Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Anakubali Ndoa ya Wake Wengi?

Je, Mungu Anakubali Ndoa ya Wake Wengi?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Mungu Anakubali Ndoa ya Wake Wengi?

Hapana hakubali; Mungu alipoanzisha ndoa ya kwanza katika Edeni aliweka kiwango cha kuoa mke mmoja. Baadaye Yesu Kristo alithibitisha kwamba wafuasi wake walipaswa kufuata kiwango hicho.—Mwanzo 2:18-24; Mathayo 19:4-6.

Lakini je, si ni kweli kwamba wanaume walioishi kabla ya nyakati za Ukristo kama vile Abrahamu, Yakobo, Daudi, na Sulemani walikuwa na wake wengi? Ndiyo, lakini Biblia inaonyesha nini kuhusu mpango huo? Inafunua vurugu na ugomvi ambao ulikuwa katika familia ya Abrahamu na ya Yakobo kwa sababu ya zoea hilo. (Mwanzo 16:1-4; 29:18–30:24) Baadaye, Sheria ya Mungu ilitia ndani amri hii iliyotolewa kwa kila mfalme: “Asizidishe wake kwa ajili yake, ili moyo wake usigeuke kando.” (Kumbukumbu la Torati 17:15, 17) Sulemani alipuuza amri hiyo kwa kuoa wake zaidi ya 700! Inasikitisha kwamba moyo wa Sulemani ulikengeushwa kikweli kutoka kwa Yehova kwa sababu ya uvutano mbaya wa wake zake wengi. (1 Wafalme 11:1-4) Kwa wazi, Biblia inaonyesha matokeo mabaya ya kuoa wake wengi.

Hata hivyo, huenda watu wengine wakajiuliza kwa nini Mungu aliruhusu watu wake waoe wake wengi. Hebu wazia: Je, umewahi kutumia kwa muda kifaa fulani hata ingawa ulihitaji kukiondoa na kuleta kingine, labda uliona kwamba kukiondoa kwa sasa kungesababisha vurugu au usumbufu? Bila shaka, mawazo ya Mungu na njia zake ziko juu zaidi kuliko mawazo na njia zetu. (Isaya 55:8, 9) Hata hivyo, huenda tukatambua sababu fulani nzuri zilizomfanya aruhusu ndoa ya wake wengi kwa muda fulani.

Kumbuka kwamba katika Edeni, Yehova aliahidi kwamba “uzao” ungetokea ambao mwishowe ungemwangamiza Shetani. Baadaye, Abrahamu aliambiwa kwamba angekuwa baba wa taifa kubwa na kwamba Uzao uliotabiriwa ungetokea katika ukoo wake. (Mwanzo 3:15; 22:18) Shetani aliazimia kuzuia Uzao huo usitokee. Kwa hivyo, alijaribu kuliangamiza taifa lote la kale la Israeli. Mara nyingi aliwashawishi Waisraeli kutumbukia katika dhambi ili taifa hilo lipoteze kibali cha Mungu na ulinzi wake.

Ili kuwasaidia Waisraeli kushinda mashambulizi ya Shetani, Yehova aliwatuma manabii wake tena na tena ili kuwaonya watu wake walipoanza kuacha viwango vya uadilifu. Hata hivyo, alijua mapema kwamba watu wake wangeshindwa mara nyingi kutii hata amri rahisi zaidi, kama vile amri iliyokataza ibada ya sanamu. (Kutoka 32:9) Kama ilikuwa vigumu sana kwao kutii amri rahisi kama hiyo, je, ingekuwa rahisi kwao kutii amri iliyowakataza kuoa wake wengi? Kwa kuwa anaelewa kikamilifu hali ya wanadamu, Yehova aliona kwamba haukuwa wakati unaofaa wa kukataza zoea hilo, ambalo tayari lilikuwa limeenea sana katika siku hizo. Ikiwa angekataza zoea hilo, Shetani angepata njia rahisi sana ya kuwashawishi Waisraeli wafanye dhambi.

Hatua ya Mungu ya kuruhusu kwa muda fulani ndoa ya wake wengi ilikuwa na faida nyingine. Ililisaidia taifa hilo kuongezeka haraka. Kuwa na watu wengi kulihakikisha kwamba taifa hilo liliendelea kuwapo mpaka wakati wa Masihi. Huenda zoea la kuoa wake wengi liliwalinda kwa kadiri fulani wanawake wengine, na kuwawezesha kupata makao na familia katika nyakati za hatari.

Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova hakuanzisha zoea hilo. Aliliruhusu kwa muda fulani tu, na aliweka sheria kali ili watu wasilitumie vibaya. (Kutoka 21:10, 11; Kumbukumbu la Torati 21:15-17) Yehova alipoamua kukomesha zoea la kuoa wake wengi kati ya waabudu wake, alimtumia Mwana wake mwenyewe kukazia tena kiwango cha ndoa ambacho kiliwekwa katika Edeni. Kwa hiyo, Yesu aliwakataza wafuasi wake kuoa wake wengi. (Marko 10:8) Hivyo, ukweli huu ukawa wazi zaidi: Sheria ya Musa ilifaa kwa wakati wake, lakini “sheria ya Kristo” ni nzuri hata zaidi.—Wagalatia 6:2.