaamini masimulizi kuhusu Adamu na Hawa.—Mwanzo 1:27; 2:24; 5:2; Mathayo 19:1-5.

Mojawapo ya mafundisho ya msingi ya Biblia ni kwamba Yesu alikuja hapa duniani ili kuwakomboa wanadamu wanaomwamini kutoka katika dhambi. (Yohana 3:16) Matarajio yetu ya kuishi wakati ujao yanategemea kukubali njia ya Yehova ya kuwakomboa wanadamu wenye imani, kutoka katika hali yenye dhambi ambayo hawana uwezo wa kuibadili. Lakini ikiwa hatuna maoni kama ya Mungu kuhusu dhambi, hatuwezi kuelewa na kuthamini njia ambayo Mungu ameandaa ili kutukomboa.

Dhabihu ya Yesu na kwa Nini Ilihitajika

Yehova alimpa mtu wa kwanza tumaini la kuishi milele. Adamu angepoteza tumaini hilo zuri ikiwa angemwasi Mungu. Adamu aliasi, na kwa kufanya hivyo, akawa mtenda-dhambi. (Mwanzo 2:15-17; 3:6) Adamu alitenda kinyume cha mapenzi ya Mungu, akapoteza ukamilifu na kuharibu uhusiano wake pamoja na Mungu. Alipofanya dhambi kwa kuvunja sheria ya Mungu, Adamu alianza kuzeeka na hatimaye akafa. Inasikitisha kwamba, wazao wote wa Adamu—kutia ndani sisi—tumezaliwa katika dhambi, na hatimaye tunakufa kwa sababu ya dhambi hiyo. Kwa nini?

Jibu ni wazi. Wazazi ambao si wakamilifu, hawawezi kuzaa watoto wakamilifu. Watoto wote wa Adamu walizaliwa wakiwa na dhambi, na kama vile mtume Paulo anavyosema, “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Hata hivyo, sehemu ya pili ya mstari huo inatupa tumaini: “Lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” Hilo linamaanisha kwamba, kupitia dhabihu ya kifo cha Yesu, inawezekana kwa wanadamu watiifu na walio na imani kuondolewa madhara ya dhambi ya Adamu. * (Mathayo 20:28; 1 Petro 1:18, 19) Hilo linapaswa kufanya uhisi namna gani?

Upendo wa Kristo “Hutulazimisha”

Akiongozwa na roho ya Mungu, mtume Paulo alionyesha maoni ya Mungu kuhusu swali hilo. Aliandika: “Kwa maana upendo alio nao Kristo hutulazimisha, kwa sababu hili ndilo tumehukumu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote; . . . naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.” (2 Wakorintho 5:14, 15) Ikiwa mtu anaamini kwamba dhabihu ya Yesu inaweza kumweka huru kutokana na madhara ya dhambi—na anataka kuonyesha kwamba anathamini uandalizi huo—anapaswa kujitahidi kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Hilo linatia ndani kupata ujuzi juu ya yale ambayo Mungu anataka, kuzoeza dhamiri yake kulingana na viwango vya Biblia, na kuishi kulingana navyo.—Yohana 17:3, 17.

Dhambi huharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu. Bila shaka, Mfalme Daudi aliaibika sana alipotambua uzito wa kufanya uzinzi na Bath-sheba na kumuua mume wake. Lakini kile kilichomhangaisha hata zaidi—na kwa kweli hilo ndilo jambo linalofaa—ni kwamba dhambi yake ilikuwa imemchukiza Mungu. Kwa kujuta alikiri kwa Yehova hivi: “Dhidi yako wewe, wewe peke yako, nimetenda dhambi, nami nimefanya lililo baya machoni pako.” (Zaburi 51:4) Vivyo hivyo, Yosefu aliposhawishiwa kufanya uzinzi, dhamiri yake ilimfanya aulize hivi: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?”—Mwanzo 39:9.

Hivyo basi, dhambi si suala la kujisikia vibaya tu kwa sababu ya aibu. Si kuhisi tu kwamba tunawajibika kwa watu au jamii kwa sababu huenda tumetenda kosa fulani. Kuvunja sheria za Mungu kuhusu ngono, unyoofu, heshima, ibada, na kadhalika, huharibu uhusiano wetu pamoja naye. Tukifanya dhambi kimakusudi, tunajifanya kuwa adui za Mungu. Huo ni ukweli tunaopaswa kuzingatia.—1 Yohana 3:4, 8.

Kwa hiyo, je, maoni kuhusu dhambi yamebadilika? Ukweli ni kwamba hakuna chochote kilichobadilika. Ni kwamba tu watu walianza kuiita dhambi kwa majina mengine wakitumaini kwamba kufanya hivyo kutapunguza uzito wake. Wengi hupuuza dhamiri zao. Wote wanaotaka kupata kibali cha Mungu wanapaswa kupinga mwelekeo huo. Kama tulivyoona, mshahara ambao dhambi hulipa si, sifa mbaya au kuaibika tu, bali kifo. Dhambi ni suala la uhai au kifo.

Habari njema ni kwamba tunaweza kupata msamaha kupitia dhabihu yenye thamani ya Yesu tukitubu dhambi zetu kikweli na kuziacha. Paulo aliandika: “Wenye furaha ni wale ambao matendo yao ya kuasi sheria yamesamehewa na ambao dhambi zao zimefunikwa; mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hatahesabu dhambi yake kamwe.”—Waroma 4:7, 8.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Kwa maelezo kamili kuhusu jinsi kifo cha kidhabihu cha Yesu kilivyo na nguvu za kuwakomboa wanadamu watiifu, ona ukurasa wa 47 mpaka 54, wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]

Kanisa Labadili Fundisho Lake

Sikuzote fundisho kuhusu Limbo limewatatanisha Wakatoliki wengi wanaoenda kanisani. Katika miaka ya karibuni, fundisho hilo limekuwa likififia hatua kwa hatua hivi kwamba halipatikani tena katika katekisimu. Katika mwaka wa 2007, Kanisa Katoliki lilitupilia mbali fundisho hilo kwa kutia sahihi hati iliyotaja “sababu za kitheolojia na za kiliturujia za kuwa na tumaini kwamba watoto wachanga wanaokufa bila kubatizwa wanaweza kuokolewa na kupata furaha ya milele.”—International Theological Commission.

Kwa nini Kanisa limebadili fundisho lake? Ili lijinasue kutokana na kile ambacho kulingana na mwandishi Mfaransa Henri Tincq, ni “urithi wenye kulemea uliotetewa tangu Enzi za Kati mpaka karne ya 20, na Kanisa lenye hila linalofurahia kutumia tisho la fundisho kuhusu Limbo ili kuwashawishi wazazi wawabatize watoto wao haraka iwezekanavyo.” Hata hivyo, kuondolewa kwa fundisho hilo kunatokeza masuala mengine.

Je, Fundisho Hilo Linategemea Mapokeo au Maandiko? Kihistoria, fundisho kuhusu Limbo lilitokana na mijadala ya kitheolojia ya karne ya 12, iliyohusu toharani. Kanisa Katoliki lilifundisha kwamba baada ya mtu kufa, nafsi inaendelea kuishi. Kwa hiyo, wakalazimika kutafuta njia ya kueleza hatima ya nafsi za watoto ambao hawangeweza kwenda mbinguni kwa sababu hawakuwa wamebatizwa, lakini ambao hata hivyo, hawakustahili kwenda motoni. Hivyo, wakaanzisha fundisho kuhusu Limbo.

Lakini, Biblia haifundishi kwamba nafsi huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Badala yake, inaeleza waziwazi kwamba badala ya kuwa zisizoweza kufa, nafsi za wanadamu wanaofanya dhambi zinaweza “kuangamizwa” na “zitakufa.” (Matendo 3:23; Ezekieli 18:4, Douay-Rheims Version) Kwa kuwa nafsi inaweza kufa, basi haiwezekani kuwa na mahali kama Limbo. Isitoshe, Biblia inataja kifo kuwa hali ya kutokuwa na fahamu, sawa na kulala usingizi.—Mhubiri 9:5, 10; Yohana 11:11-14.

Biblia hufundisha kwamba Mungu huwaona watoto wachanga ambao wazazi wao ni Wakristo, kuwa watakatifu. (1 Wakorintho 7:14) Taarifa hiyo haingekuwa na maana yoyote ikiwa watoto wachanga wangehitaji kubatizwa ili wapate wokovu.

Kwa kweli, fundisho kuhusu Limbo linamvunjia Mungu heshima. Badala ya kufundisha kwamba Mungu ni Baba mwenye upendo na haki, fundisho hilo linamtaja kuwa mtu mkatili anayewatesa watu wasio na hatia. (Kumbukumbu la Torati 32:4; Mathayo 5:45; 1 Yohana 4:8) Hivyo basi, si ajabu kwamba fundisho hilo lisilo la Kimaandiko halijawahi kamwe kuwa na maana kwa Wakristo wanyoofu!

[Picha katika ukurasa wa 9]

Kuishi kulingana na Neno la Mungu hutusaidia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu na wanadamu