Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Kwa nini mwanamke aliyepoteza imani katika dini sasa anatumia wakati wake mwingi kuwasaidia wengine wajifunze kumhusu Mungu? Ni nini kilichomchochea mtu aliyependa michezo yenye jeuri kuwa mpenda-amani? Ni nini kilichomwezesha mwanamume aliyezoea kutumia dawa za kulevya, pombe, na kupigana mitaani kubadili mtindo wake wa maisha? Soma masimulizi ya watu hao.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: PENELOPE TOPLICESCU

UMRI: 40

NCHI: AUSTRALIA

HISTORIA: ALIKATISHWA TAMAA NA DINI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa huko Sydney, Australia, lakini nilipokuwa na umri wa miaka miwili tu familia yetu ilihamia New Guinea. Tuliishi kwa miaka karibu miwili huko Rabaul, kisha tukaishi kwa miaka minane huko Bougainville. Siku hizo, hakukuwa na televisheni nchini New Guinea, hivyo, mimi na ndugu yangu tulizoea kucheza nje tulipokuwa watoto—tuliogelea, tulipiga mbizi, na kupiga kambi.

Nilipokuwa na umri wa miaka kumi hivi, nilianza kupendezwa na dini. Mama alikuwa Mkatoliki, kwa hiyo alipendekeza kwamba nihudhurie masomo ya Biblia pamoja na mtawa fulani wa kike aliyeishi katika eneo letu. Nilikubali Ukatoliki na nikabatizwa nikiwa na umri wa miaka kumi.

Hata hivyo, baada ya kurudi Australia, wakati huo nikiwa tineja, nilianza kutilia shaka mafundisho ya dini yangu. Katika miaka yote niliyokuwa katika shule ya sekondari, nilijifunza historia ya zamani, na nilizungumza na baba yangu kwa muda mrefu kuhusu mwanzo wa dini na pia hadithi za Biblia ambazo tulidhani si za kweli. Mwishowe, nilikataa Ukatoliki.

Wazazi wangu walitengana nilipokuwa na umri wa miaka 16. Mama alikabili wakati mgumu sana, mwishowe mimi nilienda kuishi na baba yangu na mchumba wake. Ndugu yangu aliishi na Mama, na walihamia katika jimbo lingine. Wakati huo nilijihisi nikiwa mpweke sana. Nilikuwa tena na uhusiano mzuri pamoja na mama yangu baada ya miaka miwili. Nilianza kunywa pombe, kutumia dawa za kulevya, na kuhudhuria karamu. Niliacha shule, nikapata kazi, na niliharibu maisha yangu mapema nikiwa na umri wa miaka ya 20 na kitu kwa kuishi maisha mapotovu kiadili.

Nilipofikia umri wa miaka 25, nilianza kufikiria tena kuhusu Biblia. Nilipata kazi mpya na nikakutana na Liene, msichana mzuri ambaye nyakati zote alikuwa mpole kwa mkubwa wake kazini, hata ingawa mkubwa huyo alimtendea kwa ujeuri sana. Nilipomuuliza msichana huyo kwa nini hakumjibu mkubwa wake kwa ukali, alinieleza kwamba alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova na alikuwa akijaribu kufuata kanuni za Biblia katika maisha yake. Liene alijitolea kunifundisha Biblia. Kwa sababu sikumwelewa, nilifikiri alimaanisha kwamba ningeweza kujifunza mambo yote aliyojua kuhusu Biblia katika kipindi kimoja tu cha saa moja. Usiku huo, Liene alijibu maswali yangu ya Biblia kwa muda wa saa tatu. Nilivutiwa kuona kwamba majibu yote aliyotoa yaliungwa mkono na maandiko ya Biblia.

Ninakumbuka nilipokuwa nikirudi nyumbani kwa gari usiku huo baada ya kuzungumza na Liene, nilikasirika kwamba Mungu hakuniruhusu nijifunze ukweli kumhusu mapema zaidi. Nilijua kwamba Mashahidi waliishi maisha safi kiadili na nilifikiri kwamba singeweza kubadili mazoea yangu kwa sababu ilikuwa kuchelewa mno. Pia, nilifikiri kwamba singeweza kamwe kuhubiri nyumba kwa nyumba kama Mashahidi wanavyofanya. Niliendelea kujifunza Biblia na Mashahidi, lakini kusudi langu lilikuwa kupata makosa katika mafundisho yao ili niweze kuacha kushirikiana nao nikiwa na dhamiri njema. Siku moja nilitambua kwamba singeweza kupata kosa lolote.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Kadiri nilivyojifunza mengi kuhusu viwango vya maadili vya Biblia, ndivyo dhamiri yangu ilivyonisumbua. Ili kuituliza dhamiri yangu, niliacha kutumia dawa za kulevya. Lakini nilihamia nchi ya ng’ambo kwa muda halafu nikaanza tena kuhudhuria karamu nyingi na kunywa pombe. Ni kana kwamba kila mara nilipojaribu kufanya maendeleo ili niishi kupatana na kanuni za Biblia, niliteleza na kurudi nyuma. Kwa aibu, nilisali kwa Yehova lakini bado nilihisi vibaya.

Nilipojifunza kuhusu kisa cha Mfalme Daudi na Bath-sheba na jinsi Yehova alivyowatendea kwa rehema, nilitiwa moyo sana. Daudi alikuwa na ujasiri wa kutosha kukubali kosa lake aliposhauriwa, naye hakujaribu kutetea matendo yake. Na alikubali kwa unyenyekevu nidhamu aliyopewa. (2 Samweli 12:1-13) Kila mara nilipojikwaa, nilifikiria simulizi hilo na ilikuwa rahisi zaidi kumwomba Yehova msamaha. Halafu niliamua kusali kabla ya kutumbukia katika kishawishi badala ya kusali baada ya kutumbukia katika kishawishi, na hilo lilinisaidia sana.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kwa kawaida, nilikuwa mtu mwenye hasira kali. Hata hivyo, andiko la Waefeso 4:29-31 lilinisaidia kuona uhitaji wa kuepuka ‘uchungu na hasira na ghadhabu.’ Kadiri nilivyojifunza kuizuia hasira yangu, ndivyo nilivyojifunza kuuzuia ulimi wangu. Kwa kuongezea, shauri la Yesu la ‘kuacha neno lenu Ndiyo limaanishe Ndiyo,’ lilinisaidia kufanya maamuzi mazuri zaidi.—Mathayo 5:37.

Mama yangu, ambaye mwanzoni alinipinga ili nisishirikiane na Mashahidi, baadaye aliniambia alijivunia mimi kuwa binti yake. Hata alisema, “Ninajua kwamba utu ulio nao sasa ukiwa mwanamke mzima hautokani na malezi yako bali unatokana na yale ambayo umejifunza kumhusu Yehova.” Nilifurahi sana kumsikia akisema hivyo.

Sasa ninahisi kwamba maisha yangu yana kusudi na maana. Kwa miaka tisa ambayo imepita, mimi na mume wangu tumekuwa walimu wa Biblia wa wakati wote. Ndiyo, ninahubiri nyumba kwa nyumba, na sasa ninahisi kwamba hii ndiyo kazi yenye kuthawabisha zaidi ambayo nimewahi kufanya.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: DENIS BUSIGIN

UMRI: 30

NCHI: URUSI

HISTORIA: ALIPENDA SANA KARATE

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nilizaliwa katika mji wa Perm’ na kulelewa huko Furmanov, mji wenye watu karibu 40,000 katika jimbo la Ivanovo, Urusi. Furmanov ni mji wenye kuvutia sana wenye miti mingi maridadi ambayo inageuka na kuwa na rangi ya manjano na nyekundu katika majira ya majani kuanguka. Katika miaka ya 1980 na 1990, uhalifu uliongezeka sana katika mji huo. Familia yetu iliishi maisha rahisi sana kwa mshahara mdogo. Niliishi na wazazi wangu na ndugu yangu mdogo katika nyumba yenye chumba kimoja cha kulala, kwa hiyo tulisongamana.

Nilianza kujifunza mchezo wa karate nikiwa na umri wa miaka saba. Niliupenda sana mchezo huo; nilitumia maisha yangu yote katika mchezo huo. Nilitumia wakati wangu wote wa ziada katika chumba cha mazoezi, hivyo, marafiki wangu wote walikuwa wanamichezo. Nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilikuwa nimepata mkanda mwekundu katika karate, na mwaka mmoja baadaye, nikapata mkanda wa kahawia. Nilikuwa mshiriki wa timu ya karate ambayo ilishiriki katika mashindano ya Urusi, ya nchi za Ulaya na Asia. Nilikuwa na matumaini makubwa sana ya wakati ujao, lakini maisha yangu yalibadilika kabisa nilipokuwa na umri wa miaka 17.

Nikiwa pamoja na marafiki fulani tulifanya uhalifu na tukakamatwa. Nilihukumiwa kifungo cha miaka miwili gerezani. Maisha yalikuwa magumu sana gerezani. Hata hivyo, niliona Biblia kwa mara ya kwanza nilipokuwa gerezani. Nilisoma kitabu cha Mwanzo, Zaburi, na Agano Jipya. Hata niliweka akilini Sala ya Bwana na kila usiku niliirudia-rudia kabla ya kulala, huku nikifikiri kwamba kufanya hivyo kungenisaidia kwa njia fulani.

Niliachiliwa huru kutoka gerezani mwaka wa 2000, lakini maisha yangu hayakuwa na kusudi wala mwelekeo. Nilianza kutumia dawa za kulevya. Mama yangu ambaye alikuwa rafiki yangu mkubwa sana alikufa wakati huo, na haikuwa rahisi kuvumilia kifo chake. Hata hivyo, nilifaulu kuacha dawa za kulevya, na nikaanza tena kwenda kufanya mazoezi ya karate. Pia, nilihamia mji wa Ivanovo. Huko, nilipata kazi katika duka la mboga. Msimamizi-msaidizi wa duka hilo alikuwa Shahidi wa Yehova. Alinieleza kweli fulani za msingi kutoka katika Biblia naye akapanga ili Shahidi mwingine anifundishe Biblia kwa ukawaida.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipokuwa nikijifunza Biblia, niliguswa moyo sana nilipojifunza kusudi la Mungu la kuifanya dunia iwe paradiso, na nilitaka kutimiza matakwa ya Mungu ili niweze kuishi katika paradiso hiyo. Punde si punde, nilitambua kwamba Yehova Mungu ana viwango vya juu ambavyo anataka watu waishi kulingana navyo. Nilikuwa nimetumia miaka mingi ya maisha yangu nikijifikiria tu mwenyewe. Lakini nilijifunza kwamba Yehova alitaka niwafikirie wengine na kusitawisha sifa ambazo sikuwa nazo wakati huo, sifa kama vile fadhili na kupenda amani.

Nilipoanza kufikiria kwa uzito mambo yote ambayo Yehova alikuwa amenifanyia, kama vile kumtoa Mwana wake akiwa dhabihu kwa ajili ya dhambi zangu, nilichochewa kufanya mabadiliko katika maisha yangu ili kuonyesha kwamba nilithamini upendo wa Mungu. Kwa mfano, nilijifunza kutokana na Zaburi 11:5 kwamba Yehova anachukia jeuri. Kwa hiyo, niliacha kutazama vipindi vya televisheni vilivyotukuza jeuri na chuki. Niliacha kucheza michezo ya jeuri hata ingawa haikuwa rahisi kuiacha. Kanuni ya andiko la 1 Wakorintho 15:33 ilinisaidia kuona kwamba wale niliochagua kushirikiana nao wangekuwa na uvutano mkubwa sana juu yangu. Uhakika wa kwamba nilifungwa gerezani unathibitisha kwamba kanuni hiyo ni ya kweli. Kwa hiyo, niliamua kuacha kushirikiana na wale ambao walipenda sana michezo yenye jeuri.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kushirikiana na Mashahidi wa Yehova na kujifunza Biblia kumenisaidia kuwa mtu mnyoofu. Kwa mfano, nilijifunza kutokana na andiko la Waebrania 13:5 uhitaji wa kuridhika na kushinda tamaa ya kupenda pesa. Kutumia shauri hilo kumenisaidia kuacha kusema uwongo na kuiba.

Kwa kawaida, ninapenda kuwa na marafiki. Zamani, nilipoteza marafiki kwa sababu ya pupa au woga. Mashahidi wa Yehova si wakamilifu, lakini nimejifunza kwamba wanaheshimu viwango vya Mungu na wanajitahidi sana kufuata mashauri yake wanaposhughulika na wengine. Sasa nimepata marafiki wa kweli kati yao.

Sijui maisha yangu yangekuwa namna gani kama singejifunza kuishi kupatana na viwango vya Biblia. Labda ningekuwa tena gerezani au ningekuwa nikiwatesa na kuwaumiza watu. Hata hivyo, sasa nina mke mzuri na wana wawili, na tukiwa familia, tunapata furaha ya kweli tunapowasaidia wengine kujifunza kweli kumhusu Mungu.

MAELEZO MAFUPI KUMHUSU

JINA: JOSÉ CARLOS PEREIRA DA SILVA

UMRI: 31

NCHI: BRAZILI

HISTORIA: ALIPIGANA NA WATU MITAANI

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa katika mabanda machafu sana ya Americana, huko São Paulo. Eneo letu lilijaa takataka na maji machafu na hatukuwa na maji safi ya kunywa. Eneo hilo lilijulikana kwa sababu ya jeuri na uhalifu mwingi.

Nilikuwa kijana mjeuri na mkatili. Kwa kawaida nilipigana na watu mitaani, hivyo, watu katika eneo letu waliniogopa. Sura na mavazi yangu yalionyesha kwamba nilikuwa mtu hatari sana. Nilikuwa mlevi kupindukia, na mara nyingi nilikunywa mpaka nilipozimia. Nilitumia dawa za kulevya kama ndugu zangu. Kwa kweli, ndugu yangu mmoja alikufa baada ya kutumia dawa za kulevya kupita kiasi.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Nilipokutana na Mashahidi wa Yehova, walinionyesha kupitia Biblia kwamba Mungu ataifanya dunia yote iwe paradiso. (Luka 23:42, 43; Ufunuo 21:3, 4) Nilijifunza pia kwamba wafu hawajui lolote, kwa hiyo Mungu hawaadhibu watu wabaya katika moto wa milele. (Mhubiri 9:5, 6) Nilifurahi sana kusikia hivyo. Mambo niliyojifunza kumhusu Mungu yalinifanya nitamani sana kubadili mtindo wangu wa maisha. Lakini haikuwa rahisi kubadilika na kuacha dawa za kulevya, ulevi, vita, na matusi ambayo nilizoea kutumia.

Hata hivyo, nilitiwa moyo sana na maneno ya mtume Paulo katika 1 Wakorintho 6:9-11. Andiko hilo linaonyesha kwamba pindi moja Wakristo fulani wa karne ya kwanza walikuwa na mazoea fulani mabaya kama yale niliyokuwa nayo. Lakini andiko hilo linasema hivi pia: “Wengine wenu mlikuwa hivyo. Lakini mmeoshwa mkawa safi, lakini mmetakaswa, lakini mmetangazwa kuwa waadilifu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo na kwa roho ya Mungu wetu.” Maneno hayo yalinipa tumaini kwamba mimi pia ningeweza kufanya mabadiliko yaliyohitajiwa katika maisha yangu ili kumpendeza Mungu.

Nilipoanza kushirikiana na Mashahidi wa Yehova, nilisadiki kwamba dini yao ni ya kweli. Walijua mazoea yangu ya zamani ya jeuri na ukatili, hata hivyo bado walinikaribisha kwa uchangamfu na upendo nishirikiane nao.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Kama singejifunza Biblia na kubadili maisha yangu, labda ningekuwa nimekufa sasa. Badala yake, nimepata furaha ya kumsaidia mmoja wa ndugu zangu kujifunza Biblia na kuacha uzoefu wa dawa za kulevya. Na sasa pia nimewatia moyo watu wengine wa familia yetu waanze kujifunza Biblia. Ninashukuru sana kwamba nimeweza kujiweka wakfu ili nimtumikie Mungu ambaye anatujali sana!

[Blabu katika ukurasa wa 24]

“Niliamua kusali kabla ya kutumbukia katika kishawishi badala ya kusali baada ya kutumbukia katika kishawishi, na hilo lilinisaidia sana”